Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Kawaida Kuhuzunika Ninavyohuzunika?

Ni Kawaida Kuhuzunika Ninavyohuzunika?

SURA YA 16

Ni Kawaida Kuhuzunika Ninavyohuzunika?

Ingawa sura hii inazungumzia kifo cha mzazi, kanuni zilizopo zinatumika wakati unapompoteza mtu yeyote wa familia au rafiki.

“Mama alipokufa, nilichanganyikiwa sana. Yeye ndiye aliyeunganisha familia yetu.”—Karyn.

KUFIWA na mzazi ni mojawapo ya mambo yenye kuumiza sana yanayoweza kukupata. Baadaye, huenda ukawa na hisia mbalimbali ambazo hujawahi kuwa nazo wakati mwingine. Brian, aliyekuwa na umri wa miaka 13 baba yake alipokufa kutokana na mshutuko wa moyo, asema: “Usiku tuliopata habari, tulilia na kukumbatiana tu.” Natalie, aliyekuwa na umri wa miaka kumi baba yake alipokufa kutokana na kansa, akumbuka: “Sikujua la kufanya. Sikuwa na hisia zozote. Ni kana kwamba nilikuwa nimekufa ganzi.”

Kifo humwathiri kila mtu kwa njia tofauti. Biblia husema kwamba “kila mmoja” ana “pigo lake na maumivu yake mwenyewe.” (2 Mambo ya Nyakati 6:29) Ukiwa na hilo akilini, hebu fikiria jinsi ambavyo kifo cha mzazi wako kimekuathiri wewe. Andika hapa chini (1) jinsi ulivyohisi ulipopata habari kwamba mzazi wako amekufa na (2) jinsi unavyohisi sasa. *

1 ․․․․․

1 ․․․․․

Huenda majibu yako yanaonyesha kwamba hisia zako zinapungua kwa kadiri fulani. Hilo ni kawaida. Haimaanishi kwamba umemsahau mzazi wako. Ama, huenda bado hisia zako hazijabadilika au labda hata zimezidi. Huenda huzuni yako huja kama mawimbi, yanayopanda na kushuka. Hilo pia ni kawaida—hata ikiwa miaka kadhaa imepita tangu mzazi afe. Swali ni, Unaweza kukabiliana na huzuni jinsi gani?

Usijizuie kulia! Kulia husaidia kupunguza uchungu unaoletwa na huzuni. Hata hivyo, huenda ukahisi kama Alicia. Alikuwa na umri wa miaka 19 mama yake alipokufa. Alicia anasema, “Nilihisi kwamba nikionyesha hisia nyingi, wengine watafikiri sina imani.” Lakini fikiria hili: Yesu Kristo alikuwa mwanadamu mkamilifu aliyekuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. Hata hivyo, ‘alitokwa na machozi’ alipowaona wale waliokuwa wakihuzunika juu ya kifo cha rafiki yake mpendwa Lazaro. (Yohana 11:35) Kwa hiyo, usiogope kulia. Haimaanishi kwamba huna imani! Alicia anasema: “Mwishowe, nililia. Tena sana. Kila siku.” *

Kabiliana na hisia za hatia. “Kila usiku nilikuwa nikimbusu mama yangu kabla ya kwenda kulala,” anasema Karyn, aliyekuwa na umri wa miaka 13 mama yake alipokufa. “Kuna siku ambayo sikufanya hivyo. Asubuhi iliyofuata, Mama alikuwa amekufa. Najua sipaswi kuwa na hisia za hatia, lakini nahisi nina hatia kwa kuwa sikumwona usiku huo wa mwisho na pia kwa sababu ya mambo yaliyotokea asubuhi iliyofuata. Baba yangu alikuwa ameenda safari ya kikazi na aliniomba mimi na dada yangu tumtunze Mama. Lakini tuliamka tukiwa tumechelewa. Nilipoingia chumbani mwake, Mama hakuwa akipumua. Nilihisi vibaya sana, kwa sababu alikuwa sawa Baba alipoondoka!”

