Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kupinga Vishawishi Jinsi Gani?

Ninaweza Kupinga Vishawishi Jinsi Gani?

SURA YA 9

Ninaweza Kupinga Vishawishi Jinsi Gani?

Karen yuko kwenye karamu na hata kabla ya dakika kumi kwisha anawaona wavulana wawili wakiingia wakiwa na mifuko kadhaa mikubwa. Kila mtu anajua kilicho katika mifuko hiyo. Mapema, alikuwa amewasikia wavulana haohao wakisema kwamba kutakuwa na “pombe ya kutosha” katika karamu hiyo.

Ghafula, Karen anasikia sauti anayoifahamu nyuma yake. “Wewe Mshamba, mbona unazubaa?” Karen anageuka na kumwona rafiki yake Jessica akiwa ameshika chupa mbili za bia ambazo zimefunguliwa. “Usiniambie wewe ni mtoto sana hivi kwamba huwezi kujifurahisha kidogo!” Jessica amwambia Karen huku akiwa ameinua chupa moja na kumwonyesha machoni.

Karen anataka kukataa. Lakini analemewa. Jessica ni rafiki yake, na Karen hataki kuonekana . . . “Mshamba,” kama Jessica anavyomwita. Isitoshe, Jessica ni msichana mzuri. Na ikiwa anakunywa, hakuna ubaya kunywa. ‘Ni bia tu,’ Karen anajiliwaza. ‘Si dawa za kulevya au ngono.’

UNAPOKUWA kijana, unapatwa na vishawishi chungu nzima. Mara nyingi, vinahusisha watu wa jinsia tofauti. “Wasichana shuleni kwetu ni wajasiri,” anasema Ramon, mwenye umri wa miaka 17. “Wanapenda kukugusa-gusa na kuona utawaruhusu kiasi gani. Hata ukiwakataza, ni kazi bure!” Deanna, ambaye pia ana umri wa miaka 17, aliona ukweli wa maneno hayo. “Mvulana mmoja alikuja na kunishika mabegani,” anasema. “Niliupiga mkono wake na kumuuliza, ‘Unafanya nini? Hata sikujui!’”

Wewe pia unaweza kujikuta katikati ya vishawishi, na huenda isionekane kana kwamba vitaisha. Vishawishi vyenye kuendelea ni kama mtu anayeendelea kupiga hodi hata kukiwa na ishara kwenye mlango inayosema “Usisumbue.” Je, ndivyo unavyohisi? Kwa mfano, je, unashawishiwa kufanya lolote kati ya mambo yafuatayo?

□ Kuvuta sigara

□ Kutazama ponografia

□ Kunywa pombe

□ Kufanya ngono

□ Kutumia dawa za kulevya

□ Mambo mengine ․․․․․

Ikiwa umetia alama ya ✔ kando ya yoyote ya mambo yaliyo juu, usione kana kwamba hustahili kuwa Mkristo. Unaweza kujifunza kuzuia tamaa mbaya na kupinga vishawishi. Jinsi gani? Kujua chanzo cha kishawishi kunaweza kukusaidia. Fikiria mambo haya matatu.

1. Kutokamilika. Wanadamu wote wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kutenda dhambi. Hata mtume Paulo aliyekuwa Mkristo mkomavu, alikiri hivi kwa unyoofu: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” (Waroma 7:21) Bila shaka mara kwa mara hata mtu mnyoofu zaidi huwa na “tamaa ya mwili na tamaa ya macho.” (1 Yohana 2:16) Hata hivyo, kufikiria nyakati zote mambo yanayochochea tamaa hizo kunaweza kufanya hali iwe mbaya zaidi, kwa kuwa Biblia inasema: “Tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.”—Yakobo 1:15.

2. Hali zinazotuzunguka. Vishawishi viko kila mahali. “Shuleni na kazini, watu huzungumza kuhusu ngono kila wakati,” anasema Trudy. “Kwenye televisheni na katika sinema, ngono hufanywa ionekane kuwa kitu cha pekee sana, chenye kusisimua sana. Si kawaida kuona matokeo yake mabaya yakionyeshwa!” Trudy anajua kutokana na mambo yaliyompata kwamba uvutano huo huwa wenye nguvu sana. “Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilifikiri kwamba ninampenda kikweli mvulana fulani,” anakumbuka. “Mama yangu aliniketisha na kuniambia kwamba nisipobadili mwenendo wangu, nitaishia kupata mimba. Nilishtuka sana kwamba mama yangu angeweza kufikiria jambo baya kama hilo juu yangu! Miezi miwili baadaye, nilikuwa na mimba.”

3. “Tamaa zinazotukia ujanani.” (2 Timotheo 2:22) Maneno hayo yanaweza kurejelea tamaa yoyote inayotokea mtu anapokuwa kijana, kama vile kutamani kukubaliwa au kutambuliwa. Tamaa zenyewe si mbaya, lakini zisipozuiwa zinaweza kufanya iwe vigumu kupinga vishawishi. Kwa mfano, tamaa ya kutaka kutambuliwa inaweza kukufanya utende kinyume na kanuni nzuri ambazo umefundishwa nyumbani. Ndivyo alivyofanya Steve alipokuwa na umri wa miaka 17. Anasema, “Niliwaasi wazazi wangu na kufanya mambo yote waliyokuwa wamenionya nisifanye, isitoshe, nilifanya hivyo muda mfupi tu baada ya kubatizwa.”

Jinsi ya Kupinga Vishawishi

Ni kweli kwamba uvutano mbalimbali unaozungumziwa hapo juu una nguvu. Hata hivyo, bado unaweza kupinga vishawishi. Jinsi gani?

● Kwanza, tambua kishawishi kilicho na uvutano mkubwa zaidi kwako. (Huenda tayari umefanya hivyo katika ukurasa wa 65.)

