Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kupata Uhuru Zaidi Jinsi Gani?

Ninaweza Kupata Uhuru Zaidi Jinsi Gani?

SURA YA 3

Ninaweza Kupata Uhuru Zaidi Jinsi Gani?

“Laiti wazazi wangu wangeniruhusu niende matembezi nikiwa peke yangu wakati mwingine.”—Sarah, mwenye umri wa miaka 18.

“Kila mara mimi huwauliza wazazi wangu kwa nini hawaniamini na kunipa ruhusa ninapotaka kwenda matembezi na rafiki zangu. Mara nyingi wao hunijibu: ‘Tunakuamini. Lakini hatuwaamini rafiki zako.’”—Christine, mwenye umri wa miaka 18.

KAMA Sarah na Christine, je, wewe hutamani kuwa na uhuru zaidi? Ili kuupata, lazima kwanza wazazi wako wakuamini. Hata hivyo, sifa ya kuaminika ni kama pesa. Kuzipata ni vigumu, kuzipoteza ni rahisi, na hata ukipewa kiasi gani, hazitoshi kamwe. “Kila mara ninapotaka kwenda matembezi, wazazi wangu huniuliza maswali yasiyo na mwisho, ‘Unaenda wapi? Utakuwa na nani? Unaenda kufanya nini? Utarudi saa ngapi?’,” asema Iliana mwenye umri wa miaka 16. “Ninajua ni wazazi wangu, lakini maswali yao yanaudhi!”

Unaweza kufanya nini ili wazazi wako wakuamini zaidi na kukupa uhuru zaidi? Kabla ya kujibu swali hilo, acha tuone ni kwa nini kutumainiana ni jambo gumu kati ya wazazi na vijana wengi.

Matatizo Unapokua

Biblia inasema kwamba “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Ndivyo pia na mwanamke. Iwe wewe ni mvulana au msichana, kubalehe kunakutayarisha kwa ajili ya maisha ya utu uzima—wakati ambapo utakuwa tayari kuondoka nyumbani na labda kuwa na familia yako mwenyewe. *

Hata hivyo, kuwa mtu mzima si kama mlango ambao unaingia tu unapofikia umri fulani. Badala yake ni kama ngazi unazopanda hatua kwa hatua wakati wa kipindi chote cha kubalehe. Ni kweli kwamba huenda wewe na wazazi wako mkawa na maoni tofauti kuhusu hatua ambazo umepiga. “Nina umri wa miaka 20 na bado naulizwa maswali,” asema Maria anayeona kwamba wazazi wake hawaamini kwamba anaweza kuchagua marafiki wazuri. “Wazazi wangu wanafikiri kwamba sina ujasiri wa kutosha kuondoka hali mbaya inapotokea. Nimejaribu kuwaambia kwamba tayari nimejiondoa katika hali nyingi mbaya, lakini wapi!”

Kama maneno ya Maria yanavyoonyesha, kutoaminiwa kunaweza kutokeza matatizo makubwa kati ya vijana na wazazi wao. Je, hivyo ndivyo familia yenu ilivyo? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini ili wazazi wako wakuamini zaidi? Na ikiwa wameacha kukuamini kwa sababu ya jambo fulani lisilo la hekima ulilofanya, unaweza kufanya nini ili kurudisha imani waliyokuwa nayo?

Onyesha Kwamba Unaweza Kuaminika

Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa karne ya kwanza: “Endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Wakorintho 13:5) Ni kweli kwamba hakuwa akizungumza hasa na vijana. Lakini kanuni hiyo inaweza kutumika. Mara nyingi uhuru unaopata hulingana na kadiri unavyoaminika. Haimaanishi kwamba unahitaji kuwa mkamilifu. Kila mtu hukosea. (Mhubiri 7:20) Hata hivyo, kwa ujumla, inawezekana kwamba mwenendo wako unawafanya wazazi wako wasikuamini?

Kwa mfano, mtume Paulo aliandika: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Jiulize, ‘Ninawaambia wazazi wangu kweli nyakati zote kuhusu ninakoenda na mambo ninayofanya?’ Fikiria maelezo ya vijana fulani ambao wamejichunguza kwa uangalifu na kuona kwamba wanahitaji kufanya marekebisho. Baada ya kusoma maelezo yao, jibu maswali yanayofuata.

Lori: “Nilikuwa nikimtumia barua-pepe kisiri mvulana fulani niliyempenda. Wazazi wangu waligundua na kuniambia niache. Nikawaambia nitaacha, lakini sikuacha. Niliendelea kwa mwaka mzima. Nilikuwa nikimtumia mvulana huyo barua-pepe, wazazi wangu wanagundua, ninaomba msamaha na kuahidi kwamba nitaacha, lakini ninaendelea. Ilifikia hatua ambapo wazazi wangu hawakuniamini kamwe kuhusu lolote!”

Unafikiri ni kwa nini wazazi wa Lori waliacha kumwamini? ․․․․․

Kama wewe ungekuwa ndiye mzazi wa Lori, ungefanya nini, na kwa nini? ․․․․․

Lori alipaswa kufanya nini baada ya wazazi wake kuzungumza naye kuhusu tatizo lake? ․․․․․

Beverly: “Wazazi wangu hawakuniamini inapohusu wavulana, lakini sasa ninaelewa ni kwa nini. Nilikuwa nikiwachezea kimapenzi wavulana mawili walionizidi umri kwa miaka miwili. Nilikuwa nikizungumza nao kwa muda mrefu kwenye simu, na katika vikusanyiko mbalimbali ningezungumza nao peke yao. Wazazi wangu walininyang’anya simu kwa mwezi mmoja, na hawakuniruhusu niende popote pamoja na wavulana hao.”

