Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 20

Baraza Linaloongoza Hufanyaje Kazi Leo?

Baraza Linaloongoza Hufanyaje Kazi Leo?

Baraza linaloongoza la karne ya kwanza

Kusomwa kwa barua ya baraza linaloongoza

Katika karne ya kwanza, kikundi kidogo, yaani, “mitume na wazee huko Yerusalemu,” kilitumikia kikiwa baraza linaloongoza lililofanya maamuzi muhimu kwa niaba ya kutaniko zima la Wakristo watiwa mafuta. (Matendo 15:2) Kuzungumzia Maandiko na kukubali mwongozo wa roho ya Mungu kuliwawezesha kufanya uamuzi kwa kauli moja. (Matendo 15:25) Ndivyo ilivyo leo pia.

Linatumiwa na Mungu kufanya mapenzi yake. Ndugu waliotiwa mafuta walio katika Baraza Linaloongoza wanapendezwa sana na Neno la Mungu nao wana uzoefu mwingi wa kutoa mwongozo kuhusu jinsi kazi inavyopaswa kufanywa, na pia kujibu maswali yanayohusiana na mambo ya kiroho. Wao hufanya mkutano kila juma ili kufikiria mahitaji ya ushirika wa akina ndugu ulimwenguni pote. Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, maagizo yanayotegemea Biblia huandaliwa kupitia barua, waangalizi wanaosafiri, au vinginevyo. Jambo hili huwasaidia watu wa Mungu wawe na umoja. (Matendo 16:4, 5) Baraza Linaloongoza husimamia kuandaliwa kwa chakula cha kiroho, huwatia moyo wote washiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme, nalo husimamia kuwekwa kwa akina ndugu katika majukumu ya usimamizi.

Linafuata mwelekezo wa roho ya Mungu. Baraza Linaloongoza humtegemea Mwenye Enzi Kuu, Yehova, na pia Kichwa cha kutaniko, Yesu, ili kupata mwongozo. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:23) Ndugu walio katika baraza hilo hawajioni kuwa viongozi wa watu wa Mungu. Wao, pamoja na Wakristo wote watiwa-mafuta, wanaendelea “kumfuata Mwanakondoo [Yesu] popote anapoenda.” (Ufunuo 14:4) Baraza Linaloongoza huthamini sala zetu kwa niaba yao.

  • Ni nani waliokuwa katika baraza linaloongoza katika karne ya kwanza?

  • Baraza Linaloongoza hutafuta mwongozo wa Mungu jinsi gani leo?