Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini ili Nijiamini Zaidi?

Nifanye Nini ili Nijiamini Zaidi?

SURA YA 12

Nifanye Nini ili Nijiamini Zaidi?

Ndiyo Hapana

Unapojitazama kwenye kioo, unavutiwa na kile unachoona? □ □

Unaona kwamba una ustadi mbalimbali unaojivunia? □ □

Unaweza kusimama imara unaposongwa na vijana wenzako? □ □

Unakubali unapokosolewa kukiwa na msingi? □ □

Unaweza kustahimili wengine wanaposema mambo yanayoudhi juu yako? □ □

Unahisi kuwa unapendwa? □ □

Wewe hutunza afya yako? □ □

Wewe hufurahi wengine wanapopata mafanikio? □ □

Kwa ujumla, unajiona mwenye mafanikio maishani? □ □

Ikiwa umejibu hapana kwa maswali fulani yaliyo juu, huenda unakosa kuona vipawa fulani ulivyo navyo kwa sababu ya kutojiamini. Sura hii imekusudiwa kukusaidia kutambua sifa hizo nzuri!

VIJANA wengi wanahangaishwa sana na sura yao, uwezo wao, na pia vile vijana wenzao wanavyowaona. Je, unahisi hivyo pia? Ikiwa unahisi hivyo, basi hauko peke yako.

“Kutokamilika kwangu hunifanya nishuke moyo. Kwa kawaida, adui yangu mkubwa ni mimi mwenyewe.”—Leticia.

“Hata uwe mrembo au mwenye sura ya kuvutia kadiri gani, bado utakutana na wengine ambao wana sura nzuri kuliko wewe.”—Haley.

“Mimi huwa na wasiwasi sana ninapokuwa na wengine. Mimi huhofu kwamba watanidharau.”—Rachel.

Ikiwa wewe huhisi kama vijana waliotajwa hapo juu, usife moyo. Unaweza kupata msaada. Ona njia tatu zinazoweza kukusaidia ujiamini zaidi na pia uwe na maoni yanayofaa kujihusu.

Jitoe Kuwasaidia Wengine

Andiko la msingi. “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Maana yake. Unapowasaidia wengine, unafaidika pia. Jinsi gani? “Mtu mkarimu atafanikishwa,” yasema methali moja ya Biblia. “Amnyweshaye mwingine maji naye atanyweshwa.” (Methali 11:25, Biblia Habari Njema) Maneno hayo ni kweli kabisa—utakuwa na hali njema unapowasaidia wengine! *

“Mimi hutafuta njia za kuwasaidia wengine kutanikoni. Mimi huhisi vizuri zaidi ninapowaonyesha wengine upendo na kuwafikiria.”—Breanna.

“Huduma ya Kikristo inathawabisha kwa kuwa inakufanya uache kujifikiria na uanze kuwafikiria wengine.”—Javon.

Tahadhari: Usiwasaidie wengine kwa sababu tu wewe pia utafaidika. (Mathayo 6:2-4) Ikiwa nia si nzuri, utaambulia patupu. Kwa kawaida watu huona unafiki!—1 Wathesalonike 2:5, 6.

Nafasi yako. Mfikirie mtu uliyesaidia wakati fulani uliopita. Ni nani, nawe ulimsaidia jinsi gani?

․․․․․

Baadaye ulihisi namna gani?

․․․․․

Mfikirie mtu mwingine unayeweza kumsaidia, na uandike jinsi unavyoweza kumsaidia.

․․․․․

Tafuta Marafiki

Andiko la msingi. “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Maana yake. Rafiki wa kweli anaweza kuwa utegemezo mkubwa wakati wa taabu. (1 Samweli 18:1; 19:2) Hata kule kujua tu kwamba mtu fulani anakujali kunaweza kukutia moyo. (1 Wakorintho 16:17, 18) Kwa hiyo, fanya urafiki na wale walio na uvutano mzuri kwako.

“Marafiki wa kweli hawatakukimbia ukiwa na shida.”—Donnell.

“Nyakati nyingine jambo la maana ni kujua kwamba mtu fulani anakujali kikweli. Kujua hilo kwaweza kukufanya ujihisi ukiwa mwenye thamani.”—Heather.

Tahadhari: Hakikisha kwamba ushirika pamoja na marafiki wako hutokeza sifa zako ulizo nazo—bali si kujibadili uwe mtu bandia ili tu ukubalike machoni pao. (Methali 13:20; 18:24; 1 Wakorintho 15:33) Ukifanya mambo ya kipumbavu ili tu kuwapendeza wengine, mwishowe utajidharau na kuhisi kwamba umetumiwa vibaya.—Waroma 6:21

Nafasi yako. Andika hapa chini jina la rafiki anayeweza kukusaidia kwa njia nzuri ujiamini zaidi.