Kama Karyn, huenda kwa kiasi fulani unahisi kwamba una hatia kwa sababu ya mambo ambayo ulipuuza kufanya. Huenda hata ukajitesa kwa kusema, “laiti.” ‘Laiti ningemhimiza Baba atafute ushauri wa daktari.’ ‘Laiti ningeenda kumwona Mama mapema.’ Ikiwa unasumbuliwa na mawazo kama hayo, kumbuka hili: Ni jambo la kawaida kujuta kwamba laiti ungefanya mambo kwa njia tofauti. Ukweli wa mambo ni kwamba ungefanya mambo kwa njia tofauti ikiwa ungejua mambo ambayo yangetokea. Lakini hukujua. Hivyo basi, hupaswi kujilemea na hisia za hatia. Hukusababisha kifo cha mzazi wako! *

Eleza hisia zako. Methali 12:25 inasema: ‘Neno jema huchangamsha.’ (Biblia Habari Njema) Kufungia hisia zako kunaweza kufanya iwe vigumu kwako kukabiliana na huzuni. Kwa upande mwingine, kuzungumza kuhusu hisia zako na mtu unayemwamini kutakuwezesha kupata ‘maneno mema’ yenye kutia moyo wakati una huzuni.

Zungumza na Mungu. Yaelekea utahisi vizuri zaidi baada ya ‘kummiminia’ Yehova Mungu ‘moyo wako’ katika sala. (Zaburi 62:8) Hiyo si njia ya kukutuliza tu. Unaposali, unamsihi “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Njia moja ambayo Mungu huandaa faraja ni kupitia Neno lake, Biblia. (Waroma 15:4) Kwa nini usiwe na orodha ya maandiko yanayoweza kukufariji? *

Huzuni huchukua muda. Lakini Biblia inaweza kutufariji, kwa kuwa inatuhakikishia kwamba katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi, “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:3, 4) Huenda wewe pia ukagundua kwamba kutafakari kuhusu ahadi kama hizo kutakusaidia kukabiliana na kifo cha mzazi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ikiwa ni vigumu kwako kujibu maswali hayo sasa, unaweza kujaribu kufanya hivyo baadaye.

^ fu. 10 Usifikiri kwamba lazima ulie ili kuonyesha huzuni. Watu huonyesha huzuni kwa njia tofauti. Jambo la maana ni hili: Ukihisi machozi yanakulenga-lenga, tambua kwamba huo ni “wakati wa kulia.”—Mhubiri 3:4.

^ fu. 12 Mawazo kama hayo yakiendelea kukusumbua, zungumza na mzazi wako mwingine au mtu mwingine mzima. Baada ya muda, utapata usawaziko.

^ fu. 14 Watu fulani wamefarijiwa na maandiko yafuatayo: Zaburi 34:18; 102:17; 147:3; Isaya 25:8; Yohana 5:28, 29.

ANDIKO MUHIMU

“[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

PENDEKEZO

Uwe na daftari utakayotumia kuandika hisia zako. Kuandika mawazo yako kuhusu mzazi aliyekufa kunaweza kukusaidia sana kukabiliana na huzuni.

JE, WAJUA . . . ?

Kulia si udhaifu. Hata wanaume wenye nguvu na ujasiri kama Abrahamu, Yosefu, na Daudi, walilia walipokuwa na huzuni.—Mwanzo 23:2; 50:1; 2 Samweli 1:11, 12; 18:33.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikihisi ninalemewa na hisia, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kumuuliza mzazi niliyebaki naye kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini ni vizuri kufikiria mambo mazuri unayokumbuka kuhusu mzazi wako aliyekufa?

● Kwa nini kuandika mawazo yako kutakusaidia kukabiliana na huzuni?

