Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 2

Ufalme Unazaliwa Mbinguni

Ufalme Unazaliwa Mbinguni

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Jinsi Mungu alivyowatayarisha watu wake kwa ajili ya kuzaliwa kwa Ufalme

1, 2. Ni tukio gani kubwa ambao limewahi kutukia katika historia ya ulimwengu, na kwa nini wanadamu hawakuona tukio hilo?

JE, UMEWAHI kujiuliza mambo yangekuwaje ikiwa ungeishi katika kipindi cha mabadiliko makubwa katika historia? Watu wengi hujiuliza swali hilo. Lakini hebu fikiria: Ikiwa ungeishi katika kipindi hicho muhimu sana, je, wewe binafsi ungeshuhudia matukio hususa ambayo yamesababisha mabadiliko hayo? Labda hungeyashuhudia. Mara nyingi matukio yanayosababisha serikali kuondolewa madarakani na kuandikwa katika vitabu vya historia hayatukii hadharani. Kwa njia fulani, mazungumzo mengi yanayobadili historia hufanywa kisiri katika vyumba vya ndani vya watawala, vyumba vya siri vya mikutano, au kwenye ofisi za serikali. Hata hivyo, mabadiliko hayo huathiri mamilioni ya watu.

2 Namna gani tukio kubwa zaidi kuwahi kutukia katika historia ya ulimwengu? Tukio hilo limebadili maisha ya mamilioni ya watu. Hata hivyo, wanadamu hawakuona tukio hilo. Bila shaka, tunazungumza kuhusu kuzaliwa kwa Ufalme wa Mungu mbinguni, serikali ya Kimasihi iliyoahidiwa zamani sana ambayo hivi karibuni itaharibu mfumo mzima wa ulimwengu huu. (Soma Danieli 2:34, 35, 44, 45.) Kwa kuwa wanadamu hawakuona tukio hilo muhimu la kuzaliwa kwa Ufalme, je, tunapaswa kukata shauri kwamba Yehova aliwaficha wanadamu tukio hilo? Au je, aliwatayarisha mapema watumishi wake washikamanifu kwa ajili ya tukio hilo? Acheni tuone.

“Mjumbe Wangu . . . Atafungua Njia Mbele Zangu”

3-5. (a) “Mjumbe wa agano” anayetajwa kwenye Malaki 3:1 alikuwa nani? (b) Ni nini ambacho kingetokea kabla ya “mjumbe wa agano” kuja kwenye hekalu?

3 Tangu nyakati za kale, Yehova alikusudia kuwatayarisha watu wake kwa ajili ya kuzaliwa kwa Ufalme wa Kimasihi. Kwa mfano, fikiria unabii ulio kwenye Malaki 3:1: “Tazama! ninamtuma mjumbe wangu, naye atafungua njia mbele zangu. Na kwa ghafula Bwana wa kweli atakuja kwenye hekalu lake, ambaye ninyi mnamtafuta, na mjumbe wa agano mnayependezwa naye.”

4 Katika utimizo wa kisasa, Yehova, “Bwana wa kweli,” alikuja lini kukagua wale waliokuwa wakimtumikia katika ua wa duniani wa hekalu lake la kiroho? Unabii huo unaeleza kwamba Yehova angekuja pamoja na “mjumbe wa agano.” Huyo alikuwa nani? Bila shaka alikuwa Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo! (Luka 1:68-73) Akiwa Mtawala aliyewekwa rasmi hivi karibuni, Yesu angewakagua na kuwasafisha watu wa Mungu duniani.—1 Pet. 4:17.

5 Hata hivyo, yule “mjumbe” mwingine anayetajwa kwanza kwenye Malaki 3:1 alikuwa nani? Mjumbe huyo aliyetabiriwa angetokea mapema sana kabla ya kuwapo kwa Mfalme wa Kimasihi. Kwa makumi ya miaka kabla ya mwaka wa 1914, je, kulikuwa na mtu yeyote ‘aliyefungua njia’ mbele ya Mfalme wa Kimasihi?

6. Ni nani aliyetenda kama “mjumbe” aliyetabiriwa ambaye alikuja kwanza ili kuwatayarisha watu wa Mungu kwa ajili ya matukio yaliyokuwa mbele?

6 Katika kitabu hiki, tutapata majibu ya maswali hayo tunapochunguza historia yenye kusisimua ya watu wa Yehova leo. Historia hiyo inaonyesha kwamba mwishoni mwa karne ya 19, hatua kwa hatua kikundi kidogo cha watu waaminifu kilianzishwa na kuwa kikundi pekee cha Wakristo wanyofu katikati ya Wakristo wengi sana wa uwongo. Kikundi hicho kilikuja kujulikana kama Wanafunzi wa Biblia. Bila shaka, wale waliokuwa wakiongoza miongoni mwao, yaani, Charles T. Russell na washiriki wenzake wa karibu walitenda kama yule “mjumbe” aliyetabiriwa, wakiwaelekeza watu wa Mungu kwenye njia inayofaa na kuwatayarisha kwa ajili ya matukio yaliyokuwa mbele. Acheni tuone njia nne ambazo “mjumbe” huyo alitumia ili kuwatayarisha watu wa Mungu.

