Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini Urafiki Ukivunjika?

Nifanye Nini Urafiki Ukivunjika?

SURA YA 31

Nifanye Nini Urafiki Ukivunjika?

“Tulikuwa na urafiki wa kimapenzi kwa miezi sita na kabla ya wakati huo tulikuwa marafiki tu kwa miaka mitano. Alipotaka kuvunja urafiki wetu, hata hakutaka kuniambia. Aliacha tu kuzungumza nami. Nilijihisi hoi. Nilivunjika moyo sana. Mara nyingi nilijiuliza, ‘Nilikosea wapi?’”—Rachel.

SHANGWE yako yote inaweza kugeuka kuwa huzuni urafiki unapovunjika. Fikiria Jeff na Susan, waliokuwa na urafiki wa kimapenzi kwa miaka miwili. Kwa muda huo, upendo wao uliimarika. Siku nzima, Jeff alimtumia Susan jumbe fupi zenye maneno matamu ya kimapenzi. Mara kwa mara, Jeff alimpa zawadi kumwonyesha kwamba bado anamfikiria. “Jeff alijitahidi sana kunisikiliza na kunielewa,” Susan anasema. “Alinifanya nijione kuwa mtu wa pekee.”

Baada ya muda, Jeff na Susan walikuwa wakizungumza kuhusu ndoa na mahali watakapoishi baada ya hapo. Jeff hata alionyesha kwamba anataka kumposa Susan. Kisha, kwa ghafula, Jeff akavunja urafiki huo! Susan alivunjika moyo sana. Ingawa aliendelea na shughuli za kawaida za maisha, ni kana kwamba alikuwa amekufa ganzi. “Nilichoka kiakili na kimwili,” anasema. *

Kinachosababisha Maumivu

Iwapo umewahi kuwa katika hali kama ya Susan, huenda ukajiuliza, ‘Nitawahi kuishi maisha ya kawaida tena?’ Huzuni yako inaeleweka. Mfalme Sulemani aliandika: “Upendo una nguvu kama kifo.” (Wimbo wa Sulemani 8:6) Kwa hiyo, huenda kuvunjika kwa urafiki ndilo jambo lenye kuvunja moyo sana ambalo umewahi kupambana nalo. Kwa kweli, watu fulani wamesema kwamba ni kama sehemu fulani ya mwili wako inakufa urafiki unapovunjika. Huenda hata ukapitia mambo haya na labda mengine mengi ambayo humpata mtu aliyefiwa:

Kutoamini. ‘Haiwezekani. Atabadili maoni yake baada ya siku moja au mbili.’

Hasira. ‘Kwa nini amenifanyia hivi? Sitaki kumwona hata kidogo!’

Kushuka moyo. ‘Sipendeki. Hakuna mtu atakayenipenda tena.’

Kukubali. ‘Mambo yatakuwa sawa. Nimeumia kutokana na kuvunjika kwa urafiki wetu, lakini ninapata nafuu.’

Habari njema ni kwamba, unaweza kufikia hatua ya kukubali hali. Muda ambao utachukua kufikia hatua hiyo unategemea mambo kadhaa, kutia ndani muda ambao mmekuwa marafiki na hatua mliyokuwa mmefikia. Kwa sasa, unaweza kupambana jinsi gani na kuvunjika moyo?

Kuendelea na Maisha Yako

Huenda umesikia watu wakisema kwamba kadiri muda unavyopita ndivyo majeraha yanavyopona. Urafiki wenu unapovunjika, huenda maneno hayo yasikufariji. Hiyo ni kwa sababu muda ni sehemu tu ya suluhisho. Kwa mfano: Unapokatwa, jeraha linapona baada ya muda, lakini kwa sasa linauma. Unahitaji kuzuia damu isivuje na kutuliza maumivu. Pia, unahitaji kuzuia kidonda hicho kisiambukizwe. Ndivyo na jeraha la kihisia. Kwa sasa, linauma. Lakini unaweza kuchukua hatua fulani ili kupunguza maumivu na kuzuia usiambukizwe na kinyongo. Muda utatimiza sehemu yake, hata hiyo, unaweza kutimiza sehemu yako jinsi gani? Jaribu kufanya mambo yafuatayo.

Usiogope kuomboleza. Hakuna ubaya wowote kulia. Isitoshe, Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kulia” na hata “wakati wa kuomboleza.” (Mhubiri 3:1, 4) Kulia hakumaanishi wewe ni dhaifu. Alipokuwa na maumivu makali ya kihisia, hata Daudi aliyekuwa shujaa wa vita, wakati mmoja alisema: “Kila usiku nalowesha kitanda changu kwa machozi; kwa kulia kwangu naulowesha mto wangu.”—Zaburi 6:6, Biblia Habari Njema.

Tunza afya yako. Kufanya mazoezi na kula vizuri kutasaidia kurudisha nguvu ulizopoteza kwa sababu ya maumivu ya kuvunjika kwa urafiki. Biblia inasema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida.”—1 Timotheo 4:8.

Unahitaji kukazia fikira mambo gani kuhusiana na afya yako?

