Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nahitaji Kujua Nini Kuhusu Uvutaji wa Sigara?

Nahitaji Kujua Nini Kuhusu Uvutaji wa Sigara?

SURA YA 33

Nahitaji Kujua Nini Kuhusu Uvutaji wa Sigara?

Tazama mambo yafuatayo, kisha utie alama ya ✔ katika kisanduku kilicho kando ya kila jambo ambalo unaona linaeleza jinsi ulivyo.

□ Mimi ni mdadisi

□ Ninapambana na mkazo

□ Nataka kukubaliwa na wengine

□ Ninahangaikia uzito wangu

IKIWA umetia alama yoyote ya masanduku katika ukurasa wa 237, basi una maoni sawa na vijana wa rika lako wanaovuta tumbaku au wanaofikiria kufanya hivyo. * Kwa mfano:

Udadisi. “Nilitaka kujua jinsi mtu anavyosikia anapovuta sigara, kwa hiyo nikachukua sigara niliyopewa na msichana fulani shuleni, kisha nikaondoka kisirisiri na kuivuta.”—Tracy.

Kupambana na mkazo na kutaka kukubaliwa. “Wanafunzi shuleni wangesema ‘Nahitaji sigara,’ kisha baadaye wangevuta pumzi na kusema, ‘Sasa nimetulia!’ Mimi pia nilipokuwa katika hali ngumu, nilihitaji kitulizo.”—Nikki.

Kupunguza uzito. “Wasichana fulani wanavuta sigara ili wasiongeze uzito—ni rahisi zaidi kuliko kujinyima chakula!”—Samantha.

Hata hivyo, kabla ya kuwasha sigara ya kwanza au nyingine, tua kidogo, ufikiri. Usiwe kama samaki anayejaribu kumeza ndoana yenye chambo. Ni kweli kwamba huenda samaki huyo akapata chakula kidogo, lakini matokeo? Badala yake, fuata mashauri ya Biblia, na utumie ‘uwezo wako mzuri wa kufikiri.’ (2 Petro 3:1) Jibu maswali yafuatayo.

Unajua Nini Kuhusu Uvutaji wa Sigara?

Tia alama taarifa hizi ikiwa ni kweli au si kweli.

a. Kuvuta sigara kutapunguza mikazo yangu.

□ Kweli □ Si kweli

b. Baada ya kuvuta moshi wote hutoka nje.

□ Kweli □ Si kweli

c. Kuvuta sigara hakuathiri afya yangu mpaka nitakapokuwa na umri mkubwa zaidi.

□ Kweli □ Si kweli

d. Kuvuta sigara kutafanya niwavutie zaidi watu wa jinsia tofauti.

□ Kweli □ Si kweli

e. Nikivuta sigara hakuna anayeumia ila mimi.

□ Kweli □ Si kweli

f. Mungu hajali iwe ninavuta sigara au hapana.

□ Kweli □ Si kweli

Majibu

a. Si kweli. Ingawa kuvuta sigara hupunguza kwa muda mkazo unaotokana na kuacha kuvuta, wanasayansi wamegundua kwamba nikotini huongeza kiwango cha homoni za mkazo.

b. Si kweli. Uchunguzi fulani unaonyesha kwamba zaidi ya asilimia 80 ya chembe za moshi unaopumua hubaki mwilini.

c. Si kweli. Ijapokuwa kila sigara unayovuta huzidisha madhara yanayoweza kutokea, madhara fulani hutokea tangu mwanzo. Watu fulani wanakuza mazoea ya kuvuta sigara baada ya kuvuta sigara moja tu. Kiasi cha hewa inayoingia ndani ya mapafu yako itapungua, na inaelekea utakuwa ukikohoa kila wakati. Ngozi yako itapata makunyanzi mapema maishani. Kuvuta sigara huongeza uwezekano wa matatizo ya viungo vya uzazi, hofu za ghafula, na kushuka moyo.

d. Si kweli. Kulingana na utafiti wa Lloyd Johnston, matineja ambao wanavuta sigara “hawavutii sana vijana wa jinsia tofauti.”

e. Si kweli. Moshi wa sigara unaua maelfu ya watu wasiovuta sigara kila mwaka; utaumiza familia yako, marafiki wako, na hata wanyama wa nyumbani.

f. Si kweli. Wanaotaka kumfurahisha Mungu lazima wajisafishe wenyewe “kila unajisi wa mwili.” (2 Wakorintho 7:1) Ni wazi kwamba kuvuta sigara kunachafua mwili. Ukiamua kuwa mchafu, ukijiumiza na kuwaumiza wengine kwa kutumia tumbaku, huwezi kuwa rafiki ya Mungu.—Mathayo 22:39; Wagalatia 5:19-21.

