Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 6

Daudi Hakuogopa

Daudi Hakuogopa

Wewe hufanya nini unapoogopa?— Labda unaenda kwa mama na baba yako ili wakusaidie. Lakini, kuna mtu mwingine ambaye anaweza kukusaidia pia. Mtu huyo ana nguvu nyingi kuliko mtu mwingine yeyote. Je, unamjua mtu huyo?— Bila shaka, ni Yehova Mungu. Sasa, ngoja tujifunze kuhusu kijana fulani anayetajwa katika Biblia, aitwaye Daudi. Alijua kwamba Yehova angemsaidia kila wakati, hivyo hakuogopa.

Daudi alimpenda sana Yehova kwa sababu tangu alipokuwa mtoto mdogo wazazi wake walimfundisha afanye hivyo. Jambo hilo lilimsaidia Daudi asiogope hata wakati ambapo alikabili mambo yenye kuogopesha. Daudi alijua kwamba Yehova ni Rafiki yake, na hivyo alikuwa na hakika kwamba atamsaidia. Siku moja, Daudi alipokuwa akichunga kondoo, simba mkubwa akaja na kumkamata kondoo! Je, unajua Daudi alifanya nini? Alimkimbiza simba huyo na hatimaye alipompata huenda alimuua bila silaha yoyote! Na katika tukio lingine dubu alivamia kondoo, lakini Daudi alimuua dubu huyo pia! Unafikiri ni nani aliyemsaidia?— Bila shaka, Yehova ndiye aliyemsaidia.

Kuna wakati mwingine tena ambapo kwa kweli Daudi alitenda kwa ujasiri mkubwa sana. Waisraeli walikuwa wakipigana na watu walioitwa Wafilisti. Mwanajeshi fulani aliyekuwa miongoni mwa Wafilisti alikuwa mrefu, mrefu kama mlingoti, lilikuwa jitu kubwa sana! Jina lake lilikuwa Goliathi. Jitu hilo lilikuwa likiwadhihaki Waisraeli na Yehova pia. Liliwaambia wanajeshi wa Israeli kwamba kama wana ujasiri waende kupigana naye. Hata hivyo, Waisraeli wote waliogopa sana hivi kwamba hawangeweza kupigana naye. Daudi aliposikia kuhusu jambo hilo, alimwambia hivi Goliathi: ‘Nitapigana nawe! Yehova atanisaidia, na nitakushinda!’ Je, unafikiri Daudi alikuwa jasiri?— Bila shaka, alikuwa jasiri sana. Je, ungependa kujua ni nini kilichotokea baada ya hapo?

Daudi alichukua kombeo lake na mawe laini matano, kisha akalisogelea jitu hilo ili kupigana nalo. Goliathi alipoona jinsi kijana Daudi alivyo, akaanza kumdhihaki. Hata hivyo, Daudi akamwambia hivi: ‘Unakuja kwangu ukiwa na upanga, lakini mimi ninakuja kwako nikiwa na jina la Yehova!’ Kisha Daudi akaweka jiwe kwenye kombeo lake, akakimbia kuelekea mahali alipokuwa Goliathi, halafu akamrushia Goliathi. Jiwe hilo likampiga Goliathi katikati ya macho yake! Jitu hilo likaanguka chini, likafa! Wafilisti waliogopa sana, kwa hiyo wote wakakimbia. Kijana mdogo kama Daudi aliwezaje kulishinda jitu kama hilo?— Yehova alimsaidia, na Yehova alikuwa na nguvu nyingi sana kuliko jitu hilo!

Daudi hakuogopa kwa sababu alijua kwamba Yehova Angemsaidia

Unajifunza jambo gani katika hadithi hii ya Daudi?— Yehova ana nguvu nyingi sana kuliko mtu mwingine yeyote, naye anaweza kuwa Rafiki yako. Kwa hiyo, wakati mwingine ukiogopa, kumbuka jambo hili, Yehova anaweza kukusaidia ili uwe jasiri!

SOMA KATIKA BIBLIA YAKO