Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nitajua Jinsi Gani Kama Ni Upendo Halisi?

Nitajua Jinsi Gani Kama Ni Upendo Halisi?

SURA YA 29

Nitajua Jinsi Gani Kama Ni Upendo Halisi?

Jibu maswali yafuatayo:

1. Unaweza kufafanua “upendo halisi” jinsi gani? ․․․․․

2. Unaweza kufafanua “upendo wa kupumbazika” jinsi gani? ․․․․․

3. Kwa maoni yako, kuna tofauti gani kati ya taarifa hizo mbili? ․․․․․

YAELEKEA hukuwa na shida kujibu maswali yaliyo juu. Isitoshe, ni rahisi kuona tofauti kati ya upendo halisi na upendo wa kupumbazika kwa kufikiria tu.

Hata hivyo, yote hayo yanaweza kubadilika mara tu unapokutana na mvulana au msichana unayefikiri anakufaa. Ghafula unajipata umenaswa, na huwezi kufikiria jambo lingine lolote. Unampenda sana. Au sivyo? Je, ni upendo halisi—au ni upendo wa kupumbazika? Utajua jinsi gani? Ili kujibu, kwanza tuone jinsi ambavyo huenda maoni yako kuelekea watu wa jinsia tofauti yamebadilika katika miaka ya karibuni. Kwa mfano, fikiria maswali yafuatayo:

● Ulipokuwa na umri wa miaka mitano, ulikuwa na maoni gani kuelekea watu wa jinsia tofauti?

● Una maoni gani kuelekea watu wa jinsia tofauti sasa?

Inaelekea majibu yako yanaonyesha kwamba ulipofikia umri wa kubalehe, ulianza kuwa na maoni tofauti kuelekea watu wa jinsia tofauti. “Nimeanza kuona wasichana kuwa warembo zaidi,” asema Brian, mwenye umri wa miaka 12. Elaine, mwenye umri wa miaka 16 anakumbuka jambo lililotokea miaka michache iliyopita. Anasema: “Wasichana marafiki wangu walianza kuzungumza kuhusu wavulana, nami nikaanza kuvutiwa kipumbavu na kila mvulana.”

Kwa kuwa sasa umeanza kupendezwa na watu wa jinsia tofauti, unaweza kupambana jinsi gani na hisia hizo zenye nguvu? Badala ya kujifanya kuwa huna hisia hizo—jambo linaloweza kuziongeza—unaweza kutumia kipindi hicho kujifunza jambo fulani kuhusu kuvutiwa na mtu, upendo wa kupumbazika, na upendo halisi. Kuelewa mambo hayo matatu ya kimahaba kutakuepusha na maumivu ya moyo na kukusaidia baadaye kupata mtu unayempenda kikweli.

KINACHOKUVUTIA Kile unachoona

“Nyakati zote mimi na marafiki wangu huzungumza kuhusu wasichana. Sisi hujaribu kuzungumzia mambo mengine, lakini mara tu msichana mrembo anapopita, tunasahau tulichokuwa tukizungumzia!”—Alex.

“Mimi huvutiwa na mwanamume kijana anayenitazama, anayetabasamu vizuri, na kutembea kwa kujiamini.”—Laurie.

Ni kawaida kuvutiwa na mtu mwenye sura nzuri. Tatizo ni kwamba, sura ya nje haisemi mengi kumhusu mtu mwenyewe. Kwa nini? Kwa sababu sura inaweza kudanganya. Biblia inasema: “Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, ndivyo alivyo mwanamke mwenye umbo la kupendeza lakini anayegeuka na kuacha kuwa na akili.” (Methali 11:22) Bila shaka, kanuni hiyo inawahusu wavulana pia.

UPENDO WA KUPUMBAZIKA Kile unachohisi

“Nilivutiwa sana na mvulana fulani nilipokuwa na umri wa miaka 12, na niliposhinda tatizo hilo, nikatambua kilichofanya nimpende. Ni kwa sababu tu marafiki wangu wote walikuwa wanapendezwa na wavulana—naye alikuwa mvulana. Hivyo tu!”—Elaine.

