Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?

Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?

Sura ya 7

Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?

‘Nyakati nyingine mimi huhisi kwamba watu wananidharau kwa sababu bado ninaishi nyumbani kwa wazazi wangu, kana kwamba siwezi kuwa mtu mzima mpaka niondoke nyumbani.’—Katie.

“Nina umri wa karibu miaka 20, nami sipendi kamwe kwamba siwezi kujifanyia maamuzi yanayohusu maisha yangu. Nafikiria kuondoka nyumbani.”—Fiona.

HATA kabla ya kuwa tayari kuondoka nyumbani, huenda ukaanza kutamani kujitegemea. Ni kawaida kuhisi hivyo. Kama Sura ya 3 ilivyoonyesha, kusudi la Mungu lilikuwa vijana wakue, wawe watu wazima na mwishowe wawaache baba na mama zao na kuanzisha familia zao wenyewe. (Mwanzo 2:23, 24; Marko 10:7, 8) Lakini unaweza kujua jinsi gani kwamba kwa kweli uko tayari kuondoka nyumbani? Fikiria maswali matatu ya maana unayohitaji kujibu. Swali la kwanza ni . . .

Nia Yangu Ni Nini?

Tazama orodha iliyo chini. Ukitumia nambari, panga sababu hizi ukianza na sababu kuu zaidi inayokufanya utake kuondoka nyumbani.

․․․․․ Kuhepa matatizo ya nyumbani

․․․․․ Kuwa huru zaidi

․․․․․ Kuheshimiwa na marafiki

․․․․․ Kumsaidia rafiki yangu anayetaka mtu wa kuishi naye

․․․․․ Kufanya kazi ya kujitolea katika eneo lingine

․․․․․ Kujifunza kujitegemea

․․․․․ Kuwapunguzia wazazi wangu mzigo wa kiuchumi

․․․․․ Sababu nyingine ․․․․․

Sababu hizo si mbaya. Lakini, Nia yako ni nini? Kwa mfano, ikiwa sababu yako ni kuhepa vizuizi tu, utashangaa!

Danielle, aliyeondoka nyumbani akiwa na umri wa miaka 20, alijionea mengi. Anasema: “Lazima sote tuwe na vizuizi vya aina fulani maishani. Unapoanza kujitegemea, kazi unayofanya au kukosa pesa kutakuwa kizuizi cha kufanya mambo ambayo unayotaka.” Carmen, aliyehamia nchi ya ng’ambo kwa miezi sita, asema: “Nilifurahia kuwa huko, lakini mara nyingi nilihisi sikuwa na wakati wa kufanya mambo ninayotaka! Nililazimika kufanya kazi za kawaida za nyumbani, kusafisha nyumba, kurekebisha vitu, kung’oa magugu, kufua, kusugua sakafu, na kadhalika.”

Usikubali wengine wakusukume kufanya uamuzi haraka-haraka. (Methali 29:20) Hata ukiwa na sababu zinazofaa za kuondoka nyumbani, mengi zaidi yanahitajika kuliko tu kuwa na nia nzuri. Unahitaji kujua jinsi ya kujitegemea, na ndiyo sababu unapaswa kujiuliza swali hili la pili . . .

Niko Tayari?

Kuondoka nyumbani na kuanza kuishi peke yako ni kama kufunga safari ya kwenda nyikani. Unaweza kwenda nyikani bila kujua jinsi ya kupiga hema, kuwasha moto, kupika, au kusoma ramani? Haiwezekani! Ajabu ni kwamba vijana wengi huondoka nyumbani bila ujuzi wa kutosha kuhusu jinsi ya kuendesha nyumba zao wenyewe.

Mfalme mwenye hekima Sulemani alisema kwamba “mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” (Methali 14:15) Ili kukusaidia kuona iwapo uko tayari kuondoka nyumbani na kwenda kuishi peke yako, fikiria vichwa vifuatavyo. Tia alama ya kando ya mambo ambayo tayari unajua na ya X kando ya mambo ambayo bado unahitaji kufanyia kazi.

Matumizi ya pesa: “Sijawahi kujilipia chochote,” asema Serena mwenye umri wa miaka 19. “Naogopa kuondoka nyumbani na kulazimika kupangia matumizi ya pesa zangu.” Unaweza kujifunza namna gani jinsi ya kutumia pesa?

Methali ya Biblia inasema: “Mtu mwenye hekima atasikiliza na kupata mafundisho zaidi.” (Methali 1:5) Hivyo basi, waulize wazazi wako inamgharimu mtu mmoja pesa ngapi kila juma kulipa kodi ya nyumba, kununua chakula, na kutunza gari au kulipia gharama nyingine za usafiri? Kisha waombe wazazi wako wakusaidie kujua jinsi ya kupanga bajeti na kulipia gharama mbalimbali. *

Kazi za nyumbani: Brian, mwenye umri wa miaka 17, anasema kwamba hofu yake kubwa ni kujifulia nguo atakapoondoka nyumbani. Unaweza kujua jinsi gani kama uko tayari kujitegemea? Aron, mwenye umri wa miaka 20, anapendekeza hivi: “Jaribu kuishi kwa juma moja kana kwamba unajitegemea. Kula chakula ambacho wewe mwenyewe umejipikia, umejinunulia, na ambacho umenunua kwa pesa ambazo wewe mwenyewe umetolea jasho. Vaa nguo ambazo wewe mwenyewe umefua na kupiga pasi. Safisha chumba chako mwenyewe. Na ujaribu kwenda kivyako mahali popote unapohitaji kwenda, bila kupelekwa wala kuchukuliwa na yeyote.” Kufanya mambo hayo kutakusaidia kwa njia mbili: (1) kuwa na ustadi unaohitajika na (2) kuthamini zaidi mambo ambayo wazazi wako wanafanya.