Kuabudu Katika Kweli

7, 8. (a) Katika miaka ya 1800, ni nani walioanza kufunua uwongo kuhusu fundisho la kutokufa kwa nafsi? (b) C. T. Russell na washiriki wenzake wa karibu walifunua mafundisho gani mengine ya uwongo?

7 Walipokuwa wakijifunza, Wanafunzi hao wa Biblia walisali ili kupata mwongozo wa Yehova; walikubaliana, wakakusanya, na kisha wakachapisha mafundisho sahihi ya kweli. Kwa karne nyingi, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimefunikwa na giza la kiroho; chanzo cha mafundisho mengi ya dini hizo ni upagani. Mfano mzuri ni fundisho la kutokufa kwa nafsi. Hata hivyo, katika miaka ya 1800, wanafunzi wachache wa Biblia walichunguza kwa undani fundisho hilo na kuona kwamba haliungwi mkono na Neno la Mungu. Henry Grew, George Stetson, na George Storrs waliandika na kutoa hotuba kwa ujasiri, wakifunua uwongo huo wa Shetani. * Kazi yao ilimsaidia C. T. Russell na washiriki wenzake wa karibu waboreshe uelewaji wao wa Maandiko.

8 Kikundi hicho kidogo cha Wanafunzi wa Biblia kiligundua kwamba mafundisho mengine yanayohusianishwa na kutokufa kwa nafsi, pia yalikuwa ya uwongo na yenye kutatanisha—kwa mfano, fundisho la kwamba watu wote wazuri huenda mbinguni au kwamba Mungu huzitesa milele katika moto wa mateso nafsi zisizokufa za watu waovu. Russell pamoja na washiriki wenzake wa karibu walifunua kwa ujasiri uwongo huo katika makala kadhaa, vitabu, vijitabu, trakti, na hotuba zilizochapishwa katika magazeti ya habari.

9. Gazeti Zion’s Watch Tower lilifunua jinsi gani kwamba fundisho la Utatu ni la uwongo?

9 Pia, Wanafunzi wa Biblia walifunua kwamba fundisho la Utatu ambalo liliheshimiwa na watu wengi lilikuwa la uwongo. Mwaka wa 1887, gazeti Zion’s Watch Tower lilisema hivi: “Maandiko yanaeleza wazi uhusiano sahihi uliopo kati ya Yehova na Bwana wetu Yesu na kwamba wao ni watu wawili tofauti.” Kisha makala hiyo ikaeleza kuwa ni jambo lenye kushangaza kwamba “fundisho la utatu, yaani, Miungu watatu katika mmoja, na wakati uleule, Mungu mmoja katika miungu watatu, limeenea sana na kukubaliwa na watu wengi. Jambo hilo linaonyesha wazi kwamba kanisa lilikuwa limelala usingizi wa kiroho Shetani alipofanikiwa kueneza fundisho hilo la uwongo.”

10. Gazeti Mnara wa Mlinzi lilikaziaje umuhimu wa mwaka wa 1914?

10 Kama vile kichwa chake kilivyodokeza, gazeti Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence (Mnara wa Mlinzi wa Sayuni Unaotangaza Kuwapo kwa Kristo) lilikazia sana unabii mbalimbali uliohusu kuwapo kwa Kristo. Watiwa-mafuta waaminifu ambao waliandika gazeti hilo waliona kwamba unabii wa Danieli kuhusu “nyakati saba” ulihusiana na wakati wa utimizo wa makusudi ya Mungu kuhusu Ufalme wa Kimasihi. Mapema zaidi katika miaka ya 1870, walitaja kwamba hizo nyakati saba zingeisha mwaka wa 1914. (Dan. 4:25; Luka 21:24) Ingawa ndugu zetu walioishi wakati huo hawakuelewa kikamili umuhimu wa mwaka huo wa pekee, walitangaza kwa mapana na marefu mambo waliyoyajua, na hadi leo tunaona matokeo mazuri ya jitihada zao.

11, 12. (a) Ndugu Russell alimpongeza nani kwa sababu ya mambo aliyofundisha? (b) Kazi iliyofanywa na Russell pamoja na washiriki wenzake kwa makumi ya miaka kabla ya mwaka wa 1914 ilikuwa muhimu kadiri gani?

11 Russell pamoja na washiriki wenzake waaminifu hawakudai kwamba wao ndio waliofunua na kuelewa kweli hizo muhimu sana za kiroho. Russell aliwapongeza wale waliofunua kweli hizo kabla yake. Zaidi ya yote, alimtukuza Yehova Mungu, ambaye hufundisha watu Wake mambo wanayohitaji kujua kwa wakati unaofaa. Ni wazi kwamba Yehova alibariki jitihada za Russell na washiriki wenzake za kutenganisha kweli na uwongo. Kadiri miaka ilivyosonga, ndivyo walivyozidi kuwa tofauti kabisa na dini zinazodai kuwa za Kikristo.

