Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Wavulana Hawanipendi?

Kwa Nini Wavulana Hawanipendi?

SURA YA 27

Kwa Nini Wavulana Hawanipendi?

Anajua mimi ni msichana maarufu kwa sababu nimemwambia wavulana wengine wanavutiwa nami. Alicheka nilipomwambia jinsi rafiki zangu wengine walivyo wapuuzi. Anajua nilivyo mwerevu—hata nimemrekebisha mara kadhaa kuhusu mambo fulani-fulani. Si aniombe tu tuwe marafiki.

Anaonekana mrembo, lakini ana utoto mwingi sana! Hata hanipi nafasi ya kuzungumza. Na nikifungua mdomo tu, anaanza kunirekebisha-rekebisha! Sijui nitorokee wapi.

UNAONA kwamba wavulana hawapendezwi nawe? Wasichana wengi huona hivyo, hata wale ambao huenda ukafikiri hawana shida! Kwa mfano, mfikirie Joanne. Ni mrembo, mwenye akili, na mwenye ufasaha. Hata hivyo, anasema: “Mara nyingi mimi huona kwamba wavulana hawanipendi. Wavulana wachache niliowapenda, walipendezwa nami kwa muda halafu baadaye wakaacha kabisa kuongea nami!”

Ni mambo gani yanayowafanya wavulana wavutiwe na wasichana? Ni mambo gani yanayowafukuza? Unaweza kufanya nini ili umvutie mvulana mwenye kuheshimika?

Mambo ya Kufanya

Fahamu akili na moyo wako. Inaelekea ulivutiwa hata zaidi na wavulana baada tu ya kuanza kubalehe. Huenda ulivutiwa na mvulana zaidi ya mmoja. Hilo ni jambo la kawaida. Lakini ikiwa ungeruhusu hisia zako zikuongoze kuwa na uhusiano wa kimahaba na mvulana wa kwanza uliyevutiwa naye, huenda hilo lingeharibu ukuzi wako wa kihisia na kiroho. Inachukua muda kukuza sifa nzuri, ‘kufanya upya akili zako’ kuhusu mambo yaliyo ya maana, na kufikia baadhi ya miradi yako.Waroma 12:2; 1 Wakorintho 7:36; Wakolosai 3:9, 10.

Ni kweli kwamba wavulana wengi huvutiwa na wasichana ambao bado hawajawa na misimamo thabiti au “wasiojua mengi.” Hata hivyo, kimsingi wavulana wa aina hiyo wanapendezwa tu na jinsi msichana alivyo kwa nje, bali si msichana mwenyewe, yaani, utu wake. Ukweli ni kwamba, mvulana mzuri atatafuta msichana ambaye wanafaana.—Mathayo 19:6.

Kile ambacho wavulana husema: “Mimi huvutiwa na msichana anayeweza kutoa maoni yake mwenyewe na anayejiamini.”—James.

“Ninapendezwa na msichana anayeweza kujieleza kwa unyoofu na kwa adabu, na asiyekubaliana tu na kila kitu ninachosema. Hata msichana awe mrembo namna gani, sifurahii kuwa pamoja naye ikiwa anasema mambo ili tu kunifurahisha.”—Darren.

Una maoni gani kuhusu maelezo ya wavulana hao?

․․․․․

Jifunze kuwaheshimu wengine. Kama vile unavyotaka kupendwa, wavulana unaowafahamu pia hutaka sana kuheshimiwa. Haishangazi kwamba Biblia inasema mume ampende mke wake na kwamba mke anapaswa “kumheshimu sana” mume wake. (Waefeso 5:33) Kupatana na hilo, uchunguzi uliohusisha mamia ya wavulana ulifunua kwamba zaidi ya asilimia 60 wanathamini sana heshima kuliko upendo. Zaidi ya asilimia 70 ya wanaume walio watu wazima walisema vivyo hivyo pia.

