Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 1

“Ufalme Wako na Uje”

“Ufalme Wako na Uje”

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Inazungumzia mambo ambayo Yesu alifundisha kuhusu Ufalme wa Mungu

1, 2. Mitume watatu wa Yesu walimsikia Yehova akisema nini, nao waliitikiaje?

IKIWA Yehova Mungu angekuagiza ufanye jambo fulani, ungeitikiaje? Bila shaka ungekuwa tayari kufanya chochote ambacho amekuagiza, sivyo?

2 Muda fulani baada ya Pasaka ya mwaka wa 32 W.K., mitume watatu wa Yesu—Petro, Yakobo, na Yohana—waliagizwa na Yehova wafanye jambo fulani. (Soma Mathayo 17:1-5.) Wakiwa wamekusanyika pamoja na Bwana wao juu ya “mlima mrefu,” walimwona Yesu katika maono akiwa Mfalme mwenye utukufu mbinguni. Maono hayo yalionekana kuwa halisi sana hivi kwamba Petro alitaka kushiriki katika maono hayo. Wakati Petro alipokuwa akizungumza, wingu likawafunika. Kisha Petro na wenzake wakasikia sauti ya Yehova, pendeleo ambalo ni wanadamu wachache sana wamewahi kupata. Baada ya kuwathibitishia kwamba Yesu alikuwa Mwana wake, Yehova alisema hivi waziwazi: “Msikilizeni.” Mitume walitii agizo hilo la Mungu. Walisikiliza yale ambayo Yesu alifundisha, na kuwahimiza wengine wafanye vivyo hivyo.—Mdo. 3:19-23; 4:18-20.

Yesu alizungumzia sana Ufame wa Mungu kuliko mambo mengine

3. Kwa nini Yehova anataka tumsikilize Mwana wake, na hivyo itafaa tuchunguze habari gani?

3 Agizo hilo—“Msikilizeni”—liliandikwa katika Biblia kwa faida yetu. (Rom. 15:4) Kwa nini? Kwa sababu Yesu ni Msemaji wa Yehova na kila wakati Yesu alipofundisha, alisema yale ambayo Baba yake alitaka tujue. (Yoh. 1:1, 14) Kwa kuwa Yesu alizungumza sana kuhusu Ufalme wa Mungu, yaani, serikali ya mbinguni ya Kimasihi inayofanyizwa na Kristo Yesu na watawala wenzake 144,000, kuliko alivyozungumzia jambo lingine lolote, itafaa tuchunguze kwa makini habari hiyo muhimu. (Ufu. 5:9, 10; 14:1-3; 20:6) Hata hivyo, acheni kwanza tuchunguze kwa nini Yesu alizungumza sana kuhusu Ufalme wa Mungu.

‘Kutokana na Mambo Yaliyojaa Katika Moyo’

4. Yesu alionyeshaje kwamba Ufalme ulikuwa jambo muhimu kwake?

4 Yesu anauona Ufalme kuwa jambo muhimu sana. Kwa nini tunasema hivyo? Kwa sababu maneno hufunua kile kilicho moyoni, yaani, maneno yetu hufunua mambo tunayoona kuwa muhimu. Yesu mwenyewe alisema: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mt. 12:34) Kila alipopata nafasi, Yesu alizungumza kuhusu Ufalme. Katika vitabu vinne vya Injili kuna zaidi ya marejeo 100 kuhusu Ufalme, na mengi ya marejeo hayo ni maneno ya Yesu. Yesu alionyesha kwamba Ufalme ulikuwa kichwa kikuu cha mahubiri yake aliposema: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Hata baada ya kufufuliwa, Yesu aliendelea kuwaambia wanafunzi wake kuhusu Ufalme. (Mdo. 1:3) Kwa hakika, Yesu aliuthamini sana Ufalme hivi kwamba alichochewa kuzungumza kuuhusu.

5-7. (a) Tunajuaje kwamba Yehova anauona Ufalme kuwa jambo muhimu sana? Toa mfano. (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba Ufalme ni jambo muhimu sana kwetu?

5 Yehova pia anauona Ufalme kuwa jambo muhimu sana. Tunajuaje? Kumbuka kwamba Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni; Yehova ndiye chanzo cha kila kitu ambacho Mwana wake alisema na kufundisha. (Yoh. 7:16; 12:49, 50) Pia, Yehova ndiye chanzo cha mambo yote yaliyoandikwa katika vile vitabu vinne vya Injili vinavyozungumzia maisha na huduma ya Yesu. Hebu fikiria kidogo, jambo hilo linamaanisha nini.

Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, ninauona Ufalme wa Mungu kuwa jambo muhimu sana?’