Ndugu Russell na washiriki wenzake wa karibu walizitetea kweli za Biblia

12 Jitihada za wanaume hao waaminifu za kutetea mafundisho ya kweli kwa makumi ya miaka kabla ya mwaka wa 1914, kwa kweli zilistaajabisha sana! Gazeti The Watch Tower and Herald of Christ’s Presence la Novemba 1, 1917, lilieleza hivi: “Mamilioni ya watu leo wako huru kutokana na mzigo wa woga, ambao walikuwa wametwikwa na mafundisho ya moto wa mateso na mafundisho mengine ya uwongo . . . Wimbi la Kweli, ambalo lilianza kuinuka zaidi ya miaka arobaini iliyopita, litaendelea kuinuka hatua kwa hatua hadi litakapoifunika dunia nzima; na wapinzani wamejaribu kuizuia Kweli isienee duniani kote, lakini jitihada zao zimekuwa kama kuyazuia mawimbi ya bahari yenye nguvu kwa kutumia ufagio.”

13, 14. (a) “Mjumbe” alimtayarishiaje njia Mfalme wa Kimasihi? (b) Tunajifunza nini kutoka kwa ndugu zetu walioishi zaidi ya karne moja iliyopita?

13 Fikiria jambo hili: Je, watu wa Mungu wangekuwa wametayarishwa kwa ajili ya kuanza kwa kuwapo kwa Kristo ikiwa hawangeweza kumtofautisha Yesu na Baba yake, Yehova? Bila shaka hapana! Pia, hawangekuwa wametayarishwa ikiwa wangefikiri kwamba uhai usioweza kufa ulikuwa zawadi aliyopewa kila mtu, na si zawadi yenye thamani sana ambayo hupewa wafuasi wachache sana wa Kristo wanaofuata hatua zake; pia hawangekuwa wametayarishwa ikiwa wangefikiri kwamba Mungu huwatesa watu milele katika moto wa mateso! Bila shaka, “mjumbe” alitayarisha njia kwa ajili ya Mfalme wa Kimasihi!

14 Namna gani sisi leo? Tunajifunza nini kutoka kwa ndugu zetu walioishi zaidi ya karne moja iliyopita? Sisi pia tunahitaji kusoma na kujifunza Neno la Mungu kwa bidii. (Yoh. 17:3) Ulimwengu huu unaopenda vitu vya kimwili unapozidi kudhoofika kwa sababu ya kukosa chakula cha kiroho, tunapaswa kuwa na hamu zaidi ya kula chakula cha kiroho!—Soma 1 Timotheo 4:15.

“Tokeni Kwake, Watu Wangu”

15. Wanafunzi wa Biblia walikuja kutambua jambo gani hatua kwa hatua? (Ona pia maelezo ya chini.)

15 Wanafunzi wa Biblia walifundisha kwamba ilikuwa lazima kujitenga na makanisa. Mwaka wa 1879, gazeti Mnara wa Mlinzi lilizungumza kuhusu “kanisa la Babiloni.” Je, lilikuwa likizungumza kumhusu papa? Kanisa Katoliki? Kwa karne nyingi dini za Kiprotestanti zilisema kwamba Babiloni, anayetajwa katika unabii wa Biblia anawakilisha Kanisa Katoliki. Hata hivyo, hatua kwa hatua Wanafunzi wa Biblia walitambua kwamba makanisa yote ya dini zinazodai kuwa za Kikristo yalikuwa sehemu ya “Babiloni” wa siku hizi. Kwa nini? Kwa sababu makanisa yote yalifundisha mafundisho ya uwongo kama yale yaliyozungumziwa katika mafungu yaliyotangulia. * Baada ya muda, machapisho yetu yalianza kueleza waziwazi mambo ambayo washiriki wanyofu wa makanisa ya Babiloni walipaswa kufanya.

16, 17. (a) Buku la 3 la Millennial Dawn na gazeti Mnara wa Mlinzi liliwahimizaje watu wajitenge na dini ya uwongo? (b) Ni jambo gani lililopunguza uzito wa maonyo hayo ya mapema? (Ona maelezo ya chini.)

16 Kwa mfano, katika mwaka wa 1891, Buku la 3 la Millennial Dawn lilizungumzia jinsi Mungu alivyomkataa Babiloni wa siku hizi na kueleza hivi: “Makanisa yote ya dini zinazodai kuwa za Kikristo yamekataliwa.” Liliongezea kusema kwamba wale wote ambao “hawakubaliani na mafundisho na mazoea yake, wanahimizwa sasa wajitenge naye.”

