Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Ubaya wa Kutaka Faragha?

Kuna Ubaya wa Kutaka Faragha?

SURA YA 15

Kuna Ubaya wa Kutaka Faragha?

Tia alama ya ✔ kando ya jibu ambalo huenda ukachagua katika kila moja ya hali zifuatazo:

1. Uko katika chumba chako cha kulala kisha ndugu au dada yako anaingia bila kubisha.

□ ‘Ni sawa tu. Mimi pia hufanya hivyo nyakati nyingine.’

□ ‘Huo ni utovu wa adabu! Namna gani ikiwa ninavaa?’

2. Umerudi tu nyumbani na wazazi wako wanaanza kukurushia maswali. “Ulikuwa wapi? Ulikuwa ukifanya nini? Ulikuwa na nani?”

□ ‘Ni sawa tu. Mimi huwaambia kila kitu.’

□ ‘Inaudhi sana! Wazazi wangu hawaniamini!’

HUENDA ulipokuwa na umri mdogo, suala la faragha halikuwa jambo kubwa sana. Ndugu na dada zako wadogo walipoingia chumbani mwako ghafla, uliwakaribisha bila kulalamika. Wazazi wako walipokuuliza swali lolote, uliwajibu bila kusitasita. Wakati huo, hukuwa na siri zozote. Sasa unatamani kuwa na faragha. “Mimi hufurahi kufanya mambo fulani kivyangu,” asema Corey mwenye umri wa miaka 14. Acha tuone maeneo mawili ambayo unapojaribu kupata faragha huenda ukakumbana na ugumu.

Unapojaribu Kuwa Peke Yako

Kuna sababu kadhaa halali zinazoweza kukufanya utake kuwa peke yako. Huenda unataka tu ‘kupumzika kidogo.’ (Marko 6:31) Au unapotaka kusali, unaweza kufanya kama Yesu alivyowashauri wanafunzi wake, ‘kuingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, usali kwa Baba yako.’ (Mathayo 6:6; Marko 1:35) Tatizo ni kwamba, unapofunga mlango wa chumba chako cha faragha (ikiwa unacho), huenda wazazi wako wasifikiri kwamba unasali! Na huenda ndugu na dada zako wasielewe wakati unapotaka kuwa peke yako.

Unachoweza kufanya. Badala ya kugombana na wengine kwa sababu ya kutaka faragha, fanya mambo yafuatayo:

● Jaribu kuwawekea ndugu na dada zako sheria fulani zinazoweza kufuatwa ili uwe na wakati wa kuwa peke yako. Ikihitajika, waombe wazazi wako wakusaidie katika jambo hilo. *

● Jaribu kuelewa maoni ya wazazi wako. “Wakati mwingine wazazi wangu hutaka kujua ninafanya nini,” asema Rebekah mwenye umri wa miaka 16. “Lakini kusema kweli ikiwa ningekuwa mzazi, hata mimi ningetaka kujua kijana wangu anafanya nini hasa kwa kuwa vijana wanakabili majaribu ya kila aina!” Kama Rebekah, je, unaweza kuelewa hangaiko la wazazi wako?—Methali 19:11.

● Jiulize hivi kwa unyoofu: ‘Kupitia mwenendo wangu, nimewapa wazazi wangu sababu ya kunishuku hivi kwamba ninapofunga mlango wa chumba changu wanafikiri ninafanya jambo lisilofaa? Nimekuwa nikificha mambo mengi kuhusu maisha yangu mpaka wanahisi kuwa wanahitaji kuwa kama polisi ili wanifahamu?’ Ikiwa sivyo na bado wazazi wako hawakuamini, basi waeleze kwa upole na heshima jinsi unavyohisi. Sikiliza kwa makini mahangaiko yao, na uhakikishe kwamba hufanyi jambo lolote linalochangia tatizo hilo.—Yakobo 1:19.

