Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kuacha Jinsi Gani Kutumia Dawa za Kulevya?

Ninaweza Kuacha Jinsi Gani Kutumia Dawa za Kulevya?

SURA YA 35

Ninaweza Kuacha Jinsi Gani Kutumia Dawa za Kulevya?

UNA mazoea ya kutumia dawa za kulevya? Huenda unajua kwamba mazoea hayo yanaharibu akili na mwili wako. Labda hata umejaribu kuvunja mazoea hayo lakini ukajikuta umeanza tena. Ikiwa ndivyo, usikate tamaa. Wengine wamefaulu, nawe pia unaweza! Kwa mfano, ona mambo ambayo watu watatu kutoka malezi tofauti kabisa wanasema kuhusu jinsi walivyoshinda mazoea hayo.

JINA Marta

MALEZI Mama yangu aliponizaa, hakuwa ameolewa, kwa hiyo, mimi na dada yangu tulilelewa bila baba. Nikiwa na umri wa miaka 12 hivi, nilianza kuenda disko na shangazi yangu aliyependa sana kucheza dansi. Nilikuwa mwenye urafiki na muda si muda nikafanya urafiki na watu waliokuwa na mwenendo mbaya. Nikaanza kutumia dawa za kulevya nikiwa na umri wa miaka 13. Pia, nikaanza kutumia kokeini. Mwanzoni, niliifurahia. Lakini baada ya muda, nikaanza kupatwa na jinamizi na kuogopa kila kitu. Dawa hizo zilipokuwa zinaisha mwilini, nilianza kufikiria kujiua. Nilitaka kuacha kutumia dawa za kulevya lakini nikashindwa.

JINSI NILIVYOACHA Nilianza kumfikiria Mungu na hata kuenda kanisani mara kadhaa. Hata hivyo, nilivunjika moyo zaidi. Nikiwa na umri wa miaka 18, nilianza kuishi na mwanamume rafiki yangu, nami nikapata mtoto. Kuwa na mtoto kulinichochea nitake kubadili maisha yangu. Mwanamke fulani aliyekuwa rafiki yangu akahamia nyumba iliyokuwa karibu na mahali nilipokuwa nikiishi. Alinitembelea na kutaka kujua ninavyoendelea. Nilimweleza kila kitu. Akaniambia kwamba yeye sasa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova na angependa kujifunza Biblia pamoja nami. Nikakubali.

Nilipata kujua kwamba maisha yangu hayamfurahishi Mungu na kwamba ninapaswa kuacha kutumia dawa za kulevya na kuvuta sigara pia. Hata hivyo, ilikuwa vigumu sana kuacha dawa za kulevya. Nilimwomba Yehova Mungu mara nyingi kwa siku anisaidie nivunje mazoea hayo mabaya. Nilitaka kumfurahisha. (Methali 27:11) Baada ya kujifunza Biblia na kushirikiana na Mashahidi wa Yehova kwa miezi sita, niliacha kabisa kutumia dawa za kulevya. Sasa maisha yangu yana kusudi. Sina tatizo la kushuka moyo kila wakati kama ilivyokuwa. Nilipata kumjua mwanamume mzuri Mkristo na tukafunga ndoa. Nimemlea mwanangu kulingana na kanuni za Biblia. Ninashukuru kwamba Yehova alisikia sala zangu na akanisaidia!

JINA Marcio

MALEZI Nililelewa nje ya mji wa Santo André, mji wenye idadi kubwa ya watu katika jimbo la São Paulo, Brazili. Nilijiingiza katika utumiaji wa tumbaku, dawa za kulevya, na wizi, nikiwa na umri mdogo. Wengi wa marafiki wangu walijihusisha na wizi wa magari na ulanguzi wa dawa za kulevya. Mmoja wao alikuwa akiwapa vijana katika eneo letu dawa za kulevya bila malipo. Baada ya kukuza mazoea ya kuzitumia, walilazimika kuzinunua kutoka kwake.

Sikuzote polisi walikuwa wakishika doria katika eneo letu, nami nilikamatwa mara kadhaa kwa makosa madogo-madogo na mara moja kwa kushukiwa kuwa mlanguzi wa dawa za kulevya. Mara nyingi nilificha bunduki na vitu vilivyoibwa katika nyumba yangu.

Watu waliniogopa. Macho yangu yalikuwa mekundu. Sikuwa nikitabasamu. Sikuzote nilionekana kama muuaji. Nilipewa jina “Tufão” (Kimbunga) kwa sababu nilisababisha matatizo kila nilikokwenda. Pia, nilikuwa mlevi na niliishi maisha machafu. Wengi wa marafiki wangu walikufa au kufungwa gerezani. Nilishuka moyo sana hivi kwamba nikafunga kamba kwenye mti na kujaribu kujiua.