․․․․․

Unaweza kupanga kutumia wakati pamoja na rafiki huyo uliyemtaja hapo juu.—Taarifa: Si lazima rafiki huyo awe wa rika lako.

Usife Moyo Unapofanya Makosa

Andiko la msingi. “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Waroma 3:23.

Maana yake. Upende, usipende, wewe si mkamilifu. Kwa hiyo, nyakati nyingine utasema au kutenda jambo lisilofaa. (Waroma 7:21-23; Yakobo 3:2) Ijapokuwa huwezi kuepuka kufanya makosa, unaweza kuamua jinsi unavyoyashughulikia. Biblia inasema hivi: “Kwa kuwa japo mtu mwenye haki huanguka mara saba, huinuka tena.”—Methali 24:16, Neno—Biblia Takatifu.

“Nyakati nyingine mtu hujidharau anapolinganisha udhaifu wake na uwezo wa mtu mwingine.”—Kevin.

“Kila mtu ana sifa nzuri na mbaya. Tunapaswa kujivunia sifa zetu nzuri na kujaribu kurekebisha zile mbaya.”—Lauren.

Tahadhari: Usitumie kutokamilika kwako kuwa kizingizio cha kutenda dhambi. (Wagalatia 5:13) Kufanya dhambi kimakusudi, kutakufanya upoteze kibali cha maana zaidi, kibali cha Yehova Mungu!—Waebrania 10:26, 27.

Nafasi yako. Andika hapa chini sifa moja ambayo ungependa kufanyia kazi.

․․․․․

Andika tarehe ya leo kando ya sifa uliyoandika. Fanya utafiti uone jinsi unavyoweza kuboresha sifa hiyo na uchunguze maendeleo utakayokuwa umefanya baada ya mwezi mmoja.

Thamani Yako ya Kweli

Biblia inasema, “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu.” (1 Yohana 3:20) Hilo linamaanisha kwamba Mungu anaweza kuona thamani yako, ambayo wewe mwenyewe huwezi kuona. Lakini je, kutokamilika kwako, kunabadili ukweli huo? Wazia kwamba una noti ya dola 100 iliyoraruka kidogo. Utaitupa au kuona kwamba haina thamani yoyote kwa sababu tu imeraruka? Haiwezekani! Iwe imeraruka au hapana bado ina thamani ya dola 100.

Hivyo ndivyo Mungu anavyokuona. Hapofushwi na kasoro ulizo nazo hivi kwamba asione thamani yako. Yeye hutambua na kuthamini jitihada unazofanya ili kumpendeza, hata ikiwa unaziona kuwa duni! Biblia inakuhakikishia kwamba “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Waebrania 6:10.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Je, nyakati nyingine wewe hulemewa na huzuni nyingi? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, wazia shangwe unayoweza kupata kwa kuwaeleza wengine kuhusu ujumbe wa Ufalme.—Isaya 52:7.

ANDIKO MUHIMU

“Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”—Wagalatia 6:4.

PENDEKEZO

Usiseme mambo kama vile ‘mimi ni mtu ovyo’ na ‘siwezi kufanya lolote sawasawa.’ Maneno kama hayo yanavunja moyo. Badala yake, kubali udhaifu wako lakini pia utambue kwamba una sifa nyingine nzuri.

JE, WAJUA . . . ?

Maoni yako juu yako mwenyewe yanaweza kuathiri jinsi wengine wanavyokuona . . . na hata kukutendea.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Rafiki zangu wakinichambua, nita ․․․․․

Nikitambua kwamba ninachoona sikuzote ni udhaifu wangu tu, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini mara nyingi vijana hukosa kujiamini?

● Kwa nini mtu anapaswa kujiheshimu kwa kiasi fulani?

[Blabu katika ukurasa wa 88]

“Mtu anaweza kuwa mwenye sura nzuri na bado ahisi kwamba hapendezi. Au, mtu anaweza kuwa na sura isiyopendeza lakini ahisi kwamba yeye ni mwenye kuvutia kuliko wote. Yote yanategemea mtazamo wa mtu.”—Alyssa

[Picha katika ukurasa wa 90]

Thamani ya pesa haipungui kwa sababu imeraruka, vivyo hivyo thamani yako haipungui kwa sababu ya kutokamilika kwako