Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kumwabudu Mungu?

Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kumwabudu Mungu?

SURA YA 38

Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kumwabudu Mungu?

Josh, mwenye umri wa miaka 16, anagaa-gaa kitandani. Mama yake amesimama mlangoni. Anasema kwa ukali: “Joshua, amka! Unajua leo ni siku ya mkutano!” Wazazi wa Josh ni Mashahidi wa Yehova, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni sehemu ya kawaida ya maisha yao. Hata hivyo, siku hizi Josh hana hamu ya kuhudhuria mikutano.

Analalamika: “Mama, sijisikii kwenda?”

“Acha kulalamika na ujitayarishe mara moja,” mama yake anamwambia. “Sitaki kuchelewa tena!” Kisha anageuka na kuanza kuondoka.

Kabla mama yake hajaenda mbali, Josh anasema: “Mama, ninataka ujue kwamba hii ni dini yako, na si lazima iwe yangu.” Anajua kwamba mama yake amesikia kwa sababu amesimama kidogo. Kisha, bila kumjibu, mama yake aendelea na shughuli zake.

Josh anahisi hatia kidogo kwa sababu ya maneno aliyosema. Kwa kweli hataki kumvunja moyo mama yake. Hata hivyo, hana nia ya kuomba msamaha. Basi, anaamua kumtii mama yake shingo upande.

Josh ashusha pumzi na kuanza kujitayarisha. Kisha anajiambia: “Hivi karibuni nitafanya uamuzi wangu mwenyewe. Mimi si kama wale wengine katika Jumba la Ufalme. Maisha ya Ukristo siyawezi!”

UMEWAHI kuhisi kama Josh anavyohisi? Je, nyakati nyingine inaonekana kwamba wengine wanafurahia utendaji wa Kikristo, huku wewe ukijihusisha katika utendaji huo kwa sababu tu huna la kufanya? Kwa mfano:

● Unaona kujifunza Biblia kama vile kufanya migawo ya shule?

● Unachukia kuhubiri nyumba kwa nyumba?

● Mara nyingi unahisi umechoka unapokuwa kwenye mikutano ya Kikristo?

Ikiwa jibu lako ni ndiyo, usife moyo. Unaweza kufurahia kumtumikia Mungu. Tuone jinsi unavyoweza kufanya hivyo.

TATIZO LA 1 Kujifunza Biblia

Kwa nini si rahisi? Huenda ukahisi kwamba hupendi kujifunza. Ni vigumu kwako kuketi na kukaza fikira kwa muda mrefu! Isitoshe, una mambo mengi ya shule ya kujifunza.

Kwa nini ujifunze Biblia? Biblia imeongozwa na roho ya Mungu na pia ‘inafaa katika kufundishia ukweli, kuonya, kusahihisha makosa, na kuwaongoza watu waishi maisha adili.’ (2 Timotheo 3:16, Biblia Habari Njema) Kujifunza Biblia na kutafakari mambo unayosoma kunaweza kukufanya uelewe mambo kwa njia tofauti kabisa. Ukweli ni kwamba, chochote kizuri hupatikana kwa jasho. Ukitaka kucheza mchezo fulani vizuri, unahitaji kujifunza sheria za mchezo huo na kufanya mazoezi. Ukitaka kuwa na afya nzuri, unahitaji kufanya mazoezi. Vivyo hivyo, ukitaka kumfahamu Muumba wako, unahitaji kujifunza Neno la Mungu.

Mambo ambayo vijana wenzako wanasema. “Nilipojiunga na shule ya sekondari, nilijikuta katika njia panda. Wanafunzi walikuwa wakifanya mambo mabaya, nami nilihitaji kufanya maamuzi fulani: ‘Je, ninataka kuwa kama wao? Je, kweli wazazi wangu wananifundisha kweli?’ Nilihitaji kujithibitishia mwenyewe.”—Tshedza.

“Sikuzote niliamini kwamba kile nilichojifunza ni kweli, lakini nilihitaji kujithibitishia. Nilihitaji kuifanya iwe dini yangu mwenyewe—badala ya kuwa dini ya familia.”—Nelisa.

Unachoweza kufanya. Panga ratiba yako mwenyewe ya funzo lako la kibinafsi kulingana na mapendezi na mahitaji yako. Chagua mwenyewe mambo utakayojifunza. Unaweza kuanzia wapi? Kwa nini usijifunze Biblia kwa undani na kuchanganua mambo unayoamini, labda ukitumia kitabu kama vile Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

Jinsi ya kuanza! Tia alama ya ✔ kando ya habari mbili au tatu za Biblia zilizo hapa chini ambazo ungependa kujifunza kwa undani—au ukipenda, andika mambo mengine yanayokupendeza.

□ Kuna Mungu?

