Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nivae Nini?

Nivae Nini?

SURA YA 11

Nivae Nini?

Heather anajitayarisha kuondoka, wazazi wake hawaamini macho yao.

“Umevaa nini?” baba yake auliza.

“Kwani!” Heather ajibu, akiwa ameshangaa. “Nafika tu madukani nikiwa na rafiki zangu.”

“Huendi popote ukiwa umevaa hivyo!” mama yake amwambia.

“Lakini Mama,” Heather alalamika, “watoto wote wanavaa hivi siku hizi. Isitoshe, ndio mtindo wa kisasa!”

“Uwe mtindo, usiwe mtindo, hatuutaki hapa!” Baba yake anamjibu kwa ukali. “Rudi ukabadili nguo hizo mara moja, la sivyo huendi popote!”

MIZOZO kuhusu mavazi si jambo jipya. Huenda wazazi wako walipokuwa vijana walizozana vivyo hivyo na wazazi wao. Na huenda wao pia walihisi kama unavyohisi leo! Lakini sasa wao ndio wazazi, na suala la mavazi yako linatokeza kutoelewana siku baada ya nyingine.

Unasema: Vazi hili linastarehesha.

Wanasema: Ni la kizembe.

Unasema: Linavutia sana.

Wanasema: Linachochea tamaa ya ngono.

Unasema: Bei yake ni nusu.

Wanasema: Si ajabu, nusu ya vazi lenyewe haipo!

Kuna njia yoyote ya kusitisha malumbano hayo? Ndiyo! Megan, mwenye umri wa miaka 23, amegundua siri. “Hakuna haja ya kubishana,” asema. “Mnaweza kuelewana.” Eti kuelewana? Yaani uvae kama mtu mwenye umri wa miaka 40? Tulia! Kuelewana kunamaanisha kwamba wewe na wazazi wako mzungumzie tofauti zenu na kutafuta suluhisho ambalo linawafurahisha wao, na wewe pia. Kuna faida gani kufanya hivyo?

1. Utapendeza, hata machoni pa rafiki zako.

2. Wazazi wako watakupa nafasi ya kupumua kuhusiana na mavazi.

3. Baada ya kuona jinsi unavyojiendesha kwa ukomavu, huenda wazazi wako wakakupa uhuru zaidi.

Haya basi, fikiria vazi fulani ambalo umeona kwenye Intaneti au duka ambalo “lazima” uwe nalo. Jambo la kwanza unalopaswa kufanya ni . . .

Kufikiria Kanuni za Biblia

Biblia haisemi mengi kuhusu mavazi. Hata, unaweza kusoma Maandiko yote yanayozungumzia mavazi kwa dakika chache tu! Hata hivyo, bado Maandiko yana mwongozo unaofaa. Kwa mfano:

● Biblia huwashauri wanawake wajipambe kwa “kiasi na utimamu wa akili.” *1 Timotheo 2:9, 10.

Huenda neno “kiasi” likakutia wasiwasi. ‘Inamaanisha nivae gunia?’ huenda ukajiuliza. Hapana! Katika muktadha huu, kuwa na kiasi kunamaanisha uvae nguo zinazoonyesha kwamba unajiheshimu na unajali hisia za wengine. (2 Wakorintho 6:3) Kuna mavazi mengi yanayoweza kuingizwa katika kikundi hicho. “Huenda ikawa vigumu,” asema Danielle, mwenye umri wa miaka 23, “lakini bado unaweza kuvaa mavazi ya kisasa yasiyopita kiasi.”

● Biblia inasema kwamba badala ya kukazia sura ya nje, unapaswa kukazia “mtu wa siri wa moyoni”—au, kama vile Swahili New Testament SpeedBible inavyosema, “hali ya ndani ya utu wa kweli.”—1 Petro 3:4.