17 Mnamo Januari 1900, gazeti Mnara wa Mlinzi liliwashauri wale ambao bado majina yao yalikuwa kwenye orodha ya washiriki wa makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo na wale ambao walijitetea kwa kusema, “Ninaiunga mkono kweli kwa moyo wote, na ni mara chache sana ninahudhuria mikutano mingine.” Makala hiyo iliuliza hivi: “Je, jambo hilo ni sawa, yaani, kuwa mguu mmoja ndani na mwingine nje ya Babiloni? Je, Mungu hukubali na kufurahishwa . . . na utii wa aina hiyo? Hapana. Mshirika wa kanisa alifanya agano hadharani na dhehebu alipojiunga nalo, na anapaswa kuwa mwaminifu na kufuata masharti yote ya agano hilo hadi . . . anapokana au kuvunja rasmi ushirika wake na dhehebu hilo.” Kwa miaka mingi, shauri hilo lilirudiwa tena na tena. * Ni lazima watumishi wa Yehova wakate vifungo vyote walivyofunga pamoja na dini ya uwongo.

18. Kwa nini ilikuwa lazima watu watoke katika Babiloni Mkubwa?

18 Ikiwa maonyo hayo ya kutoka katika Babiloni Mkubwa hayangetolewa kwa ukawaida, je, Kristo akiwa Mfalme aliyetoka tu kuwekwa rasmi angekuwa na kikundi hapa duniani cha watumishi watiwa-mafuta waliotayarishwa? Bila shaka hapana, kwa kuwa ni lazima Wakristo watoke katika Babiloni ili waweze kumwabudu Yehova kwa “roho na kweli.” (Yoh. 4:24) Namna gani sisi, je, tumeazimia kujitenga kabisa na dini ya uwongo? Acheni tuendelee kutii amri hii: “Tokeni kwake, watu wangu”!—Soma Ufunuo 18:4.

Kukusanyika kwa Ajili ya Ibada

19, 20. Gazeti Mnara wa Mlinzi liliwatiaje moyo watu wa Mungu wakusanyike pamoja kwa ajili ya ibada?

19 Wanafunzi wa Biblia walifundisha kwamba waumini wenzao walipaswa kukusanyika ili kuabudu pamoja, ikiwa hali zingeruhusu. Haitoshi tu kwa Wakristo wa kweli kutoka katika dini ya uwongo. Ni muhimu pia washiriki katika ibada safi. Tangu lilipoanza kuchapishwa, gazeti Mnara wa Mlinzi liliwatia moyo wasomaji wake wakusanyike pamoja kwa ajili ya ibada. Kwa mfano, mnamo Julai 1880, Ndugu Russell aliripoti kuhusu ziara aliyofanya akiwa msemaji, na kueleza jinsi mikutano hiyo ilivyokuwa yenye kutia moyo. Kisha akawahimiza wasomaji wa gazeti hilo wawe wakituma ripoti kuhusu maendeleo yao na baadhi ya ripoti hizo zingechapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi. Kwa kusudi gani? “Tungependa kujua . . . jinsi Bwana anavyowabariki; na ikiwa mnaendelea kukutanika pamoja na wale walio na imani kama yenu.”

Charles Russell akiwa pamoja na kikundi cha Wanafunzi wa Biblia huko Copenhagen, Denmark, mwaka wa 1909

20 Mwaka wa 1882, gazeti Mnara wa Mlinzi lilikuwa na makala yenye kichwa “Kukusanyika Pamoja.” Makala hiyo iliwahimiza Wakristo wafanye mikutano ili “kufundishana, kutiana moyo, na kuimarishana.” Lilieleza hivi: “Si lazima kuwe na msomi au mtu mwenye kipawa miongoni mwenu. Kwa kadiri inavyowezekana, . . . acheni kila mtu alete Biblia yake, karatasi, na penseli na kutumia vifaa vyovyote vinavyoweza kumsaidia kujifunza kama vile Fahirisi. Chagueni kichwa cha mazungumzo; ombeni mwongozo wa Roho ili kuelewa habari hiyo; kisha someni, tafakarini, mlinganishe andiko na andiko na bila shaka roho takatifu itawaongoza kwenye ukweli.”

21. Kutaniko lililokuwa Allegheny, Pennsylvania, liliweka mfano gani kuhusiana na mikutano na ziara za uchungaji?

21 Makao makuu ya Wanafunzi wa Biblia yalikuwa huko Allegheny, Pennsylvania, Marekani. Katika makao hayo, waliweka mfano mzuri kwa kukusanyika pamoja ili kutii shauri lilioongozwa na roho ambalo limeandikwa kwenye Waebrania 10:24, 25. (Soma.) Miaka mingi baadaye, ndugu Charles Capen alisema kwamba alihudhuria mikutano hiyo alipokuwa mvulana. Aliandika hivi: “Bado ninakumbuka mojawapo ya maandiko yaliyoandikwa kwenye ukuta wa jumba la kusanyiko la Sosaiti. ‘Mnaye Bwana mmoja, ambaye ni Kristo; na ninyi nyote ni ndugu.’ Siku zote andiko hilo limekuwa akilini mwangu—hakuna tabaka la makasisi na waumini kati ya watu wa Yehova.” (Mt. 23:8, Neno—Biblia Takatifu) Ndugu Capen alikumbuka pia jinsi mikutano hiyo ilivyokuwa yenye kujenga, kutia moyo, na jinsi Ndugu Russell alivyojitahidi sana kumfanyia ziara ya uchungaji kila mshiriki wa kutaniko.

