Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini ili Nielewane na Ndugu na Dada Zangu?

Nifanye Nini ili Nielewane na Ndugu na Dada Zangu?

SURA YA 6

Nifanye Nini ili Nielewane na Ndugu na Dada Zangu?

Kwa kutumia kipimo cha 1 mpaka 5, nambari 1 ikiwakilisha “mbovu kabisa” na 5 ikiwakilisha “mzuri kabisa,” ungesema uhusiano kati yako na ndugu na dada zako uko katika kiwango gani? ․․․․․

NDUGU na dada fulani huwa na uhusiano mzuri sana. Kwa mfano, Felicia, mwenye umri wa miaka 19, anasema, “Dadangu, Irena, mwenye umri wa miaka 16, ni mmoja wa rafiki zangu wa karibu zaidi.” Naye Carly, mwenye umri wa miaka 17, anasema hivi kuhusu ndugu yake mwenye umri wa miaka 20, anayeitwa Eric: “Tunaelewana kabisa. Hatugombani kamwe.”

Kwa upande mwingine, vijana wengi wana uhusiano kama ule wa Lauren na Marla. “Tunagombania kila kitu,” asema Lauren. “Hata kiwe ni kidogo kadiri gani.” Au labda hali yako ni sawa na ya Alice mwenye umri wa miaka 12, anayesema hivi kuhusu ndugu yake mwenye umri wa miaka 14, anayeitwa Dennis: “Ananiudhi sana! Yeye huingia chumbani mwangu bila kupiga hodi na kuchukua vitu vyangu bila kuomba. Dennis ana utoto mwingi sana!”

Una ndugu au dada anayekuudhi kila wakati? Bila shaka, wazazi wako wana daraka la kudumisha amani katika familia. Hata hivyo, muda si muda, utahitaji kujifunza jinsi ya kuishi na watu wengine. Unaweza kujifunza ukiwa bado nyumbani.

Fikiria mizozo ambayo wewe na ndugu au dada yako mmekuwa nayo. Mara nyingi ninyi huzozania nini? Tazama orodha iliyo hapa chini, kisha utie alama ya ✔ kando ya jambo ambalo hukufanya ulipuke!

Vitu ulivyo navyo. Ndugu au dada yangu huchukua vitu vyangu bila kuomba.

Nyutu zinazotofautiana. Ndugu au dada yangu ana ubinafsi sana au hanijali au hujaribu kunitawala.

Faragha. Ndugu au dada yangu huingia chumbani mwangu bila kupiga hodi au husoma barua zangu au jumbe zangu kwenye simu bila kuomba ruhusa.

Sababu nyingine ․․․․․

Ikiwa ndugu au dada yako anakuudhi kila mara, akijaribu kukuongoza, au hakupi nafasi ya kupumua, huenda ukajikuta umeanza kumchukia. Methali moja ya Biblia inasema: “Kufinya pua ndiko hutokeza damu, na kuchochea hasira ndiko hutokeza ugomvi.” (Methali 30:33) Ukiweka kinyongo, itakuwa rahisi kulipuka kwa hasira kama vile tu kufinya pua kunavyoweza kufanya damu itoke. Kisha tatizo lililopo litazidi kuwa baya. (Methali 26:21) Unaweza kuzuia jinsi gani hasira isitokeze magombano? Hatua ya kwanza ni kutambua chanzo cha tatizo

Tofauti Kati ya Tatizo na Kisababishi

Matatizo kati ya mtu na ndugu au dada yake ni kama chunusi. Kwa kawaida chunusi huwasha na ina sura isiyopendeza, hata hivyo chanzo cha tatizo hilo ni ambukizo fulani. Vivyo hivyo, ndugu na dada katika familia wanapozozana vikali lazima kuna kisababishi.

Unaweza kuamua kuifinya chunusi inapotokea. Hata hivyo, utakuwa ukishughulikia dalili tu, na huenda ukabaki na kovu au kuzidisha maambukizo. Njia nzuri zaidi ni kujaribu kutatua tatizo lenyewe na kuzuia lisitokee tena. Ndivyo ilivyo pia kuhusu matatizo kati ya mtu na ndugu au dada zake. Jifunze kutambua chanzo cha tatizo, nawe utaweza kufikia tatizo lenyewe. Pia, utaweza kutumia shauri la Mfalme Sulemani mwenye hekima aliyeandika: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake.”—Methali 19:11.

