Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Niache Shule?

Niache Shule?

SURA YA 19

Niache Shule?

Unafikiri unaweza kuacha shule ukifika darasa la ngapi? ․․․․․

Wazazi wako wangependa uache shule ukifika darasa la ngapi? ․․․․․

MAJIBU hayo mawili yanafanana? Hata ikiwa yanafanana na bado uko shuleni, huenda siku fulani ukatamani kuacha shule. Umewahi kuwa na maoni kama yafuatayo?

“Nyakati nyingine ningechoka sana hivi kwamba sikutaka kutoka kitandani. Ningefikiria, ‘Kuna haja gani ya kwenda shuleni kujifunza mambo ambayo sitayatumia kamwe maishani?’”—Rachel.

“Mara nyingi nimechoshwa na shule na kutaka kuacha shule na kutafuta kazi. Ninaona kwamba shule hainisaidii hata kidogo na kwamba ni afadhali nifanye kazi itakayonipa pesa.”—John.

“Nilienda shule ya sekondari iliyokuwa katika mtaa wa mabanda na ilikuwa vigumu kupata marafiki. Sikuwa na shida yoyote na masomo, hata hivyo, nilikuwa nimetengwa na wengine na mara nyingi nilikaa peke yangu. Ajabu ni kwamba hata wanafunzi wengine waliokuwa wametengwa kama mimi hawakutaka kuzungumza nami! Nilitaka sana kuacha shule.”—Ryan.

“Nilifanya kazi za shule kwa saa nne kila siku! Nilichoshwa sana na kazi nyingi za shule, miradi mbalimbali, na mitihani hivi kwamba nikahisi siwezi kuendelea na hali hiyo, afadhali niache shule.”—Cindy.

“Shuleni, kumekuwa na tishio la bomu, wanafunzi watatu walijaribu kujiua, mmoja alijiua, magenge yenye jeuri. Nyakati nyingine hali zilikuwa mbaya sana, nikataka kuacha shule!”—Rose.

Umepatwa na hali kama hizo? Ikiwa ndiyo, ni hali gani zinazokufanya utake kuacha shule?

․․․․․

Huenda sasa umeamua kabisa kuacha shule. Hata hivyo, unaweza kujua jinsi gani ikiwa unaacha shule kwa sababu ni wakati unaofaa wa kufanya hivyo au ni kwa sababu tu umechoshwa na shule? Ili kujibu swali hilo, kwanza tunahitaji kuelewa maana ya kuacha shule.

Kuacha au Kuondoka?

Unaweza kueleza jinsi gani tofauti kati ya kuondoka shuleni na kuacha shule?

․․․․․

Unajua kwamba katika nchi fulani ni kawaida kwa kijana kuhitimu baada ya kuwa shuleni kwa kati ya miaka mitano na minane? Katika nchi nyingine, wanafunzi hukaa shuleni kwa angalau miaka kumi. Kwa hiyo, hakuna umri au darasa hususa linalowafaa watu wote ulimwenguni pote.

Isitoshe, nchi au majimbo fulani yanaweza kumruhusu mwanafunzi afanyie masomo fulani au hata masomo yake yote nyumbani, pasipo kwenda shule za kawaida. Wanafunzi wanaosomea nyumbani, kwa ruhusa ya wazazi wao, hawajaacha shule.

Hata hivyo, ikiwa unafikiria kukatiza masomo kabla ya kuhitimu, iwe unasoma katika shule ya kawaida au nyumbani, unahitaji kufikiria maswali yafuatayo:

Sheria inasema nini? Kama ilivyotajwa mapema, sheria za nchi zinatofautiana. Ni kiwango gani cha chini zaidi cha elimu kilichowekwa na sheria katika eneo lenu? Umefikia kiwango hicho? Ukipuuza shauri la Biblia la ‘kujitiisha kwa mamlaka zilizo kubwa’ na kukatiza masomo yako kabla ya kufikia kiwango kilichowekwa na sheria, basi unaacha shule.—Waroma 13:1.

Nimetimiza miradi yangu kuhusiana na elimu? Ungependa elimu ikusaidie kutimiza nini? Hujui? Unahitaji kujua! Ikiwa hujui, utakuwa kama mtu anayesafiri katika gari-moshi lakini hajui anakoenda. Kwa hiyo, keti chini na wazazi wako, na ujaze sehemu yenye kichwa “ Miradi Yangu ya Kielimu,” katika ukurasa wa 139. Kufanya hivyo kutakusaidia kukaza fikira na kukusaidia wewe na wazazi wako kuamua utakaa shuleni kwa muda gani.—Methali 21:5.

