Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kuelezaje Maoni ya Biblia Kuhusu Ugoni-Jinsia-Moja?

Ninaweza Kuelezaje Maoni ya Biblia Kuhusu Ugoni-Jinsia-Moja?

SURA YA 23

Ninaweza Kuelezaje Maoni ya Biblia Kuhusu Ugoni-Jinsia-Moja?

Umati unashangilia huku wasanii wawili wa kike wanapobusiana kimapenzi katika sherehe ya kuwatuza wasanii! Watazamaji wavuta pumzi kwa mshangao, kisha waanza kushangilia. Wagoni-jinsia-moja wauona huo kuwa ushindi. Wengine waliona jambo hilo kuwa kituko cha kujitafutia umaarufu tu. Picha za video za wasanii hao wakibusiana zitaonyeshwa tena na tena kwenye televisheni—na kuvutia upendezi wa wengi katika Intaneti—kwa siku nyingi.

KAMA inavyoonyeshwa katika kisa kinachotajwa hapo juu, mtu mashuhuri anapodokeza au kutangaza waziwazi kwamba yeye ni mgoni-jinsia-moja au mgoni-jinsia-mbili, hizo huwa habari moto-moto kwenye vyombo vya habari. Watu fulani huwasifu watu kama hao kwa kuonyesha ujasiri; wengine huwashutumu wakiwaona kuwa wapotovu. Hata hivyo, walio wengi huuona ugoni-jinsia-moja kuwa tu mtindo tofauti wa maisha. “Nilipokuwa shuleni,” asema Daniel mwenye umri wa miaka 21, “hata vijana ambao hawakuwa wagoni-jinsia-moja, walimwona yeyote aliyechukizwa na wazo la ugoni-jinsia-moja kuwa mwenye ubaguzi na mwenye kuhukumu wengine.”

Maoni kuhusu ugoni-jinsia-moja yanaweza kutofautiana kutoka kwa kizazi kimoja hadi kingine au nchi moja hadi nyingine. Hata hivyo, Wakristo ‘hawachukuliwi huku na huku na kila upepo wa fundisho.’ (Waefeso 4:14) Badala yake, wanashikamana na maoni ya Biblia.

Biblia ina maoni gani? Na ikiwa unaishi kulingana na viwango vya Biblia vya maadili, unaweza kuwajibu namna gani wale wanaokuona kuwa mwenye ubaguzi, mwenye kuwahukumu wengine, au hata mwenye chuki kuelekea vikundi fulani vya watu? Fikiria maswali au taarifa zifuatazo na jinsi zinavyoweza kujibiwa.

“Biblia inasema nini kuhusu ugoni-jinsia-moja?”

“Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu alikusudia ngono iwe kati ya mwanamume na mwanamke katika mpango wa ndoa tu. (Mwanzo 1:27, 28; Mambo ya Walawi 18:22; Methali 5:18, 19) Biblia inaposhutumu uasherati, inatia ndani mazoea kati ya watu wa jinsia moja na pia ngono haramu kati ya watu wa jinsia tofauti.” *Wagalatia 5:19-21.

Una maoni gani kuhusu ugoni-jinsia-moja?”

“Siwachukii watu wenyewe, hata hivyo sikubaliani na mwenendo wao.”

Kumbuka: Ikiwa unaongozwa na viwango vya Biblia vya maadili, basi huo ni mtindo wako wa maisha, na una haki ya kuwa na msimamo huo. (Yoshua 24:15) Usionee haya maoni yako.—Zaburi 119:46.

“Wakristo wanapaswa kuwaheshimu watu wote, haidhuru maelekeo yao ya kingono, sivyo?”

“Ni kweli. Biblia inasema: ‘Waheshimuni watu wa namna zote.’ (1 Petro 2:17) Kwa hiyo, Wakristo hawawachukii. Wakristo huwatendea watu wote kwa fadhili, kutia ndani wagoni-jinsia-moja.”—Mathayo 7:12.

“Huoni kwamba maoni yako kuhusu ugoni-jinsia-moja yanaweza kuchochea ubaguzi dhidi yao?”

“Hapana. Ninachokataa ni mwenendo wenyewe, bali si watu wenyewe.”

Unaweza kuongeza hivi: “Kwa mfano, nimeamua pia kutovuta sigara. Hata wazo lenyewe naliona kuwa lenye kuchukiza. Lakini tuseme wewe ni mvutaji wa sigara nawe huoni ubaya wowote. Siwezi kukubagua kwa sababu ya maoni yako, nami nina hakika pia huwezi kunibagua kwa sababu ya maoni yangu—sivyo? Ndivyo pia na maoni yetu yanayotofautiana kuhusu ugoni-jinsia-moja.”