“Nimevutiwa na wasichana wengi, lakini mara nyingi, nilikuwa nikitazama sura ya nje tu. Nilipopata kujua jinsi mtu alivyo kwa ndani, nilitambua kwamba hatufaani kama nilivyofikiri.”—Mark.

Upendo wa kupumbazika huonekana kama upendo halisi. Kwa kweli, upendo huhusisha hisia za kimahaba. Lakini msingi wa kila moja ya hisia hizo ni tofauti. Upendo wa kupumbazika unategemea sifa za kijuujuu tu. Pia, upendo huo hauoni udhaifu wa mtu nao hutilia chumvi sifa za mtu huyo. Kwa hiyo, upendo wa kupumbazika hauna msingi, ni kama nyumba ya mchanga. “Haudumu,” asema msichana anayeitwa Fiona. “Leo, unavutiwa na mtu fulani, mwezi ujao, ni mtu mwingine tofauti!”

UPENDO Kile unachojua

“Nafikiri ukiwa na upendo halisi, una sababu ya kuvutiwa na mtu fulani, nayo ni sababu nzuri, si ya kibinafsi.”—David.

“Mimi naona kwamba upendo halisi unapaswa kuchukua muda kukua. Mnaanza kwa kuwa marafiki wazuri. Kisha, pole kwa pole, baada ya kumfahamu vizuri, unaanza kusitawisha hisia ambazo hujawahi kuwa nazo.”—Judith.

Upendo unategemea kujua vizuri sifa na udhaifu wa mtu. Haishangazi basi kwamba Biblia inafafanua upendo kuwa zaidi ya hisia tu. Inasema kwamba kati ya mambo mengine, upendo ni “wenye ustahimilivu na wenye fadhili. . . . Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.” (1 Wakorintho 13:4, 7, 8) Upendo humfanya mtu atende hivyo kulingana na ujuzi bali si kwa sababu ya kukosa ujuzi au kuwa mjinga.

Mfano wa Upendo Halisi

Masimulizi ya Biblia kuhusu Yakobo na Raheli yanaonyesha waziwazi upendo halisi. Walikutana kwenye kisima, ambapo Raheli alikuwa ameenda kuwanywesha maji kondoo wa baba yake. Mara moja Yakobo akavutiwa naye. Kwa nini? Kwanza, alikuwa “na umbo zuri na sura nzuri.”—Mwanzo 29:17.

Hata hivyo, kumbuka kwamba upendo halisi hautegemei sura ya nje tu. Mbali na sura nzuri, Yakobo alitambua mengi kumhusu Raheli. Biblia inasema kwamba baada ya muda, Yakobo hakuvutiwa tu naye. “Alimpenda Raheli.”—Mwanzo 29:18.

Huo ulikuwa mwisho wa hadithi ya kimahaba? Hapana—kwa kuwa hadithi hiyo haikuishia hapo. Baba ya Raheli alimwomba Yakobo asubiri miaka saba kabla ya kumuoa Raheli. Iwe ilikuwa haki au si haki, upendo wa Yakobo ulitahiniwa. Kama ungekuwa upendo wa kupumbazika tu, Yakobo hangemngojea. Ni upendo halisi tu unaoweza kuvumilia. Ikawa namna gani? Biblia inasema: “Yakobo akatumikia miaka saba kwa ajili ya Raheli, lakini machoni pake hiyo ikawa kama siku chache kwa sababu alimpenda.”—Mwanzo 29:20.

Unaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yakobo na Raheli? Kwamba upendo halisi unaweza kuvumilia. Pia, hautegemei tu sura ya nje. Kwa kweli, mtu atakayekuwa mwenzi wako wa ndoa huenda asiwe mwenye kuvutia sana unapomwona kwa mara ya kwanza. Kwa mfano, Barbara, alifahamiana na kijana mmoja ambaye Barbara hakuvutiwa sana naye mwanzoni. Anasema: “Lakini nilipopata kumjua vizuri, mambo yakabadilika. Niliona jinsi Stephen anavyowahangaikia watu na jinsi nyakati zote anavyotanguliza masilahi ya wengine. Hizo ni sifa ambazo nilijua mume mzuri anapaswa kuwa nazo. Nikavutiwa na nikaanza kumpenda.” Matokeo yakawa, ndoa yenye msingi mzuri.