Kushirikiana na wengine: Uhusiano wako na wazazi au ndugu na dada zako uko namna gani? Ikiwa si mzuri, huenda ukadhani kwamba hali itakuwa afadhali utakapoanza kuishi na rafiki yako. Lakini fikiria anayosema Eve, mwenye umri wa miaka 18: “Rafiki zangu wawili walianza kuishi pamoja. Walikuwa marafiki wakubwa kabla ya kuanza kuishi pamoja, hata hivyo, walishindwa kuishi pamoja. Mmoja alipenda kuwa nadhifu, na yule mwingine alikuwa shaghalabaghala. Mmoja alipenda mambo ya kiroho, yule mwingine alikuwa na moyo nusunusu. Hawakusikilizana hata kidogo!”

Siri ni nini? Erin, mwenye umri wa miaka 18, anasema: “Unaweza kujifunza mengi kuhusu jinsi ya kuishi na wengine ukiwa bado nyumbani. Unaweza kujifunza jinsi ya kutatua matatizo na kutoshikilia sana mapendezi yako. Nimegundua kwamba wale wanaoondoka nyumbani ili kuepuka kubishana na wazazi wao, huwa wanajifunza kukimbia ubishi wala si kutatua matatizo.”

Mambo ya kiroho: Vijana fulani huondoka nyumbani wakiwa na kusudi moja tu, kuepuka mambo ya kidini ya wazazi wao. Wengine hukusudia kuendelea kuwa na mazoea mazuri kuhusu kujifunza Biblia na ibada lakini punde si punde huanza kupeperuka na kupotoka. Unaweza kuepuka jinsi gani ‘kuvunjika kwa imani yako’? *1 Timotheo 1:19.

Yehova Mungu anataka kila mmoja wetu ajihakikishie mwenyewe mambo anayoamini. (Waroma 12:1, 2) Jitahidi kuwa na mazoea mazuri ya kibinafsi kuhusu kujifunza Biblia na ibada, nawe ushikamane nayo. Jaribu kuandika utendaji wako wa kiroho kwenye kalenda na uone ikiwa unaweza kushikamana na ratiba yako kwa mwezi mmoja bila wazazi wako kukusukuma-sukuma?

Mwishowe, unahitaji kujiuliza swali la tatu . . .

Nina Mradi Gani?

Je, unataka kuondoka nyumbani ili kuepuka matatizo? Au ili kutokuwa chini ya mamlaka ya wazazi? Ikiwa hizo ndizo sababu, basi unakazia fikira unakotoka, bali si unakoelekea. Kufanya hivyo ni kama kuendesha gari ukitazama kioo cha nyuma, yaani, unakazia fikira sana vitu vilivyobaki nyuma hivi kwamba huoni kilicho mbele yako. Somo? Usikazie fikira zako zote kuondoka nyumbani—kazia macho yako mbele kwenye mradi unaofaa.

Vijana fulani Mashahidi wa Yehova wamehama kwenda kuhubiri katika maeneo mengine katika nchi za kwao au hata nchi nyingine. Wengine wanahama kwenda kusaidia katika ujenzi wa majengo ya ibada au kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Na wengine wanaona kwamba wanahitaji kuishi peke yao kwa muda kabla ya kufunga ndoa. *

Hata mradi wako uwe nini, fikiria uamuzi wako kwa uzito. Methali moja ya Biblia inasema: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” (Methali 21:5) Fuata mashauri ya wazazi wako. (Methali 23:22) Sali kuhusu jambo hilo. Na unapofanya uamuzi, fikiria kanuni za Biblia zilizo katika sura hii.

Swali kuu si Niko tayari kuondoka nyumbani? bali, Niko tayari kusimamia nyumba yangu? Ikiwa jibu la swali la pili ni ndiyo, basi huenda uko tayari kuondoka nyumbani na kuanza maisha mapya.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 23 Unaweza kupata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 19.

^ fu. 27 Unaweza kupata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 34 na 35.

^ fu. 32 Katika tamaduni fulani, ni kawaida kwa mtoto, hasa binti, kuishi nyumbani mpaka atakapoolewa. Biblia haitoi shauri hususa kuhusu hilo.

ANDIKO MUHIMU

“Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.”—Mathayo 19:5.

PENDEKEZO

Kwa kipindi fulani, wape wazazi wako jumla ya pesa za kugharimia chakula, makao, na gharama zako nyingine. Ikiwa huwezi au hungependa kulipia gharama hizo ukiwa nyumbani, basi hujawa tayari vya kutosha kuhama na kwenda kuishi peke yako.

JE, WAJUA . . . ?

Kinachokusukuma kuondoka nyumbani kinaweza kufanya uwe na furaha au ukose furaha ukishaondoka.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Jambo ninalokusudia kutimiza nikihama kutoka nyumbani ni ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Hata ikiwa maisha ni magumu, kukaa nyumbani kwa muda kunaweza kuwa na faida gani?

● Ukiwa nyumbani, unaweza kufanya nini kitakachosaidia familia yenu na wewe pia kujitayarisha kwa ajili ya wakati ambapo utakuwa na familia yako mwenyewe?

[Blabu katika ukurasa wa 52]

“Ni kawaida kutaka uhuru. Lakini ikiwa sababu yako ya kuondoka nyumbani ni ili tu kutokuwa chini ya sheria, basi kwa kweli hauko tayari kuondoka.”—Aron

[Picha katika ukurasa wa 50, 51]

Kuondoka nyumbani ni kama kufunga safari ya kwenda nyikani—unahitaji kujifunza jinsi ya kufanya mambo kadha wa kadha ya maana kabla ya kuondoka