Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kukabiliana Jinsi Gani na Mikazo Shuleni?

Ninaweza Kukabiliana Jinsi Gani na Mikazo Shuleni?

SURA YA 18

Ninaweza Kukabiliana Jinsi Gani na Mikazo Shuleni?

“Nilikuwa na mikazo mingi sana shuleni hivi kwamba mara nyingi nilitamani kulia na kupiga mayowe wakati uleule.”—Sharon.

“Mikazo unayopata shuleni haipungui kadiri unavyoendelea kukua—badala yake inabadilika.”—James.

UNAONA kuwa wazazi wako hawaelewi hata kidogo mikazo unayokabili shuleni? Huenda wakakuambia kwamba huna mahangaiko ya kulipia mikopo ya benki, kutunza familia, wala mwajiri mwenye kudai mengi. Hata hivyo, huenda unaona kwamba hakuna tofauti kati ya mikazo unayopata shuleni na mikazo ya wazazi wako kazini, au hata zaidi.

Kule tu kwenda na kurudi kutoka shuleni ni shida. Tara anayeishi Marekani anasema: “Mara nyingi wanafunzi walikuwa wakipigana ndani ya basi la shule. Dereva angesimamisha basi, na kumwamuru kila mtu ashuke. Sote tungechelewa kufika shuleni kwa nusu saa au zaidi.”

Je, mikazo inapungua unapofika shuleni? Wapi! Labda unakabili hali zifuatazo:

Mikazo kutoka kwa walimu.

“Walimu wangu wananisukuma nifanye vema kwenye masomo na kupita mitihani kwa alama za juu sana, si rahisi kuwapendeza.”Sandra.

“Walimu huwasukuma wanafunzi wafanye vema katika masomo, hasa ikiwa mwanafunzi anaonekana mwerevu.”—April.

“Hata ikiwa una miradi mizuri maishani, walimu fulani wanafanya uone kana kwamba hufai kitu ikiwa huna miradi ya masomo ambayo wao wanafikiri kwamba unapaswa kufuatia.” *—Naomi.

Unaathiriwa jinsi gani na mikazo kutoka kwa walimu?

․․․․․

Mikazo kutoka kwa marafiki.

“Katika shule za sekondari, wanafunzi wana uhuru mwingi zaidi nao ni wakaidi zaidi. Usipojiunga nao, wanakuona kuwa mshamba.”Kevin.

“Kila siku, ninashawishiwa kunywa pombe na kufanya ngono. Nyakati nyingine si rahisi kusimama imara hali kama hizo zinapotokea.”Aaron.

“Kwa kuwa sasa nina umri wa miaka 12, kila mtu anataka niwe na mpenzi. Kila mtu shuleni huniuliza, ‘Utabaki bila mpaka wakati gani?’”—Alexandria.

“Nilishinikizwa sana niwe na urafiki na mvulana fulani. Nilipokataa, nikaanza kuitwa msagaji. Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 10 tu!”Christa.

Unaathiriwa jinsi gani na mikazo kutoka kwa vijana wenzako?

․․․․․

Mambo mengine yanayosababisha mikazo. Tia alama ya ✔ kando ya jambo linalokuhangaisha zaidi—au uandike jambo hilo.

□ Mitihani

□ Kazi za shule za kufanyia nyumbani

□ Wazazi kutazamia mengi mno

□ Kufikia malengo yako yaliyo mengi mno

□ Kuonewa au kunyanyaswa kingono

□ Mengine ․․․․․

Hatua Nne za Kupunguza Mikazo

Kwa kweli, huwezi kutazamia kumaliza shule bila kupata mikazo kwa njia moja au nyingine. Hata hivyo, mikazo ikizidi inaweza kukulemea. Mfalme mwenye hekima Sulemani aliandika: “Uonevu mtupu unaweza kumfanya mtu mwenye hekima atende kiwazimu.” (Mhubiri 7:7) Lakini hupaswi kuruhusu hilo likupate. Siri ni kujifunza kushughulika na mikazo.

Kukabiliana na mikazo ni kama kunyanyua vyuma. Ili mnyanyua-vyuma afaulu, anahitaji kujitayarisha vya kutosha kabla ya kuanza. Hapakii uzito mwingi kupita anaoweza kunyanyua, naye huwa mwangalifu anaponyanyua. Akifanya hivyo, atajenga misuli bila kujiumiza. Kwa upande mwingine, asipokuwa mwangalifu, anaweza kukata misuli au hata kuvunjika mfupa.

Vivyo hivyo, unaweza kushughulika na mikazo na kutimiza kazi zako kwa mafanikio pasipo kujiumiza. Jinsi gani? Chukua hatua zifuatazo:

1. Tambua visababishi vyenyewe. “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha,” yasema methali moja yenye hekima. (Methali 22:3) Hata hivyo, huwezi kujificha kutokana na mikazo inayokulemea kabla ya kutambua chanzo chenyewe ni nini. Kwa hiyo tazama tena mambo uliyotia alama ya ✔ hapo mwanzo. Ni jambo gani linalokuhangaisha zaidi sasa?