Unapotafuta Marafiki

Unapobalehe, ni jambo la kawaida kutafuta marafiki nje ya familia yenu. Pia, ni kawaida kwa wazazi wako kutaka kujua rafiki zako ni nani na kile mnachofanya mnapokuwa pamoja. Hata hivyo, wakati mwingine huenda ukahisi kwamba wazazi wako wana wasiwasi usio na msingi. “Kile ninachotaka ni kutumia simu yangu na kutuma barua pepe bila wazazi wangu kunichunguza-chunguza kila baada ya dakika kumi na kuniuliza ninazungumza na nani,” asema Amy, mwenye umri wa miaka 16.

Unachoweza kufanya. Badala ya marafiki wako kuharibu uhusiano wako na wazazi wako, jaribu kufanya mambo yafuatayo.

● Watambulishe marafiki wako kwa wazazi wako. Bila shaka, hungependa wazazi wako wawe kama polisi, lakini ikiwa hutaki wawajue rafiki zako, huenda wakalazimika kufanya hivyo. Kumbuka kuwa wazazi wako wanavyozidi kuwajua watu unaoshirikiana nao ndivyo watakavyozidi kukuruhusu ujichagulie rafiki zako.

● Jichunguze kwa unyoofu: Je, jambo ambalo hasa unatafuta ni kupata faragha au kuficha mambo? Brittany, mwenye umri wa miaka 22, asema hivi: “Ikiwa unaishi nyumbani na wazazi wako wanataka kujua unachofanya, fikira zako zinapaswa kuwa, ‘Kile ninachofanya si kosa, kwa hiyo mbona nijifiche?’ Kwa upande mwingine, ikiwa unahitaji kuficha unachofanya, basi kuna tatizo.”

Jinsi ya Kupata Faragha

Sasa una nafasi ya kuchemsha bongo na utatuzi wa mambo fulani yanayokuhangaisha kuhusu faragha. Kwenye nafasi iliyo hapa chini andika majibu yako kwa maswali yanayoambatana na hatua zifuatazo:

Hatua ya 1: Tambua tatizo. Ni kuhusu mambo gani unahisi ungependa kuwa na faragha?

․․․․․

Hatua ya 2: Fikiria maoni ya wazazi wako. Unafikiri ni nini hasa kinachowahangaisha?

․․․․․

Hatua ya 3: Tafuta suluhisho. Ni katika njia gani huenda unachangia tatizo hilo bila kukusudia? Ni marekebisho gani unayoweza kufanya kupatana na jibu lako hapo juu? Ungependa wazazi wako washughulikie matatizo yako jinsi gani?

․․․․․

Hatua ya 4: Zungumzeni. Eleza jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu faragha.

․․․․․

KATIKA SURA INAYOFUATA

Je, mmoja wa wazazi wako amelala katika kifo? Ikiwa ndivyo, unaweza kupata faraja wapi?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Unaweza kupata habari zaidi katika Sura ya 6 ya kitabu hiki.

ANDIKO MUHIMU

“Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu.”—2 Timotheo 2:15.

PENDEKEZO

Unapozungumza na wazazi wako kuhusu faragha, usinung’unike. Waeleze kinachokuhangaisha hasa. Kuna tofauti gani kati ya manung’uniko na mahangaiko? Kunung’unika ni kukazia mambo ambayo unafikiri wazazi wako wanakosea. Kuzungumzia mahangaiko kutawasaidia ninyi nyote mtafute utatuzi.

JE, WAJUA . . . ?

Kadiri unavyozidi kujifunua kwa wazazi wako, ndivyo wanavyozidi kukuamini.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ili wazazi wangu waniamini (au waanze kuniamini tena), nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini wazazi wako wana haki ya kutaka kujua mambo yanayoendelea maishani mwako?

● Kujitahidi kusitawisha ustadi wa kupashana habari na wazazi wako kutakusaidia jinsi gani kupashana habari na watu wengine utakapokuwa mtu mzima?

[Blabu katika ukurasa wa 108]

“Wazazi hawataki upatwe na jambo lolote baya, na nyakati nyingine huenda ikaonekana ni kama wanaingilia mambo yako ya kibinafsi. Huenda hilo lisionekane kuwa sawa. Lakini, kusema kweli, kama ningekuwa mzazi, ningefanya vivyo hivyo.”—Alana

[Picha katika ukurasa wa 109]

Sifa ya kuaminika ni kama mshahara, lazima uufanyie kazi ili uupate