Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniachi Nijifurahishe?

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniachi Nijifurahishe?

SURA YA 37

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniachi Nijifurahishe?

Kulingana na Allison, kijana anayeishi Australia, kila Jumatatu (Siku ya 1) asubuhi huwa wakati wenye kufadhaisha sana.

“Kila mtu anazungumzia mambo aliyofanya mwishoni mwa juma,” anasema. “Wanazungumzia mambo yenye kusisimua kwelikweli, kama vile ni karamu ngapi walizoalikwa, ni wavulana wangapi waliowabusu—hata jinsi walivyowakimbia polisi . . . Inaogopesha sana, lakini inafurahisha! Wanarudi nyumbani saa 11 za asubuhi, na wazazi wao hawajali. Mimi huwa nimelala hata kabla hawajaanza shughuli zao za usiku!

“Baada ya kunisimulia jinsi mambo yalivyokuwa, wanataka kujua mimi nilifanya nini. . . . Nilikuwa katika mikutano ya Kikristo. Nilishiriki katika utumishi. Nahisi kwamba nimekosa mengi mazuri. Kwa hiyo, kwa kawaida mimi ninawaambia kwamba sikufanya chochote. Kisha wanauliza kwa nini sikujiunga nao.

“Jumatatu ikiisha kupita, unadhani kwamba mambo yatakuwa sawa. Lakini wapi. Jumanne (Siku ya 2), kila mtu anazungumzia mwisho-juma ujao! Mimi huketi na kuwasikiliza tu. Najiona mpweke!”

KILA Jumatatu asubuhi unapokuwa shuleni, wewe hupatwa na hali kama hiyo? Huenda ukahisi kwamba vijana wengine wanafurahia maisha huku wewe ukiwa kizuizini. Si kwamba unataka kufanya kila kitu ambacho vijana wenzako wanafanya. Hata hivyo, ungependa tu kufurahia maisha mara kwa mara! Kwa mfano, ni burudani gani ambayo wewe ungependa kushiriki mwisho-juma huu?

□ kucheza dansi

□ karamu

□ tamasha ya muziki

□ kutazama sinema

□ jambo lingine ․․․․․

Unahitaji tafrija. Muumba wako anataka ufurahie ujana wako. (Mhubiri 3:1, 4) Na ingawa huenda nyakati nyingine usiamini, wazazi wako pia wanataka ujifurahishe. Hata hivyo, yaelekea wazazi wako wana wasiwasi kwa sababu hizi mbili: (1) mambo utakayochagua kufanya na (2) wale utakaoshirikiana nao.

Namna gani ikiwa rafiki zako wanakualika kwenye tafrija lakini hujui wazazi wako watasema nini? Fikiria hatua tatu unazoweza kuchukua na matokeo yake.

HATUA YA A USIOMBE RUHUSA—NENDA TU

Sababu inayoweza kufanya ufikirie kuchukua hatua hiyo: Unataka kuwavutia marafiki wako na kuwaonyesha kwamba unajitegemea. Unahisi kwamba wazazi wako hawakuelewi, au huheshimu maoni yao.—Methali 14:18.

Matokeo: Huenda marafiki wako wakavutiwa, lakini watapata pia kujua jambo fulani pia kukuhusu, kwamba wewe ni mdanganyifu. Ikiwa unaweza kuwadanganya wazazi wako, basi unaweza kuwadanganya marafiki wako pia. Wazazi wako wakigundua, watavunjika moyo na kuhisi kuwa umewasaliti na huenda ukawekewa vizuizi vingi zaidi! Kukosa kuwatii wazazi wako na kuondoka tu ni hatua ya kipumbavu.—Methali 12:15.

HATUA YA B USIOMBE RUHUSA—USIENDE

Sababu inayoweza kufanya ufikirie kuchukua hatua hiyo: Unafikiria kuhusu tafrija yenyewe na kuona kwamba haipatani na viwango vyako au kwamba baadhi ya wale waliokaribishwa si mashirika mazuri. (1 Wakorintho 15:33; Wafilipi 4:8) Au, ungependa kwenda lakini huna ujasiri wa kuwaomba wazazi wako ruhusa.

Matokeo: Usipoenda kwa sababu unaona haifai kwenda, utakuwa na uhakika zaidi unapowajibu rafiki zako. Lakini usipoenda kwa sababu tu huna ujasiri wa kuwaomba wazazi wako ruhusa, utashinda nyumbani ukiwa umekasirika na ukihisi kwamba ni wewe tu unayekosa kufurahia maisha.

HATUA YA C OMBA RUHUSA—NA USUBIRI

Sababu inayoweza kufanya ufikirie kuchukua hatua hiyo: Unatambua kwamba wazazi wako wana mamlaka juu yako na unaheshimu uamuzi wao. (Wakolosai 3:20) Unawapenda wazazi wako na hutaki kuwakasirisha kwa kuwadanganya na kwenda pamoja na marafiki wako. (Methali 10:1) Pia una nafasi ya kueleza maoni yako.

Matokeo: Wazazi wako wanaona kwamba unawapenda na kuwaheshimu. Na wakiona kwamba ombi lako linafaa wanaweza kukubali.

Sababu Inayoweza Kuwafanya Wazazi Wakatae

Namna gani wazazi wako wakikataa? Hilo linaweza kuvunja moyo sana. Hata hivyo, kuelewa maoni yao kunaweza kukusaidia kukabiliana na vizuizi vyao. Kwa mfano, wanaweza kukataa kwa sababu moja au zaidi kati ya mambo yafuatayo.

