Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini Mzazi Wangu Akifunga Ndoa Upya?

Nifanye Nini Mzazi Wangu Akifunga Ndoa Upya?

SURA YA 5

Nifanye Nini Mzazi Wangu Akifunga Ndoa Upya?

HUENDA mzazi wako akawa na furaha nyingi siku anayofunga ndoa upya. Hata hivyo, huenda wewe usiwe na furaha hata kidogo! Kwa nini? Mzazi anapofunga ndoa upya, hakuna matumaini tena ya wazazi wako halisi kurudiana. Kwa upande mwingine, huenda ndoa hiyo mpya ikaumiza sana hasa ikiwa ni muda mfupi tu baada ya kifo cha mzazi mpendwa.

Ulihisi namna gani mzazi wako alipofunga ndoa upya? Tia alama ya ✔ kando ya hali yoyote inayofafanua jinsi ulivyohisi.

Nilikuwa na . . .

□ Furaha

□ Wasiwasi

□ Hisia za kusalitiwa

□ Wivu kumwelekea mzazi wa kambo

□ Hisia za kuwa msaliti kwa kumpenda mzazi wa kambo

Hisia za kuwa msaliti zinaweza kutokana na upendo wako kwa mzazi ambaye hayupo kwa sasa. Hata sababu iwe nini, hisia zinazotajwa juu zinaweza kukufanya utende kwa njia isiyofaa kwa sababu ya kutojua jinsi ya kushughulika na hali hizo.

Kwa mfano, huenda ukaamua kufanya maisha ya mzazi wako wa kambo yawe magumu nyakati zote. Huenda hata ukajaribu kusababisha matatizo kati ya mzazi wako na mzazi wa kambo, ukitaka watengane. Hata hivyo, methali moja yenye hekima inaonya: “Yeye aletaye taabu kwa jamaa yake atarithi tu upepo,” yaani, hatakuwa na chochote. (Methali 11:29, Neno—Biblia Takatifu) Si lazima unaswe na mtego huo. Unaweza kushughulikia hisia zako kwa njia bora zaidi. Fikiria mifano michache.

Changamoto ya 1: Kutambua Mamlaka ya Mzazi wa Kambo

Si rahisi kutambua mamlaka ya mzazi mpya. Unapoombwa ufanye jambo fulani, huenda ukapayuka, ‘Wewe si mama/baba yangu!’ Huenda ukaona kwamba umetimiza jambo kubwa kwa kusema hivyo, hata hivyo unafunua kwamba bado unahitaji kukomaa.

Kwa upande mwingine, kukubali mamlaka ya mzazi wako wa kambo ni njia moja ya kuonyesha kwamba unatii shauri hili la Biblia: “Katika kufikiri kwenu, mwe watu wazima.” (1 Wakorintho 14:20, NBT) Kwa kweli, mzazi wa kambo anatimiza mambo yaleyale yanayopaswa kutimizwa na mzazi halisi, naye anastahili kuheshimiwa.—Methali 1:8; Waefeso 6:1-4.

Mzazi wa kambo anapokutia nidhamu, anaonyesha kwamba anakupenda na anakuhangaikia. (Methali 13:24) “Baba yangu wa kambo hututia nidhamu,” asema Yvonne, mwenye umri wa miaka 18, “lakini hivyo ndivyo akina baba wanavyopaswa kufanya. Naona kwamba nikikataa mashauri yake, basi sithamini jinsi ambavyo amekuwa akituandalia kimwili na kiroho kwa miaka mingi. Na kufanya hivyo ni kukosa shukrani.”

Hata hivyo, huenda bado ukawa na sababu ya kulalamika. Ikiwa ndivyo, onyesha kwamba wewe ni ‘mtu mzima,’ kwa kufanya vile andiko la Wakolosai 3:13 linavyohimiza: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”

Andika hapa chini sifa nzuri mbili au zaidi za mzazi wako wa kambo.

․․․․․

Kukumbuka sifa nzuri za mzazi wako wa kambo kunaweza kukusaidia jinsi gani kumheshimu zaidi?

․․․․․

Changamoto ya 2: Kujifunza Kushiriki Vitu na Kutokuwa Mgumu Sana

“Baba yangu alifunga ndoa upya mara mbili,” akumbuka Aaron mwenye umri wa miaka 24. “Ilikuwa vigumu kwangu kuzipenda familia hizo mpya. Mwanzoni walikuwa wageni tu kwangu, lakini niliambiwa ni lazima niwapende. Hali hiyo ilinitatiza sana.”

Wewe pia unaweza kukabili hali ngumu. Kwa mfano, huenda sasa wewe si mtoto wa kwanza tena, au mtoto pekee katika familia yenu. Ikiwa wewe ni mwana, huenda kwa muda mrefu umekuwa ukijiona kuwa una daraka la kutunza familia yenu, daraka ambalo sasa limechukuliwa na baba wa kambo. Au huenda hali zako ni kama za Yvonne. Anasema: “Baba yangu mzazi hakumjali mama yangu hata kidogo, kwa hiyo, nilitumia muda mwingi naye. Lakini mama yangu alipoolewa tena, baba yangu wa kambo alimpenda sana. Walitumia muda mwingi pamoja na kuzungumza pamoja, nami nikaanza kuhisi kwamba ananitenganisha na mama yangu. Hata hivyo, mwishowe, nilibadilika kulingana na hali.”

