Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Wasichana Hawanipendi?

Kwa Nini Wasichana Hawanipendi?

SURA YA 28

Kwa Nini Wasichana Hawanipendi?

Ninamfurahisha kwelikweli. Nimemwambia kila kitu, yaani, kuhusu vitu nilivyo navyo, sehemu ambazo nimetembelea, watu ninaowafahamu. Lazima anatamani sana tuwe wapenzi!

Natamani ardhi ifunguke inimeze! Kwa nini haelewi? Nitafanya nini ili kukomesha mazungumzo haya bila kumuudhi?

UNA umri wa kutosha kuwa na mpenzi. Ungependa kupata mtu anayevutia na aliye na imani ya kidini kama yako. (1 Wakorintho 7:39) Hata hivyo, wakati uliopita, kila ulipojaribu kuanzisha urafiki, uliona kwamba ni kazi bure. Shida ilikuwa nini? Kwani wasichana wanatafuta wavulana wenye sura nzuri tu? “Napenda wavulana wenye misuli,” asema msichana anayeitwa Lisa. Hata hivyo, wasichana wengi wanatafuta mengi zaidi. “Nyakati nyingine wavulana wenye sura nzuri hawana sifa nzuri,” asema Carrie mwenye umri wa miaka 18.

Wasichana wanatafuta sifa gani? Ikiwa unataka kumfahamu msichana vizuri zaidi, ni mambo gani unayopaswa kufikiria? Na unapaswa kufikiria kanuni gani za Biblia?

Mambo Unayopaswa Kufanya Kwanza

Kabla ya kuamua kuanzisha uhusiano na msichana fulani, kuna mambo ya msingi unayohitaji kujua ambayo yatakusaidia kufanya urafiki na mtu yeyote. Fikiria mambo yafuatayo.

Jifunze kuwa na adabu. Biblia inasema kwamba upendo “haukosi kuwa na adabu.” (1 Wakorintho 13:5, Neno—Biblia Takatifu) Ukiwa na adabu unaonyesha kwamba unawaheshimu wengine na kwamba unasitawisha ukomavu kama wa Kristo. Hata hivyo, adabu si kama suti unayovaa ili kuwafurahisha wengine na unayovua unapofika nyumbani. Jiulize, ‘Mimi huwa na adabu ninaposhughulika na watu wa familia yetu?’ Ikiwa hufanyi hivyo, basi itaonekana wazi kwamba unajilazimisha tu unaposhirikiana na wengine. Kumbuka, ili kukufahamu vizuri, msichana mwenye utambuzi atachunguza jinsi unavyowatendea watu wa familia yenu.—Waefeso 6:1, 2.

Kile ambacho wasichana husema: “Mimi huvutiwa na mvulana mwenye adabu hata katika mambo madogo kama vile, kunifungulia mlango, na katika mambo makubwa kama vile, kuwa mwenye fadhili na ufikirio, si kwangu tu bali pia kuelekea watu wa familia yetu.”—Tina.

“Sipendi mtu ambaye tunafahamiana tu na mara moja anaanza kuniuliza maswali ya kibinafsi sana, kama vile ‘Una mpenzi?’ na ‘Una miradi gani?’ Ni kukosa adabu na hunifanya nione haya!”—Kathy.

“Naliona kuwa jambo lisilo la adabu wavulana wanapofikiria kwamba wanaweza kuchezea hisia zetu, kana kwamba hisia zetu hazifai na tunataka watuhurumie kwa sababu tunatamani sana kuolewa.”—Alexis.

Tunza usafi wako. Usafi huonyesha kwamba unajiheshimu na unawaheshimu wengine pia. (Mathayo 7:12) Ukijiheshimu, yaelekea wengine watakuheshimu pia. Kwa upande mwingine, ukipuuza usafi, hutaweza kumvutia msichana.

Kile ambacho wasichana husema: “Mvulana mmoja aliyekuwa anapendezwa nami alikuwa ananuka mdomo sana. Singeweza kuvumilia jambo hilo.”—Kelly.

Jifunze jinsi ya kupashana habari. Kupashana habari ndio msingi wa uhusiano wenye kudumu. Zungumzia, si mapendezi yako tu, bali pia mapendezi ya rafiki yako. (Wafilipi 2:3, 4) Unamsikiliza kwa makini na kuthamini maoni yake.

Kile ambacho wasichana husema: “Mimi hufurahi mvulana anapozungumza nami kwa njia ya kawaida, anapokumbuka mambo niliyomwambia na kuuliza maswali yanayoendeleza mazungumzo.”—Christine.

