Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 18

Tunawasaidiaje Ndugu Zetu Wakati wa Taabu?

Tunawasaidiaje Ndugu Zetu Wakati wa Taabu?

Jamhuri ya Dominika

Japani

Haiti

Janga linapotokea, mara moja Mashahidi wa Yehova hupanga kuwasaidia ndugu zao ambao wanahitaji msaada. Jitihada hizo huonyesha upendo wa kweli tulio nao. (Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:17, 18) Tunatoa msaada katika njia zipi?

Tunatoa msaada wa kifedha. Njaa kali ilipotokea Yudea, Wakristo wa karne ya kwanza huko Antiokia waliwatumia ndugu zao wa kiroho msaada wa kifedha. (Matendo 11:27-30) Vivyo hivyo, tunaposikia kwamba ndugu zetu katika sehemu nyingine za dunia wanakabili hali ngumu, tunatuma fedha kupitia kutaniko letu ili kuwasaidia.—2 Wakorintho 8:13-15.

Tunatoa huduma zinazohitajika. Wazee wanaotumikia katika eneo lililokumbwa na janga hujitahidi kuwasiliana na kila mshiriki wa kutaniko na kuhakikisha wote wako salama. Halmashauri ya kutoa misaada inaweza kuratibu kugawanywa kwa chakula, maji safi ya kunywa, nguo, makao, na matibabu. Mashahidi wengi wenye ujuzi hujitolea kusafiri kwa gharama zao wenyewe ili kushiriki katika kazi hiyo ya kutoa misaada au kurekebisha nyumba na Majumba ya Ufalme yaliyoharibiwa. Umoja tunaofurahia tukiwa tengenezo na uzoefu ambao tumepata kwa kufanya kazi pamoja, hutuwezesha kupanga mambo haraka uhitaji unapotokea. Ijapokuwa sisi huwasaidia “wale ambao ni ndugu zetu katika imani,” tunawasaidia wengine pia iwezekanapo, haidhuru dini yao.—Wagalatia 6:10.

Tunatoa msaada wa kiroho na faraja. Waliokumbwa na janga mara nyingi huhitaji faraja. Katika nyakati hizo, tunatiwa nguvu na Yehova, “Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Tunafurahia kuzungumza pamoja na wale walio katika hali hizo kuhusu ahadi za Biblia zinazowahakikishia kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utakomesha majanga yote yanayosababisha uchungu na kuteseka.—Ufunuo 21:4.

  • Kwa nini Mashahidi huitikia haraka majanga yanapotokea?

  • Ni ujumbe gani wa kiroho wenye kufariji tunaoweza kuzungumzia na watu waliokabili hali ngumu?