Kama Yvonne, unaweza kubadilika jinsi gani? Biblia inapendekeza: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Katika lugha ya awali iliyotumiwa kuandika Biblia, neno linalotafsiriwa “usawaziko” linamaanisha “kusalimu amri, kukubali kushindwa, kuacha upinzani, au kuachia nafasi” na linaonyesha mtazamo wa mtu ambaye hasisitizi haki zake zote zifuatwe. Basi, unaweza kutumia jinsi gani shauri hilo? (1) Epuka kufikiria sana mambo yaliyopita. (Mhubiri 7:10) (2) Kuwa tayari kushiriki vitu pamoja na mzazi wako wa kambo, na ndugu na dada zako wa kambo. (1 Timotheo 6:18) (3) Usiwatendee kama wapita-njia.

Kati ya mambo yaliyotajwa, ni mambo gani unayohitaji kufanyia kazi zaidi? ․․․․․

Changamoto ya 3: Kutendewa Isivyo Haki

“Baba yangu wa kambo aliwapenda watoto wake kuliko alivyonipenda mimi na dada yangu,” asema Tara. “Alikuwa akiwanunulia chakula chochote wanachopenda na kuwachukulia filamu wanazotaka kutazama. Alifanya kila kitu ili kuwafurahisha.” Kuvumilia hali kama hiyo si rahisi. Ni nini kinachoweza kukusaidia? Jaribu kuelewa ni kwa nini huenda mzazi wa kambo asimwonyeshe mtoto wa kambo hisia zilezile alizo nazo kuelekea mtoto wake halisi. Huenda hafanyi hivyo kwa sababu damu ni nzito kuliko maji, lakini labda ni kwa sababu wamefanya mambo mengi maishani wakiwa pamoja. Hata wewe, haikosi una uhusiano wa karibu zaidi na mzazi wako halisi kuliko na mzazi wa kambo.

Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya kutendewa kama wengine na kutendewa kwa haki. Watu wana nyutu na mahitaji tofauti. Kwa hiyo, badala ya kuhangaikia sana iwapo mzazi wako wa kambo anakutendea sawa na watoto wake, jaribu kuona ikiwa anajitahidi kukutimizia mahitaji yako.

Ni mahitaji gani uliyo nayo ambayo mzazi wako wa kambo anakutimizia?

․․․․․

Ni mahitaji gani unayoona kwamba yamepuuzwa?

․․․․․

Ikiwa unaona kwamba mahitaji fulani yanapuuzwa, jaribu kuzungumza kwa heshima na mzazi wako wa kambo kuhusu jambo hilo.

Subira Huvuta Heri!

Kwa kawaida, kuzoeana na kuaminiana kati ya washiriki wa familia ya kambo huchukua miaka mingi. Na baada ya muda mrefu ndipo mazoea na sifa mbalimbali zinapoingiana na kuwa kawaida ya maisha. Kwa hiyo, onyesha subira! Usitazamie kuonyeshwa upendo mara moja, wala usitazamie kwamba mtakuwa familia nzuri siku ya kwanza.

Mama ya Thomas alipoolewa tena, Thomas hakuwa na raha hata kidogo. Mama yake alikuwa na watoto wanne, na mwanamume aliyemwoa alikuwa na watoto watatu. “Tulipigana, tukabishana, tukavurugana, na tulikuwa na mikazo ya kihisia,” akasema Thomas. Ni nini kilichowasaidia? “Tulitatua matatizo kwa kutumia kanuni za Biblia.”

KATIKA SURA INAYOFUATA

Namna gani ikiwa ndugu na dada zako si wa kambo lakini wanakuudhi?

ANDIKO MUHIMU

“Mwisho wa jambo ni bora kuliko mwanzo wake. Mtu mwenye subira ni bora kuliko mwenye roho ya majivuno.”—Mhubiri 7:8.

PENDEKEZO

Kuishi pamoja na ndugu au dada zako wa kambo wa jinsia tofauti kwaweza kuamsha tamaa za ngono. Kwa hiyo, ondolea mbali kabisa mawazo yoyote ya kingono akilini, na uhakikishe kwamba huvalii wala kujiendesha kwa njia inayoamsha tamaa za ngono.

JE, WAJUA . . . ?

Huenda ni vigumu pia kwa ndugu au dada zako wa kambo kuzoea maisha mapya ya familia ya kambo.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nitajitahidi kumheshimu zaidi mzazi wangu wa kambo kwa kukumbuka mambo mazuri yafuatayo ambayo ameifanyia familia yetu (andika mambo mawili mazuri): ․․․․․

Ndugu au dada zangu wa kambo wakinipuuza, ninaweza kutumia kanuni ya Waroma 12:21 kwa kufanya yafuatayo: ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Huenda mzazi, ndugu, au dada zako wa kambo, wakawa na wasiwasi gani kuhusu kujiunga na familia yenu?

● Kwa nini ni vizuri kufikiria jinsi maisha ya familia yenu yatakavyokuwa siku za usoni badala ya kukazia fikira mambo madogo-madogo yanayotokea sasa?

[Blabu katika ukurasa wa 38]

“Ndoa ya pili ya mama iliishia katika talaka. Lakini mpaka leo hii bado nina uhusiano mzuri na ndugu na dada zangu wa kambo. Ninafurahi sana kwamba nilipata kuwajua.”—Tara

[Picha katika ukurasa wa 39]

Kuchanganya familia mbili ni kama kuchanganya maji na sementi, huchukua muda na kazi, lakini mwishowe matokeo yanaweza kuwa yenye kudumu