22. Watu waaminifu waliitikiaje walipotiwa moyo wahudhurie mikutano ya Kikristo, na hilo linatufundisha nini?

22 Watu waaminifu waliiga mfano huo na kufuata maagizo waliyopewa. Makutaniko yakaanzishwa katika majimbo mengine, kama vile Ohio na Michigan, na kisha katika maeneo yote ya Amerika Kaskazini na katika nchi nyingine pia. Fikiria hili: Je, kweli watu waaminifu wangekuwa wametayarishwa kwa ajili ya kuwapo kwa Kristo ikiwa hawakuwa wamezoezwa kutii shauri lilioongozwa na roho kwamba wakusanyike pamoja kwa ajili ya ibada? Bila shaka hapana! Namna gani sisi leo? Tunahitaji kuazimia kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na kutumia kila nafasi tunayopata kuabudu pamoja na kujengana kiroho.

Kuhubiri kwa Bidii

23. Gazeti Mnara wa Mlinzi lilielezaje wazi kwamba watiwa-mafuta wote wanapaswa kuwa wahubiri wa ile kweli?

23 Wanafunzi wa Biblia walifundisha kwamba watiwa-mafuta wote wanapaswa kuwa wahubiri wa ile kweli. Mwaka wa 1885, gazeti Mnara wa Mlinzi lilieleza hivi: “Hatupaswi kusahau kwamba kila mshiriki wa kikundi cha watiwa-mafuta ametiwa mafuta ili ahubiri (Isa. 61:1), ameitwa katika huduma.” Toleo moja la mwaka wa 1888 lilikuwa na himizo hili: “Tunajua vizuri utume wetu . . . Ikiwa tunaupuuza na kujitetea, basi sisi ni watumishi wavivu, na hivyo tunathibitisha kwamba hatustahili kuwa watiwa-mafuta.”

24, 25. (a) Russell pamoja na washiriki wenzake wa karibu walifanya nini mbali na kuwatia moyo watu wahubiri? (b) Kolpota mmoja alifanyaje kazi yake katika siku hizo ambazo magari yalikuwa machache sana?

24 Ndugu Russell na washiriki wenzake wa karibu walifanya mambo mengi mbali na kuwatia moyo watu wahubiri. Walianza pia kuchapisha trakti zilizoitwa Bible Students’ Tracts, ambazo baadaye zilikuja kuitwa Old Theology Quarterly. Wasomaji wa Mnara wa Mlinzi walipewa trakti hizo ili wazigawanye kwa watu bila malipo.

Inafaa tujiulize hivi, ‘Je, kazi ya kuhubiri ndilo jambo kuu maishani mwangu?’

25 Wale ambao walishiriki katika huduma wakati wote waliitwa makolpota. Charles Capen, aliyetajwa awali, alikuwa mmoja wao. Baadaye alisema hivi: “Nilitumia ramani zilizochorwa na Shirika la Uchunguzi wa Jiolojia la Serikali ya Marekani ili kunisaidia nihubiri eneo lote katika jimbo la Pennsylvania. Ramani hizo zilionyesha barabara zote, na hivyo kufanya iwezekane kufika kwa miguu katika maeneo yote katika kila mkoa. Nyakati fulani, baada ya kusafiri kwa siku tatu katika maeneo mbalimbali nchini nikikusanya majina ya watu waliotaka mabuku ya Studies in the Scriptures, nilikodi gari linalokokotwa na farasi ili niwapelekee watu mabuku waliyoagiza. Mara kwa mara nililala kwenye nyumba za wakulima. Siku hizo kulikuwa na magari machache sana.”

Kolpota. Ona “Chati ya Enzi” iliyochorwa kwenye gari linalokokotwa na farasi

26. (a) Kwa nini watu wa Mungu walihitaji kushiriki katika kazi ya kuhubiri ili wawe tayari kwa ajili ya utawala wa Kristo? (b) Inafaa tujiulize maswali gani?

26 Kwa hakika jitihada hizo za kuhubiri zilihitaji ujasiri na bidii. Je, Wakristo wa kweli wangekuwa wametayarishwa kwa ajili ya utawala wa Kristo ikiwa hawangekuwa wamefundishwa umuhimu wa kazi ya kuhubiri? Bila shaka hapana! Kwa kweli, kazi ya kuhubiri ingekuja kuwa sehemu muhimu ya ile ishara ya kuwapo kwa Kristo. (Mt. 24:14) Watu wa Mungu walipaswa kutayarishwa ili waifanye kazi hiyo ya kuokoa uhai iwe jambo kuu maishani mwao. Sisi pia, inafaa tujiulize: ‘Je, kazi ya kuhubiri ndilo jambo kuu maishani mwangu? Je, ninajinyima mambo fulani ili nishiriki kikamili katika utendaji huo?’

Ufalme wa Mungu Unazaliwa!

27, 28. Mtume Yohana aliona nini katika maono, na Shetani na roho wake waovu walitendaje Ufalme ulipozaliwa?