Kwa mfano, Alice, aliyetajwa mwanzoni, alisema hivi kuhusu ndugu yake Dennis, “Yeye huingia chumbani mwangu na kuchukua vitu vyangu bila kuomba.” Hilo ni tukio. Lakini unafikiri shida hasa ni nini? Huenda ikawa heshima. Alice anaweza kuamua kumwambia Dennis asiingie tena kamwe chumbani mwake wala kugusa vitu vyake. Lakini kufanya hivyo ni kama kutibu tu dalili na huenda hilo likatokeza mizozo mingine. Kwa upande mwingine, ikiwa Alice angemsaidia Dennis aone umuhimu wa kuheshimu vitu vyake na kumpa nafasi ya kuwa na faragha, bila shaka, uhusiano wao ungekuwa mzuri zaidi.

Jifunze Kutatua au Kuepuka Mizozo

Kutambua chanzo cha matatizo kati yako na ndugu au dada yako ni sehemu tu ya utatuzi. Unaweza kufanya nini ili kutatua tatizo na kuepuka kuzozana tena wakati ujao? Jaribu kufuata hatua sita zifuatazo.

1. Wekeni sheria fulani za msingi. Tazama tena mambo uliyotaja kuwa chanzo cha ugomvi kati yako na ndugu au dada yako. Jaribuni kuweka sheria fulani ambazo nyote wawili mnakubaliana na ambazo zitawasaidia kutatua chanzo cha matatizo. Kwa mfano, ikiwa mnagombania vitu, Sheria ya 1 inaweza kuwa: “Kabla ya kuchukua kitu cha mtu mwingine, omba ruhusa kwanza.” Sheria ya 2 inaweza kuwa: “Heshimu haki ya ndugu au dada yako ya kusema, ‘Hapana, usiguse kitu hicho.’” Mnapoweka sheria hizo, kumbukeni amri hii ya Yesu: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Kukumbuka maneno hayo kutawasaidia kuweka sheria ambazo wewe na ndugu au dada yako mnaweza kufuata. Kisha, zungumzeni na wazazi wenu kuhusu sheria hizo ili kuhakikisha kwamba wanakubaliana nazo.—Waefeso 6:1.

2. Fuata sheria hizo wewe mwenyewe. Mtume Paulo aliandika: “Hata hivyo, je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba?” (Waroma 2:21) Unaweza kutumia kanuni hiyo jinsi gani? Ikiwa ungetaka ndugu au dada yako aheshimu haki yako ya kutoingiliwa, wewe pia unapaswa kupiga hodi kabla ya kuingia chumbani mwake au kuomba ruhusa kabla ya kusoma barua zake au ujumbe katika simu yake.

3. Usikasirike upesi. Kwa nini shauri hilo linafaa? Kwa sababu, kama methali moja ya Biblia inavyosema, “wajinga ndio hukasirika upesi na kuweka kinyongo.” (Mhubiri 7:9, Contemporary English Version) Ikiwa unakasirika upesi, utakuwa na maisha magumu sana. Ni kweli kwamba huenda ndugu au dada zako wakafanya au kusema mambo yanayokuudhi. Lakini jiulize, ‘Je, mimi nimewahi kuwaudhi kwa njia hiyohiyo wakati uliopita?’ (Mathayo 7:1-5) Jenny anasema: “Nilipokuwa na umri wa miaka 13, nilijiona kuwa bora kuliko kila mtu na kwamba maoni yangu ndiyo ya maana zaidi na lazima yasikiwe. Sasa dada yangu mdogo amefikia hatua hiyo. Kwa hiyo, mimi hujaribu sana nisiudhike kwa sababu ya mambo anayosema.”

4. Samehe na usahau. Matatizo mazito yanahitaji kuzungumziwa na kutatuliwa. Lakini je, ni lazima umfuate-fuate ndugu au dada yako kwa sababu ya kila kosa ambalo anafanya? Yehova Mungu huthamini sana unapokuwa tayari ‘kupita kosa.’ (Methali 19:11) Alison, mwenye umri wa miaka 19, anasema: “Kwa kawaida mimi na dada yangu Rachel hutatua matatizo kati yetu vizuri. Sote huwa tayari kuomba msamaha kwanza halafu tunaeleza kile ambacho tunafikiri kimesababisha tofauti kati yetu. Wakati mwingine tatizo linapotokea silizungumzii mpaka siku inayofuata. Mara nyingi, siku inayofuata ni kana kwamba kila kitu kimesahaulika, na hata si lazima tulizungumzie.”

