Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 28

Ni Habari Gani Zinazopatikana Kwenye Tovuti Yetu?

Ni Habari Gani Zinazopatikana Kwenye Tovuti Yetu?

Ufaransa

Poland

Urusi

Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake hivi: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili waone matendo yenu mema na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:16) Hiyo ndiyo sababu tunatumia teknolojia ya kisasa, kutia ndani Intaneti. Tovuti yetu, jw.org, ni kituo rasmi chenye taarifa kuhusu imani na utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Mambo hayo yanatia ndani nini?

Majibu ya Biblia ya maswali ambayo huulizwa kwa ukawaida. Unaweza kupata majibu ya maswali muhimu ambayo watu hujiuliza. Kwa mfano trakti, Je, Kuteseka Kutaisha? na Je, Kweli Wafu Wataishi Tena? zinapatikana kwenye mtandao katika lugha zaidi ya 600. Pia unaweza kupata Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha zaidi ya 130 pamoja na vifaa vya kukusaidia kujifunza Biblia, kutia ndani kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? na matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Machapisho mengi yanaweza kusikilizwa au kusomwa kwenye mtandao au hata kupakuliwa kama MP3, PDF, au EPUB. Hata unaweza kuchapisha kurasa kadhaa za kusoma na mtu anayependezwa katika lugha yake! Video zinapatikana katika lugha nyingi za ishara. Pia, unaweza kupakua drama za Biblia na muziki mtamu unaoweza kusikiliza unapopumzika.

Habari za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova. Pia kwenye tovuti kuna habari za karibuni kuhusu kazi yetu ya ulimwenguni pote, matukio yanayowahusu Mashahidi wa Yehova, na jitihada zetu za kutoa misaada. Unaweza kupata taarifa kuhusu makusanyiko yajayo na anwani za ofisi zetu za tawi.

Kupitia njia hizi tunaangaza nuru ya kweli kwa mapana na marefu. Watu wa kila bara, kutia ndani Antaktika, wanafaidika. Tunasali “neno la Yehova lizidi kuenea upesi” duniani kote kwa utukufu wa Mungu.—2 Wathesalonike 3:1.

  • Tovuti ya jw.org inawasaidiaje watu wengi kujifunza Biblia?

  • Ungependa kuchunguza nini katika tovuti yetu?