Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ubaya wa Kunywa Kupindukia Ni Nini?

Ubaya wa Kunywa Kupindukia Ni Nini?

SEHEMU YA 34

Ubaya wa Kunywa Kupindukia Ni Nini?

Jibu maswali yafuatayo. Tia alama ya ✔ katika kisanduku kilicho karibu na jibu lako.

Kuna yeyote kati ya marafiki wako ambaye hunywa pombe kabla ya kufikia umri unaoruhusiwa kisheria, au hunywa kupindukia?

□ Ndiyo □ Hapana

Vijana wenzako wamewahi kukuchochea unywe pombe?

□ Ndiyo □ Hapana

Umewahi kunywa kupindukia?

□ Ndiyo □ Hapana

INAMAANISHA nini kunywa kupindukia? Wengine husema ni kunywa kwa kusudi la kulewa. Ripoti moja iliyotayarishwa na Taasisi ya Kitaifa ya Marekani ya Matumizi Mabaya ya Pombe (NIAAA) ilitoa maelezo hususa zaidi. Ilisema kwamba kunywa kupindukia ni “kunywa mfululizo gilasi tano au zaidi za pombe kwa wanaume, au gilasi nne au zaidi kwa wanawake.”

Ikiwa umeshawishiwa kunywa kupita kiasi au kunywa nawe hujafikia umri unaokubalika kisheria, huko peke yako. Vijana wengi wanatumia pombe vibaya. * Hata hivyo, jiulize, ‘Ni nini ninachojua hasa kuhusu sababu inayonifanya nitake kunywa, nayo pombe inaweza kuwa na madhara gani kwangu?’ Kwa mfano, ungejibu namna gani maswali yanayofuata? Tia alama ya ✔ katika kisanduku kilicho kando ya jibu lako, kisha ufikirie ukweli wa mambo.

a. Vijana hunywa kwa sababu tu wanapenda ladha ya pombe.

□ Kweli □ Si kweli

b. Kwa kuwa vijana wana umri mdogo na afya nzuri, hawaathiriwi sana na ulevi kama watu wazima.

□ Kweli □ Si kweli

c. Kunywa kupindukia hakuwezi kukuua.

□ Kweli □ Si kweli

d. Biblia inakataza pombe

□ Kweli □ Si kweli

e. Matokeo pekee ya kunywa kupindukia ni afya mbaya.

□ Kweli □ Si kweli

a. Vijana hunywa tu kwa sababu wanapenda ladha ya pombe. Jibu—Si kweli. Katika uchunguzi uliofanywa nchini Australia kuhusu pombe, asilimia 36 ya vijana waliohojiwa walisema kwamba walikunywa katika sherehe ili tu wakubaliwe na marafiki wao. Nchini Marekani, uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 66 ya vijana walisema kwamba walikunywa kwa sababu ya kushinikizwa na marafiki. Hata hivyo, zaidi ya nusu ya vijana hao walisema pia kwamba walikunywa ili kusahau matatizo.

b. Kwa kuwa vijana wana umri mdogo na afya nzuri, hawaathiriwi sana na ulevi kama watu wazima. Jibu—Si kweli. “Utafiti wa karibuni unadokeza kwamba vijana wanaokunywa wanahatarisha afya yao,” kulingana na makala moja katika gazeti la Discover. Kwa nini? “Vijana wanaokunywa kupita kiasi wanaweza kuharibu uwezo wao wa akili.”

Kunywa kupita kiasi kunahusianishwa pia na kuongezeka kwa chunusi, kupata makunyanzi mapema, kunenepa, kutegemea kileo, na kuwa na mazoea ya kutumia dawa za kulevya. Pia, kunaweza kuharibu kabisa mfumo wa neva, ini, na moyo.

c. Kunywa kupindukia hakuwezi kukuua. Jibu—Si kweli. Pombe nyingi sana huzuia oksijeni isifike kwenye ubongo; na mifumo muhimu ya mwili inaweza kuacha kufanya kazi. Dalili zinaweza kutia ndani kutapika, kupoteza fahamu, na kupumua polepole au kwa njia isiyo ya kawaida. Katika visa fulani, kifo kinaweza kutokea.

d. Biblia inakataza pombe. Jibu—Si kweli. Biblia haikatazi kunywa pombe, wala haiwakatazi vijana wasijifurahishe. (Zaburi 104:15; Mhubiri 10:19) Ni wazi kwamba, hupaswi kunywa ikiwa hujafikia umri unaoruhusiwa kisheria.—Waroma 13:1.

Hata hivyo, Biblia inaonya dhidi ya kunywa kupita kiasi. “Divai ni mdhihaki, kileo husababisha msukosuko, na kila mtu anayepotezwa nacho hana hekima,” yasema Methali 20:1. Pombe inaweza kukufanya utende kijinga! Ni kweli kwamba pombe inaweza kukufurahisha kwa muda mfupi, lakini ukinywa kupita kiasi, “inauma kama nyoka” na kukuacha ukiwa na matatizo mengi.—Methali 23:32.

e. Matokeo pekee ya kunywa kupindukia ni afya mbaya. Jibu—Si kweli. Ukiwa mlevi, inakuwa rahisi kwako kudhulumiwa kwa njia mbalimbali—kutia ndani kulalwa kinguvu. Wakati huohuo, unaweza kuhatarisha maisha ya wengine, kwa kufanya mambo ambayo hungefikiria kufanya ukiwa na akili timamu. Biblia inaonya kwamba ukinywa kupita kiasi, “moyo wako utatoa maneno yasiyofaa.” (Methali 23:33, Zaire Swahili Bible) Kwa ufupi, utajivunjia heshima! Matokeo mengine yenye kuumiza yanaweza kutia ndani kupoteza marafiki, kutofanya vizuri shuleni na kazini, umaskini na kuhusika katika uhalifu.—Methali 23:21.

