Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 24

Kazi Yetu ya Ulimwenguni Pote Inagharimiwaje?

Kazi Yetu ya Ulimwenguni Pote Inagharimiwaje?

Nepal

Togo

Uingereza

Tengenezo letu linachapisha na kusambaza mamia ya mamilioni ya Biblia na machapisho mengine kila mwaka bila malipo. Tunajenga na kurekebisha Majumba ya Ufalme na ofisi za tawi. Tunatunza maelfu ya Wanabetheli na wamishonari, na pia kutoa msaada wakati wa majanga. Kwa hiyo, huenda ukajiuliza, ‘Kazi yote hii inagharimiwaje?’

Hatukusanyi sadaka wala fungu la kumi. Ingawa gharama za kutegemeza kazi ya kuhubiri habari njema ni kubwa, hatuombi-ombi fedha. Zaidi ya miaka 100 iliyopita, toleo la pili la Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba tunaamini Yehova ndiye anayetusaidia na kwamba ‘hatutawaomba-omba watu au kuwasihi watutegemeze,’ nasi hatujawahi kufanya hivyo!—Mathayo 10:8.

Kazi yetu inategemezwa kwa michango ya hiari. Watu wengi wanathamini kazi yetu ya kufundisha Biblia, nao hutoa michango ili kuiunga mkono. Mashahidi wenyewe wanatumia wakati, nguvu, fedha, na rasilimali zao nyingine ili kutimiza mapenzi ya Mungu duniani kote. (1 Mambo ya Nyakati 29:9) Kuna masanduku ya michango katika Majumba ya Ufalme na makusanyikoni, na wote wanaopenda wanaweza kutoa michango ya hiari. Pia, michango inaweza kutolewa kupitia tovuti yetu ya jw.org. Sehemu kubwa ya fedha tunazopokea ni michango ya watu wa kawaida ambao si matajiri, kama yule mjane maskini ambaye Yesu alimsifu. Mjane huyo alitumbukiza sarafu mbili ndogo kwenye sanduku la hazina la hekalu. (Luka 21:1-4) Kwa hiyo mtu yeyote anaweza “kuweka kando kitu fulani” kwa ukawaida ili atoe mchango “kama alivyoazimia moyoni mwake.”—1 Wakorintho 16:2; 2 Wakorintho 9:7.

Tuna hakika kwamba Yehova ataendelea kuchochea mioyo ya wale wanaotaka ‘kumheshimu kwa vitu vyao vyenye thamani,’ kwa kuunga mkono kazi ya Ufalme, ili mapenzi yake yatendeke.—Methali 3:9.

  • Ni nini kinachofanya tengenezo letu liwe tofauti na dini nyinginezo?

  • Michango inatumika jinsi gani?