Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 2

Kuzaliwa Kwa Ufalme Mbinguni

Kuzaliwa Kwa Ufalme Mbinguni

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Inazungumuzia namna Mungu alitayarisha watu wake juu ya kuzaliwa kwa Ufalme

1, 2. Ni tukio gani kubwa zaidi ambalo lilitokea katika historia ya ulimwengu, na sababu gani haishangaze kuona kwamba watu hawakujionea namna tukio hilo lilifanyika?

UNAPOSIKIA kwamba kulitokea mabadiliko makubwa wakati fulani katika historia, pengine unajiuliza: maisha yangu yangekuwa namna gani wakati huo? Watu wengi wanaweza pia kujiuliza hivyo. Lakini fikiria jambo hili: Ikiwa ulikuwa unaishi wakati huo wa maana sana, uko hakika kwamba ungejionea namna kila jambo lilifanyika ili kutokeza mabadiliko hayo? Pengine hapana. Kwa mufano, wakati mabadiliko fulani ya serikali ao guvernema yanatokea, kile watu wanaona ni mabadiliko tu, lakini kuna mambo mengi ambayo hawakuona ambayo yamefanyika katika siri ili kufikia mabadiliko hayo. Hata hivyo, mabadiliko kama hayo yanabadilisha maisha ya watu wengi.

2 Tuseme nini sasa juu ya tukio kubwa zaidi kuliko matukio mengine yote, ambalo lilitokea katika historia ya ulimwengu? Tukio hilo limebadilisha maisha ya watu wengi. Hata hivyo, watu hawakujionea namna tukio hilo lilifanyika. Tunazungumuzia kuzaliwa kwa Ufalme wa Mungu mbinguni, ni kusema, serikali ya Masiya, ambayo iliahidiwa tangu zamani, na ambayo hivi karibuni itaharibu ulimwengu huu muovu. (Soma Danieli 2:34, 35, 44, 45.) Kwa kuwa wanadamu hawakujionea namna tukio hilo la maana sana lilifanyika, tunaweza kusema kwamba Yehova hakupenda wanadamu wajue juu ya tukio hilo? Ulizo lingine ni hili, je, Yehova aliwatayarisha watu wake waaminifu juu ya tukio hilo? Acha tuchunguze jambo hilo.

‘Mujumbe Wangu . . . Atafungua Njia Mbele Yangu’

3-5. (a) Ni nani ‘mujumbe wa agano’ anayezungumuziwa katika andiko la Malaki 3:1? (b) Ni nini ingepaswa kufanyika mbele ya kuja kwa ‘mujumbe wa agano’ kwenye hekalu?

3 Tangu zamani, Yehova aliona ni vizuri kutayarisha watu wake juu ya kuzaliwa kwa Ufalme wa Masiya. Kwa mufano, fikiria unabii wa Malaki 3:1, unaosema hivi: ‘Tazama! ninamutuma mujumbe wangu, naye atafungua njia mbele yangu. Na kwa gafula, Bwana wa kweli atakuja kwenye hekalu Lake, ambaye ninyi munamutafuta, na mujumbe wa agano munayependezwa naye. Tazama! Atakuja hakika.’

4 Katika utimizo wa unabii huo leo, ni wakati gani “Bwana wa kweli,” ni kusema, Yehova alikuja kuchunguza wale waliokuwa wanamutumikia katika uwanja wa hekalu lake la kiroho hapa duniani? Unabii huo unasema kwamba Yehova angekuja pamoja na ‘mujumbe wa agano.’ Mujumbe huyo ni nani? Ni Masiya-Mufalme, Yesu Kristo! (Lu. 1:68-73) Kwa hiyo, Yesu angepaswa kuja kuchunguza na kusafisha watu wa Mungu duniani, kwa sababu yeye ndiye Mufalme mupya aliyewekwa.​—1 Pet. 4:17.

5 Ni nani aliyekuwa ‘mujumbe’ wa kwanza, ambaye unabii wa Malaki 3:1 unazungumuzia? Mujumbe huyo alipaswa kutokea mbele ya kuwapo kwa Masiya-Mufalme, katika mwaka wa 1914. Je, miaka fulani mbele ya mwaka huo, kuna mutu fulani aliyemufungulia njia Masiya-Mufalme?

6. Ni nani walifanya kazi ya ‘mujumbe’ ambaye alitabiriwa, ni kusema, walikuwa wa kwanza kuja ili kutayarisha watu wa Mungu kwa ajili ya matukio yaliyokuwa mbele?

