Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nina Huzuni Nyakati Zote—Nifanye Nini?

Nina Huzuni Nyakati Zote—Nifanye Nini?

SURA YA 13

Nina Huzuni Nyakati Zote—Nifanye Nini?

“Rafiki zangu wanapokuwa na shida, mimi huwa tayari kuwasaidia kutatua matatizo na kuwafariji. Hata hivyo, jambo ambalo wengi hawajui ni kwamba, ninaporudi nyumbani, mimi huingia chumbani mwangu na kulia.”—Kellie.

“Ninapokuwa na huzuni, mimi hujitenga na wengine. Nikialikwa mahali, ninatoa kisababu cha kutoenda. Mara nyingi watu wa familia yetu hawajui kwamba nina huzuni. Wao hufikiri niko sawa.”—Rick.

UMEWAHI kuwa na maoni kama ya Kellie au Rick? Ikiwa ndiyo, usikate kauli kwamba una kasoro fulani. Ukweli ni kwamba kila mtu huwa na huzuni mara kwa mara. Hata wanaume na wanawake waaminifu katika Biblia walihuzunika nyakati nyingine.—1 Samweli 1:6-8; Zaburi 35:14.

Katika visa fulani, huenda ukajua ni kwa nini una huzuni, katika visa vingine huenda usijue. “Si lazima uwe katika hali mbaya ili uwe na huzuni.” asema Anna, mwenye umri wa miaka 19. “Huzuni inaweza kutokea wakati wowote, hata wakati ambapo huna matatizo. Ni jambo lisiloeleweka, lakini ndivyo ilivyo!”

Haidhuru kisababishi ni nini, au hata kama hakuna kisababishi, unaweza kufanya nini unapolemewa na huzuni? Jaribu mambo yafuatayo:

1. Zungumza. Akiwa amevurugika, Ayubu alisema: “Nitasema kwa uchungu wa nafsi yangu!”—Ayubu 10:1.

Kellie: “Baada ya kuzungumza na mtu, mimi huwa na utulivu wa ajabu. Ninahisi kwamba angalau kuna mtu anayenielewa. Anaweza kunishushia kamba na kunitoa shimoni—niwe huru hatimaye!”

Dokezo: Andika hapa chini jina la rafiki unayeweza kuzungumza naye unapolemewa na huzuni.

․․․․․

2. Andika. Huzuni inapotanda kama wingu maishani mwako, huenda ikafaa uandike jinsi unavyohisi. Katika zaburi zake zilizoongozwa na roho, nyakati nyingine Daudi alieleza hisia zake za huzuni. (Zaburi 6:6) Kuandika hisia hizo kunaweza kukusaidia ‘kulinda hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.’—Methali 3:21.

Heather: “Kuandika hunisaidia kupanga mawazo yangu yaliyovurugika. Unapoandika kuhusu hisia mbalimbali ulizo nazo, huzuni hupungua.”

Dokezo: Tumia chati kwenye  ukurasa wa 93 kupata msaada wa kushinda hali ngumu. Kufanya hivyo kutakusaidia kupunguza huzuni.

3. Sali. Biblia inasema ukisali kuhusu mahangaiko yako, ‘amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itaulinda moyo wako na nguvu zako za akili.’—Wafilipi 4:6, 7.

Esther: “Nilikuwa nikijaribu kuelewa ni kwa nini nimeshuka moyo sana, lakini sikuelewa. Nikamwomba Yehova anisaidie niwe na furaha. Nilikuwa nimechoka kuhuzunika bila sababu. Mwishowe nikafaulu. Usipuuze kamwe nguvu ya sala!”

Dokezo: Unaposali, fuata mfano wa sala iliyo katika Zaburi 139:23, 24. Mmiminie Yehova moyo wako, na umwombe akusaidie kuelewa chanzo cha huzuni yako.

Pamoja na madokezo yaliyo juu, Neno la Mungu, Biblia, ni msaada mkubwa. Kujaza akili yako mambo yenye kujenga yanayopatikana katika masimulizi ya Biblia kunaweza kufanya uhisi vizuri. (Zaburi 1:1-3) Madokezo ya usomaji wa Biblia wenye kujenga yanaweza kupatikana kwa kuchunguza kurasa zenye kichwa “Mfano wa Kuigwa” katika mabuku ya kitabu hiki. Katika ukurasa wa 227 wa Buku la 2, utaona jinsi mtume Paulo alivyofanikiwa kushughulika na hisia zisizofaa alizokuwa nazo nyakati nyingine kwa sababu ya kutokamilika.