Kama wewe ungekuwa mzazi wa Beverly, ungefanya nini, na kwa nini? ․․․․․

Unafikiri vizuizi ambavyo wazazi wa Beverly walimwekea havikustahili? Ikiwa havikustahili, ni kwa nini? ․․․․․

Beverly angeweza kufanya nini ili wazazi wake waanze kumwamini tena? ․․․․․

Kuaminiwa Tena

Namna gani ikiwa, kama vijana waliotajwa hapo juu, mwenendo wako umewafanya wazazi wako wasikuamini? Hata ikiwa hivyo ndivyo ilivyo, uwe na hakika kwamba unaweza kubadili hali. Jinsi gani?

Haikosi wazazi wako watakuamini zaidi na kukupa uhuru zaidi ukiendelea kujiendesha kwa njia inayofaa. Msichana anayeitwa Annette, alijionea hilo mwishowe. Anasema: “Unapokuwa na umri mdogo, huelewi kabisa kwa nini ni jambo la maana kuwa mwenye kuaminika. Sasa najiona kuwa mwenye kuwajibika zaidi na kwamba ninahitaji kujiendesha kwa njia itakayowafanya wazazi wangu waendelee kuniamini.” Siri ni nini? Badala ya kulalamika kwamba wazazi wako hawakuamini, jitahidi sikuzote kujiendesha kwa njia inayofaa. Huenda utapata uhuru zaidi.

Kwa mfano, je, unategemeka katika mambo yaliyoorodheshwa hapa chini? Tia alama ya ✔ katika kisanduku kilicho kando ya mambo unayohitaji kufanyia kazi.

□ Kurudi nyumbani wakati niliowekewa na wazazi

□ Kutimiza ahadi zangu

□ Kutunza wakati

□ Kutumia pesa kwa hekima

□ Kumaliza kazi za nyumbani

□ Kutoka kitandani bila kuambiwa-ambiwa

□ Kudumisha chumba changu kikiwa safi

□ Kusema kweli

□ Kuwa na usawaziko kuhusu matumizi ya simu au kompyuta

□ Kukubali makosa na kuomba msamaha

□ Jambo lingine ․․․․․

Kwa nini usiazimie kuthibitika kuwa mwaminifu katika mambo uliyotia alama? Fuata himizo hili la Biblia: ‘Ondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wako wa kwanza.’ (Waefeso 4:22) ‘Acha Ndiyo yako imaanishe Ndiyo.’ (Yakobo 5:12) “Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.” (Waefeso 4:25) “Watiini wazazi wenu katika kila jambo.” (Wakolosai 3:20) Baada ya muda, maendeleo yako yatakuwa wazi kwa watu wengine, kutia ndani wazazi wako.—1 Timotheo 4:15.

Lakini namna gani ukihisi kwamba hata baada ya kufanya yote uwezayo, bado wazazi wako hawakupi uhuru unaostahili? Unaweza kuzungumza nao kuhusu jambo hilo. Badala ya kulalamika kwamba wao wanahitaji kukuamini zaidi, waulize kwa heshima wanataka wewe ufanye nini ili wakuamini. Waeleze waziwazi unachokusudia kufanya ili wakuamini zaidi.

Usitazamie wazazi wako wakubaliane nawe mara moja. Bila shaka, wangependa kuhakikisha kwamba utatimiza ahadi zako. Tumia kipindi hicho kujithibitisha kuwa unaaminika. Baada ya muda, wazazi wako watakuamini zaidi na kukupa uhuru zaidi. Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa kwa Beverly aliyetajwa mapema. “Si rahisi kuaminiwa lakini ni rahisi sana kuacha kuaminiwa,” anasema huku akiongezea, “nimeanza kuaminiwa sasa, na ninahisi vizuri!”

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 22

KATIKA SURA INAYOFUATA

Je, wazazi wako wametalikiana? Unaweza kuwa na usawaziko jinsi gani wakati ambapo kila kitu kinaonekana kwenda kombo maishani mwako?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Unaweza kupata habari zaidi katika Sura ya 7 ya kitabu hiki.

ANDIKO MUHIMU

“Msitumie uhuru wenu kama kisingizio cha kutenda uovu.” —1 Petro 2:16, Neno—Biblia Takatifu.

PENDEKEZO

Badala ya kulinganisha vizuizi ulivyo navyo sasa na uhuru ambao ndugu au dada yako mkubwa anao, linganisha vizuizi ulivyokuwa ukiwekewa ulipokuwa na umri mdogo zaidi na uhuru ulio nao sasa.

JE, WAJUA . . . ?

Kupewa uhuru usio na mipaka si ishara ya kupendwa na wazazi bali ni ishara ya kupuuzwa na wazazi.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nitakuwa mwenye kutegemeka zaidi katika mambo yafuatayo: ․․․․․

Wazazi wangu wakiacha kunitumaini, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini huenda wazazi wako wakasita kukupa uhuru zaidi hata unapojitahidi sana kuwa mtu mwenye kutegemeka?

● Kwa nini wakati mwingine kupata uhuru zaidi kunategemea jinsi unavyopashana habari na wazazi wako?

[Blabu katika ukurasa wa 24]

“Ninapozungumza na wazazi wangu, ninawaambia waziwazi matatizo yangu na mambo yanayonihangaisha. Nafikiri hilo linafanya iwe rahisi kwao kuniamini.”—Dianna

[Mchoro/​Picha katika ukurasa wa 23]

Kufikia kuwa mtu mzima anayeaminiwa ni kama kupanda ngazi hatua kwa hatua katika kipindi chote cha kubalehe

[Mchoro]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

UTU UZIMA

KUBALEHE

UTOTO