6 Tuseme unapanga picha za familia yenu kwenye albamu. Una picha nyingi za kuweka, lakini albamu inaweza kuchukua picha chache tu. Utafanya nini? Utachagua zile tu ambazo ungependa kuziweka kwenye albamu. Vivyo hivyo, vitabu vya Injili ni kama albamu ya picha ambayo inatupatia picha halisi ya Yesu. Yehova hakuwaongoza waandishi wa vitabu vya Injili kuandika kila jambo ambalo Yesu alisema na kufanya alipokuwa duniani. (Yoh. 20:30; 21:25) Badala yake, roho ya Yehova iliwaongoza kuandika maneno na matendo ambayo yanatusaidia kuelewa kusudi la huduma ya Yesu na mapenzi ya Yehova. (2 Tim. 3:16, 17; 2 Pet. 1:21) Kwa kuwa vitabu vya Injili vimejaa mafundisho ya Yesu kuhusu Ufalme wa Mungu, hatutakuwa tumekosea tukisema kwamba Yehova anauona Ufalme kuwa jambo muhimu sana. Bila shaka, Yehova anataka tujue kusudi la Ufalme wake!

7 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, ninauona Ufalme wa Mungu kuwa jambo muhimu sana?’ Ikiwa ndivyo, tutakuwa na hamu ya kusikiliza yale ambayo Yesu alisema na kufundisha kuhusu Ufalme huo, yaani, umuhimu wake, jinsi utakavyokuja, na utakuja lini.

“Ufalme Wako na Uje”—Jinsi Gani?

8. Yesu alielezaje umuhimu wa Ufalme?

8 Fikiria ile sala ya kielelezo. Akitumia maneno yaliyo wazi na rahisi kueleweka, Yesu alieleza umuhimu wa Ufalme kwa kuonyesha yale ambayo utatimiza. Sala hiyo ina maombi saba. Maombi matatu ya kwanza yanahusu makusudi ya Yehova, yaani, kutakaswa kwa jina lake, kuja kwa Ufalme wake, na kufanywa kwa mapenzi yake duniani kama ilivyo mbinguni. (Soma Mathayo 6:9, 10.) Maombi hayo matatu yanahusiana sana. Yehova atatumia Ufalme wa Kimasihi kutakasa jina lake na kufanya mapenzi yake.

9, 10. (a) Ufalme wa Mungu utakuja jinsi gani? (b) Ni ahadi gani ya Biblia ambayo ungependa kuona ikitimizwa?

9 Ufalme wa Mungu utakuja jinsi gani? Tunaposali, “Ufalme wako na uje,” tunaomba kwamba Ufalme uchukue hatua thabiti. Ufalme huo utakapokuja, utaonyesha mamlaka yake kikamili duniani. Utaondoa mfumo huu mwovu wa mambo, kutia ndani serikali zote za wanadamu, na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. (Dan. 2:44; 2 Pet. 3:13) Halafu, chini ya utawala wa Ufalme, dunia yote itakuwa paradiso. (Luka 23:43) Wale wote walio katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa na kuungana na wapendwa wao. (Yoh. 5:28, 29) Wanadamu watiifu watafikia ukamilifu na kufurahia uzima wa milele. (Ufu. 21:3-5) Mwishowe, mapenzi ya Yehova Mungu yatatendeka duniani kama ilivyo mbinguni! Je, hungependa kuona ahadi hizo za Biblia zikitimia? Kumbuka kwamba kila mara unaposali Ufalme wa Mungu uje, unaomba ahadi hizo bora zitimizwe.

10 Ni wazi kwamba Ufalme wa Mungu bado ‘haujaja’ ili kutimiza ile sala ya kielelezo. Bado serikali za wanadamu zinatawala na ulimwengu mpya wenye uadilifu bado haujafika. Lakini kuna habari njema. Ufalme wa Mungu tayari umesimamishwa, kama tutakavyozungumzia katika sura inayofuata. Acheni sasa tuchunguze yale ambayo Yesu alisema kuhusu wakati ambapo Ufalme huo ungesimamishwa na wakati ambapo ungekuja.

Ufalme wa Mungu Ungesimamishwa Lini?

11. Yesu alisema nini kuhusu kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu?

11 Yesu alionyesha kwamba Ufalme wa Mungu haungesimamishwa katika karne ya kwanza W.K., licha ya matarajio ya baadhi ya wanafunzi wake. (Mdo. 1:6) Fikiria mifano miwili aliyoitoa katika vipindi viwili tofauti.

12.. Mfano wa ngano na magugu unaonyeshaje kwamba Ufalme haukusimamishwa katika karne ya kwanza W.K.?