Wana ujuzi na uzoefu mwingi zaidi. Ungekuwa na nafasi ya kuogelea, haikosi ungependa kuogelea mahali palipo na waokoaji. Kwa nini? Kwa sababu unapokuwa ndani ya maji ukifurahia kuogelea, huenda usitambue hatari kwa urahisi. Lakini waokoaji wanaweza kutambua hatari haraka.

Vivyo hivyo, kwa kuwa wazazi wako wana ujuzi na uzoefu mwingi, wanaweza kutambua hatari ambazo wewe huzioni. Kama waokoaji kwenye ufuo, kusudi la wazazi wako si kukuharibia furaha yako bali wanataka kukusaidia uepuke hatari zinazoweza kukuzuia usifurahie maisha.

Wanakupenda. Wazazi wako wanataka sana kukulinda. Upendo unawasukuma kukubaliana nawe inapowezekana na kutofautiana nawe wanapolazimika kufanya hivyo. Unapowaomba ruhusa ufanye jambo fulani, wanajiuliza ikiwa wanaweza kukupa ruhusa na bado wakubaliane na matokeo ya uamuzi wao. Watasema ndiyo iwapo tu watakuwa na hakika kwamba hakuna jambo baya litakalokupata.

Jinsi ya Kufanya Iwe Rahisi Zaidi kwa Wazazi Wako Kukupa Ruhusa

Mambo manne yanayohusika.

Unyoofu: Kwanza, unahitaji kujiuliza hivi kwa unyoofu: ‘Kwa nini hasa ninataka kwenda? Ni kwa sababu ninafurahia tafrija yenyewe, au ni kwa sababu tu ninataka kukubaliwa na marafiki wangu? Je, ni kwa sababu mtu fulani ninayevutiwa naye atakuwapo?’ Kisha waambie wazazi wako ukweli. Wakati fulani hata wao walikuwa vijana, na wanakuelewa vizuri. Kwa hiyo, kuna uwezekano kwamba watatambua nia yako, hata usipowaambia. Watafurahi kwamba umewaambia ukweli, nawe utafaidika kutokana na hekima yao. (Methali 7:1, 2) Kwa upande mwingine, ikiwa hutawaambia ukweli, wataacha kukuamini na huenda wasikupe ruhusa.

Chagua wakati unaofaa: Usiwahangaishe wazazi wako kwa maombi mengi mara tu baada ya wao kufika nyumbani kutoka kazini au wanapokazia fikira mambo mengine. Zungumza nao wanapokuwa wametulia. Lakini usisubiri mpaka dakika ya mwisho kisha uanze kuwashinikiza wakujibu haraka. Wazazi wako hawatafurahi kufanya uamuzi haraka-haraka. Ukiomba ruhusa mapema, wazazi wako watapata wakati wa kufikiria jambo hilo na wataona kwamba unawajali.

Sema mambo waziwazi: Usizungumzie mambo kijuujuu tu. Eleza jambo unalotaka kufanya hasa. Wazazi huwa na wasiwasi wanapoambiwa “Sijui,” hasa ikiwa wamekuuliza: “Ni nani atakayekuwapo?” “Je, kutakuwa na mtu mzima atakayesimamia mambo?” au “Tafrija hiyo itakwisha saa ngapi?”

Mtazamo: Usiwaone wazazi wako kama adui. Waone kuwa wako upande mmoja nawe—kwa sababu, kwa kweli wako upande wako. Ukiwa na mtazamo huo, hutasikika ni kama unawagombeza, nao watakuwa tayari kushirikiana nawe. Epuka kusema maneno kama “Hamniamini,” “Kila mtu anaenda,” au “Wazazi wa marafiki wangu wamewaruhusu waende!” Waonyeshe wazazi wako kwamba umekomaa kiasi cha kutosha kukubali uamuzi wao na kuuheshimu. Ukifanya hivyo, watakuheshimu. Na wakati ujao, huenda wakafikiria kukupa ruhusa.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 32

ANDIKO MUHIMU

“Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie.”—Methali 27:11.

PENDEKEZO

Unapokwenda kwenye tafrija, panga hatua utakayochukua mambo yakiharibika. Kabla ya kwenda kwenye tafrija yoyote panga mambo utakayofanya au kusema ili kwamba, ikihitajika, unaweza kuondoka ukiwa na dhamiri safi.

JE, WAJUA . . . ?

Wazazi wenye upendo huona afadhali watahadhari kupita kiasi kuliko waje kujuta baadaye. Iwapo wazazi wako hawaelewi unachoomba au wakihisi kwamba kuna habari muhimu ambazo hujawaeleza, kuna uwezekano kwamba watakataa.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ikiwa dhamiri yangu inanisumbua kwa sababu ya mambo ninayoona au kusikia kwenye sinema au katika tafrija, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini huenda ukasita kuwapa wazazi wako habari zote wanazohitaji ili kufanya uamuzi?

● Huenda matokeo yakawa nini ikiwa wazazi wako watakubali ombi lako kwa msingi wa habari ulizowapa, na kumbe umewaficha habari fulani muhimu?

[Blabu katika ukurasa wa 268]

“Nilikuwa mjinga sana nilipokuwa kijana. Baadhi ya mambo niliyofanya ili ‘kujifurahisha’ mwishowe nilikuja kutambua kwamba hayakuwa yenye kufurahisha. Baada ya muda, utavuna unachopanda. Ninajuta kwamba sikuwasikiliza wazazi wangu.”—Brian

[Picha katika ukurasa wa 269]

Kama waokoaji kwenye ufuo, wazazi wana uwezo mzuri zaidi wa kutambua hatari