JINSI NILIVYOACHA Nilimwomba Mungu anisaidie. Mwishowe, nikakutana na Mashahidi wa Yehova na kuanza kujifunza Biblia. Nilijifunza kwamba Mungu ana jina, Yehova, na kwamba anawajali na kuwasaidia wale wanaojaribu kuishi kulingana na kanuni zake. (Zaburi 83:18; 1 Petro 5:6, 7) Nilihitaji kufanya mabadiliko mengi. Lililokuwa gumu zaidi ni kujifunza kutabasamu.

Sikuzote nilimwomba Yehova anisaidie, na kutumia ushauri wa Biblia. Kwa mfano, niliacha kushirikiana na “marafiki” wangu wa zamani na kuepuka kwenda baa. Badala yake, nikaamua kushirikiana na watu wanaoishi kulingana na kanuni za Biblia. Haikuwa rahisi, hata hivyo, sasa mimi si mwizi wala mtu msumbufu tena. Na kwa zaidi ya miaka 10 sasa, sijatumia dawa za kulevya.

JINA Craig

MALEZI Nililelewa vijijini nchini Australia Kusini. Baba yangu alikuwa mlevi. Alitengana na mama yangu nilipokuwa na umri wa miaka nane. Mama yangu aliolewa tena, nami nikaishi naye mpaka nilipokuwa na umri wa miaka 17. Mwaka huo nilijifunza kukata kondoo manyoya na nikaanza kuishi na kikundi cha wakataji-manyoya waliokuwa wakisafiri popote kazi ilipopatikana. Nilianza kulewa na kutumia dawa mbalimbali za kulevya. Nikafuga nywele, nikaitia nta na kuisuka na kuzitia ushanga. Nikawa mwenye wivu na mtukanaji na mwenye hasira. Zaidi ya mara moja nilitiwa gerezani.

Nilihamia mji mdogo Magharibi mwa Australia na kuanza kuishi na msichana rafiki yangu, ambaye alikuwa mhudumu wa baa. Tulivuta misokoto na kunywa pombe, na tulipanda bangi yetu wenyewe.

JINSI NILIVYOACHA Tulikuwa tu tumemaliza kuvuna bangi yetu wakati Mashahidi wa Yehova walipobisha mlango wa nyumba yetu iliyokuwa imeharibika sana. Sikukubaliana tu na mambo waliyosema. Badala yake, baada ya muda, nilithibitisha mwenyewe kwamba mambo ambayo Biblia inasema ni ya kweli. Kisha, hatua kwa hatua, nikapambana na matatizo yangu.

Muda si muda nikaelewa kwamba ninahitaji kuacha mazoea yangu ya kutumia bangi. Hilo lingehusisha nini? Nilikuwa nimefanya mengi sana kuikuza, kwa hiyo, mwanzoni nilifikiria nimpe mtu fulani. Lakini nikaamua kwamba huo si uamuzi mzuri na badala yake nikaiharibu. Sala ilinisaidia sana kushinda tatizo la kutumia dawa za kulevya na pombe. Niliomba roho ya Mungu inisaidie kupambana na kushinda mambo niliyokuwa nikikabili. Pia, niliacha kushirikiana na watu walionichochea kutenda mabaya. Kadiri nilivyojifunza na kutumia mafundisho ya Biblia, nilipata usalama niliohitaji ili kushinda baadhi ya kasoro zangu za kiutu. Mpenzi wangu alijifunza Biblia pia na kubadili mwenendo wake na maisha yake. Kisha tukafunga ndoa. Kwa miaka 21 tumefurahia afya nzuri, na tunafurahia kulea watoto wawili. Sijui maisha yangu yangekuwaje kama Yehova hangenisaidia kubadili maisha yangu.

ANDIKO MUHIMU

“Yehova ni nguvu zangu na uwezo wangu.”—Isaya 12:2.

PENDEKEZO

Ikiwezekana, epuka watu, mahali, na vitu vinavyohusiana na mazoea yako ya zamani ya kutumia dawa za kulevya. Uchunguzi unaonyesha kwamba kuona tu chochote kati ya vitu hivyo kunaweza kuamsha tamaa yako upya.

JE, WAJUA . . . ?

Kutumia vibaya dawa za kulevya kunaweza kuharibu ubongo wako.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ikiwa nitarudia tena mazoea niliyoacha, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini huenda mtu akahitaji kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yake ikiwa anataka kuvunja mazoea ya kutumia dawa za kulevya?

● Kujifunza kweli za Mungu kunaweza kumsaidia mtu jinsi gani?

[Blabu katika ukurasa wa 253]

“Kuishi kupatana na viwango vya Biblia, kumenisaidia kupata furaha na kusudi maishani sasa.”—Marta

[Picha katika ukurasa wa 256]

Kushinda mazoea mabaya ni kama kukimbia kutoka katika nyumba inayoteketea—unalazimika kuacha vitu fulani ili uokoe uhai wako