12 Mfano wa ngano na magugu. (Soma Mathayo 13:24-30.) Baada ya kuzungumzia mfano huo, labda mwanzoni mwa mwaka wa 31 W.K., Yesu aliwafafanulia wanafunzi wake. (Mt. 13:36-43) Jambo kuu na maana ya mfano huo ni: Baada ya kifo cha mitume, Ibilisi angepanda magugu (Wakristo wa uwongo) katikati ya ngano (“wana wa Ufalme,” au Wakristo watiwa-mafuta). Ngano na magugu yangeachwa yakue pamoja wakati wa majira ya ukuzi ambayo yangeendelea mpaka wakati wa mavuno, ambayo ni “umalizio wa mfumo wa mambo.” Baada ya majira ya mavuno kuanza, magugu yangekusanywa. Kisha, ngano ingekusanywa. Kwa hiyo, mfano huo unaonyesha kwamba Ufalme haungesimamishwa katika karne ya kwanza  W.K., bali ungesimamishwa baada ya majira ya ukuzi kumalizika. Kama ilivyotukia, majira ya ukuzi yalimalizika na majira ya mavuno yakaanza mwaka wa 1914.

13. Yesu alitumia mfano gani kuonyesha kwamba hangewekwa rasmi kuwa Mfalme wa Kimasihi baada tu ya kurudi mbinguni?

13 Mfano wa mina. (Soma Luka 19:11-13.) Yesu alitoa mfano huo mwaka wa 33 W.K. alipokuwa akielekea Yerusalemu kwa mara ya mwisho. Baadhi ya wasikilizaji wake walifikiri kwamba angeusimamisha Ufalme wake mara tu walipofika Yerusalemu. Ili kusahihisha wazo hilo na kuonyesha kwamba Ufalme ungesimamishwa miaka mingi baadaye, Yesu alijifananisha na “mtu fulani mashuhuri” ambaye alisafiri “mpaka nchi ya mbali ili ajipatie mamlaka ya kifalme.” * Katika kisa cha Yesu, “nchi ya mbali” ilikuwa mbinguni, ambako angepokea mamlaka ya kuwa Mfalme kutoka kwa Baba yake. Hata hivyo, Yesu alijua kwamba hangewekwa rasmi kuwa Mfalme wa Kimasihi baada tu ya kurudi mbinguni. Badala yake, angeketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu na kusubiri mpaka wakati uliowekwa. Kama ilivyotukia, alisubiri kwa karne nyingi.—Zab. 110:1, 2; Mt. 22:43, 44; Ebr. 10:12, 13.

Ufalme wa Mungu Utakuja Lini?

14. (a) Yesu alijibuje swali aliloulizwa na mitume wake wanne? (b) Kutimia kwa unabii wa Yesu kunaonyesha nini kuhusu kuwapo kwake na kusimamishwa kwa Ufalme?

14 Siku chache kabla ya Yesu kuuawa, mitume wake wanne walimuuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:3; Marko 13:4) Yesu alijibu kwa kutaja unabii wenye mambo mengi unaopatikana kwenye Mathayo sura ya 24 na 25. Yesu alizungumzia kwa kina matukio mbalimbali ulimwenguni ambayo yangekuwa ishara ya kutambulisha kipindi cha wakati kinachoitwa “kuwapo” kwake. Kuwapo kwake kunaanza wakati Ufalme unaposimamishwa na kutaisha wakati Ufalme utakapoanza kutawala duniani kote. Tuna uthibitisho wa kutosha kwamba unabii wa Yesu umekuwa ukitimia tangu 1914. * Hivyo, mwaka huo ndio uliokuwa mwanzo wa kuwapo kwake na kusimamishwa kwa Ufalme.

15, 16. Maneno “kizazi hiki” yanarejelea nani?

15 Hata hivyo, Ufalme wa Mungu utakuja lini? Yesu hakutaja wakati hususa ambao Ufalme huo ungekuja. (Mt. 24:36) Lakini alisema jambo fulani ambalo linapaswa kutuhakikishia kwamba Ufalme huo uko karibu sana. Yesu alisema kwamba Ufalme ungekuja baada ya “kizazi hiki” kushuhudia utimizo wa ishara ya unabii. (Soma Mathayo 24:32-34.) Maneno “kizazi hiki” yanarejelea nani? Acheni tuchunguze kwa makini maneno hayo ya Yesu.