“Kwa kuwa Yesu alitufundisha kuwavumilia wengine, Wakristo wanapaswa kuyakubali maoni ya wengine kuhusu ugoni-jinsia-moja, sivyo?”

“Yesu hakuwahimiza wafuasi wake wakubali mitindo yoyote ile ya maisha. Badala yake, alifundisha kwamba njia ya wokovu iko wazi kwa ‘kila mtu anayemwamini.’ (Yohana 3:16) Kumwamini Yesu kunatia ndani kuishi kulingana na kanuni za Biblia za maadili, vinavyokataza aina fulani za mwenendo, kutia ndani ugoni-jinsia-moja.”—Waroma 1:26, 27.

“Wagoni-jinsia-moja hawawezi kujibadili wawe kitu wasicho; walizaliwa hivyo.”

“Biblia haizungumzii maumbile ya wagoni-jinsia-moja, ijapokuwa inakubali kwamba mazoea fulani yametia mizizi. (2 Wakorintho 10:4, 5) Hata ikiwa watu fulani wana maelekeo hayo, Biblia inawaambia Wakristo wajiepushe na mazoea ya ugoni-jinsia-moja.”

Pendekezo: Badala ya kunaswa katika mtego wa kujadiliana kuhusu chanzo hasa cha tamaa za kigoni-jinsia-moja, kazia kwamba Biblia inaukataza mwenendo huo. Kwa mfano, unaweza kusema: “Unajua watu wengi hudai kwamba watu fulani wamerithi maelekeo ya kutenda kijeuri, kwamba walizaliwa hivyo. (Methali 29:22) Huenda ni kweli, hata hivyo, kama ujuavyo, Biblia inashutumu milipuko ya hasira. (Zaburi 37:8; Waefeso 4:31) Je, tunaweza kusema kanuni hiyo haifai eti kwa sababu watu fulani huenda wakawa na maelekeo ya kutenda kijeuri?”

“Mungu anaweza kumwagizaje mtu anayevutiwa na watu wa jinsia yake ajiepushe na ugoni-jinsia-moja? Huo ni ukatili.”

“Maoni hayo yanatokana na wazo lenye kosa kwamba wanadamu hawana budi kutosheleza tamaa zao za ngono. Biblia inawakweza wanadamu kwa kuwahakikishia kwamba wanaweza kuchagua kutotenda kulingana na tamaa zao zisizofaa za ngono ikiwa kwa kweli wanataka kufanya hivyo.”—Wakolosai 3:5.

“Hata kama wewe si mgoni-jinsia-moja, unahitaji kubadili maoni yako.”

“Tuseme sipendi kamari, lakini wewe unapenda. Utasisitiza nibadili maoni yangu, eti kwa sababu mamilioni ya watu wanapenda kucheza kamari?”

Kumbuka: Wagoni-jinsia-moja, na watu wengine wengi, wana misimamo fulani ambayo inawafanya wachukizwe na mambo fulani, huenda mambo kama vile udanganyifu, ukosefu wa haki, au vita. Biblia inakataza mambo hayo; pia inakataza mwenendo fulani wa ngono, kutia ndani ugoni-jinsia-moja.—1 Wakorintho 6:9, 10.

Biblia haidai mno wala haiwatii watu moyo waonyeshe ubaguzi. Badala yake, inawaagiza wote ‘waukimbie uasherati,’ iwe wana tamaa za ugoni-jinsia-moja au ugoni-jinsia-tofauti.—1 Wakorintho 6:18.

Ukweli ni kwamba, hata mamilioni ya wagoni-jinsia-tofauti wanaotaka kuishi kulingana na viwango vya Biblia, wanahitaji sifa ya kujizuia ili kutoshindwa na vishawishi vyovyote wanavyoweza kupata. Miongoni mwao kuna wengi ambao ni waseja, wasio na matumaini ya kufunga ndoa, na wengi ambao wamefunga ndoa na mwenzi ambaye kwa sababu moja au nyingine hawezi kushiriki tendo la ngono. Wameweza kuishi kwa furaha bila kutosheleza tamaa zao za ngono. Walio na maelekeo ya ugoni-jinsia-moja wanaweza kufanya hivyo pia ikiwa kwa kweli wanataka kumpendeza Mungu.—Kumbukumbu la Torati 30:19.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 28

KATIKA SURA INAYOFUATA

Wasichana fulani wanaamini kwamba kufanya ngono na wapenzi wao kutaimarisha uhusiano wao. Sivyo hata kidogo! Sura inayofuata inaeleza ni kwa nini.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Neno “uasherati” katika Biblia halimaanishi ngono tu bali pia linatia ndani vitendo kama vile kuchua au kupiga punyeto viungo vya uzazi vya mtu mwingine, ngono ya kinywa, au ngono ya mkundu.