“Nafikiri wavulana huvutiwa na mambo wanayoona, lakini wasichana huvutiwa zaidi na mambo wanayosikia”—Laura.

“Zawadi ni nzuri. Lakini ikiwa mvulana anaweza kuendeleza mazungumzo, ikiwa anaweza kukufariji na kukutia moyo kwa maneno yake . . . Basi, huyo anavutia.”—Amy.

“Ninamfahamu mvulana fulani ambaye ni mpole na si mwenye kujipendekeza. Tunaweza kuwa na mazungumzo pamoja naye bila kusikia akisema maneno kama vile, ‘Unanukia’ au ‘Leo, unapendeza kweli.’ Yeye anasikiliza ninapozungumza, na hilo linaweza kumpendeza msichana yeyote.”—Beth.

“Bila shaka ningependa kumfahamu vizuri mtu mcheshi lakini ambaye pia anaweza kuzungumza mambo mazito bila kusikika ni kama anajifanya.”—Kelly.

Uwe mwenye kuwajibika. Biblia inasema: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5) Wasichana hawavutiwi na mwanamume ambaye hawezi kufanya kazi kwa sababu ni mvivu au kwa sababu anatumia wakati mwingi katika michezo.

Kile ambacho wasichana husema: “Laiti wavulana fulani wangewajibika zaidi. Haivutii hata kidogo wasipofanya hivyo. Haipendezi kamwe.”—Carrie.

“Wavulana wengine hawana miradi iliyo wazi. Wanapopendezwa na msichana, wanamuuliza kuhusu miradi yake kisha wanasema, ‘Hiyo ndiyo miradi yangu pia!’ Lakini matendo yao yanaonyesha kinyume.”—Beth.

Kuwa mwenye kuwajibika kama inavyoonyeshwa hapo juu, kutakusaidia kuwa na marafiki wazuri. Hata hivyo, ukiona kwamba uko tayari kuanzisha uhusiano wa karibu na msichana fulani, unapaswa kufanya nini?

Hatua Inayofuata

Chukua hatua ya kwanza. Ikiwa unafikiri kwamba rafiki anayekuvutia anaweza kuwa mwenzi mzuri wa ndoa, mwambie unapendezwa naye. Eleza hisia zako waziwazi na moja kwa moja. Ni kweli kwamba si rahisi kufanya hivyo. Unaogopa kukataliwa. Lakini unapochukua hatua ya kwanza unaonyesha kwamba umekomaa. Hata hivyo, kuna onyo: Huo si uchumba. Kwa hiyo, tumia utambuzi. Ukizungumza kwa undani na kwa uzito sana, huenda msichana akakuogopa badala ya kuvutiwa nawe.

Kile ambacho wasichana husema: “Siwezi kusoma mioyo. Kwa hiyo, ikiwa mtu anataka kunifahamu vizuri, anapaswa kuwa mnyoofu na kuniambia waziwazi.”—Nina.

“Huenda hilo likawa badiliko lisilo la kawaida hasa ikiwa mmekuwa marafiki kwa muda. Hata hivyo, nitamheshimu rafiki ikiwa ataniambia kwamba angependa tuwe na uhusiano wa karibu zaidi.”—Helen.

Heshimu uamuzi wa msichana. Namna gani rafiki yako akisema kwamba hataki kuwa na uhusiano wa karibu zaidi nawe? Onyesha kwamba unamheshimu kwa kuamini kuwa anajielewa na anaposema hapana anamaanisha hivyo. Utaonyesha kwamba hujakomaa ukiendelea kusisitiza. Ikiwa utapuuza jibu lililo wazi la msichana, hata kukasirika kwa sababu amekukataa, je, kweli unafikiria masilahi yake au yako mwenyewe?—1 Wakorintho 13:11.

Kile ambacho wasichana husema: “Mimi huchukizwa sana ninapomwambia mvulana waziwazi kwamba sitaki uhusiano naye lakini anaendelea kujaribu.”—Colleen.

“Nilimwambia mvulana mmoja kuwa sipendezwi naye lakini akaendelea kusisitiza eti nimpe namba yangu ya simu. Sikutaka kumuudhi. Isitoshe, inaelekea haikuwa rahisi kwake kupata ujasiri wa kunieleza hisia zake. Hata hivyo, mwishowe nililazimika kuzungumza naye kwa uthabiti zaidi.”—Sarah.