16 “Kizazi hiki.” Je, Yesu alikuwa akirejelea watu wasioamini? Hapana. Fikiria wasikilizaji wake. Yesu alitoa unabii huo kwa mitume wake wachache ambao ‘walimkaribia faraghani.’ (Mt. 24:3) Punde si punde mitume wangetiwa mafuta kwa roho takatifu. Fikiria pia muktadha. Kabla hajasema kuhusu “kizazi hiki,” Yesu alisema: “Basi jifunzeni jambo hili kutokana na mtini kama mfano: Mara tu tawi lake changa linapokuwa jororo na kutoa majani, mnajua kwamba kiangazi kiko karibu. Vivyo hivyo ninyi pia, mnapoona mambo yote hayo, jueni kwamba yuko karibu milangoni.” Wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta—na si watu wasioamini—ndio wangeona mambo ambayo Yesu alitabiri na kutambua maana yake, yaani, kwamba Yesu “yuko karibu milangoni.” Kwa hiyo, Yesu aliposema kuhusu “kizazi hiki,” alikuwa akirejelea wafuasi wake watiwa-mafuta.

17. Maneno “kizazi” na “mambo yote hayo” yanamaanisha nini?

17 “Hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote hayo yatukie.” Maneno hayo yatatimiaje? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kujua mambo mawili: maana ya “kizazi” na “mambo yote hayo.” Neno “kizazi” mara nyingi hurejelea watu wenye umri mbalimbali ambao maisha yao yanapishana katika kipindi fulani hususa cha wakati. Kizazi si kipindi kirefu sana, na kina mwisho. (Kut. 1:6) Maneno “mambo yote hayo” yanatia ndani matukio yote yaliyotabiriwa kwamba yangetukia wakati wa kuwapo kwa Yesu, kulikoanza mwaka wa 1914 na kutamalizika wakati wa “dhiki kuu.”—Mt. 24:21.

18, 19. Tunaweza kuelewaje maneno ya Yesu kuhusu “kizazi hiki,” na tunaweza kufikia mkataa gani?

18 Hivyo basi, tueleweje maneno ya Yesu kuhusu “kizazi hiki”? Kizazi hicho kinafanyizwa na vikundi viwili vya watiwa-mafuta ambao maisha yao yanapishana. Kikundi cha kwanza kinafanyizwa na watiwa-mafuta ambao waliona mwanzo wa utimizo wa ile ishara katika mwaka wa 1914 na kikundi cha pili kinafanyizwa na watiwa-mafuta ambao kwa muda fulani waliishi wakati mmoja na wale wa kikundi cha kwanza. Angalau baadhi ya watiwa-mafuta walio katika kikundi cha pili wataona mwanzo wa dhiki kuu inayokuja. Vikundi vyote viwili vinafanyiza kizazi kimoja kwa sababu maisha yao wakiwa Wakristo watiwa-mafuta yanapishana kwa muda fulani. *

19 Tunaweza kufikia mkataa gani? Tunajua kwamba ishara ya kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Kifalme inaonekana wazi ulimwenguni pote. Pia, tunaona kwamba watiwa-mafuta ambao bado wako hai na ni sehemu ya “kizazi hiki” wanaendelea kuzeeka; hata hivyo, hawatakufa wote kabla ya dhiki kuu kuanza. Hivyo basi, tunaweza kufikia mkataa kwamba hivi karibuni pasipo shaka Ufalme wa Mungu utakuja na kutawala juu ya dunia! Itasisimua sana kuona utimizo wa sala tuliyofundishwa na Yesu: “Ufalme wako na uje”!

20. Ni habari gani muhimu itakayozungumziwa katika kitabu hiki, na tutachunguza nini katika sura inayofuata?

20 Tusisahau kamwe jambo ambalo Yehova mwenyewe alisema kutoka mbinguni kuhusu Mwana wake: “Msikilizeni.” Tukiwa Wakristo wa kweli, tuna hamu ya kutii agizo hilo la Mungu. Tunapendezwa kabisa na kila kitu ambacho Yesu alisema na kufundisha kuhusu Ufalme wa Mungu. Mambo ambayo Ufalme huo umetimiza na yale utakayofanya wakati ujao ndiyo habari muhimu itakayozungumziwa katika kitabu hiki. Sura inayofuata itazungumzia matukio yenye kusisimua ambayo yaliambatana na kuzaliwa kwa Ufalme wa Mungu mbinguni.

^ fu. 13 Mfano wa Yesu huenda uliwakumbusha wasikilizaji wake kuhusu Arkelao, mwana wa Herode Mkuu. Kabla ya Herode kufa, alimchagua Arkelao arithi utawala wa Yudea na maeneo mengine. Hata hivyo, kabla ya kuanza kutawala, ilibidi Arkelao asafiri safari ndefu hadi Roma ili kupata kibali cha Kaisari Augusto.

^ fu. 18 Yeyote ambaye alitiwa mafuta baada ya kifo cha mtiwa-mafuta wa mwisho katika kikundi cha kwanza, yaani, baada ya wale walioshuhudia “mwanzo wa maumivu ya taabu” katika mwaka wa 1914, si sehemu ya “kizazi hiki.”—Mt. 24:8.