Vazi lisilo na kiasi linaweza kuwavutia watu kwa muda, lakini urembo wa ndani ndio utakaowafanya watu wazima na rafiki zako wakuheshimu kwa muda mrefu. Eti rafiki zako? Ndiyo—hata wao wanaweza kuona upumbavu wa kuvaa mavazi yanayopita kiasi. “Inakera sana kuona jinsi wanawake wanavyojianika mbele za wanaume kwa mavazi wanayovaa!” asema Brittany, mwenye umri wa miaka 16. Kay anakubaliana naye. Akieleza jinsi rafiki yake wa zamani alivyokuwa akivalia, anasema: “Ni kana kwamba kila vazi alilovaa lilikuwa limeandikwa ‘niangalieni.’ Alitaka kuwavutia wanaume, na ili kufanya hivyo alivaa mavazi yanayovuta fikira za watu.”

Waombe Wazazi Wako Mashauri

Kuficha vazi la kiajabu-ajabu katika mfuko wako unapoondoka nyumbani na kulivaa unapofika shuleni si suluhisho. Wazazi wako watakuamini zaidi ikiwa utakuwa mnyoofu na kusema mambo waziwazi, hata kuhusiana na mambo ambayo unafikiri unaweza kufanya na wasijue. Kwa kweli, ingefaa uwaombe mashauri unapochagua mavazi. (Methali 15:22) —Tumia “Ukurasa wa Mazoezi Kuhusu Mavazi” kwenye ukurasa wa 82 na 83.

Lakini kuna haja gani ya kuwaomba mashauri? Kwani kazi ya wazazi ni kukuzuia kuvaa mavazi unayotaka? Hapana, sivyo ilivyo. Ni kweli kwamba huenda wazazi wako wakawa na maoni tofauti na yako, hata hivyo, nyakati nyingine hilo ndilo unalohitaji. Nataleine, mwenye umri wa miaka 17 anasema, “Ninathamini sana mashauri ya wazazi wangu, kwa sababu sitaki kutoka nje na kujiaibisha au kufanya watu waniseme vibaya kwa sababu ya mavazi yangu.”

Isitoshe, kumbuka jambo hili: Maadamu unaishi na wazazi, uko chini ya mamlaka yao. (Wakolosai 3:20) Hata hivyo, ukielewa maoni yao, nao waelewe yako, utashangaa kuona kwamba kumbe mnaweza kukubaliana kuhusu mengi. Kwa sababu hiyo, huenda mkaacha kuzozana kuhusu mavazi!

Dokezo: Unapojipima kwa kuvaa nguo fulani, usifikirie tu kile unachoona kwenye kioo. Vazi linaloonekana kuwa lenye kiasi huenda lisiwe hivyo unapoketi au unapoinama ili kuokota kitu. Ikiwezekana, waombe mashauri wazazi wako au rafiki mkomavu.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Je, adui yako mkubwa ni wewe mwenyewe? Unaweza kufanya nini ikiwa hujipendi?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 23 Ijapokuwa mashauri hayo ya Biblia yameelekezwa kwa wanawake, kanuni hizo zinawahusu wanaume pia.

ANDIKO MUHIMU

“Kujipamba kwenu kusiwe . . . kuvaa mavazi ya nje, bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni.”—1 Petro 3:3, 4.

PENDEKEZO

Epuka mavazi yanayokazia fikira ngono. Yanawafanya watu wafikiri kwamba unawataka sana watu wa jinsia tofauti au unajifikiria mwenyewe tu.

JE, WAJUA . . . ?

Mwanzoni, mara nyingi watu hukuhukumu kulingana na mavazi yako.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Mtu wa familia au rafiki mkomavu ambaye ningependa kumwomba mashauri kuhusiana na vazi fulani ambalo ningependa kununua ni ․․․․․

Nyakati nyingine nitakaponunua vazi, nitafikiria mambo yafuatayo: ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini mara nyingi wazazi na vijana hukosa kuelewana kuhusu mavazi?

● Unaweza kukuza sifa gani kwa kuzungumzia mambo yanayohusu mavazi na wazazi wako?