Ukiwa mtu mzima anayeweza kuwa na urafiki wa kimapenzi, ukiwa na lengo la kufunga ndoa, utajua jinsi gani kwamba umempata mtu unayempenda kikweli? Moyo wako unaweza kukuongoza, lakini tegemea kanuni za Biblia. Usitegemee sura ya nje tu. Chukua muda kusitawisha uhusiano huo. Kumbuka, upendo wa kupumbazika hufifia baada ya muda mfupi. Upendo wa kweli huimarika kadiri wakati unavyopita na kuwa “kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:14.

Uwe na hakika kwamba unaweza kupata upendo wa aina hiyo, ikiwa utajifunza mengi zaidi ya mambo unayoona na kuhisi. Kurasa tatu zinazofuata zitakusaidia kufanya hivyo.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 1 NA 3

KATIKA SURA INAYOFUATA

Tuseme unampenda mtu fulani kikweli na si upendo wa kupumbazika, unaweza kujua namna gani ikiwa uko tayari kufunga ndoa?

ANDIKO MUHIMU

“Maji mengi hayawezi kuuzima upendo, wala mito haiwezi kuufagilia mbali.”—Wimbo wa Sulemani 8:7.

PENDEKEZO

Ili kujua kama unamfahamu vizuri mtu ambaye unavutiwa naye, jibu maswali yaliyo kwenye chati katika Buku la 2, ukurasa wa 39 (kwa wasichana) na ukurasa wa 40 (kwa wavulana).

JE WAJUA . . . ?

Kwa njia fulani, vijana ambao huingia na kutoka katika uhusiano wa kimapenzi bila kufikiri, “wanajizoeza” kuwataliki wenzi wao baada ya kufunga ndoa.

HATUA ZA KUCHUKUA

Ili kupata msaada wa kutambua ikiwa hisia zangu kumwelekea mtu fulani ni ishara ya upendo wa kupumbazika au ni upendo halisi, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na hisia zenye nguvu sana kuwaelekea watu wa jinsia tofauti?

● Kwa nini mahusiano mengi ya “kimapenzi” kati ya vijana hayafanikiwi?

[Blabu katika ukurasa wa 207]

“Upendo unaweza kushinda vizuizi, lakini upendo wa kupumbazika huisha mara tu mambo yanapobadilika au matatizo yanapotokea. Inachukua muda mwingi kukuza upendo halisi.”—Daniella

[Sanduku katika ukurasa wa 209]

Ukurasa wa Mazoezi

Ungefanya Nini?

Michael na Judy wamekuwa marafiki kwa miezi mitatu, na Judy anasema “anampenda sana.” Michael pia anampenda Judy sana na hata humwambia jinsi anavyopaswa kuvalia, watu anaopaswa kushirikiana nao, na wale hapaswi kushirikiana nao. Alimtendea kama binti ya mfalme, mpaka mambo yalipobadilika juma lililopita. Michael alimpiga kofi Judy “alipompata” akizungumza na mvulana mwingine.

Michael anasema: “Judy anapaswa kujua kwamba naogopa kumpoteza. Wazo lenyewe la mvulana mwingine kuchukua mpenzi wangu linanikasirisha! Nasikitika kwamba nilimpiga kofi Judy. Lakini nilifanya hivyo kwa sababu siwezi kuvumilia kumwona hata akimtazama mtu mwingine. Isitoshe, nilimwomba msamaha!”

Judy anasema: “Wazazi wangu wanasema kwamba Mike ananiongoza, lakini ni kanuni tu anazo za juu. Yaani, hajawahi kujaribu kunilazimisha tufanye ngono. Na aliponipiga kofi—jambo ambalo sikuwaambia wazazi wangu—ni kwa sababu nilikuwa nikizungumza na mvulana mwingine. Mike huona wivu, jambo ambalo nyakati nyingine naona linafaa. Hata hivyo, aliomba msamaha na kuahidi kuwa hatafanya hivyo tena.”

