Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ninaogopa Kuhubiri Shuleni?

Kwa Nini Ninaogopa Kuhubiri Shuleni?

SURA YA 17

Kwa Nini Ninaogopa Kuhubiri Shuleni?

“Kumekuwa na pindi fulani ambazo ningeweza kuhubiri shuleni. Lakini sikuzitumia.”—Kaleb.

“Mwalimu wetu aliwauliza wanafunzi maoni yao kuhusu mageuzi. Nilijua kwamba huo ni wakati mzuri wa kuhubiri. Badala yake nilishikwa na woga sana na nikakaa kimya. Baadaye, nilihisi vibaya sana.”—Jasmine.

IKIWA wewe ni kijana Mkristo, labda umewahi kujikuta katika hali kama ya Kaleb na Jasmine. Kama wao, huenda unapenda kweli za Biblia ambazo umejifunza. Huenda hata ungependa kuwaambia wengine kuzihusu. Hata hivyo, huenda ukaogopa kuzungumza. Lakini, unaweza kusitawisha ujasiri. Jinsi gani? Chukua hatua zifuatazo:

1. Tambua unachoogopa. Unapofikiria kuwahubiria wengine, ni rahisi kuwazia tu mambo mabaya yanayoweza kutokea! Hata hivyo, nyakati nyingine unaweza kupunguza woga kwa kutaja au kuandika jinsi unavyohisi.

Kamilisha sentensi ifuatayo:

● Naogopa kwamba huenda jambo hili litatokea nikihubiri shuleni: ․․․․․

Huenda ukafarijika kujua kwamba vijana wengine Wakristo wanahisi kama wewe. Kwa mfano, Christopher, mwenye umri wa miaka 14 anasema, “Ninaogopa watoto watanicheka na kumwambia kila mtu kwamba mimi ni mtu wa ajabu.” Naye Kaleb, aliyetajwa mwanzoni, anasema, “Nilikuwa na wasiwasi kwamba mtu angeniuliza swali ambalo singeweza kujibu.”

2. Kabiliana na kipingamizi. Kuna sababu yoyote ya kuogopa? Huenda ipo, kama Ashley mwenye umri wa miaka 20 anavyokumbuka. “Vijana fulani walijifanya wanapendezwa na imani yangu,” asema Ashley. “Lakini baadaye waliyapotosha maneno yangu na kuyatumia mbele ya wengine ili nichekwe.” Nicole, mwenye umri wa miaka 17, anasema hivi kuhusu hali iliyompata: “Mvulana mmoja alilinganisha mstari fulani katika Biblia yake na mstari huohuo katika Biblia yangu, na maneno yaliyotumiwa yalikuwa tofauti. Akasema kwamba Biblia yangu imebadilishwa. Nilishtuka! Sikujua la kusema.” *

Huenda hali kama hizo zikaonekana kuwa zenye kuogopesha sana! Lakini badala ya kuhepa, kubali hali hizo kuwa mambo ya kawaida katika maisha ya Mkristo. (2 Timotheo 3:12) “Yesu alisema wafuasi wake watateswa,” anasema Matthew mwenye umri wa miaka 13, “kwa hiyo, hatutarajii kila mtu atupende kwa sababu ya imani yetu.”—Yohana 15:20.

3. Fikiria faida. Je, hali inayoonekana kuwa mbaya inaweza kuwa na matokeo yoyote mazuri? Amber, mwenye umri wa miaka 21, anafikiri inawezekana. “Si rahisi kuwahubiria watu wasioheshimu Biblia,” anasema, “lakini kufanya hivyo kunakusaidia kuielewa vizuri imani yako.”—Waroma 12:2.

Tazama tena mambo uliyoandika katika Hatua ya 1. Fikiria angalau faida mbili unazoweza kupata kutokana na hali hiyo, na uziandike hapa chini.

1 ․․․․․

2 ․․․․․

Dokezo: Ni kwa njia gani kuwahubiria wengine kunaweza kukupunguzia mkazo unaopata kutoka kwa marafiki? Kuhubiri kutakusaidiaje ujiamini zaidi? Kutaboresha jinsi gani hisia zako kumwelekea Yehova Mungu? Yehova atahisi namna gani kukuhusu?—Methali 23:15.