27 Hatimaye, mwaka muhimu sana wa 1914 ukafika. Kama tulivyozungumza mwanzoni mwa sura hii, hakuna mwanadamu aliyeshuhudia matukio hayo matukufu yaliyotokea mbinguni. Hata hivyo, mtume Yohana alipewa maono ambayo yanaelezea matukio hayo kwa njia ya mfano. Hebu wazia: Yohana anaona “ishara kubwa” mbinguni. “Mwanamke” wa Mungu, yaani, tengenezo la Mungu la viumbe wa roho mbinguni, ana mimba na anazaa mtoto wa kiume. Tunaambiwa kwamba hivi karibuni mwana huyo wa mfano ‘atayachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma.’ Hata hivyo, baada tu ya kuzaliwa, mtoto huyo ‘ananyakuliwa mpaka kwa Mungu na kwenye kiti chake cha ufalme.’ Sauti kubwa mbinguni inasema: “Sasa kumekuwa na wokovu na nguvu na ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake.”—Ufu. 12:1, 5, 10.

28 Hakuna shaka kwamba Yohana aliona katika maono kuzaliwa kwa Ufalme wa Kimasihi. Kwa hakika tukio hilo lilikuwa tukufu sana, lakini si wote waliofurahishwa nalo. Shetani na roho wake waovu walipigana vita dhidi ya malaika waaminifu, ambao walikuwa chini ya uongozi wa Mikaeli, au Kristo. Matokeo yalikuwaje? Tunasoma hivi: “Yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.”—Ufu. 12:7, 9.

Katika mwaka wa 1914, Wanafunzi wa Biblia walianza kutambua ishara ya kuwapo kwa Kristo kusikoonekana

29, 30. Baada ya kuzaliwa kwa Ufalme wa Kimasihi, hali zilibadilikaje (a) duniani? (b) mbinguni?

29 Miaka mingi kabla ya mwaka wa 1914, Wanafunzi wa Biblia walisema kwamba wakati wa taabu ungeanza mwaka huo wa pekee. Hata hivyo, wao wenyewe hawakujua kwamba utabiri wao ungetimia kwa usahihi kabisa. Kama vile maono ya Yohana yalivyofunua, Shetani angeanza kuwaathiri wanadamu kwa njia kubwa sana: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufu. 12:12) Katika mwaka wa 1914, vita vya kwanza vya ulimwengu vilianza na ishara ya kuwapo kwa Kristo akiwa katika mamlaka ya kifalme ikaanza kutimia ulimwenguni pote. “Siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo zikaanza.—2 Tim. 3:1.

30 Hata hivyo, kulikuwa na shangwe mbinguni. Shetani na roho wake waovu walikuwa wamefukuzwa milele. Simulizi la Yohana linasema hivi: “Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake!” (Ufu. 12:12) Sasa, mbingu zikiwa zimesafishwa na Yesu akiwa amewekwa rasmi kuwa Mfalme, Ufalme wa Kimasihi ulikuwa tayari kutenda kwa niaba ya watu wa Mungu duniani. Ufalme huo ungechukua hatua gani? Kama tulivyoona mwanzoni mwa sura hii, Kristo akiwa “mjumbe wa agano,” kwanza angetenda akiwa msafishaji wa watumishi wa Mungu hapa duniani. Hilo lingemaanisha nini?

Kipindi cha Majaribu

31. Malaki alitabiri nini kuhusiana na kipindi cha kusafishwa, na unabii huo ulianza kutimia lini? (Ona pia maelezo ya chini.)

31 Malaki alitabiri kwamba kipindi cha kusafishwa hakingekuwa rahisi. Aliandika hivi: “Ni nani atakayeistahimili siku ya kuja kwake, naye ni nani atakayesimama wakati atakapoonekana? Kwa maana atakuwa kama moto wa msafishaji na kama sabuni ya wafuaji wa nguo.” (Mal. 3:2) Maneno hayo yalithibitika kuwa kweli kabisa! Kuanzia mwaka wa 1914, watu wa Mungu duniani walikabili majaribu mengi na hali ngumu sana. Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipozidi kupamba moto, Wanafunzi wengi wa Biblia waliteswa vikali sana na kutupwa gerezani. *

32. Ni msukosuko gani uliotokea ndani ya tengenezo na kuwaathiri watu wa Mungu kuanzia mwaka wa 1916?

32 Pia msukosuko ulitokea ndani ya tengenezo. Mnamo 1916, Ndugu Russell alikufa akiwa na umri wa miaka 64 tu, na watu wengi wa Mungu walishtushwa sana na kifo chake. Kifo chake kilifunua kwamba baadhi ya watu walikuwa wamekazia fikira kupita kiasi kwa mtu mmoja aliyekuwa mfano bora. Ingawa Ndugu Russell hakutaka heshima ya namna hiyo, watu wengi walikuwa na mwelekeo wa kumwabudu. Watu wengi walifikiri kwamba kweli iliyokuwa ikifunuliwa hatua kwa hatua ilikoma Ndugu Russell alipokufa, na baadhi ya watu walipinga vikali sana jitihada za kusonga mbele. Mtazamo huo ulichangia kutokea kwa uasi-imani ambao uliligawanya tengenezo.

