Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Afadhali Nijiue?

Afadhali Nijiue?

SURA YA 14

Afadhali Nijiue?

“AFADHALI nife kuliko kuwa hai.” Ni nani aliyesema maneno hayo? Mtu ambaye hakumwamini Mungu? Mtu aliyekuwa amemwacha Mungu? Mtu ambaye Mungu alikuwa amemwacha? Hapana. Mwenye kuyasema ni mtu mwenye kumcha Mungu, lakini aliyekuwa amefadhaika, Yona.—Yona 4:3.

Biblia haisemi Yona alitaka kujiua. Hata hivyo, maneno yake yanaonyesha jambo moja hakika—nyakati fulani hata mtumishi wa Mungu anaweza kulemewa na mawazo yenye kufadhaisha.—Zaburi 34:19.

Vijana fulani hufadhaika kabisa hivi kwamba hawaoni haja ya kuendelea kuishi. Huenda wakahisi kama Laura, mwenye umri wa miaka 16, anayesema: “Kwa miaka mingi, nimekuwa na mshuko wa moyo. Mara nyingi nimefikiria kujiua.” Ikiwa unamfahamu mtu ambaye amekuwa akisema kwamba anataka kujiua—au ikiwa wewe mwenyewe umefikiria kujiua—unaweza kufanya nini? Hebu tuchunguze ni kwa nini huenda mtu akawa na mawazo kama hayo.

Kinachomfanya Mtu Akate Tamaa

Ni nini kinachoweza kumfanya mtu afikirie kujiua? Huenda mambo kadhaa yakahusika. Kwanza, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na vijana wengi wanalemewa na maisha hayo hata zaidi. (2 Timotheo 3:1) Pia, kutokamilika kunaweza kufanya watu fulani wahisi vibaya kujihusu na kuhusu ulimwengu unaowazunguka. (Waroma 7:22-24) Nyakati nyingine hisia hizo hutokana na jinsi wanavyotendewa. Au, huenda ugonjwa ukamfanya mtu ahisi hivyo. Makadirio yenye kushangaza katika nchi moja yanaonyesha kwamba zaidi ya asilimia 90 ya watu waliojiua walikuwa na ugonjwa fulani wa akili. *

Bila shaka, kila mtu hupatwa na matatizo. Biblia inasema kwamba “uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Vijana pia wanatiwa ndani. Kwa kweli, vijana wanaweza kuathiriwa sana na matukio mabaya, kama yafuatayo:

Kifo cha mtu wa ukoo, au rafiki

Mgogoro katika familia

Kuanguka mtihani

Kuvunjika kwa uhusiano wa kimahaba

Kutendewa vibaya (kutia ndani kimwili au kingono)

Ni kweli kwamba, mwishowe karibu kila kijana atapatwa na mojawapo ya hali zilizotajwa. Kwa nini vijana fulani hufanikiwa kukabiliana na hali hizo kuliko wengine? Wataalamu wanasema kwamba vijana wanaokata tamaa huhisi hakuna anayeweza kuwasaidia na matatizo yao hayawezi kutatuliwa. Si kwamba wanataka kufa, ni kwamba wanataka kuondolea mbali maumivu waliyo nayo.

Kuna Tumaini?

Huenda unamfahamu mtu ambaye anataka kuondolea mbali maumivu aliyo nayo—anatamani sana kufanya hivyo hivi kwamba amesema anataka kujiua. Katika hali kama hiyo, unaweza kufanya nini?

Ikiwa rafiki yako ametaabika kiasi cha kutaka kujiua, mhimize atafute msaada. Kisha, zungumza na mtu mzima mkomavu, haidhuru maoni ya rafiki yako. Usihofu kwamba urafiki wenu utaharibika. Kufanya hivyo kwaweza kuokoa uhai wa rafiki yako!

Lakini namna gani ikiwa wewe mwenyewe umekuwa ukifikiria kujiua? Usifiche hisia zako. Zungumza na mtu fulani—mzazi, rafiki, au mtu yeyote anayekujali, atakayekusikiliza, na kuchukulia mambo unayosema kwa uzito. Kwa kuzungumzia matatizo yako waziwazi, hakuna hasara utakayopata, badala yake, utafaidika sana. *

Bila shaka, matatizo yako hayatatoweka kwa kuwa tu umezungumza na mtu fulani. Hata hivyo, huenda msaada mkubwa unaohitaji ni kuzungumza na mtu unayeweza kumtumaini ili akusaidie kuiona hali yako kwa njia inayofaa. Huenda hata kufanya hivyo kukakusaidia kutafuta njia nzuri ya kutatua hali.

Mambo Hubadilika

Unapokabili matatizo, kumbuka: Hata hali ionekane kuwa mbaya kadiri gani, baada ya muda mambo yatabadilika. Pindi moja, mtunga-zaburi Daudi, ambaye alikuwa na matatizo mengi, alimwambia Mungu hivi katika sala: “Umenibadilishia maombolezo yangu yakawa kucheza dansi.”—Zaburi 30:11.