Maoni yako: Unaona hatari yoyote katika uhusiano huo? Ikiwa unaona, ni hatari gani? ․․․․․

Judy anapaswa kufanya nini? ․․․․․

Ungefanya nini? ․․․․․

[Sanduku katika ukurasa wa 210]

Ukurasa wa Mazoezi

Ungefanya Nini?

Ethan na Alyssa wamekuwa na urafiki wa kimapenzi kwa miezi miwili, naye Ethan ameona jinsi Alyssa alivyo mwenye ugomvi, hasa akiwa na wazazi wake. Alyssa hubishana na wazazi wake kila mara, na nyakati zote yeye anashinda. Ana “ujuzi” sana katika kushikilia maoni yake mpaka wazazi wake wanachoka na kuachana naye. Alyssa hata amewahi kujigamba mbele ya Ethan kwamba “amewatia wazazi wake mfukoni,” hawawezi kumwambia lolote.

Ethan anasema: “Alyssa husema yaliyo moyoni. Hamtii yeyote, hata wazazi wake. Baba yake anaweza kuudhi, na ndio sababu Alyssa hupandwa na hasira. Lakini hapigi kelele tu. Alyssa anaweza kulia, kununa, au kujifanya mzuri sana—atafanya chochote ili apate anachotaka kutoka kwa Baba na Mama.”

Alyssa anasema: “Sijali wewe ni nani au una cheo au mamlaka gani, nitazungumza nawe moja kwa moja wala sijaribu kubadili njia yangu ya kuzungumza eti ili kuepuka ugomvi. Mpenzi wangu, Ethan, anajua hivyo. Ameniona nikiwa na wazazi wangu.”

Maoni yako: Unaona hatari yoyote katika uhusiano huo? Ikiwa unaona, ni hatari gani? ․․․․․

Ethan anapaswa kufanya nini? ․․․․․

Ungefanya nini? ․․․․․

[Sanduku katika ukurasa wa 211]

Ukurasa wa Mazoezi

Ni Upendo Halisi au Ni Upendo wa Kupumbazika?

Katika taarifa zilizonukuliwa hapa chini, andika aina ya upendo inayozungumziwa ikiwa ni upendo halisi au ni upendo wa kupumbazika.

1. “․․․․․ ni upofu na hupenda kubaki hivyo. Haupendi kuona uhalisi wa mambo.”—Calvin.

2. “Ikiwa nahitaji kubadili utu wangu ninapokuwa na msichana ninayevutiwa naye, basi huo ni ․․․․․.”—Thomas.

3. “Huenda jambo fulani kumhusu mtu huyo likakuudhi. Lakini ikiwa ni ․․․․․, bado utataka kuwa pamoja naye na kutatua tatizo hilo.”—Ryan.

4. “Ikiwa ni ․․․․․, mambo pekee unayofikiria ni yale yanayowahusu ninyi wawili.”—Claudia.

5. “Ikiwa ni ․․․․․, hutajaribu kuficha utu wako.”—Eve.

6. “․․․․․ ni ubinafsi wa kutaka kupata kile unachotaka, kama vile tu kudai kwamba una mpenzi.” —Allison.

7. “․․․․․ hutambua makosa na utu wa yule mtu mwingine na bado unaweza kuvumilia mambo hayo.”—April.

8. “Ikiwa ni ․․․․․, huwezi kueleza ni nini hasa kinachokuvutia, unavutiwa tu.”—David.

9. “Ikiwa ni ․․․․․, yule mtu mwingine hawezi kukosea.”—Chelsea.

10. “Ikiwa ni ․․․․․, huvutiwi na watu wengine wa jinsia tofauti kama ilivyokuwa zamani, kwa sababu ya uaminifu wako kwake.”—Daniel.

Majibu: Upendo wa kupumbazika: 1, 2, 4, 6, 8, 9. Upendo halisi: 3, 5, 7, 10.

[Picha katika ukurasa wa 206, 207]

Upendo wa kupumbazika hauna msingi, ni kama nyumba ya mchanga, baada ya muda mfupi inafagiliwa mbali