[Blabu katika ukurasa wa 81]

“Ninapowaona wasichana wakiwa wamevaa mavazi yanayochochea tamaa za ngono, wanapoteza heshima machoni pangu. Kwa upande mwingine, ninapowaona watu wakiwa wamevaa mavazi yenye kiasi lakini yanayovutia, mimi hujiambia, ‘Hivyo ndivyo ninavyotaka watu wanione.’”—Nataleine

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 82, 83]

Ukurasa wa Mazoezi

Ukurasa wa Mazoezi Kuhusu Mavazi

Maagizo: Fanyiza nakala ya kurasa hizi. Waombe wazazi wako wajaze ukurasa wa mazoezi ulio upande wa kulia nawe ujaze upande wa kushoto. Baadaye, badilishaneni kurasa hizo na kujadiliana majibu yenu. Kuna majibu yoyote ya kushangaza? Kila mmoja wenu amejifunza nini ambacho hakujua awali kuhusu mapendezi ya mwingine?

Safu Yako Wazia nguo fulani ambayo ungependa kuivaa au kuinunua.

Kwa nini unaipenda? Ukitumia nambari, panga sababu zilizo hapa chini ukianza na sababu kuu zaidi inayokuchochea.

․․․․․ Jina la kampuni

․․․․․ Kuwavutia watu wa jinsia tofauti

․․․․․ Kukubalika na vijana wenzangu

․․․․․ Ni yenye kustarehesha

․․․․․ Bei ni nzuri

․․․․․ Sababu nyingine ․․․․․

Huenda wazazi wangu wakiiona tu watasema

□ “Haiwezekani!”

□ “Labda.”

□ “Ni sawa.”

Wakiikataa, huenda ni kwa sababu

□ “Inachochea tamaa za ngono.”

□ “Inaonekana ya kizembe sana.”

□ “Ni mtindo wa ajabu.”

□ “Inatuvunjia heshima tukiwa wazazi wako.”

□ “Ni bei ghali sana.”

□ Sababu nyingine ․․․․․

Tunaweza Kupatanisha Mawazo Yetu?

Kuna lolote katika maoni ya wazazi wangu linaloweza kunisaidia?

․․․․․

Kuna lolote linaloweza kufanywa ili nguo hiyo ikubalike?

․․․․․

Safu ya Wazazi Wazia nguo fulani ambayo kijana wenu angependa kuivaa au kuinunua.

Unafikiri ni kwa nini anaipenda? Ukitumia nambari, panga sababu zilizo hapa chini ukianza na sababu kuu zaidi ambayo unafikiri inamchochea.

․․․․․ Jina la kampuni

․․․․․ Kuwavutia watu wa jinsia tofauti

․․․․․ Kukubalika na vijana wenzake

․․․․․ Ni yenye kustarehesha

․․․․․ Bei ni nzuri

․․․․․ Sababu nyingine ․․․․․

Nikiiona tu nitasema

□ “Haiwezekani!”

□ “Labda.”

□ “Ni sawa.”

Sababu yangu ya kuikataa ni kwamba

□ “Inachochea tamaa za ngono.”

□ “Inaonekana ya kizembe sana.”

□ “Ni mtindo wa ajabu.”

□ “Inatuvunjia heshima tukiwa wazazi wako.”

□ “Ni bei ghali sana.”

□ Sababu nyingine ․․․․․

Tunaweza Kupatanisha Mawazo Yetu?

Sababu yetu ya kuikataa nguo hiyo ni mapendezi tu?

□ Ndiyo □ Labda □ Hapana

Kuna lolote linaloweza kufanywa ili nguo hiyo ikubalike?

․․․․․

Uamuzi ․․․․․

[Sanduku katika ukurasa wa 84]

Vipi Kuhusu Wavulana?

Kanuni za Biblia zilizo katika sura hii zinawahusu wavulana pia. Uwe na kiasi. Acha watu waone yule mtu wa siri wa moyoni, sifa zako za ndani. Unapofikiria kuvaa vazi au nguo fulani, jiulize: ‘Mavazi haya yanasema nini kunihusu? Yanawakilisha jinsi nilivyo kikweli?’ Kumbuka, mavazi ni mojawapo ya njia za kujitambulisha. Hakikisha kwamba mavazi yako yanawakilisha kanuni zako maishani!

[Picha katika ukurasa wa 80]

Mavazi yako ni kama ishara inayowaambia watu wewe ni nani. “Ishara” yako inasema nini kukuhusu?