Haikosi walimu wako na watu wengine watakupa mashauri tofauti-tofauti kuhusu kiwango cha elimu unachopaswa kufikia. Hata hivyo, wazazi wako ndio walio na mamlaka ya kufanya uamuzi. (Methali 1:8; Wakolosai 3:20) Ukikatiza masomo yako kabla ya kutimiza miradi yako kuhusiana na elimu, na ambayo wewe na wazazi wako mmeweka, basi unaacha shule.

Kwa nini ninataka kuacha shule? Usijidanganye. (Yeremia 17:9) Ni kawaida ya wanadamu kufikiri kwamba wana sababu nzuri ya kufanya jambo fulani, hata wakati wanapotenda kwa ubinafsi.—Yakobo 1:22.

Andika hapa sababu nzuri ambazo huenda unazo za kutaka kuacha masomo kabla ya kuhitimu.

․․․․․

Andika hapa baadhi ya sababu za kibinafsi za kuacha shule.

․․․․․

Ni sababu gani nzuri ulizoandika? Huenda baadhi ya sababu hizo zikawa kuitegemeza familia yenu kiuchumi au kufanya utumishi wa kujitolea ili kuwafundisha wengine kumhusu Mungu. Sababu za kibinafsi zinaweza kuwa ni kuepuka mitihani au kazi za shule. Tatizo ni kutambua sababu hasa inayokuchochea, na ikiwa ni sababu nzuri au ina ubinafsi.

Tazama tena orodha uliyoandika, na kwa unyofu ukadirie uzito wa sababu hizo ukitumia kipimo cha 1 mpaka 5 (1 ikiwakilisha kutokuwa na maana, 5 ikiwakilisha kuwa na maana zaidi). Ikiwa unaacha shule kwa sababu tu unataka kuepuka matatizo, utashangaa.

Kuna Ubaya Gani Kuacha Shule?

Kuacha shule ni kama kuruka kutoka katika gari-moshi kabla ya kufika unakoenda. Huenda safari yenyewe ikawa yenye kuchosha na huenda hata wasafiri wasiwe wenye urafiki. Lakini ukiruka na kutoka, hutafika unakoenda, na huenda ukaumia. Vivyo hivyo, ukiacha shule, huenda usitimize miradi yako ya elimu nawe utajisababishia matatizo sasa na baadaye, kama yafuatayo:

Matatizo ya sasa: Yaelekea haitakuwa rahisi kwako kupata kazi. Na ikiwa utapata, huenda ukapata mshahara au malipo ya chini kuliko vile ungepata kama ungemaliza masomo yako. Ili kuishi maisha ya kawaida tu, huenda ukahitajika kufanya kazi kwa muda mrefu katika mazingira mabaya hata kuliko mazingira uliyokuwa nayo shuleni.

Matatizo ya baadaye: Utafiti unaonyesha kwamba wale wanaoacha shule yaelekea watakuwa na afya mbaya, wataishia gerezani, au watalazimika kutegemea mashirika ya misaada.

Haimaanishi kwamba ukimaliza masomo hutapata matatizo hayo. Hata hivyo, kwa nini ujiletee matatizo kwa kuacha shule?

Faida za Kutoacha Shule

Ikiwa umeanguka mtihani au ulikuwa na siku mbaya shuleni, huenda ukakata tamaa. Huenda matatizo yoyote ya wakati ujao yakaonekana duni kwa kulinganishwa na hali yako ya sasa. Lakini kabla ya kuamua kuchukua njia “rahisi,” fikiria yale ambayo wanafunzi walionukuliwa mwanzoni mwa sura hii wanasema kuhusu jinsi walivyofaidika kwa kutoacha shule.

“Nimejifunza uvumilivu, ukakamavu wa kiakili. Pia nimegundua kwamba ukitaka kufurahia kufanya jambo fulani, lazima ubadili mtazamo wako. Kwa kuendelea na masomo, nimepata ujuzi wa sanaa nitakaotumia baada ya kuhitimu.”—Rachel.

“Sasa ninajua kwamba nikitia bidii nitaifikia miradi yangu. Ninajifunza somo la kiufundi katika shule ya sekondari ambalo litanisaidia kupata kazi ninayopenda, fundi wa matbaa.”—John.

