Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 19

Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara Ni Nani?

Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara Ni Nani?

Sote tunafaidika na chakula chetu cha kiroho

Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alifanya mazungumzo ya faragha pamoja na wanafunzi wake wanne—Petro, Yakobo, Yohana, na Andrea. Yesu alipokuwa akitabiri ishara ya kuwapo kwake katika siku za mwisho, aliuliza swali muhimu: “Kwa kweli ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi asimamie watumishi wake wa nyumbani na kuwapa chakula chao kwa wakati unaofaa?” (Mathayo 24:3, 45; Marko 13:3, 4) Yesu alikuwa akiwahakikishia wanafunzi wake kwamba akiwa “bwana” wao, angewaweka rasmi wale ambao wangekuwa wakiwaandalia wafuasi wake chakula cha kiroho katika siku za mwisho. Watu hao wangekuwa akina nani?

Ni kikundi kidogo cha wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta. “Mtumwa” huyo huhusianishwa hasa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Anawaandalia waabudu wenzake chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Tunamtegemea mtumwa huyo mwaminifu aendelee kutuandalia “kipimo [chetu] cha chakula kwa wakati unaofaa.”—Luka 12:42.

Anasimamia nyumba ya Mungu. (1 Timotheo 3:15) Yesu alimpa mtumwa jukumu zito la kusimamia kazi ya sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Kazi hiyo inatia ndani kutunza mali zake, kuelekeza utendaji wa kuhubiri, na kutufundisha kupitia makutaniko. Kwa hiyo, ili kutuandalia kile tunachohitaji wakati tunapokihitaji, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anatuandalia chakula cha kiroho kupitia machapisho tunayotumia katika huduma, na pia kupitia mikutano na makusanyiko.

Mtumwa huyo ni mwaminifu kwa kushikamana na kweli za Biblia na utume wa kuhubiri habari njema, naye ni mwenye busara katika kutunza kwa hekima mali za Kristo duniani. (Matendo 10:42) Yehova anabariki kazi ya mtumwa huyo kwa maandalizi mengi ya kiroho na ongezeko.—Isaya 60:22; 65:13.

  • Ni nani aliyewekwa na Yesu kuwalisha wanafunzi wake kiroho?

  • Ni katika njia gani mtumwa huyo ni mwaminifu na mwenye busara?