□ Ninaweza kuwa na hakika jinsi gani kwamba waandikaji wa Biblia waliongozwa na roho ya Mungu?

□ Kwa nini niamini uumbaji badala ya mageuzi?

□ Ufalme wa Mungu ni nini, na ninaweza kuthibitisha jinsi gani kwamba upo?

□ Ninaweza kueleza jinsi gani imani yangu kuhusu kile kinachotupata tunapokufa?

□ Kwa nini ninapaswa kuwa na hakika kwamba kutakuwa na ufufuo?

□ Ninaweza kuitambua dini ya kweli jinsi gani?

․․․․․

TATIZO LA 2 Kuhubiri

Kwa nini si rahisi? Kuzungumza na wengine kuhusu Biblia, au kukutana na mwanafunzi mwenzako unapohubiri, kunaweza kukuogopesha.

Kwa nini uhubiri? Yesu aliwaagiza wafuasi wake: ‘Fanyeni wanafunzi na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.’ (Mathayo 28:19, 20) Hata hivyo, kuna sababu nyingine za kufanya hivyo. Uchunguzi unadokeza kwamba katika maeneo fulani vijana wengi wanamwamini Mungu na wanaiamini Biblia. Hata hivyo, vijana hao hawana tumaini hakika la wakati ujao. Kupitia kujifunza Biblia, una habari ambayo vijana wengi wa rika lako wanatafuta na wanahitaji! Kwa kuwahubiria wengine, utajihisi vizuri, isitoshe, utaufurahisha moyo wa Yehova.—Methali 27:11.

Mambo ambayo vijana wenzako wanasema. “Mimi na rafiki yangu tulitayarisha tangulizi mbalimbali zenye matokeo, na tukajifunza jinsi ya kupambana na upinzani na jinsi ya kufanya ziara za kurudia. Nilipojitahidi kushiriki zaidi katika huduma, nilifurahia sana kuhubiri.” —Nelisa.

“Dada mmoja Mkristo amenisaidia sana! Amenizidi umri kwa miaka sita, naye huandamana nami katika huduma na mara nyingine hata ananinunulia kiamsha-kinywa. Alinionyesha maandiko yenye kutia moyo yaliyonisaidia kubadili maoni yangu. Mfano wake mzuri umenichochea nitake kuwasaidia watu. Ninashukuru sana kwa msaada wake!”—Shontay.

Unachoweza kufanya. Wazazi wako wakikuruhusu, tafuta mtu kutanikoni aliye na umri mkubwa kuliko wako ambaye unaweza kuhubiri naye. (Matendo 16:1-3) Biblia inasema: “Chuma hunolewa kwa chuma. Ndivyo mtu anavyounoa uso wa mwingine.” (Methali 27:17) Kuna faida nyingi za kushirikiana na watu wenye umri mkubwa walio na uzoefu mwingi. “Kwa kweli, ni afadhali zaidi kushirikiana na watu wenye umri mkubwa,” asema Alexis, mwenye umri wa miaka 19.

Jinsi ya kuanza! Mbali na wazazi wako, andika hapa chini jina la mtu mwingine katika kutaniko lenu anayeweza kukusaidia katika huduma.

․․․․․

TATIZO LA 3 Kuhudhuria Mikutano ya Kikristo

Kwa nini si rahisi? Baada ya kuwa shuleni siku nzima, huenda ikawa vigumu sana kusikiliza hotuba zinazotegemea Biblia kwa saa moja au zaidi.

Kwa nini uhudhurie mikutano? Biblia inawahimiza Wakristo: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.”—Waebrania 10:24, 25.

Mambo ambayo vijana wenzako wanasema. “Ili ufurahie mikutano ya kutaniko, ni lazima utayarishe. Nyakati nyingine unahitaji tu kuchochea hamu yako ya kujifunza. Unapotayarisha, unafurahia mikutano kwa sababu unajua kinachozungumziwa, na hata unaweza kushiriki.”—Elda.

“Wakati fulani, niligundua kwamba ninafurahia mikutano zaidi ninapotoa maelezo.”—Jessica.

Unachoweza kufanya. Tumia wakati kutayarisha mapema, na ukiweza, toa maelezo. Hilo litakufanya uhisi unahusika katika mikutano hiyo.

Kwa mfano: Ni nini kinachokufurahisha zaidi, kutazama michezo kwenye televisheni au kucheza uwanjani? Bila shaka, kucheza kunafurahisha zaidi kuliko kutazama tu. Kwa nini usifanye vivyo hivyo kuhusiana na mikutano ya Kikristo?

Jinsi ya kuanza! Andika katika nafasi iliyo hapa chini, siku unayoweza kupata dakika 30 kila juma ili kujitayarisha kwa ajili ya mkutano wa kutaniko.