4. Jitayarishe. “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu,” lasema andiko la Methali 15:28. Mbali na kutafakari mambo utakayosema, jaribu kufikiria maswali ambayo huenda wengine wakauliza. Fanya utafiti kuhusu habari hizo, na utayarishe jibu unaloweza kutoa kwa urahisi.—Ona chati “ Panga Jinsi Utakavyojibu,” kwenye ukurasa wa 127.

5. Jinsi ya kuanza. Ukishajitayarisha kuwahubiria wengine, utaanza namna gani? Una njia mbalimbali. Kwa njia fulani, kuwahubiria wengine ni kama kuogelea: Watu fulani huingia ndani ya maji polepole; wengine hujitosa moja kwa moja. Vivyo hivyo, unaweza kuanza kwa kuzungumzia mambo yasiyohusu dini kisha hatua kwa hatua uone jinsi mtu huyo anavyoitikia. Lakini ikiwa una wasiwasi kwa sababu hujui linaloweza kutokea, huenda ikawa afadhali ‘kujitosa moja kwa moja.’ (Luka 12:11, 12) “Kufikiria tu kuhusu kuhubiria watu kulinitia wasiwasi zaidi kuliko kuhubiri kwenyewe” asema Andrew mwenye umri wa miaka 17. “Mazungumzo yalipoanza, mambo yalikuwa rahisi kuliko nilivyofikiri!” *

6. Uwe mwenye busara. “Mtu aliye mwerevu atatenda kwa ujuzi,” akaandika Sulemani. (Methali 13:16) Kama vile huwezi kujitosa ndani ya maji yasiyo na kina, uwe mwangalifu usijiingize katika mabishano yasiyo na maana. Kumbuka, kuna wakati wa kusema na wakati wa kukaa kimya. (Mhubiri 3:1, 7) Nyakati nyingine, hata Yesu alikataa kujibu maswali.—Mathayo 26:62, 63.

Ukiamua kujibu, huenda ikafaa kutoa jibu fupi na kwa busara. Kwa mfano, mwanafunzi mwenzako akikuuliza kwa dhihaka, ‘Kwa nini huvuti sigara?’ unaweza kusema, ‘Kwa sababu sipendi kuuchafua mwili wangu!’ Ikitegemea itikio lake, utaamua ikiwa utamweleza zaidi kuhusu imani yako au hapana.

Hatua sita zilizotajwa katika sura hii zinaweza kukusaidia ‘kuwa tayari kuitetea’ imani yako. (1 Petro 3:15) Bila shaka, kuwa tayari hakumaanishi kwamba hutaogopa. Hata hivyo, Alana, mwenye umri wa miaka 18, anasema: “Unapowahubiria wengine hata ingawa unaogopa, unahisi umetimiza jambo fulani—umeushinda woga wako ingawa ulijua kwamba huenda hutapata matokeo mazuri. Na ukipata matokeo mazuri, unahisi vizuri hata zaidi! Utafurahi kwamba ulikuwa na ujasiri wa kuhubiri.”

KATIKA SURA INAYOFUATA

Una mikazo mingi shuleni? Pata kujua jinsi unavyoweza kukabiliana na hali hiyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Tafsiri za Biblia hutumia maneno tofauti. Hata hivyo, tafsiri fulani hushikamana kwa uaminifu na lugha za awali ambazo zilitumiwa kuiandika Biblia.

^ fu. 18 Ona sanduku “ Jinsi ya Kuanzisha Mazungumzo,” kwenye ukurasa uliotangulia.

ANDIKO MUHIMU

“Sikuzote [uwe] tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hutaka kutoka kwenu sababu ya tumaini lililo ndani yenu, lakini [ukifanya] hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.”—1 Petro 3:15.

PENDEKEZO

Badala ya kuwaambia wanafunzi wenzako mambo wanayopaswa au wasiyopaswa kuamini, waambie kwa usadikisho mambo unayoamini na kwa nini mambo unayoamini yanapatana na akili.

JE, WAJUA . . . ?