Bila shaka, Daudi hakutazamia kucheza dansi kudumu milele. Alijua kutokana na mambo aliyojionea maishani kwamba matatizo huja na kwenda. Umetambua ukweli huo kuhusiana na matatizo yako? Huenda matatizo mengine yakaonekana kuwa yenye kulemea—angalau kwa sasa. Lakini uwe na subira. Mara nyingi mambo hubadilika na kuwa mazuri. Katika visa fulani, matatizo yanaweza kupunguzwa katika njia ambayo hungewazia kamwe. Katika visa vingine, unaweza kugundua njia ya kukabiliana na matatizo, njia ambayo hukuwa umeifikiria awali. Jambo kuu ni kwamba matatizo yanayohangaisha hayatadumu milele.—2 Wakorintho 4:17.

Faida ya Sala

Njia ya maana zaidi ya kupashana habari ni kusali. Unaweza kusali kama Daudi: “Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza, na uniongoze katika njia ya mpaka wakati usio na kipimo.”—Zaburi 139:23, 24.

Sala si kama gongo tu la kujitegemeza, kama linalotumiwa na walemavu. Ni njia halisi ya kupashana habari na Baba yako wa mbinguni, anayetaka ‘ummiminie moyo wako.’ (Zaburi 62:8) Fikiria kweli za msingi zifuatazo kumhusu Mungu:

Anafahamu hali zinazokutaabisha.—Zaburi 103:14.

Anakujua vema kuliko unavyojijua.—1 Yohana 3:20.

‘Anakujali wewe.’—1 Petro 5:7.

Katika ulimwengu wake mpya, Mungu “atafuta kila chozi” kutoka katika macho yako.—Ufunuo 21:4.

Tatizo Linapotokana na Ugonjwa

Kama ilivyotajwa mapema, mara nyingi hisia za kutaka kujiua zinatokana na ugonjwa fulani. Ikiwa unaugua ugonjwa fulani, usiaibike kutafuta msaada. Yesu alisema kwamba wenye kuugua wanahitaji tabibu. (Mathayo 9:12) Inapendeza kwamba magonjwa mengi yana tiba. Na matibabu yanaweza kukufanya uhisi vema zaidi! *

Biblia inatoa ahadi yenye kufariji kwelikweli kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Mungu anasema kwamba wakati huo, “mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Kwa sasa, fanya kila uwezalo kukabiliana na matatizo ya maisha, ukiwa na hakika kwamba katika wakati uliowekwa wa Mungu, tatizo la kushuka moyo halitakuwako.—Ufunuo 21:1-4.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 9

KATIKA SURA INAYOFUATA

Wazazi wako wanataka kujua kila kitu kuhusu maisha yako—hata mambo mengine ambayo hungependa wajue. Unaweza kufanya nini ili wakupe nafasi unayohitaji?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Hata hivyo, ni muhimu kujua kwamba vijana wengi walio na ugonjwa wa akili hawajiui.

^ fu. 18 Wakristo wanaotaabika wana msaada mwingine—wazee wa kutaniko.—Yakobo 5:14, 15.

^ fu. 31 Unaweza kupata habari zaidi katika Sura ya 13 ya kitabu hiki.

ANDIKO MUHIMU

“Maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”—Wafilipi 4:6, 7.

PENDEKEZO

Unapohisi umeshuka moyo, fanya mazoezi ya kutembea. Kufanya mazoezi kunaweza kukufanya uhisi umetulia na kuwa na hali njema.

JE, WAJUA . . . ?

Katika visa vya kujiua, hasara si kwa wenye kujiua tu, bali pia jamaa na marafiki.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikihisi kuwa sifai na hakuna mtu anayenipenda, nitazungumza na (andika jina la mtu utakayezungumza naye) ․․․․․

Baraka moja katika maisha yangu ambayo ninaweza kukumbuka na kuithamini ni ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Hata matatizo makubwa ni ya muda tu. Kutafakari ukweli huo kunaweza kukusaidia jinsi gani?

● Ni kwa njia gani kujiua ni kumtwika mtu mwingine matatizo yako?

[Blabu katika ukurasa wa 104]

“Nyakati nyingine, nilishuka moyo sana hivi kwamba nilitaka kufa tu, lakini sasa nimerudia hali yangu ya kawaida kwa sababu ya kudumu katika sala na kupata matibabu.”—Heidi

[Picha katika ukurasa wa 100]

Unapohisi Umelemewa

Mara kwa mara hata baadhi ya wanaume na wanawake waaminifu wa nyakati za Biblia walihisi kulemewa na mahangaiko ya maisha. Fikiria mifano ifuatayo.

Rebeka: “Ikiwa hivi ndivyo ilivyo, hasa kwa nini niko hai?”—Mwanzo 25:22.

Musa: “Tafadhali niue kabisa, . . . wala usiache niutazame msiba wangu.”—Hesabu 11:15.

Eliya: “Ee Yehova, iondoe nafsi yangu, kwa maana mimi si bora kuliko mababu zangu.”—1 Wafalme 19:4.

Ayubu: “Laiti ungenificha katika Kaburi, . . . kwamba ungeniwekea kikomo cha wakati na kunikumbuka!”​—Ayubu 14:13.

Katika kila kisa kilicho juu, mwishowe hali zilibadilika na kuwa nzuri, tena kwa njia ambayo mwenye kuhusika hakuwazia kamwe. Uwe na hakika kwamba inaweza kuwa hivyo kwako pia!

[Picha katika ukurasa wa 102]

Hisia za kukata tamaa ni kama mawingu ya dhoruba—baada ya muda yatapita