Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 14

Mapainia Huzoezwa Katika Shule Gani?

Mapainia Huzoezwa Katika Shule Gani?

Marekani

Shule ya Gileadi, Patterson, New York

Panama

Kwa miaka mingi elimu ya kitheokrasi imekaziwa sana na Mashahidi wa Yehova. Shule za pekee huandaliwa kwa ajili ya wale wanaotumikia wakiwa wahubiri wa wakati wote wa Ufalme ili ‘watimize kikamili huduma yao.’—2 Timotheo 4:5.

Shule ya Utumishi wa Painia. Mwaka mmoja baada ya kuwa painia wa kawaida, mapainia huhudhuria shule ya siku sita ambayo hufanywa kwenye Jumba la Ufalme. Kusudi la shule hiyo ni kumsaidia painia amkaribie zaidi Yehova, aboreshe uwezo wake katika sehemu mbalimbali za huduma, na aendelee kutumikia kwa uaminifu.

Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Shule hii ya miezi miwili imekusudiwa kuwazoeza mapainia wenye uzoefu ambao wako tayari kuhama nyumbani na kwenda kokote wanakohitajiwa. Ni kana kwamba wanasema, “Mimi hapa! Nitume mimi!” kwa kumwiga Mweneza-Injili mkuu zaidi, Yesu Kristo. (Isaya 6:8; Yohana 7:29) Baada ya kuhamia eneo lingine, huenda wakalazimika kuishi maisha rahisi. Huenda utamaduni, hali ya hewa, na vyakula vikawa tofauti na walivyozoea. Huenda pia wakahitaji kujifunza lugha mpya. Shule hii huwazoeza ndugu na dada waseja pamoja na wenzi wa ndoa, wenye umri kati ya miaka 23 na 65, wasitawishe sifa za kiroho watakazohitaji katika migawo yao na ustadi utakaowasaidia kumtumikia Yehova na tengenezo lake kikamili zaidi.

Shule ya Gileadi. Katika Kiebrania neno “Gileadi” linamaanisha “Rundo la Ushahidi.” Tangu mwaka wa 1943, zaidi ya wamishonari 8,000 waliozoezwa katika Shule ya Gileadi wametumwa ili kutoa ushahidi “mpaka miisho ya dunia” na hiyo imeleta mafanikio makubwa. (Matendo 13:47) Wamishonari wetu walipofika nchini Peru, hakukuwa na kutaniko lolote huko. Sasa kuna zaidi ya makutaniko 1,000. Wamishonari wetu walipoanza kutumikia nchini Japani, kulikuwa na Mashahidi wasiozidi kumi. Sasa kuna zaidi ya Mashahidi 200,000. Mazoezi ya Gileadi yanayofanywa kwa miezi mitano yanatia ndani kujifunza Neno la Mungu kwa undani. Wale wanaotumikia wakiwa mapainia wa pekee au wamishonari, wale wanaotumikia kwenye ofisi za tawi, au wanaofanya kazi ya kuzungukia makutaniko hualikwa kwenye shule hii ili wajifunze kwa kina na hivyo kusaidia kuimarisha kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.

  • Shule ya Utumishi wa Painia inatimiza kusudi gani?

  • Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme iliandaliwa kwa ajili ya akina nani?