33. Matarajio ambayo hayakutimia yaliwajaribu watu wa Mungu jinsi gani?

33 Jaribu lingine lilikuwa kutotimia kwa matarajio ya watu wa Mungu. Ingawa gazeti Mnara wa Mlinzi lilikuwa limetaja kwa usahihi kabisa kwamba Nyakati za Mataifa zingeisha mwaka wa 1914, bado akina ndugu hawakujua mambo ambayo yangetokea mwaka huo. (Luka 21:24) Walifikiri kwamba katika mwaka wa 1914, Kristo angechukua jamii yake ya bibi-arusi waliotiwa mafuta ili wakatawale pamoja naye mbinguni. Matumaini hayo hayakutimia. Mwishoni mwa mwaka wa 1917, gazeti Mnara wa Mlinzi lilitangaza kwamba kipindi cha mavuno chenye urefu wa miaka 40 kingeisha mwanzoni mwa mwaka wa 1918. Lakini kazi ya kuhubiri haikukoma. Iliendelea kusitawi hata baada ya mwaka huo kupita. Gazeti hilo lilidokeza kwamba pasipo shaka mavuno yalikuwa yamemalizika, lakini kipindi cha kukusanya masalio kilikuwa kimebaki. Hata hivyo, watu wengi waliacha kumtumikia Yehova kwa sababu ya kuvunjika moyo.

34. Ni jaribu gani gumu zaidi lililotokea mwaka wa 1918, na kwa nini dini zinazodai kuwa za Kikristo zilifikiri kwamba watu wa Mungu walikuwa “wamekufa”?

34 Jaribu gumu zaidi lilitokea mwaka wa 1918. J. F. Rutherford, aliyewaongoza watu wa Mungu baada ya C. T. Russell kufa, alikamatwa pamoja na ndugu wengine saba wenye madaraka. Walihukumiwa isivyo haki vifungo vya muda mrefu na kufungwa katika gereza kuu huko Atlanta, Georgia, Marekani. Kwa muda fulani, kazi ya watu wa Mungu ilionekana kuwa imesimama. Viongozi wengi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walishangilia sana. Walidhani kwamba kwa kuwa “viongozi” walikuwa gerezani, makao makuu huko Brooklyn yamefungwa, na kazi ya kuhubiri ilikuwa ikishambuliwa barani Ulaya na Amerika, basi Wanafunzi hao wasumbufu wa Biblia walikuwa “wamekufa,” hawakuwa tishio tena. (Ufu. 11:3, 7-10) Kwa kweli, walikuwa wamekosea sana!

Kipindi cha Kuamka Kiroho!

35. Kwa nini Yesu aliruhusu wafuasi wake wapatwe na hali ngumu, naye alichukua hatua gani ili kuwasaidia?

35 Maadui wa ile kweli hawakujua kwamba Yesu aliruhusu watu wake wapatwe na hali hizo ngumu kwa sababu tu wakati huo Yehova alikuwa ameketi “kama msafishaji na mtakasaji wa fedha.” (Mal. 3:3) Yehova na Mwana wake walikuwa na hakika kwamba baada ya majaribu hayo makali watu waaminifu wangekuwa wamesafishwa, wametakaswa, na kufaa zaidi kumtumikia Mfalme. Kuanzia mapema mwaka wa 1919, ilikuwa wazi kabisa kwamba roho ya Mungu ilikuwa imefanya jambo ambalo adui za watu wake walifikiri kwamba halingewezekana. Watu waaminifu waliamka kiroho! (Ufu. 11:11) Wakati huo, Kristo alitimiza sehemu muhimu ya ile ishara ya siku za mwisho. Alimweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” kikundi kidogo cha wanaume watiwa-mafuta ambacho kingewaongoza watu wake kwa kuwaandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.—Mt. 24:45-47.

36. Ni nini kilichoonyesha kwamba watu wa Mungu walikuwa wakiamka kiroho?

36 Ndugu Rutherford na wenzake waliachiliwa huru kutoka gerezani Machi 26, 1919. Baada ya muda mfupi wakapanga kuwe na kusanyiko mwezi wa Septemba mwaka huo. Mipango ya kuanzisha gazeti lingine ambalo lingeitwa The Golden Age ilianza kufanywa. Lingechapishwa pamoja na gazeti Mnara wa Mlinzi, na lilikusudiwa litumiwe katika huduma ya shambani. * Katika mwaka huohuo, toleo la kwanza la Bulletin, sasa linaitwa Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo lilichapishwa. Tangu ilipoanza kuchapishwa, siku zote imewachochea watu kushiriki katika huduma ya shambani. Bila shaka, kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea huduma ya nyumba kwa nyumba ilipewa kipaumbele.