․․․․․

Vijana wengi wamejionea ukweli wa Zaburi 34:8, ambayo inasema: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.” Je, ungeridhika kwa kusikia tu kuhusu mlo mtamu? Je, si afadhali kula mlo huo wewe mwenyewe? Ndivyo ilivyo pia kuhusu kumwabudu Mungu. Onja na ujionee jinsi inavyoridhisha kushiriki katika utendaji wa kiroho. Biblia inasema kwamba mtu ambaye si msikiaji tu bali mtendaji wa kazi “atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.”—Yakobo 1:25.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Jifunze jinsi ya kuweka na kufikia miradi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

ANDIKO MUHIMU

“Mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Waroma 12:2.

PENDEKEZO

Tafuta kitabu na uwe ukiandika mambo makuu katika mikutano ya Kikristo. Muda utasonga haraka, na itakuwa rahisi zaidi kwako kujifunza.

JE WAJUA . . . ?

Si vibaya kuchunguza imani yako ya kidini. Kwa kweli, kuuliza maswali na kufanya utafiti ni njia nzuri ya kupata kujua ikiwa mambo unayoamini kumhusu Mungu ni ya kweli.—Matendo 17:11.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nitatenga dakika ․․․․․ kwa ajili ya usomaji wa Biblia kila siku nami nitatumia muda wa ․․․․․ kila juma kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ya Kikristo.

Ili niweze kukazia fikira mikutano ya Kikristo, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kwa nini huenda kijana akaona mambo ya kiroho kuwa yenye kuchosha?

● Kati ya sehemu tatu zinazohusu ibada ambazo zimezungumziwa katika sura hii, ungependa kufanyia kazi sehemu gani?

[Blabu katika ukurasa wa 278]

“Hii ni dini yangu bali si ya wazazi wangu tu. Yehova ndiye Mungu wangu, na sitaki kufanya jambo lolote litakaloharibu uhusiano wangu pamoja naye.”—Samantha

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 280]

Walijiwekea Miradi

Biblia inasema: “Hamjui uzima wenu utakuwa namna gani kesho.” (Yakobo 4:14) Katika visa fulani, kifo kinatokea bila kutazamiwa na katika umri mdogo. Unaposoma masimulizi kuhusu Catrina na Kyle, ona jinsi walivyojifanyia jina zuri na Yehova Mungu katika maisha yao mafupi kwa kujiwekea na kufikia miradi ya kiroho.—Mhubiri 7:1.

Catrina alikufa akiwa na umri wa miaka 18, lakini alipokuwa na umri wa miaka 13 tayari alikuwa amejiwekea miradi ambayo alitaka kufikia. Miradi yake ilitia ndani kuingia katika utumishi wa wakati wote, kutumika katika nchi yenye uhitaji wa walimu wa Biblia, na kufanya kazi ya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme pamoja na baba yake. Aliandika: “Nimeweka maisha yangu wakfu kwa Yehova Mungu!” Lengo la Catrina lilikuwa “kuishi kulingana na kanuni za Mungu, na kwa njia inayomfurahisha.” Wakati wa maziko yake, Catrina alifafanuliwa kuwa “msichana mrembo aliyekuwa amepanga kumtumikia Yehova maisha yake yote.”

Tangu alipokuwa mdogo, Kyle alifundishwa kuwa na miradi. Baada ya kufa katika msiba mbaya wa barabarani akiwa na umri wa miaka 20, watu wa familia yao walipata “kitabu cha miradi” ambacho mama yake alikuwa amemsaidia kukiandika alipokuwa na umri wa miaka minne tu. Miradi yake ilitia ndani kubatizwa, kutoa hotuba kwenye Jumba la Ufalme, kutumika katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, ambapo angeweza kusaidia kuchapisha vitabu ambavyo vingewasaidia watu kujifunza kumhusu Mungu. Baada ya kukipitia kitabu cha miradi cha Kyle, kilichoandikwa miaka mingi iliyopita, mama yake alisema, “Alifikia miradi yote hiyo.”

Wewe umejiwekea miradi gani? Hujui maisha yako yatakuwa namna gani kesho. Kwa hiyo, tumia kikamili kila siku ya maisha yako. Kama Catrina na Kyle, tumia wakati wako kwa njia yenye kuthawabisha zaidi. Fuata mfano wa mtume Paulo, ambaye alipokaribia kufa alisema: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.” (2 Timotheo 4:7) Sura inayofuata itakusaidia kufanya vivyo hivyo!

[Picha katika ukurasa wa 275]

Ukitaka kuwa na afya nzuri, unahitaji kufanya mazoezi. Ukitaka kuwa na afya nzuri ya kiroho, unahitaji kujifunza Neno la Mungu