Jambo la maana hata zaidi, fikiria madhara ya kiroho yanayoweza kusababishwa na kunywa kupita kiasi. Yehova Mungu anataka umtumikie “kwa akili yako yote,” si akili iliyoharibiwa kwa kunywa pombe kupita kiasi! (Mathayo 22:37) Mbali na kushutumu kunywa “divai kupita kiasi,” Neno la Mungu linashutumu pia “mashindano ya kunywa.” (1 Petro 4:3) Kwa hiyo, kunywa kupita kiasi ni kinyume cha mapenzi ya Muumba wetu, na kufanya hivyo kutakuzuia usiwe na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.

Utachukua Hatua Gani?

Utaamua tu kuwafuata vijana wenzako wanaotumia pombe vibaya? Biblia inasema: “Je, hamjui kwamba ikiwa mnaendelea kujitoa wenyewe kwa yeyote kuwa watumwa ili kumtii yeye, ninyi ni watumwa wake kwa sababu mnamtii yeye?” (Waroma 6:16) Je, kweli unataka kuwa mtumwa wa vijana wenzako au wa pombe?

Unaweza kufanya nini ikiwa umenaswa na mazoea ya kunywa kupindukia? Tafuta msaada upesi kwa kuzungumza na mzazi au rafiki mkomavu. Zungumza na Yehova Mungu katika sala, na umwombe akusaidie. Yehova ni “msaada unaopatikana kwa utayari wakati wa taabu.” (Zaburi 46:1) Kwa kuwa mara nyingi watu hunywa kupindukia au kunywa kabla ya kufikisha umri unaoruhusiwa kisheria kwa sababu ya kuchochewa na marafiki, unahitaji kufanya mabadiliko makubwa kuhusu uchaguzi wa marafiki. * Si rahisi kufanya mabadiliko hayo, lakini kwa msaada wa Yehova unaweza kufanikiwa.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Mtu anaweza kushinda mazoea ya kutumia dawa za kulevya. Pata kujua jinsi inavyowezekana.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Ona sanduku “ Ni Nani Wanaokunywa Kupindukia?” katika ukurasa wa 249.

^ fu. 32 Pata habari zaidi katika Sura ya 8 na ya 9 katika kitabu hiki na Sura ya 15 katika Buku la 2.

ANDIKO MUHIMU

‘Mlevi atakuwa maskini.’ —Methali 23:21.

PENDEKEZO

Tambua sababu zinazofanya utake kunywa pombe. Kisha ujaribu kufikiria njia nyinginezo bora unazoweza kutumia kujifurahisha au kutuliza hisia zako za huzuni.

JE, WAJUA . . . ?

Kulingana na uchunguzi mmoja nchini Marekani, “vijana ambao mara nyingi wanakunywa kupindukia wanakosa kwenda shuleni, hawafanyi vizuri katika masomo yao, wanaumizwa au kujeruhiwa, na kuharibu mali, mara nane zaidi ya wale ambao hawanywi kupindukia.”

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ikiwa marafiki wangu wanataka nitumie pombe vibaya nikiwa pamoja nao, nitasema ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini vijana wa rika lako wanataka watu wengine wajiunge nao kutumia pombe isivyofaa?

● Je, kutumia pombe isivyofaa kutakufanya uwavutie watu wa jinsia tofauti, na kwa nini unajibu hivyo?

[Blabu katika ukurasa wa 250]

“Wanafunzi wenzangu wanaponipa pombe, mimi huwaambia kwamba sihitaji kunywa ili nijifurahishe.”—Mark

[Sanduku katika ukurasa wa 249]

 Ni Nani Wanaokunywa Kupindukia?

Kulingana na uchunguzi uliofanywa kuhusu watoto wa shule za sekondari nchini Uingereza, Scotland, na Wales, asilimia 25 ya watoto walio kati ya umri wa miaka 13 na 14 “walidai kwamba wamewahi kunywa angalau glasi tano za pombe katika kikao kimoja.” Karibu nusu ya watoto waliochunguzwa wenye umri wa miaka 15 na 16 walidai kwamba wamewahi kunywa hivyo pia. Kulingana na Wizara ya Marekani ya Afya na Huduma za Jamii (HHS), “vijana milioni 10.4 hivi walio kati ya umri wa miaka 12 na 20 walisema kwamba wao hunywa pombe. Milioni 5.1 kati yao hunywa kupindukia na milioni 2.3 hunywa kupindukia angalau mara tano kila mwezi.” Uchunguzi uliofanywa nchini Australia ulionyesha kwamba wasichana wengi kuliko wavulana hunywa pombe kupindukia​—wao hunywa glasi 13 hadi 30 katika kikao kimoja!

[Picha katika ukurasa wa 251]

Pombe inaweza kuuma kama nyoka