Huzuni Inapodumu

“Asubuhi fulani,” asema Ryan, “ningehisi kwamba ni afadhali kukaa kitandani ili kuepuka kukabili siku nyingine isiyo na maana.” Ryan ana ugonjwa wa kushuka moyo sana, na kuna wengi kama yeye. Kulingana na uchunguzi mbalimbali, kijana 1 kati ya 4 huugua aina fulani ya ugonjwa wa kushuka moyo kabla ya kufikia kuwa mtu mzima.

Unaweza kujua jinsi gani ikiwa unaugua ugonjwa wa kushuka moyo? Dalili fulani zinatia ndani badiliko kubwa la hisia na mwenendo, kujitenga na watu, kutopendezwa na karibu kila kitu, badiliko kubwa katika mazoea ya kula na kulala, na hisia kali za kujidharau au kuhisi hatia isiyo na msingi.

Ni kweli kwamba mara kwa mara karibu kila mtu huwa na dalili moja au zaidi kati ya hizo. Hata hivyo, dalili hizo zikiendelea kwa zaidi ya majuma kadhaa, zungumza na wazazi wako ili wafanye mpango umwone daktari. Daktari anaweza kujua iwapo huzuni yako inatokana na ugonjwa fulani. *

Ikiwa una ugonjwa wa kushuka moyo sana, usiaibike. Baada ya kupata matibabu, wengi wanaougua wamepata nafuu—na huenda hata sasa wana furaha kuliko wakati mwingine wowote! Iwe huzuni yako inasababishwa na kushuka moyo au la, kumbuka maneno yenye kufariji ya Zaburi 34:18: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”

KATIKA SURA INAYOFUATA

Namna gani ikiwa una huzuni nyingi sana hivi kwamba umekuwa ukifikiria kujiua?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Huzuni inapoendelea kwa muda mrefu, vijana fulani huanza kufikiria kujiua. Iwapo umekuwa na mawazo ya aina hiyo, zungumza na mtu mzima unayemwamini haraka iwezekanavyo.—Unaweza kupata habari zaidi katika Sura ya 14 ya kitabu hiki.

ANDIKO MUHIMU

“Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18.

PENDEKEZO

Eleza jinsi unavyohisi unapokuwa na huzuni na kile unachofikiri kinasababisha huzuni hiyo. Baada ya mwezi mmoja, soma ulichoandika. Hisia zako zimebadilika? Ikiwa zimebadilika, andika kilichokusaidia.

JE, WAJUA . . . ?

Ni sawa kulia, hata kama wewe ni mvulana. Pindi moja katika maisha yake, Mfalme Daudi alikiri hivi: “Kila usiku . . . nalilowesha godoro langu kwa machozi yangu.”—Zaburi 6:6, Union Version.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ili nipate faraja, ninaweza kufanya mambo yafuatayo: ․․․․․

Kushirikiana na marafiki wafuatao kutanisaidia kupunguza huzuni: ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kulia kuna faida yoyote?

● Kuwa pamoja na wengine kunaweza kukusaidia jinsi gani kupunguza huzuni?

[Blabu katika ukurasa wa 96]

“Ninapokuwa na huzuni, nahitaji kuepuka kujitenga na watu. Ni kweli kwamba huenda nikahitaji kuwa peke yangu ili kutafakari yanayoendelea na hata labda kulia. Lakini baada ya hapo, najua nahitaji kuwa na watu ili kuondoa akilini kinachofanya niwe na huzuni.”—Christine

[Chati/​Picha katika ukurasa wa 93]

 Ukurasa wa Mazoezi

Ili Kupunguza Huzuni Yako

Kamilisha chati

Tukio

Mwalimu ananifanya nijidharau

Njia isiyofaa

Nitaacha kutia bidii katika masomo

Njia nzuri zaidi

Dokezo: Ona Sura ya 20 ya kitabu hiki

Tukio

Rafiki yangu ananipuuza

Njia isiyofaa

Nitaeneza uvumia usiofaa kumhusu

Njia nzuri zaidi

Dokezo: Ona Sura ya 10 ya Buku la 2

Tukio

Wazazi wangu wanatalikiana

Njia isiyofaa

Nitakuwa na kinyongo kuelekea mzazi mmoja au wote wawili

Njia nzuri zaidi

Dokezo: Ona Sura ya 4 ya kitabu hiki

Tukio

․․․․․

Njia isiyofaa

․․․․․

Njia nzuri zaidi

․․․․․

Tukio

․․․․․

Njia isiyofaa

․․․․․

Njia nzuri zaidi

․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 95]

Ukijitahidi na kutafuta msaada, unaweza kutoka katika lindi la huzuni