[Blabu katika ukurasa wa 112]

“Nilifungia hisia zangu. Hali yangu ya kimwili na kihisia ingekuwa afadhali kama ningezungumzia hisia zangu. Ingesaidia sana kukabiliana na huzuni yangu.”—David

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 113]

CHANTELLE

“Baba yangu alikuwa mgonjwa kwa miaka mitano hivi, na afya yake ilikuwa ikizidi kuzorota. Nilikuwa na umri wa miaka 16 alipojiua. Baadaye mama yangu alinieleza mimi na kakangu mambo yote yaliyokuwa yakiendelea. Hata alituruhusu tusaidie kufanya maamuzi kuhusu mipango ya mazishi. Hilo liliturahisishia mambo. Nafikiri kwamba watoto hawapendi kufichwa mambo yanayoendelea, hasa mambo makubwa kama haya. Kadiri muda ulivyopita ndivyo ilivyokuwa rahisi zaidi kwangu kuzungumza waziwazi kuhusu kifo cha baba yangu. Wakati wowote nilipohisi nataka kulia, ningeenda mahali fulani au kwa rafiki na kulia. Pendekezo langu ni hili: Ikiwa unahitaji kuzungumza kuhusu jambo hilo, zungumza na watu wa familia au marafiki. Unapokuwa na huzuni, usiizuilie.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 113, 114]

LEAH

“Mama alipatwa na kiharusi nilipokuwa na umri wa miaka 19, na miaka mitatu baadaye akafa. Baada ya kifo chake, nilihisi kwamba nahitaji kuwa na nguvu. Baba angelemewa hata zaidi ikiwa mimi pia ningelemewa na hisia. Nilipokuwa nikikua, Mama alikuwa nami sikuzote nilipokuwa mgonjwa au nilipokuwa sijisikii vizuri. Nakumbuka jinsi alivyokuwa akinigusa ili kuona ikiwa nina homa. Ninaumia sana ninapokumbuka kwamba hayupo. Mimi hujaribu kuficha hisia zangu, ijapokuwa najua haifai. Hivyo, nyakati nyingine mimi hutazama picha ili niweze kulia. Kuzungumza na marafiki husaidia pia. Biblia inaahidi kwamba wale ambao wamekufa watafufuliwa na waishi katika dunia itakayokuwa paradiso. (Yohana 5:28, 29) Ninapokazia fikira tumaini la kumwona mama yangu tena—na ninapokazia fikira kile ninachohitaji kufanya ili niwepo—huzuni yangu hupungua.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 114]

BETHANY

“Laiti ningeweza kukumbuka nikimwambia baba yangu ‘ninakupenda.’ Nina hakika nilimwambia, lakini sikumbuki, na ningependa kujua hivyo. Nilikuwa na umri wa miaka mitano tu baba yangu alipokufa. Baba yangu alipatwa na kiharusi akiwa usingizini, akakimbizwa hospitalini. Asubuhi, nikaambiwa kwamba amekufa. Baadaye ilikuwa vigumu sana kwangu kuzungumza kuhusu baba yangu, lakini nilifurahi niliposikia watu wakizungumza kumhusu kwa sababu hilo lilinisaidia kumjua vizuri. Ningemshauri yeyote ambaye amefiwa na mzazi wake akumbuke kwa furaha kila pindi waliyokuwa pamoja na mzazi wake na kuandika mambo waliyofanya pamoja ili asiyasahau. Kisha, afanye awezayo kujenga imani yake ili awepo wakati mzazi wake atakapofufuliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu.”

[Sanduku katika ukurasa wa 116]

Ukurasa wa Mazoezi

Kuwa na Daftari

Andika pindi kadhaa nzuri ulizofurahia na mzazi wako. ․․․․․

Andika mambo ambayo unatamani ungemwambia mzazi wako alipokuwa angali hai. ․․․․․

Wazia kwamba una ndugu au dada mdogo ambaye analemewa na hisia za hatia kuhusu kifo cha mzazi wako. Andika mambo ambayo unaweza kusema ili kumfariji. (Hilo linaweza kukusaidia wewe pia uwe na usawaziko kuhusu hisia zako za hatia.) ․․․․․

Andika mambo mawili au matatu ambayo unatamani ungalijua kuhusu mzazi wako aliyekufa, kisha umwombe mzazi wako ambaye yupo mzungumzie angalau moja ya mambo hayo. ․․․․․

Soma Matendo 24:15. Tumaini linalozungumziwa katika andiko hilo linaweza kukusaidia jinsi gani kukabiliana na kifo cha mzazi wako? ․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 115]

Huzuni inaweza kuwa kama mawimbi ambayo hupiga ufuo bila kutazamiwa