Heshima haimaanishi kukubali kila kitu—kwamba hupaswi kuwa na maoni tofauti na ya wengine na kwamba hupaswi kuyaeleza. (Mwanzo 21:10-12) Hata hivyo, mvulana anaweza kuvutiwa au kutovutiwa kwa kutegemea jinsi unavyoeleza maoni yako. Ikiwa wakati wote unarekebisha au kupinga kile anachosema, huenda akaona kuwa humheshimu. Lakini, ukisikiliza maoni yake na kumpongeza inapofaa, huenda akakubali na kuthamini maoni yako. Bila shaka, mvulana aliye na utambuzi ataona pia ikiwa unawatendea watu wa familia yenu na wengine kwa heshima.

Kile ambacho wavulana husema: “Nafikiri heshima ndilo jambo muhimu zaidi mwanzoni mwa urafiki. Upendo unaweza kusitawi baadaye.”—Adrian.

“Ikiwa msichana anaweza kuniheshimu, naamini kwamba anaweza kunipenda.”—Mark.

Una maoni gani kuhusu maelezo ya wavulana hao?

․․․․․

Valia kwa kiasi, na udumishe usafi. Mavazi na mapambo yako ni kama vipaza sauti ambavyo hutangaza maoni yako ya ndani na mtazamo wako. Hata kabla hujaanza kuongea na mvulana, tayari mavazi yako yamesema mengi kukuhusu. Ikiwa mavazi yako ni yenye mpangilio mzuri na ya kiasi, yatasema mambo mazuri kukuhusu. (1 Timotheo 2:9) Ikiwa mavazi yako ni yenye kuchochea watu kingono au ni ya kizembe, yatatangaza ujumbe ulio wazi na mbaya kukuhusu!

Kile ambacho wavulana husema: “Jinsi msichana anavyovalia husema mengi kuhusu mtazamo wake kuhusu maisha. Ikiwa anavalia nguo zenye kuonyesha uchi au za kizembe, ni wazi kwamba anataka sana kuwavutia watu wa jinsia tofauti.”—Adrian.

“Mimi huvutiwa na msichana anayetunza nywele zake, anayenukia vizuri, na aliye na sauti yenye kupendeza. Kwa upande mwingine, ingawa nilikuwa nimevutiwa na msichana mmoja mrembo, niliachana naye kwa sababu hakudumisha usafi.”—Ryan.

“Ni kweli kwamba msichana akivalia kwa njia yenye kuvutia kingono, atawavutia watu fulani mwanzoni. Hata hivyo, singependa kuanzisha uhusiano na msichana wa aina hiyo.”—Nicholas.

Una maoni gani kuhusu maelezo ya wavulana hao?

․․․․․

Mambo ya Kuepuka

Usichezee hisia za watu. Wanawake wana uvutano mkubwa sana kwa wanaume. Uvutano huo unaweza kutumiwa vizuri au vibaya. (Mwanzo 29:17, 18; Methali 7:6-23) Ukipima uvutano wako kila mara unapokutana na mvulana, mwishowe utajipatia sifa mbaya.

Kile ambacho wavulana husema: “Kuketi tu karibu na msichana mwenye kuvutia na kugusana mabega kunaweza kusisimua, kwa hiyo, nafikiri msichana anayependa kukugusa-gusa anapozungumza nawe, anachezea hisia zako.”—Nicholas.

“Ikiwa nyakati zote msichana anapenda kumgusagusa mkono kila mvulana anayekutana naye au kumtazama kwa macho yenye utongozi kila mwanamume anayepita, basi msichana huyo anapenda kuchezea hisia za watu, na msichana kama huyo hanivutii.”—José.

