Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Sikuzote Tunabishana?

Kwa Nini Sikuzote Tunabishana?

SURA YA 2

Kwa Nini Sikuzote Tunabishana?

Katika utangulizi wa sura hii, Rachel anaongeza kuni kwenye moto kwa njia tatu. Unaweza kutambua njia hizo? Andika majibu yako hapa chini, kisha uyalinganishe na majibu yaliyo katika kisanduku cha “ Majibu” katika ukurasa wa 20.

․․․․․

Ni Jumatano (Siku ya 3) jioni. Rachel, mwenye umri wa miaka 17, amemaliza kazi zake za nyumbani naye anataka kupumzika! Anawasha televisheni na kuketi kwenye kiti anachopenda.

Wakati huohuo, mama yake anaingia, naye hana furaha. “Rachel! Kwa nini unapoteza wakati ukitazama televisheni badala ya kumsaidia dada yako kufanya kazi za shule? Hufanyi kamwe unachoambiwa!”

“Umeanza tena,” Rachel asema kimyakimya.

Mama amkaribia. “Unasema nini?”

“Hakuna,” Rachel anasema akishusha pumzi, akizungusha macho kwa dhihaka.

Sasa Mama amekasirika kwelikweli. “Hutazungumza nami kwa njia hiyo!”

“Na wewe je?” Rachel amjibu.

Mapumziko kwisha . . . ubishi mwingine umeanza.

UMEWAHI kujionea kisa kama hicho? Je, wewe na wazazi wako mnabishana kila wakati? Ikiwa ndivyo, tenga wakati uchanganue hali. Ni mambo gani ambayo ninyi hubishania zaidi? Tia alama ya ✔ katika visanduku vinavyohusika, au unaweza kuandika jibu tofauti kando ya maneno “Sababu nyingine.”

Mtazamo

Kazi za nyumbani

Mavazi

Saa unazopaswa kurudi nyumbani

Burudani au starehe

Marafiki

Watu wa jinsia tofauti

Sababu nyingine ․․․․․

Hata chanzo cha ubishi kiwe nini, kubishana kwenyewe kutakuacha wewe na wazazi wako katika hali isiyopendeza. Ijapokuwa unaweza tu kunyamaza na kujifanya unakubaliana na kila jambo ambalo wazazi wako wanasema, unafikiri hivyo ndivyo Mungu angependa ufanye? Hapana. Ni kweli kwamba Biblia inasema ‘umheshimu baba yako na mama yako.’ (Waefeso 6:2, 3) Lakini pia inakutia moyo ukuze “uwezo wa kufikiri” na utumie ‘nguvu zako za kufikiri.’ (Methali 1:1-4; Waroma 12:1) Hivyo basi, inatazamiwa kwamba utakuwa na maoni fulani ambayo huenda nyakati nyingine yakatofautiana kabisa na ya wazazi wako. Hata hivyo, katika familia zinazofuata kanuni za Biblia, wazazi na vijana wanaweza kuzungumza kwa amani—hata wakati ambapo maoni yao yanatofautiana.Wakolosai 3:13.

Basi, unaweza kujieleza kwa njia gani ambayo haitabadili mazungumzo ya kawaida yawe mabishano makali? Huenda ukasema: “Wenye shida ni wazazi wangu. Kwanza, wao ndio hunifuata-fuata kila wakati!” Lakini fikiri kidogo: Kwa kweli, una uwezo wa kubadili jinsi wengine walivyo, kutia ndani wazazi wako? Yule tu unayeweza kumbadili ni wewe mwenyewe. Na jambo lenye kutia moyo ni kwamba wewe ukifanya sehemu yako na kupunguza uwezekano wa ubishi kutokea, yaelekea wazazi wako watakuwa watulivu na kukusikiliza unapokuwa na jambo la kusema.

Kwa hiyo, acha tuone kile ambacho wewe unaweza kufanya ili kubadili hali. Tumia mapendekezo yafuatayo na huenda ukawashangaza wazazi wako—au hata ukajishangaza—na njia zako mpya za mawasiliano.

Fikiri kabla ya kujibu. Usiropoke unapohisi kana kwamba unashambuliwa. Kwa mfano, tuseme mama yako anakuambia: “Mbona hukusafisha vyombo? Hufanyi kamwe unachoambiwa!” Bila kufikiri, huenda ukasema, “Kwa nini unanisumbua?” Badala yake, tumia uwezo wako wa kufikiri. Jaribu kuelewa sababu inayomfanya mama yako aseme maneno hayo. Kwa kawaida, maneno “sikuzote” au “kamwe” hayapaswi kuchukuliwa kihalisi. Hata hivyo, yanatokana na hisia fulani. Hisia gani?

Huenda mama yako amevunjika moyo na anahisi kwamba analemewa na kazi za nyumbani. Labda anataka tu kuhakikishiwa kwamba unamhangaikia. Ikiwa ndivyo, kusema “Mbona unanisumbua?” hakutakufikisha popote—ila tu kutokeza ugomvi! Hivyo basi, kwa nini usimtulize mama yako? Kwa mfano, unaweza kusema: “Pole, Mama. Nitavisafisha sasa hivi.” Uwe mwangalifu: Usiseme hivyo kwa dhihaka. Onyesha kwamba unamjali, na huenda hasira yake ikapoa naye akueleze tatizo hasa ni nini. *

Andika hapa chini maneno ambayo baba au mama yako anaweza kusema na ambayo yanaweza kukukasirisha.

․․․․․

Sasa fikiria jinsi unavyoweza kujibu kwa njia inayoonyesha kwamba unajali.