5. Wahusishe wazazi wenu wawe wapatanishi. Ikiwa wewe na ndugu au dada yako hamwezi kutatua tatizo fulani, huenda wazazi wenu wanaweza kuwasaidia mfanye amani. (Waroma 14:19) Hata hivyo, kumbuka kwamba uwezo wa kutatua tatizo bila kuwahusisha wazazi ni kipimo cha ukomavu wa kweli.

6. Thamini sifa nzuri za ndugu au dada yako. Huenda ndugu au dada yako ana sifa ambazo zinakuvutia. Andika jambo moja ambalo unathamini kuhusu kila mmoja wa ndugu na dada zako.

Jina

․․․․․

Sifa inayonipendeza

․․․․․

Badala ya kukazia fikira sana makosa ya ndugu au dada yako, jaribu kutafuta nafasi ya kumweleza kuhusu sifa zake zinazokuvutia.—Zaburi 130:3; Methali 15:23.

Biblia inasema wazi kwamba huenda ndugu au dada yako wa kimwili asiwe rafiki yako wa karibu zaidi. (Methali 18:24) Hata hivyo, unaweza kuimarisha urafiki kati yako na ndugu au dada zako ‘mkiendelea kuvumiliana,’ hata kunapokuwa na “sababu ya kulalamika.” (Wakolosai 3:13) Ukifanya hivyo, yaelekea wewe hutaudhika sana kwa sababu ya jinsi ambavyo ndugu au dada zako wanatenda. Na hata wewe pia huenda ukaacha kuwaudhi mara nyingi!

KATIKA SURA INAYOFUATA

Ni nini kitakachokusaidia kujua ikiwa uko tayari kuondoka nyumbani?

ANDIKO MUHIMU

“Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.”—Wafilipi 4:5.

PENDEKEZO

Ikiwa unaona ni vigumu kuishi na ndugu au dada yako, sitawisha maoni yanayofaa kwa kumwona kama mtu anayekusaidia kukuza sifa muhimu unazohitaji maishani!

JE, WAJUA . . . ?

Utakapoondoka nyumbani, mara kwa mara utajikuta katikati ya watu wanaokera—wafanyakazi wenzako na wengine wanaoonekana kuwa wakaidi, wasiojali, na wenye ubinafsi. Nyumbani ndipo mahali pa kujifunzia kushughulika kwa amani na hali kama hizo.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Baadhi ya mambo ya msingi tunayoweza kukubaliana na ndugu na dada zangu ni ․․․․․

Naweza kupunguza kuwaudhi ndugu na dada zangu kwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini ni muhimu kuona tofauti kati ya tukio fulani na chanzo cha tatizo lenyewe?

● Unafikiri kuna faida gani ya kuwa na ndugu na dada?

[Blabu katika ukurasa wa 46]

“Kama singekuwa na ndugu na dada zangu, singekuwa na kumbukumbu zozote nzuri. Wale walio na ndugu na dada, nawaambia, ‘Msiwaone vivi hivi tu!’”—Marilyn

[Sanduku katika ukurasa wa 42]

Ukurasa wa Mazoezi

Tambua Chanzo cha Tatizo

Ungependa kuwa na ustadi wa kutambua shina la matatizo kati ya mtu na ndugu au dada zake? Basi, soma masimulizi ya Yesu kuhusu mwana aliyeondoka nyumbani na kutumia vibaya urithi wake. (Luka 15:11-32) Chunguza kwa makini jinsi ndugu mkubwa alivyotendea mdogo wake aliporudi nyumbani kisha ujibu maswali yafuatayo.

Ni tukio gani lililomchochea ndugu mkubwa kutenda alivyotenda? ․․․․․

Unafikiri chanzo cha tatizo lenyewe ni nini? ․․․․․

Baba yao alijaribu kutatua hali hiyo jinsi gani? ․․․․․

Ndugu mkubwa alihitaji kufanya nini ili kutatua mambo? ․․․․․

Sasa fikiria ugomvi uliotokea karibuni kati yako na ndugu au dada yako kisha uandike majibu ya maswali yafuatayo.

Ni tukio gani lililotokeza hali hiyo? ․․․․․

Unafikiri chanzo cha tatizo lenyewe ni nini? ․․․․․

Ni mambo gani ya msingi unayoweza kukubaliana nayo, ambayo yanaweza kusaidia kutatua tatizo hili na kuepusha ugomvi zaidi? ․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 43]

Matatizo kati ya ndugu na dada ni kama chunusi, unahitaji kushughulikia chanzo chake si dalili tu