Mambo Hupaswi Kufanya

Vijana fulani hufikiri kwamba ni rahisi kuwavutia wasichana. Huenda hata wakajaribu kushindana na marafiki wao kuona ni nani anayeweza kuwa na wasichana wengi zaidi. Hata hivyo, mashindano ya aina hiyo ni mabaya na yanafanya uwe na sifa mbaya. (Methali 20:11) Unaweza kuepuka hali hiyo ukikumbuka mambo yafuatayo.

Usichezee hisia za wengine. Mtu anayechezea hisia za wengine anatumia maneno matamu na ishara za mwili zinazoamsha hamu ya ngono. Hana nia ya kuwa na uhusiano wa kimapenzi unaoheshimika. Matendo na mtazamo kama huo unapuuza shauri la Biblia la kuwatendea “wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.” (1 Timotheo 5:2) Watu wanaochezea hisia za wengine huwa marafiki wabaya na wenzi wa ndoa wasiofaa. Wasichana wenye utambuzi wanajua jambo hilo.

Kile ambacho wasichana husema: “Nafikiri haivutii mtu anapokuambia maneno matamu lakini unajua kwamba alimwambia rafiki yako maneno hayohayo mwezi uliopita.”—Helen.

“Kijana mmoja mwenye kuvutia alianza kuchezea hisia zangu, akizungumza hasa kujihusu. Msichana mwingine alipokuja, akafanya vivyo hivyo. Kisha msichana mwingine akaja na akaanza kutumia maneno yaleyale tena. Haikuvutia hata kidogo!”—Tina.

Usichezee hisia za msichana. Usitazamie kwamba urafiki na mtu wa jinsia tofauti utakuwa sawa na urafiki na mtu wa jinsia yako. Kwa nini? Fikiria hili: Ukimwambia rafiki yako wa kiume kwamba anapendeza akiwa amevalia suti yake mpya au ikiwa wewe huzungumza naye kwa ukawaida na kumwambia mambo ya siri, haielekei kwamba atafikiri unavutiwa naye kimapenzi. Lakini ukimwambia msichana kwamba anapendeza au ikiwa wewe unazungumza naye kwa ukawaida na kumwambia mambo ya siri, huenda akafikiri kwamba unapendezwa naye.

Kile ambacho wasichana husema: “Sidhani wavulana wanaelewa kwamba hawawezi kuwatendea wasichana kama vile wanavyowatendea marafiki wao wa kiume.”—Sheryl.

“Mvulana atapata namba yangu ya simu, kisha anitumie ujumbe. Akiwa na kusudi gani? Nyakati nyingine mnaweza kuwa marafiki kupitia kuwasiliana kwa ujumbe mfupi wa simu na huenda mkaanzisha uhusiano wa kimapenzi, hata hivyo, huwezi kusema mengi kupitia ujumbe huo.”—Mallory.

“Sidhani wavulana wanaelewa jinsi ilivyo rahisi kwa msichana kuvutiwa kihisia, hasa ikiwa mvulana anajali na ni rahisi kuzungumza naye. Si kwamba msichana anataka sana kuwa na uhusiano wa karibu. Nafikiri wasichana wengi hutaka kumpenda mtu fulani nao hutafuta mtu anayewafaa zaidi.”—Alison.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 3

KATIKA SURA INAYOFUATA

Kuna tofauti gani kati ya upendo halisi na upendo wa kupumbazika?

ANDIKO MUHIMU

‘Vaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’—Waefeso 4:24.

PENDEKEZO

Waulize watu fulani wakomavu kuhusu ustadi ambao wanafikiri ni muhimu sana kijana mwanamume kusitawisha, na uone ikiwa unahitaji kufanyia kazi ustadi huo.

JE, WAJUA . . . ?

Jinsi ulivyo kwa ndani ni muhimu zaidi kuliko jinsi ulivyo kwa nje.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Sehemu moja ninayoweza kuwa mwenye adabu zaidi ni ․․․․․

Ili niboreshe ustadi wangu wa kuzungumza, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unajiheshimu?

● Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unaheshimu maoni na hisia za msichana?

[Blabu katika ukurasa wa 198]

“Wavulana wanafikiri kwamba ili wawavutie wasichana, lazima wavalie kwa njia fulani au wawe na sura fulani. Ingawa ni kweli kwa kiasi fulani, nafikiri wasichana wengi wanavutiwa zaidi na sifa nzuri.”—Kate

[Picha katika ukurasa wa 197]

Adabu si kama suti unayovaa ili kuwafurahisha wengine na unayovua unapofika nyumbani