․․․․․

Zungumza kwa heshima. Michelle amejifunza umuhimu wa kuzingatia jinsi anavyozungumza na mama yake. Anasema, “Hata iwe tunazungumzia tatizo gani, kila mara Mama husema hapendi jinsi ninavyozungumza naye.” Ikiwa mara nyingi ndivyo ilivyo kwako pia, jifunze kuzungumza kwa sauti ya chini na polepole, na uepuke kuzungusha-zungusha macho yako au kuonyesha kwa njia nyingine yoyote kwamba umekasirika. (Methali 30:17) Ukiona kwamba unakaribia kulipuka kwa hasira, toa sala fupi ya kimyakimya. (Nehemia 2:4) Bila shaka, kusudi lako si kwamba Mungu awazuie wazazi wako wasikusumbue bali kwamba ujizuie na usifanye hali iwe mbaya zaidi.—Yakobo 1:26.

Kwenye nafasi iliyo hapa chini, andika maneno na matendo fulani ambayo umezoea kufanya na ambayo unapaswa kuepuka.

Maneno (yale unayosema):

․․․․․

Matendo (ishara za uso na za mwili):

․․․․․

Sikiliza. Biblia inasema: “Wakati maneno ni mengi, dhambi haikosekani.” (Methali 10:19, Neno–Biblia Takatifu) Kwa hiyo, hakikisha kwamba unampa baba au mama yako nafasi ya kuzungumza na kwamba unawasikiliza wazazi wako kwa makini. Usiwakatize ili kujitetea. Sikiliza tu. Baadaye, wakimaliza kuzungumza, utakuwa na nafasi ya kutosha kuuliza maswali au kueleza maoni yako. Kwa upande mwingine, ukisisitiza kwamba lazima ueleze maoni yako sasa, huenda ukaharibu mambo hata zaidi. Hata ikiwa kuna mengi ungependa kusema, huenda ukawa ni “wakati wa kukaa kimya.”—Mhubiri 3:7.

Uwe tayari kuomba msamaha. Sikuzote inafaa kuomba msamaha kwa sababu ya jambo lolote ulilofanya kuchangia ugomvi. (Waroma 14:19) Hata unaweza kusema kwamba unasikitika kuna ugomvi. Ukiona ni vigumu kusema hilo moja kwa moja, jaribu kuandika hisia zako. Kisha, usiachie hapo, ‘nenda kilomita mbili,’ yaani, jitahidi sana kubadili tabia iliyochangia mabishano. (Mathayo 5:41) Kwa mfano, ikiwa ubishi ulitokea kwa sababu hukufanya kazi fulani, washangaze wazazi wako kwa kuifanya. Hata ikiwa hupendi kufanya kazi hiyo, je, si afadhali kuifanya kuliko kuwakasirisha wazazi wako wanapogundua kwamba hujaifanya? (Mathayo 21:28-31) Fikiria faida za kufanya sehemu yako ili kupunguza uwezekano wa kutokea kwa ubishi kati yako na wazazi wako.

Familia zenye mafanikio huwa na matatizo, lakini zinajua jinsi ya kuyatatua kwa amani. Jizoeze kufanya mambo yaliyotajwa katika sura hii, na huenda ukaona kwamba unaweza kuzungumzia hata mambo magumu pamoja na wazazi wako—bila kubishana!

KATIKA SURA INAYOFUATA

Unafikiri wazazi wako wanapaswa kukupa uhuru zaidi? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 26 Unaweza kupata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 21.

ANDIKO MUHIMU

“Moyo wa mwadilifu hufikiri kabla ya kujibu.”—Methali 15:28, Biblia Habari Njema.

PENDEKEZO

Wazazi wako wanapozungumza nawe, zima muziki, weka kando kitabu au gazeti unalosoma, na uwatazame.

JE, WAJUA . . . ?

Kujitahidi kutatua au kuzuia ugomvi kutakurahisishia mambo maishani mwako. Biblia inasema kwamba mtu “mwenye fadhili zenye upendo anaitendea kwa kuipa thawabu nafsi yake mwenyewe.” Methali 11:17.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Jambo kuu katika sura hii ambalo ninahitaji kufanyia kazi zaidi ni ․․․․․

Nimeazimia kuanza kutumia pendekezo hilo kuanzia (andika tarehe) ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini vijana wenzako hujivunia uwezo wa kushinda mabishano?

● Kwa nini Yehova Mungu anamwona mtu mgomvi kuwa mpumbavu?—Methali 20:3.

Wewe binafsi, unaweza kupata faida gani kwa kupunguza mambo yanayosababisha ugomvi kati yako na wazazi wako?

[Blabu katika ukurasa wa 18]

“Nyakati nyingine mama yangu hunikumbatia na kusema ‘pole,’ nami napenda hivyo. Kisha tunasahau yaliyopita. Mimi hujaribu kufanya hivyo pia. Kujinyenyekeza na kusema ‘pole’ kwa unyoofu kuna faida kubwa, ingawa kufanya hivyo si rahisi.”—Lauren

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

 Majibu

1. Kuzungumza kwa dhihaka au kwa kutumia maneno yenye kuumiza (“Umeanza tena”) kuliongeza kuni kwenye moto na kumfanya mama yake akasirike hata zaidi.

2. Kwa uso wake (kuzungusha macho), Rachel alikuwa akimchokoza mama yake.

3. Kujibizana (“Na wewe je?”), sikuzote huharibu mambo hata zaidi.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kubishana na mzazi wako ni kama kukimbia juu ya mtambo wa mazoezi—unatumia nguvu nyingi lakini hufiki popote