Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 9

Yeremia Hakuacha Kuongea na Watu Kuhusu Yehova

Yeremia Hakuacha Kuongea na Watu Kuhusu Yehova

Kwa nini watu walimkasirikia Yeremia?

Yehova alimwokoa Yeremia

Wakati fulani watu wanatucheka au wanatukasirikia tunapoongea nao kuhusu Yehova. Jambo hilo linaweza kutufanya tutamani kuacha kuongea kuhusu Mungu. Je, umewahi kuhisi hivyo?— Biblia inatuambia kuhusu kijana fulani ambaye alimpenda Yehova, lakini ilibaki kidogo tu aache kuongea kuhusu Yehova. Kijana huyo aliitwa Yeremia. Sasa, ngoja tujifunze mambo fulani kuhusu kijana huyo.

Yeremia alipokuwa kijana, Yehova alimwambia kwamba alipaswa kuwaonya watu ili waache kufanya mambo mabaya. Yeremia aliona jambo hilo kuwa gumu sana, na aliogopa kufanya hivyo. Kwa hiyo akamwambia hivi Yehova: ‘Sijui jambo la kusema. Kwa sababu mimi ni mvulana tu.’ Lakini Yehova akamwambia: ‘Usiogope. Mimi nitakusaidia.’

Kwa hiyo Yeremia akaanza kuwaonya watu kwamba wangeadhibiwa ikiwa hawangebadilika. Je, unafikiri watu walibadili njia zao kama Yeremia alivyowaambia?— Hapana. Walimcheka au kumkasirikia Yeremia. Baadhi yao hata walitaka kumuua! Unafikiri Yeremia alihisije?— Aliogopa, na kisha akasema hivi: ‘Sitaongea tena kuhusu Yehova.’ Hata hivyo, je, aliacha kuongea kuhusu Yehova?— Hapana, hakuacha. Yeremia alimpenda sana Yehova, hivi kwamba hakuacha kuongea na watu kuhusu Yehova. Na kwa sababu Yeremia hakuacha kuongea kuhusu Yehova, Yehova alimlinda.

Kwa mfano, siku moja watu fulani wabaya walimtupa Yeremia ndani ya shimo lililojaa matope. Akiwa ndani ya shimo hilo hakuwa na chakula wala maji. Watu hao walitaka kumwacha Yeremia kwenye shimo hilo ili afe. Lakini Yehova alimsaidia Yeremia, na hivyo akatoka ndani ya shimo hilo!

Unajifunza jambo gani katika mfano wa Yeremia?— Ingawa wakati fulani aliogopa, hakuacha kuongea na watu kuhusu Yehova. Unapoongea na watu kuhusu Yehova, huenda wakakucheka au wakakukasirikia. Huenda ukaaibika au hata kuogopa. Hata hivyo, usiache kamwe kuongea na watu kuhusu Yehova. Siku zote atakusaidia, kama alivyomsaidia Yeremia.