Usimkwamilie mwenzako. Biblia inasema kwamba watu wanapofunga ndoa, wanakuwa “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Katika uhusiano huo, mume na mke hawana uhuru mwingi sana kama walivyokuwa nao walipokuwa waseja; wanajitoa kwa mmoja na mwenzake. (1 Wakorintho 7:32-34) Hata hivyo, ikiwa urafiki wenu ndio unaanza tu, hupaswi kutazamia awajibike au kujiendesha kama mume wako tangu mwanzoni, wala yeye pia hapaswi kuutazamia hivyo kutoka kwako. * Ukweli ni kwamba, ukionyesha kwamba unatambua ana haki ya kuwa na marafiki wengine, huenda ukamvutia hata zaidi. Na kutokana na jinsi anavyotumia uhuru huo, utaonyesha waziwazi yeye ni mtu wa aina gani.—Methali 20:11.

Kile ambacho wavulana husema: “Nafikiri msichana anayenikwamilia ni yule anayetaka kujua kila kitu ninachofanya na hawezi kuwa na marafiki wengine au kupendezwa na mambo mengine isipokuwa mimi.”—Darren.

“Ikiwa msichana ambaye tumejuana karibuni ananitumia ujumbe kila wakati na anataka kujua niko na nani, na majina ya wasichana wowote waliopo, hiyo ni ishara ya hatari.”—Ryan.

“Msichana asiyekuruhusu ufanye mambo na marafiki wako wa kiume na anayekasirika usipomwalika awe pamoja nawe kila wakati, anakutegemea kwa njia yenye kuudhi.”—Adrian.

Una maoni gani kuhusu maelezo ya wavulana ambao wametajwa hapo juu?

․․․․․

Jiheshimu

Huenda unawafahamu wasichana ambao wanaweza kufanya chochote ili kumvutia na kumpendeza mvulana fulani. Huenda wengine wakashusha viwango vyao ili tu wapate rafiki au hata mume. Hata hivyo, kanuni ya ‘unavuna unachopanda’ inatumika katika jambo hili. (Wagalatia 6:7-9) Ikiwa hujiheshimu wala kuheshimu msimamo wako, basi utawavutia wavulana ambao hawakuheshimu wala kuheshimu msimamo wako.

Ukweli ni kwamba, hutapendwa na wavulana wote, na hilo ni jambo zuri! Lakini ikiwa unahangaikia urembo wako wa nje na wa ndani pia, ‘utakuwa na thamani kubwa machoni pa Mungu’—nawe utamvutia mwanamume atakayekufaa zaidi.—1 Petro 3:4.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Namna gani ikiwa wewe ni mvulana na unajiuliza, ‘Kwa nini wasichana hawanipendi?’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 30 Bila shaka, uchumba unapoanza rasmi, wote wawili wanapaswa kuwajibika zaidi kwa mmoja na mwenzake.

ANDIKO MUHIMU

“Uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejiletea sifa.”—Methali 31:30.

PENDEKEZO

Tumia vipodozi kwa kiasi! Ukitumia vipodozi kupita kiasi unaweza kueleweka vibaya—kwamba una majivuno au hata unataka sana kuwavutia wengine.

JE, WAJUA . . . ?

Ikiwa kila mara unadai uangalifu usiogawanyika kutoka kwa mvulana, unaweza kuharibu uhusiano wako pamoja naye.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Sifa ambayo ningependa kujitahidi kuboresha ni ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI

● Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unaheshimu maoni na hisia za mwanamume kijana?

● Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unajiheshimu?

[Blabu katika ukurasa wa 190]

“Ni kweli kwamba mara nyingi ninapokutana na msichana mrembo kwa mara ya kwanza, ninavutiwa naye. Hata hivyo, maoni yangu hubadilika haraka ikiwa msichana huyu hana miradi hususa na inayofaa. Kwa upande mwingine, ikiwa anajua anachotaka maishani—hasa ikiwa amefikia baadhi ya miradi yake—hilo linaweza kufanya avutie sana.”—Damien

[Picha katika ukurasa wa 191]

Upendo na heshima ni kama magurudumu mawili ya baiskeli, yote ni muhimu