Jinsi ya Kupinga

Utafanya nini mtu akikupa sigara? Unaweza tu kusema hivi kwa uthabiti, “Pole, mimi sivuti sigara.” Mtu huyo akisisitiza au hata kukudhihaki, kumbuka kwamba huo ni uamuzi wako. Unaweza kusema:

● “Nilifanya uchunguzi kuhusu madhara yanayotokana na kuvuta sigara, na nikaamua sitavuta.”

● “Nina miradi kadhaa muhimu ya wakati ujao inayotia ndani kupumua.”

● “Kwani sina uhuru wa kujifanyia uamuzi?”

Kama vijana waliotangulia kutajwa katika sura hii, huenda ukatambua kwamba mkazo mkubwa wa kuvuta sigara unatokana na wewe mwenyewe. Ikiwa ndivyo, unaweza kushinda tamaa hiyo kwa kufikiria maswali kama haya:

● ‘Kweli nitapata faida yoyote kwa kuvuta sigara? Kwa mfano, nikiamua kuvuta sigara ili tu nikubaliwe na wengine, je, watanikubali ikiwa sikubaliani nao katika mambo mengine? Je, kwa kweli ninataka kukubaliwa na watu ambao watafurahi kuona nikiharibu afya yangu?’

● ‘Kuvuta sigara kutanigharimu kiasi gani kifedha, kiafya, na heshima yangu machoni pa wengine?’

● ‘Niko tayari kuacha urafiki wangu pamoja na Mungu kwa sababu tu ya sigara?’

Namna gani ikiwa tayari umezoea? Unaweza kufanya nini ili uache?

Jinsi ya Kuacha

1. Jisadikishe. Andika sababu zako za kuacha, na uzipitie kwa ukawaida. Unaweza kuchochewa zaidi na tamaa ya kutaka kuwa safi mbele za Mungu.—Waroma 12:1; Waefeso 4:17-19.

2. Tafuta msaada. Ikiwa umekuwa ukivuta sigara kisiri, huu ndio wakati wa kuweka mambo wazi. Waambie wale ambao hukutaka wajue unavuta sigara kwamba unaacha, na uwaombe msaada. Ikiwa unataka kumtumikia Mungu, mwombe msaada.—1 Yohana 5:14.

3. Jiwekee tarehe ya kuacha. Jipatie majuma yasiyozidi mawili, kisha utie alama kwenye kalenda tarehe ambayo umeazimia kuacha kuvuta sigara. Waambie watu wa familia na marafiki kwamba utaacha kabisa kuvuta sigara tarehe hiyo.

4. Zitafute na uziharibu. Kabla ya tarehe ya kuacha, tafuta chumbani, ndani ya gari, na katika mavazi yako, sigara zote. Ziharibu. Haribu viberiti na vyombo vya kuwekea majivu ya sigara.

5. Tafuta njia za kushughulikia maumivu yanayotokana na kuacha. Kunywa maji ya matunda au maji mengi, na ulale vya kutosha. Kumbuka kwamba hali hiyo ni ya muda tu, lakini faida ni za kudumu!

6. Epuka vishawishi. Epuka mahali au hali zinazoweza kukushawishi kuvuta sigara. Huenda pia ukahitaji kuacha kushirikiana na watu wanaovuta sigara.—Methali 13:20.

Usidanganywe

Kila mwaka, makampuni ya tumbaku hutumia mabilioni ya dola kwa ajili ya matangazo. Wanalenga nani hasa? Hati moja ya kampuni fulani ya tumbaku inasema: “Kijana wa leo ndiye mteja wa kesho.”

Usiwaruhusu wauzaji wa tumbaku watie mikono yao mfukoni mwako. Kwa nini ukubali kunaswa na mtego wao? Watu hao au marafiki wako wanaovuta sigara hawakutakii mema. Badala ya kuwasikiliza, sikiliza shauri lililo katika Biblia na ujifunze ‘kujifaidi mwenyewe.’—Isaya 48:17.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Je, marafiki wako hukushawishi unywe pombe? Jifunze ni kwa nini unahitaji kujua mipaka yako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ingawa sura hii inazungumzia watu wanaovuta sigara, matatizo na hatari zinazozungumziwa zinawahusu pia wale wanaotafuna tumbaku.

ANDIKO MUHIMU

“Tujisafishe wenyewe kila unajisi.” —2 Wakorintho 7:1.