Huenda baadhi ya wanafunzi wenzako wakakuheshimu kwa sababu ya kushikamana na kanuni za Biblia za maadili, lakini labda wanaona haya kukuuliza kuhusu imani yako.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Mwanafunzi ninayeweza kuzungumza naye kuhusu imani yangu ni [andika angalau jina la mtu mmoja] ․․․․․

Habari ambayo nafikiri inaweza kumpendeza sana ni ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Unafikiri ni kwa nini wanafunzi wenzako wanadhihaki imani yako?

● Ukiamua kuzungumzia imani yako, kwa nini ni muhimu kuzungumza kwa usadikisho?

[Blabu katika ukurasa wa 126]

“Nilipokuwa mdogo, nilitaka sana kuwa kama watoto wengine. Lakini nilianza kutambua jinsi imani yangu ilivyochangia maisha mazuri. Kujua hivyo kuliimarisha uhakika wangu—kulifanya nijivunie mambo ninayoamini.”—Jason

[Sanduku katika ukurasa wa 124]

 Jinsi ya Kuanzisha Mazungumzo

“Unapanga kufanya nini wakati wa likizo?” [Baada ya kupata jibu, taja mipango yako ya kiroho, kama vile kuhudhuria kusanyiko au kutumia wakati mwingi zaidi katika kazi ya kuhubiri.]

● Taja habari fulani ya karibuni, kisha uulize: “Ulisikia habari hiyo? Una maoni gani kuihusu?”

“Unafikiri hali ya kiuchumi ya ulimwengu [au tatizo lingine] itakuwa bora? [Mruhusu ajibu.] Kwa nini unaamini hivyo?”

“Unashirikiana na dini yoyote?”

“Unafikiri maisha yako yatakuwa namna gani miaka mitano ijayo?” [Baada ya kupata jibu, mwambie kuhusu miradi yako ya kiroho.]

[Chati katika ukurasa wa 127]

 (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Ukurasa wa Mazoezi

Panga Jinsi Utakavyojibu

Toa kopi!

Pendekezo: Zungumzia chati hii pamoja na wazazi wako na vijana wenzako Wakristo. Kamilisha chati. Kisha uone kama unaweza kufikiria maswali mengine ambayo huenda wanafunzi wenzako wakauliza, na upange majibu ambayo unaona yatakufaa.

Kutounga Mkono Upande Wowote

Swali

Kwa nini Hamsalimu bendera? Kwani hupendi nchi yenu?

Jibu

Ninaheshimu Nchi ninayoishi, lakini siiabudu.

Swali Lingine

Kwa hiyo huwezi kupigania nchi yako?

Jibu

Hapana, na mamilioni ya Mashahidi katika nchi nyinginezo hawawezi kupigana na nchi hii.

Damu

Swali

Kwa nini hamkubali kutiwa damu mishipani?

Jibu

Ninakubali matibabu mengine yasiyohatarisha maisha yangu kwa magonjwa kama vile UKIMWI au ugonjwa wa ini Hata hivyo, Biblia inatuambia tujiepushe na damu, kwa hiyo kwa hiyo sikubali kutiwa damu mishipani.

Swali Lingine

Lakini namna gani kama utakufa usipotiwa damu? Mungu atakusamehe, sivyo?

Jibu

․․․․․

Maamuzi

Swali

Fulani wa fulani ni wa dini yenu, na yeye alifanya hivi na vile. Mbona wewe unakataa?

Jibu

Kabla ya kuwa mmoja wa mashahidi wa Yehova mtu hufundishwa matakwa ya Mungu. Kila mmoja wetu anapaswa kujifanyia uamuzi.

Swali Lingine

Kwani hamna msimamo?

Jibu

․․․․․

Uumbaji

Swali

Kwa nini huamini Mageuzi?

Jibu

Niamini kwa Nini? Hata wanasayansi hawakubaliani kuhusu mageuzi, na eti wao ni wataalamu!

Swali Lingine

․․․․․

Jibu

․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 125]

Kuhubiri ni kama kuogelea. Unaweza kuamua kuanza polepole—au kujitosa moja kwa moja!