ANDIKO MUHIMU

“Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.”—Wakolosai 3:5.

PENDEKEZO

Ijapokuwa mwenendo wa wengine unaweza kukuudhi, unapozungumza nao epuka kuonekana kana kwamba unajiona kuwa mwadilifu. Ukweli ni kwamba wana haki ya kuchagua mambo wanayotaka kuamini, kama vile wewe ulivyo na haki ya kufanya hivyo.

JE, WAJUA . . . ?

Wakristo fulani wa karne ya kwanza ambao hapo awali walifanya ngono na watu wa jinsia moja waliacha njia zao chafu, ‘wakaoshwa wakawa safi’ mbele za Mungu.—1 Wakorintho 6:9-11.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Mtu akisema kwamba maoni ya Biblia kuhusu ugoni-jinsia-moja ni ya zamani, nitasema ․․․․․

Ili iwe wazi kwamba ninachukia mwenendo wa ugoni-jinsia-moja bali si watu wenyewe, nitasema ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini Mungu ana haki ya kuwawekea wanadamu sheria za maadili?

● Unapata faida gani kwa kushikamana na sheria za Biblia za maadili?

[Blabu katika ukurasa wa 170]

“Mvulana mmoja shuleni alichukizwa nami kwa sababu niliukataa mtindo wake wa maisha. Lakini nilipomweleza kwamba simkatai yeye binafsi—na alipogundua kwamba sichukizwi tu na ugoni-jinsia-moja bali pia upotovu wowote wa maadili—alianza kuniheshimu na hata kunitetea wengine walipoleta upinzani.”—Aubrey

[Sanduku katika ukurasa wa 168]

Namna Gani Ugoni-Jinsia-Mbili?

Ingawa watu wa jinsia zote mbili wanaweza kuwa na maelekeo hayo, inaonekana walio wengi hasa ni wasichana. Kwa baadhi yao ni “kutaka tu kujua.” Lisa, mwenye umri wa miaka 26, anasema: “Vijana wanapotazama sinema, televisheni, na kusikiliza muziki wenye mazoea ya wasichana kuwabusu wasichana wenzao, wanaanza kushawishika kujaribu, hasa ikiwa hawaoni ubaya wowote wa kufanya hivyo.”

Kwa wengine, inaonekana kwa kweli wanavutiwa na watu wa jinsia yao. “Nilipokuwa kwenye karamu fulani, nilikutana na wasichana wawili ambao ni wagoni-jinsia-mbili,” asema Vicky, mwenye umri wa miaka 13, “baadaye rafiki yangu akaniambia kwamba wanavutiwa nami. Punde si punde tukaanza kuwasiliana kupitia ujumbe mfupi na mmoja wao, nami nikaanza kuvutiwa naye.”

Umewahi kuhisi jinsi Vicky alivyohisi? Huenda watu wengi wakakuhimiza ukubali ukweli wa mambo na kujitokeza waziwazi utambuliwe kuwa mgoni-jinsia mbili. Hata hivyo, unapaswa kujua kwamba kuvutiwa na mtu wa jinsia yako mara nyingi huwa jambo la kupita tu. Hivyo ndivyo, Vicky, alivyotambua. Na ndivyo ilivyokuwa pia kwa Lisette, mwenye umri wa miaka 16. Anasema: “Nilitulia baada ya kuzungumza na wazazi wangu kuhusu hisia zangu. Pia, nilijifunza shuleni katika somo la biolojia kwamba katika miaka ya kubalehe, kiasi cha homoni mwilini hubadilika-badilika sana. Ikiwa tu vijana wangejua mengi zaidi kuhusu miili yao, wangeelewa kwamba kuvutiwa kingono na mtu wa jinsia yako ni jambo la muda tu, na kwa hiyo hakuna haja ya kushinikizwa kuwa wagoni-jinsia-moja.”

Hata ikiwa hisia zako zinaonekana kuwa zimetia mizizi na si za muda mfupi tu ujanani, kumbuka kwamba Biblia inakupa mradi unaoweza kufikia: Unaweza kuamua kutotosheleza tamaa zisizofaa, hata ziwe za aina gani.

[Picha katika ukurasa wa 169]

Kuhusu maoni yanayopendwa na wengi, Wakristo huwa na ujasiri wa kuwa tofauti