PENDEKEZO

Epuka kutafuta visingizio, kama vile kufikiri, ‘Nitavuta mara moja tu.’ Wanaofanya hivyo mara nyingi hujikuta wametumbukia tena katika mazoea hayo.—Yeremia 17:9.

JE, WAJUA . . . ?

Tumbaku isiyo na moshi —kama vile tumbaku inayotafunwa—ina nikotini nyingi kuliko sigara na ina sumu mbalimbali 25 zinazoweza kusababisha ugonjwa wa kansa ambazo zinaongeza uwezekano wa kupata kansa ya koo na mdomo.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Mwanafunzi mwenzangu akisisitiza nivute sigara nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Ingawa unajua hatari za kuvuta sigara, kwa nini huenda bado ukashawishiwa kuvuta sigara?

● Ni nini kinachokusadikisha kwamba ni vibaya kuvuta sigara?

[Blabu katika ukurasa wa 240]

“Mtu anaponipa sigara, mimi hutabasamu tu na kusema, ‘Asante, sitaki kupata kansa.’”—Alana

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 241]

Bangi Ni Mbaya Kweli?

“Watu fulani husema kwamba kuvuta bangi ni njia moja ya kuepuka matatizo,” asema Ellen, anayeishi Ireland, “na kwamba haina madhara yoyote.” Umewahi kusikia mambo kama hayo kuhusu bangi? Linganisha dhana hizi za kawaida na ukweli wa mambo.

Dhana. Bangi haina madhara.

Ukweli wa mambo. Yafuatayo ni madhara ya kudumu yanayojulikana au yanayoaminika kuwa yanasababishwa na kuvuta bangi: kutokuwa na kumbukumbu nzuri, kudhoofika kwa uwezo wa kujifunza, kudhoofika kwa kinga ya mwili, vilevile kuharibika kwa viungo vya uzazi vya wanaume na wanawake. Bangi inaweza kusababisha wasiwasi wa ghafula, kuchanganyikiwa, na woga unaopita kiasi. Kuna uwezekano mkubwa kwa watoto ambao wamezaliwa na wanawake wanaovuta bangi kuwa na tabia zisizo za kawaida, kutoweza kukaza fikira, na kutoweza kufanya maamuzi.

Dhana. Moshi wa bangi hauna madhara kama moshi wa sigara.

Ukweli wa mambo. Unapolinganishwa na moshi wa sigara, moshi mweusi wa bangi unaweza kuchafua zaidi ya mara 4 mfumo wako wa kupitishia hewa na kubeba zaidi ya mara 5 ya kiwango cha gesi yenye sumu ya kaboni monoksidi katika damu yako. Kuvuta misokoto 5 ya bangi kunaweza kusababisha kiwango kilekile cha sumu inayosababisha kansa kama ile inayotokezwa na pakiti nzima ya sigara.

Dhana. Mvutaji wa bangi hawezi kunaswa na mazoea ya kuivuta.

Ukweli wa mambo. Vijana walio na matatizo ya kiakili au kihisia wanaweza kwa urahisi kuwa na mazoea ya kuvuta bangi. Wengine wanaweza kuwa na mazoea hayo baada ya kuitumia kwa muda mrefu. Isitoshe, uchunguzi mbalimbali unaonyesha kwamba kuna hatari kwa vijana wanaovuta bangi kuanza kutumia dawa nyingine za kulevya, kama vile kokeini.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 244, 245]

Madhara ya Tumbaku Mwilini

Watazame watu wenye afya wanaoonyeshwa katika matangazo ya sigara; kisha linganisha picha hizo na madhara halisi ya kuvuta sigara.

Mdomo na koo Unaweza kupata kansa

[Picha]

Ulimi wenye kansa

Moyo Hufanya moyo kuwa mgumu na mishipa ya damu kuwa myembamba, moyo unakosa oksijeni, huongeza mara nne hatari ya kupata ugonjwa wa moyo

[Picha]

Mishipa ya damu iliyoziba

Mapafu Huharibu mifuko ya hewa, huvimbisha njia za hewa, na kuongeza mara 23 hatari ya kupata kansa ya mapafu

[Picha]

Pafu la mvutaji wa sigara

Ubongo Huongeza kwa mara nne hatari ya kupata kiharusi

Ngozi Inaweza kuzeeka mapema

Meno Yanabadilika rangi

Tumbo Husababisha kansa

Kongosho Husababisha kansa

Kibofu Husababisha kansa

Figo Husababisha kansa

[Picha katika ukurasa wa 239]

Kama samaki anayemeza chambo, mtu anayevuta sigara hupata thawabu ndogo kwa gharama kubwa sana