Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Namna Gani Kufanya Ngono Bila Kuwajibika?

Namna Gani Kufanya Ngono Bila Kuwajibika?

SURA YA 26

Namna Gani Kufanya Ngono Bila Kuwajibika?

“Vijana ‘huchukuana wawili-wawili’ ili tu kuona wanaweza kufanya ‘utundu’ kadiri gani, au hata kuona wanaweza kufanya ngono na watu wangapi.”—Penny.

“Wavulana huzungumza waziwazi kuhusu ngono. Wao hujivuna kwamba ingawa wana mpenzi bado wanafanya ngono na wasichana wengine wengi.”—Edward.

VIJANA wengi leo hujivuna kwa sababu ya kufanya ngono bila kuwajibika, hata na watu wasiowajua. Wengine hata wana “marafiki” wanaoweza kufanya ngono nao wakati wowote wanapotaka, pasipo uhusiano wowote wa kimahaba.

Usishangae ikiwa wewe pia unavutiwa kwa kiasi fulani na hali kama hiyo! (Yeremia 17:9) Edward, aliyetajwa mapema, anasema: “Wasichana wengi wameniomba nifanye ngono nao, na kwangu mimi, kukataa maombi hayo ndilo pambano kali zaidi ninalokabili nikiwa Mkristo. Ni vigumu kukataa!” Ni kanuni gani za Biblia unazopaswa kukumbuka unapoombwa kufanya ngono?

Ubaya wa Kufanya Ngono Bila Kuwajibika

Uasherati ni dhambi nzito sana hivi kwamba walio na mazoea hayo “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Huo ndio ukweli wa mambo, iwe wahusika wenyewe “wanapendana” au wanataka tu kutosheleza tamaa zao za ngono pasipo hata kujuana. Vyovyote vile, ili kuepuka kushawishika, unapaswa kuuona uasherati kama vile Yehova anavyouona.

“Ninaamini kabisa kwamba njia ya Yehova ndiyo njia bora zaidi.”—Karen, Kanada.

“Kumbuka wewe ni mwana au binti ya mtu fulani, rafiki ya watu wengi, na mshiriki wa kutaniko. Utawavunja moyo watu wote hao ukikubali kushindwa na kishawishi hicho!”—Peter, Uingereza.

Kwa kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu uasherati, utaweza ‘kuchukia yaliyo mabaya,’ hata kama yanavutia mwili.—Zaburi 97:10.

Unaweza kusoma: Mwanzo 39:7-9. Ona ujasiri wa Yosefu aliposhawishiwa kufanya ngono na kilichomwezesha kukataa.

Jivunie Imani Yako

Si ajabu kuwaona vijana wakichukua msimamo na kujivunia jambo fulani wanaloamini. Wewe una pendeleo la pekee la kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Usiaibikie maoni au msimamo wako kuhusu kufanya ngono kabla ya ndoa.

“Eleza waziwazi tangu mwanzo kwamba una kanuni za maadili zinazokuongoza maishani.”—Allen, Ujerumani.

“Vijana niliosoma nao katika shule ya sekondari walinielewa, nao walijua kwamba kujaribu kunishawishi ni kazi bure.”—Vicky, Marekani.

Kuwa na msimamo kuhusu mambo unayoamini ni ishara kwamba umeanza kuwa Mkristo mkomavu.—1 Wakorintho 14:20.

Unaweza kusoma: Methali 27:11. Ona jinsi matendo yako mazuri yanavyoweza kufurahisha moyo wa Yehova!

Uwe na Msimamo Imara!

Ni muhimu kukataa. Hata hivyo, huenda wengine wakadhani unataka tu kubembelezwa.

“Mambo yote, kutia ndani jinsi unavyovalia, jinsi unavyotembea, watu unaozungumza nao, na jinsi unavyoshughulika na watu, yanapaswa kuonyesha kwamba umekataa kata kata.”—Joy, Nigeria.

“Unapaswa kueleza waziwazi kwamba haiwezekani hata kidogo. Usikubali kamwe zawadi kutoka kwa wavulana wanaojaribu kukutongoza. Baadaye wanaweza kudai wana haki kwa kuwa umekuwa ukipokea zawadi zao.”—Lara, Uingereza.

Yehova atakusaidia ukiwa na msimamo imara. Kutokana na mambo yaliyompata yeye mwenyewe, mtunga-zaburi Daudi angeweza kusema hivi kumhusu Yehova: “Kwa mtu mshikamanifu utatenda kwa ushikamanifu.”—Zaburi 18:25.

Unaweza kusoma: 2 Mambo ya Nyakati 16:9. Ona kwamba Yehova yuko tayari kuwasaidia wanaotaka kufanya yaliyo sawa.

Tumia Utambuzi

Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Unaweza kutumia shauri hilo jinsi gani? Kwa kutumia utambuzi!

“Jitenge kabisa na watu wanaozungumzia mambo kama hayo.”—Naomi, Japani.

“Usimpe yeyote habari zako za kibinafsi, kama vile anwani yako au namba yako ya simu.”—Diana, Uingereza.

Chunguza usemi wako, mwenendo, na watu unaoshirikiana nao, vilevile sehemu unazopenda kwenda. Kisha jiulize, ‘Kwa kutojua ninawapa wengine sababu za kunishawishi nifanye ngono?’

Unaweza kusoma: Mwanzo 34:1, 2. Ona matokeo mabaya yaliyompata msichana anayeitwa Dina kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa.

Kumbuka, kufanya ngono bila kuwajibika ni jambo zito machoni pa Yehova Mungu; nawe pia unapaswa kuwa na maoni hayo. Kwa kuchukua msimamo unaofaa, unaweza kudumisha dhamiri safi mbele za Mungu na utajiheshimu. Kama msichana anayeitwa Carly anavyosema, “kwa nini uruhusu mtu mwingine ‘akutumie’ ili tu kutosheleza tamaa zake anavyotaka? Tunza msimamo wako mzuri mbele za Yehova ambao umejitahidi sana kuwa nao!”

KATIKA SURA INAYOFUATA

Ni wasichana wa aina gani ambao wavulana husema wanavutiwa nao hasa? Huenda ukashangaa!

ANDIKO MUHIMU

“Fanyeni yote mnayoweza ili mwishowe [Mungu] awapate ninyi mkiwa bila doa na bila dosari na mkiwa katika amani.”—2 Petro 3:14.

PENDEKEZO

Kuza sifa nzuri. (1 Petro 3:3, 4) Ukiwa na sifa nzuri, utamvutia mtu mwenye sifa nzuri.

JE, WAJUA . . . ?

Yehova anataka ufurahie ngono vile alivyoikusudia—iwe chanzo cha furaha katika ndoa—bila wasiwasi, mahangaiko, na majuto ambayo mara nyingi hutokana na uasherati.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ninaweza kuiga azimio la Yosefu la kuwa na maadili safi ikiwa nita ․․․․․

Nitaepuka makosa ambayo Dina alifanya ikiwa nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Ijapokuwa huenda ngono haramu ikavutia mwili usio mkamilifu, kwa nini ni kosa?

● Utafanya nini mtu fulani akikuomba mfanye ngono?

[Blabu katika ukurasa wa 185]

“Kuwa imara! Kijana mmoja alipojaribu kunitongoza, nilimwambia, ‘Ondoa mkono wako begani mwangu!’ kisha nikaondoka nikimtazama kwa ukali.”—Ellen

[Picha katika ukurasa wa 187]

Ukifanya ngono bila kuwajibika, unajishushia heshima