․․․․․

Kuwa na shughuli nyingi. Usiache kufanya mambo unayopenda. Na usijitenge kamwe. (Methali 18:1) Kushirikiana na watu wanaokujali kutakusaidia kukazia fikira mambo yanayofaa.

Unaweza kujiwekea miradi gani?

․․․․․

Mweleze Mungu hisia zako katika sala. Huenda hilo lisiwe rahisi. Baada ya urafiki kuvunjika, watu fulani hata huona kuwa Mungu amewaacha. Wanasema, ‘Nilisali sana kwamba nipate mtu anayenifaa, na sasa ona mambo ambayo yamenipata!’ (Zaburi 10:1) Hata hivyo, je, itakuwa sawa kumwona Mungu kama anayewatafutia watu wachumba? Bila shaka hapana; wala hawezi kulaumiwa mtu fulani anapokataa kuendeleza urafiki. Tunajua jambo hili kumhusu Yehova: ‘Anakujali wewe.’ (1 Petro 5:7) Kwa hiyo, mmiminie hisia zako katika sala. Biblia inasema: “Maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

Ni mambo gani hasa unayoweza kumwambia Yehova katika sala huku ukijitahidi kupambana na maumivu ya kuvunjika kwa urafiki?

․․․․․

Kufikiria Wakati Ujao

Baada ya kupona, huenda ikafaa kufikiria kilichotokea katika urafiki wenu. Unapokuwa tayari kufanya hivyo, huenda ukapata msaada kwa kuandika majibu ya maswali katika sanduku lenye kichwa “ Ninaweza Kujifunza Nini Kutokana na Kuvunjika kwa Urafiki?” kwenye ukurasa wa 224.

Ni kweli kwamba, urafiki uliokuwa nao haukufaulu kama ulivyotarajia. Lakini kumbuka: Kunapokuwa na dhoruba, ni rahisi kukazia fikira mawingu mazito na mvua inayonyesha. Hata hivyo, mwishowe mvua inaacha kunyesha na mawingu yanakuwa mangavu. Vijana waliotangulia kutajwa katika sura hii walitambua kwamba baada ya muda, wangeweza kuendelea na maisha yao. Uwe na hakika kwamba inaweza kuwa hivyo kwako pia!

KATIKA SURA INAYOFUATA

Unaweza kuchukua hatua gani ili kujilinda na washambuliaji wa kingono?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ingawa wanaozungumziwa katika sura hii ni wanawake, kanuni zinazozungumziwa zinawahusu wanaume pia.

ANDIKO MUHIMU

“[Yehova] anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.”—Zaburi 147:3.

PENDEKEZO

Susan, aliyetajwa mwanzoni mwa sura hii, aliandika orodha ya maandiko na kuyahifadhi ili ayasome wakati anapohisi kulemewa na hisia. Wewe pia unaweza kuandika orodha ya baadhi ya maandiko yaliyoonyeshwa katika sura hii.

JE, WAJUA . . . ?

Mara nyingi, matineja wenye urafiki wa kimapenzi hawaishii kufunga ndoa, na wale wanaofunga, nyingi zinavunjika.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ili niweze kurudia hali yangu ya kawaida baada ya urafiki wetu kuvunjika, nita ․․․․․

Mambo ninayoweza kufanyia kazi ili kuwa mwenzi bora katika uhusiano wangu wa wakati ujao ni ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Umejifunza nini kujihusu kutokana na urafiki wako wa wakati uliopita?

● Umejifunza nini kuhusu watu wa jinsia tofauti?

[Blabu katika ukurasa wa 227]

“Muda unakusaidia kuwa na mtazamo bora. Baadaye, utatulia, na labda hata kuamua kusahau kilichotokea. Pia, utapata kujielewa na kuelewa sifa ambazo ungependa mwenzi wa ndoa awe nazo, vilevile mambo unayopaswa kuepuka ili usije ukajipata katika hali kama hiyo wakati ujao.”—Corrina

[Sanduku katika ukurasa wa 224]

 Ukurasa wa Mazoezo

Ninaweza Kujifunza Nini Kutokana na Kuvunjika kwa Urafiki?

Je, uliambiwa sababu ya kuvunja urafiki wenu? Ikiwa uliambiwa, andika sababu hiyo hapa chini, iwe unaona ilifaa au haikufaa. ․․․․․

Unafikiri huenda kulikuwa na sababu gani nyingine? ․․․․․

Unapofikiria mambo yalivyokuwa, kuna lolote ambalo ungefanya ili urafiki wenu usivunjike? Ikiwa ndiyo, ungefanya nini? ․․․․․

Kuvunjika kwa urafiki huo kumekusaidia kuona mambo ambayo ungependa kufanyia kazi ili ukomae kiroho na kihisia? ․․․․․

Ukianzisha urafiki na mtu mwingine, ni jambo gani utakalofanya tofauti na ulivyofanya wakati uliopita? ․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 223]

Kuvunjika kwa urafiki ni kama jeraha lenye maumivu makali, linauma, lakini baada ya muda litapona