2. Fanya utafiti. Kwa mfano, ikiwa kazi nyingi za shuleni zinakuhangaisha, fanya utafiti kwa kuchunguza mapendekezo yaliyo katika Sura ya 13 katika Buku la 2. Ikiwa unahisi unashinikizwa sana ufanye ngono na mwanafunzi mwenzako, unaweza pia kupata mashauri yanayoweza kukusaidia kushughulika na hali hiyo katika Sura ya 2, ya 5, na ya 15 katika buku hilo.

3. Usikawie. Matatizo hayawezi kutatuliwa kwa kuyapuuza. Badala yake, kwa kawaida yatakuwa makubwa zaidi, na hivyo kukuhangaisha hata zaidi. Ukiisha kuamua jinsi utakavyoshughulikia mkazo fulani, usikawie. Chukua hatua mara moja. Kwa mfano, ikiwa wewe ni Shahidi wa Yehova na unajaribu kuishi kulingana na viwango vya Biblia vya maadili, jitambulishe mara moja kwa wengine. Kufanya hivyo kunaweza kukupunguzia mkazo. Marchet, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Kila mwaka shule zinapofunguliwa, nilikuwa nikianzisha mazungumzo kuhusu habari ninayojua itanipa nafasi ya kueleza viwango vya Biblia. Niligundua kwamba kadiri nilivyokawia kujitambulisha kuwa Shahidi, ndivyo ilivyozidi kuwa vigumu kujitambulisha baadaye.” Ilikuwa rahisi zaidi nilipoeleza msimamo wangu mwanzoni na kuishi kupatana na msimamo wangu.”

4. Tafuta msaada. Hata mnyanyua-vyuma mwenye nguvu ana mipaka. Wewe pia una mipaka. Lakini si lazima uubebe mzigo huo mzito peke yako. (Wagalatia 6:2) Unaweza kuzungumza na wazazi wako au Mkristo mwingine mkomavu. Waonyeshe majibu uliyoandika mapema katika sura hii. Waulize maoni yao.

Kuna Mkazo Unaofaa?

Amini usiamini, ni vizuri kuwa na mikazo nyakati nyingine. Kwa nini? Mikazo inaonyesha kwamba una bidii na dhamiri yako inafanya kazi. Ona jinsi Biblia inavyomfafanua mtu anayejiona kuwa hana mikazo yoyote: “Utalala hapo mpaka lini? Utaamka lini katika usingizi wako? Wasema: ‘Acha nilale kidogo tu, acha nisinzie kidogo! niache nikunje mikono nipumzike kidogo!’ Wakati huo umaskini utakuvamia kama mnyang’anyi, ufukara utakufuata kama jambazi.”—Methali 6:9-11, Biblia Habari Njema.

Heidi, mwenye umri wa miaka 16, anafafanua vizuri jambo hilo. Anasema: “Huenda shule ikaonekana kuwa mahali pabaya, lakini mikazo unayokabili huko ndiyo ileile utakayokabili utakapoanza kufanya kazi.” Ni kweli kwamba si rahisi kukabiliana na mikazo. Lakini ikishughulikiwa kwa njia inayofaa, mikazo haitakuumiza. Badala yake, inaweza kukufanya uwe na nguvu zaidi.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Kuacha shule ndilo jibu la matatizo yako?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Unaweza kupata habari zaidi katika Sura ya 20 ya kitabu hiki.

ANDIKO MUHIMU

“Huku mkitupa mahangaiko yenu yote juu yake [Mungu], kwa sababu yeye anawajali ninyi.”—1 Petro 5:7.

PENDEKEZO

Panga matatizo ambayo hukuletea mikazo katika vikundi viwili, matatizo unayoweza kutatua na yale usiyoweza kutatua. Kwanza, shughulikia matatizo ambayo unaweza kutatua. Kisha, baada ya kuyatatua yote—ikiwa kwa kweli inawezekana—utakuwa na wakati mwingi zaidi wa kufikiria matatizo usiyoweza kutatua.

JE, WAJUA . . . ?

Kupata usingizi wa kutosha kila usiku, angalau saa nane, kutakusaidia kukabiliana na mkazo na pia kuboresha uwezo wako wa kukumbuka mambo.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ili niweze kukabiliana na mikazo, nimeamua kwamba ikiwezekana nitakuwa nikilala saa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini kutazamia ukamilifu kunaweza kukuongezea mikazo?

● Unaweza kuzungumza na nani ukilemewa na mikazo?

[Blabu katika ukurasa wa 132]

“Kila siku baba yangu alisali pamoja nami kabla ya kunipeleka shuleni. Sikuzote ilinifanya nihisi nikiwa salama.”—Liz

[Picha katika ukurasa wa 131]

Kama vile tu kuinua vyuma kwa njia inayofaa kunaweza kukufanya uwe na nguvu za kimwili, kushughulikia mikazo kwa njia inayofaa kunaweza pia kukuimarisha kihisia