“Kwa sababu nilivumilia, nimekuwa stadi katika kuandika na kusoma. Shule imenifunza jinsi ya kufaidika kutokana na uchambuzi na jinsi ya kujieleza waziwazi na kwa njia inayopatana na akili—ustadi unaohitajika katika huduma ya Kikristo.”—Ryan.

“Shule imenisaidia kujua jinsi ya kutatua matatizo, iwe darasani au kwingineko. Kujua jinsi ya kushughulikia matatizo ya kimasomo, kijamii, na kimwili kumenisaidia sana kukomaa.”—Cindy.

“Shule ilinitayarisha kwa ajili ya matatizo ninayoweza kukabili kazini. Pia, nilikabili hali mbalimbali zilizonisaidia kuchunguza imani yangu. Hivyo, kuwa shuleni kumeimarisha usadikisho wangu wa kiroho.”—Rose.

Mfalme mwenye hekima Sulemani aliandika: “Mwisho wa jambo ni bora kuliko mwanzo wake. Mtu mwenye subira ni bora kuliko mwenye roho ya majivuno.” (Mhubiri 7:8) Hivyo basi, badala ya kuacha shule, jifunze kushughulikia kwa subira matatizo unayokabili shuleni. Ukifanya hivyo, mwishowe utagundua kwamba matokeo yatakuwa mazuri kwako.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Namna gani ikiwa sababu moja inayofanya uchukie shule ni kutoelewana na mwalimu wako?

ANDIKO MUHIMU

“Kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.”—Methali 21:5.

PENDEKEZO

Ikiwa hupendi mazingira ya shuleni, jaribu kuona kama unaweza kujiandikisha katika mitalaa ya masomo ya haraka itakayokuwezesha kufuzu mapema.

JE, WAJUA . . . ?

Mara nyingi, vijana wanaoruka-ruka masomo hatimaye hushindwa kumaliza shule.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ikiwa ninalemewa na somo fulani, badala ya kuacha shule nita ․․․․․

Ikiwa ninataka kuacha shule kwa sababu ya uchovu, ninaweza kushughulika inavyofaa na hali hiyo ikiwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini ni muhimu ujifunze kusoma, kuandika, na kufanya hesabu vizuri?

● Kujiwekea miradi ya muda mfupi kuhusu mambo ya elimu kunaweza kukusaidia jinsi gani kutumia vizuri wakati ulio nao shuleni?

● Kufikiria kwa kadiri fulani kazi ambayo ungependa kufanya baada ya kukamilisha masomo kunaweza kukusaidia jinsi gani?

[Blabu katika ukurasa wa 140]

“Huwezi kuyakimbia matatizo. Kuwa shuleni kunakusaidia kujua jinsi ya kujitegemea, jambo unalohitaji utakapokuwa kazini na kwingineko.”—Ramona

[Sanduku katika ukurasa wa 139]

 Ukurasa wa Mazoezi

Miradi Yangu ya Kielimu

Kusudi hasa la elimu ni kukutayarisha kupata kazi itakayokusaidia na kuisaidia familia ambayo huenda ukawa nayo wakati ujao. (2 Wathesalonike 3:10, 12) Umeamua ni aina gani ya kazi unayotaka na jinsi wakati unaotumia shuleni unavyoweza kukusaidia kujitayarisha kwa ajili ya kazi hiyo? Ili kukusaidia kujua ikiwa elimu yako inakuelekeza mahali panapofaa, jibu maswali yafuatayo:

Nina uwezo gani? (Kwa mfano, wewe hushirikiana vizuri na watu? Wewe hufurahia kufanya kazi kwa mikono yako au kuunda au kurekebisha vitu? Unajua kuchunguza na kutatua matatizo?) ․․․․․

Ni kazi za aina gani zitakazoniwezesha kutumia uwezo wangu? ․․․․․

Ni kazi gani za kuajiriwa zinazopatikana mahali ninakoishi? ․․․․․

Ni masomo gani sasa yanayonitayarisha kwa ajili ya kupata kazi wakati ujao? ․․․․․

Ni masomo gani ninayoweza kuchagua yatakayonisaidia kufikia miradi yangu kwa njia inayofaa zaidi? ․․․․․

Kumbuka, mradi wako ni kufuzu ukiwa na elimu unayoweza kutumia. Kwa hiyo, usipite mipaka na kuwa mwanafunzi daima, na kukwepa majukumu ya utu-uzima. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 69 Unaweza kupata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 38.

[Picha katika ukurasa wa 138, 139]

Kuacha shule ni kama kuruka kutoka katika gari-moshi kabla ya kufika unakoenda