37. Miaka iliyofuata mwaka wa 1919, baadhi ya watu wasio washikamanifu walitendaje?

37 Kazi ya kuhubiri iliendelea kuwasafisha watumishi wa Kristo, kwa kuwa watu wenye kiburi na majivuno miongoni mwao hawakuwa tayari kufanya kazi hiyo ya hali ya chini. Wale ambao hawakutaka kufanya kazi hiyo waliacha kushirikiana na watu waliokuwa waaminifu. Miaka iliyofuata mwaka wa 1919, baadhi ya watu ambao hawakuwa washikamanifu wakaanza kuwa na uchungu dhidi ya watumishi wa Mungu, na hivyo wakawachongea na kuwakashifu, na hata wakashirikiana na wale waliowatesa watumishi waaminifu wa Yehova.

38. Mafanikio na ushindi mbalimbali ambao wafuasi wa Kristo duniani walipata unatuthibitishia nini?

38 Hata hivyo, licha ya mashambulizi hayo, wafuasi wa Kristo duniani waliendelea kukua na kusitawi kiroho. Mafanikio yao na ushindi waliopata tangu wakati huo, unatuthibitishia wazi kwamba Ufalme wa Mungu unatawala! Kikundi hicho cha wanadamu wasio wakamilifu kilipata ushindi mkubwa dhidi ya Shetani na mfumo huu mwovu wa mambo kwa sababu tu Mungu aliwasaidia sana na kuwabariki kupitia Mwana wake na Ufalme wa Kimasihi!—Soma Isaya 54:17.

Ndugu Rutherford akitoa hotuba yenye kuchochea katika kusanyiko miezi michache baada ya kuachiliwa kutoka gerezani

39, 40. (a) Kitabu hiki kina sehemu gani mbalimbali? (b) Utanufaikaje kwa kujifunza kitabu hiki?

39 Katika sura zinazofuata, tutachunguza mambo ambayo Ufalme wa Mungu umetimiza duniani kwa karne moja tangu ulipozaliwa mbinguni. Kila sehemu ya kitabu hiki itazungumzia jambo tofauti linalohusiana na kazi ya Ufalme hapa duniani. Katika kila sura, kuna sanduku la pitio ambalo litamsaidia kila mmoja wetu auone Ufalme wa Mungu ni halisi kadiri gani kwake. Katika sura za mwisho za kitabu hiki, tutazungumzia mambo ambayo tunatarajia wakati Ufalme wa Mungu utakapokuja kuwaangamiza waovu na kuleta paradiso duniani. Utanufaikaje kwa kujifunza kitabu hiki?

40 Shetani anataka kudhoofisha imani yako katika Ufalme wa Mungu. Lakini Yehova anataka kuimarisha imani yako ili ikulinde na kukupa nguvu. (Efe. 6:16) Kwa hiyo, tunakuhimiza ujifunze kitabu hiki kwa bidii. Endelea kujiuliza hivi, ‘Je, Ufalme wa Mungu ni halisi kwangu?’ Kadiri Ufalme unavyokuwa halisi kwako, ndivyo utakavyoendelea kuuunga mkono kwa uaminifu hadi siku ambayo kila mtu aliye hai ataona kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi na kwamba unatawala!

^ fu. 7 Ili kupata habari zaidi kuhusu Grew, Stetson, na Storrs, ona kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 45-46.

^ fu. 15 Ingawa Wanafunzi wa Biblia waliona uhitaji wa kujitenga na mashirika ya kidini ambayo yalikuwa na urafiki na ulimwengu, kwa miaka mingi waliendelea kuwaona kuwa ndugu zao wale wote waliodai kuwa na imani katika fidia na kwamba wamejiweka wakfu kwa Mungu ingawa Wakristo hao hawakuwa Wanafunzi wa Biblia.

^ fu. 17 Jambo moja lililopunguza uzito wa maonyo hayo ni kwamba yalihusu hasa kundi dogo la Kristo la watu 144,000. Katika Sura ya 5 tutaona kwamba kabla ya mwaka wa 1935, ilidhaniwa kuwa “mkutano mkubwa” unaotajwa kwenye Ufunuo 7:9, 10 katika tafsiri ya Union Version, ungetia ndani washiriki wengi wa makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo na kwamba washiriki hao wangekuwa kundi la pili lenye tumaini la kwenda mbinguni, hiyo ikiwa thawabu yao kwa kumuunga mkono Kristo hadi kuja kwake.

^ fu. 31 Mnamo Septemba 1920, gazeti The Golden Age (sasa Amkeni!) lilichapisha toleo la pekee ambalo lilitaja kwa kina visa vingi vya mateso waliyopata watu wa Mungu katika nchi ya Kanada, Marekani, Uingereza, na Ujerumani wakati wa vita. Baadhi ya mateso hayo yalikuwa ya kikatili sana. Kinyume cha hilo, miaka kadhaa kabla ya vita vya kwanza vya ulimwengu hakukuwa na mateso makali sana kama hayo.

^ fu. 36 Kwa miaka mingi gazeti Mnara wa Mlinzi lilichapishwa hasa kwa ajili ya washiriki wa kundi dogo ili wajifunze kibinafsi.