● Kisha, jiulize, ‘Ni wakati gani ambapo ni rahisi zaidi kukumbana na kishawishi hiki?’ Tia alama ya ✔ kando ya mojawapo ya mambo yafuatayo:

□ Nikiwa shuleni

□ Nikiwa peke yangu

□ Nikiwa kazini

□ Wakati mwingine ․․․․․

Kujua wakati ambapo kishawishi kinaweza kutokea, huenda kukakusaidia kukiepuka. Kwa mfano, fikiria mfano uliotolewa mwanzoni mwa makala hii. Ni jambo gani lililopaswa kumtahadharisha Karen kwamba huenda kukawa na matatizo katika karamu aliyohudhuria?

․․․․․

Angeweza kuepuka jinsi gani kujikuta katika hali hiyo yenye kushawishi?

․․․․․

● Sasa kwa kuwa umetambua kishawishi na umejua wakati ambapo kinaweza kutokea, uko tayari kuchukua hatua zinazofaa. Jambo la kwanza unalopaswa kufanya ni kufikiria jinsi ya kupunguza au kuepuka kishawishi hicho. Andika hapa chini mambo unayoweza kufanya.

․․․․․

(Mifano: Ikiwa baada ya shule wewe hukutana na wanafunzi wenzako ambao wanakuhimiza mvute sigara, unaweza kubadili njia unayotumia ili kuepuka kukutana nao. Ikiwa mara nyingi unapokea habari au picha za ponografia kwenye Intaneti bila kutaka, unaweza kuamua kutumia programu za kuzuia chanzo hicho na vingine kama hivyo. Pia, unapotafuta habari kwenye Intaneti, unaweza kuchagua maneno kwa uangalifu zaidi.)

Bila shaka, huwezi kuepuka vishawishi vyote. Huenda siku moja ukakabiliana na kishawishi chenye nguvu sana, tena wakati usiotazamia. Unaweza kufanya nini?

Uwe Tayari

Yesu alipokuwa “akijaribiwa na Shetani,” alikataa mara moja. (Marko 1:13) Kwa nini? Kwa sababu tayari alijua msimamo wake kuhusu masuala yaliyotokezwa. Tayari Yesu alikuwa ameazimia kumtii Baba yake nyakati zote. (Yohana 8:28, 29) Hakuwa akicheza aliposema: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.”—Yohana 6:38.

Katika ukurasa unaofuata, andika sababu mbili za kupinga kishawishi ambacho wewe hukabili mara nyingi, na mambo mawili yanayoweza kukusaidia kukipinga.

Sababu za kupinga:

1 ․․․․․

2 ․․․․․

Mambo yatakayokusaidia kupinga:

1 ․․․․․

2 ․․․․․

Kumbuka, unaposhindwa na kishawishi, unakuwa mtumwa wa tamaa zako. (Tito 3:3) Kwa nini uruhusu tamaa zako zikutawale? Jizoeze kuwa na ukomavu wa kutawala tamaa zako badala ya kuziacha zikutawale. (Wakolosai 3:5) Na usisahau kumwomba Yehova akusaidie kushikilia msimamo huo.—Mathayo 6:13. *

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 15

KATIKA SURA INAYOFUATA

Unajisikia mchovu-mchovu? Pata kujua jinsi unavyoweza kuboresha afya yako na kupata nguvu tena!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 43 Ona pia Sura ya 33 na 34 ya kitabu hiki.

ANDIKO MUHIMU

“Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.

PENDEKEZO

Tumia sehemu yenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo,” katika ukurasa wa 132 na 133 wa kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, kupanga jinsi utakavyojibu mtu anapojaribu kukushawishi kufanya makosa.

JE, WAJUA . . . ?

Mungu alitabiri kwamba Yesu angekuwa mwaminifu, lakini hilo halikumaanisha kwamba Yesu angekuwa kama mashini iliyopangiwa kutii. Badala yake, Yesu alikuwa na uhuru wa kuchagua. Alichagua kuwa mwaminifu. Halikuwa jambo alilopangiwa kimbele, lisiloepukika. Ndiyo sababu alipojaribiwa, alisali kwa bidii.—Waebrania 5:7.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ili niwe tayari kupinga vishawishi, nita ․․․․․

Watu, maeneo, na hali ninazohitaji kuepuka zinatia ndani ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Je, viumbe wakamilifu wanaweza kushawishiwa? —Mwanzo 6:1-3; Yohana 8:44.

● Unapopinga vishawishi, uaminifu wako unakuwa na matokeo gani kwa wengine? —Mwanzo 27:11; 1 Timotheo 4:12.

[Blabu katika ukurasa wa 68]

“Kinachonisaidia ni kujua kwamba Mungu mwenye nguvu zote yuko nami na kwamba ninaweza kumwomba msaada wakati wowote!”—Christopher

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 67]

Jaribu Hili!

Chukua dira, kisha uiweke mshale wake ukielekea kaskazini. Sasa, weka sumaku kando ya dira hiyo. Imekuwaje? Mshale hauonyeshi upande sahihi tena. Badala yake, unaelekea upande wa sumaku.

Dhamiri yako ni kama dira hiyo. Ikizoezwa vizuri, itaelekea upande wa “kaskazini” na kukusaidia kufanya maamuzi ya hekima. Lakini marafiki wabaya, kama vile sumaku, wana uvutano unaoweza kupotosha maamuzi yako. Somo? Jaribu kuepuka watu na hali zinazoweza kupotosha uwezo wako wa kufanya maamuzi!—Methali 13:20.

[Picha katika ukurasa wa 69]

Unaposhindwa na kishawishi, unakuwa mtumwa wa tamaa zako