6 Tutapata majibu ya maulizo hayo katika kitabu hiki kinachozungumuzia historia yenye kufurahisha ya watu wa Yehova wa wakati wetu. Historia hiyo inaonyesha kwamba katika sehemu ya mwisho ya miaka ya 1800, kikundi kidogo cha watu waaminifu kilitokea katika ulimwengu uliokuwa na Wakristo wa jina tu. Kikundi hicho kidogo kilikuwa ndicho kikundi cha Wakristo wa kweli. Waliitwa Wanafunzi wa Biblia. Wale waliowaongoza, ni kusema, Charles T. Russell na wenzake, walifanya kazi ya ‘mujumbe’ kama ilivyotabiriwa. Walitolea watu wa Mungu uongozi wa kiroho na kuwatayarisha kwa ajili ya matukio yaliyokuwa mbele. Acha tuzungumuzie njia ine ambazo ‘mujumbe’ huyo alitumia ili kutimiza jambo hilo.

Kuabudu Katika Kweli

7, 8. (a) Katika mwaka wa 1850 hivi, ni nani walianza kufunua uongo wa fundisho linalosema kwamba nafsi haiwezi kufa? (b) Ndugu C. T. Russell na wenzake walifunua mafundisho gani mengine ya uongo?

7 Wanafunzi hao wa Biblia walijifunza kwa bidii na kusali ili kujua mafundisho ya kweli yaliyo wazi; walikubaliana juu ya mafundisho hayo, waliyakusanya na kuyachapisha katika vichapo. Kwa miaka mingi dini zinazojidai kuwa za Kikristo zilikuwa katika giza la kiroho; mafundisho mengi ya dini hizo yalikuwa ya kipagani. Mufano wa kwanza ni lile fundisho linalosema kwamba nafsi haiwezi kufa. Lakini, katika mwaka wa 1850 hivi, watu wengine wachache wenye moyo muzuri ambao walikuwa wanajifunza Biblia walichunguza fundisho hilo na waliona kwamba Neno la Mungu halifundishe hivyo. Wanaume kama vile Henry Grew, George Stetson, na George Storrs waliandika na kuhubiria watu kwa bidii ili kufunua uongo huo wa Shetani. Kazi ya wanaume hao ilimusaidia sana ndugu C. T. Russell na wenzake.

8 Kikundi hicho kidogo cha Wanafunzi wa Biblia waliona kwamba mafundisho mengine yanayohusiana na fundisho hilo la kwamba nafsi haiwezi kufa, ni mafundisho ya uongo na yenye kupingana. Kwa mufano, fundisho linalosema kwamba watu wote wazuri wanaenda mbinguni ao kwamba Mungu anatesa nafsi za watu wabaya katika moto wa milele. Russell na wenzake walifunua mafundisho hayo ya uongo bila woga: waliandika na kuchapisha habari hizo katika vitabu, magazeti, trakte, na waliandikisha hotuba mbalimbali katika magazeti.

9. Gazeti Munara wa Mulinzi lilisema nini ili kufunua uongo wa fundisho la Utatu?

9 Vilevile, Wanafunzi hao wa Biblia walifunua waziwazi uongo wa fundisho la Utatu, fundisho ambalo lilikuwa linaheshimiwa sana katika ulimwengu. Katika mwaka wa 1887, gazeti Munara wa Mulinzi lilisema hivi: “Maandiko yanaonyesha waziwazi kabisa kwamba Yehova na Bwana wetu Yesu si mutu mumoja na yanaonyesha pia uhusiano ulio kati yao.” Kisha gazeti hilo lilionyesha namna ni jambo lenye kushangaza kuona “kwamba wazo la Miungu watatu, ni kusema, Miungu watatu katika mungu moja, na Mungu mumoja katika watatu, lilipendwa sana na kukubaliwa na watu wengi. Ikiwa jambo hilo liko hivyo, hilo linaonyesha tu namna kanisa lilikuwa linalala kabisa, na wakati huo adui alilifunga minyororo ya chuma ya udanganyifu.”

10. Gazeti Munara wa Mulinzi lilisema nini ili kuonyesha kwamba mwaka wa 1914 ni mwaka uliotiwa alama?

10 Kichwa cha gazeti Munara wa Mulinzi kilionyesha kwamba gazeti hilo linahangaikia sana unabii mbalimbali ambao unazungumuzia kuwapo kwa Kristo. Ndugu watiwa-mafuta waaminifu waliokuwa wanaandika gazeti hilo waliona kwamba unabii wa Danieli kuhusu zile “nyakati saba” unazungumuzia wakati Mungu angetimiza kusudi lake juu ya Ufalme wa Masiya. Mwanzo-mwanzo tu wa miaka ya 1870, walionyesha kwamba nyakati hizo saba zingemalizika mwaka wa 1914. (Dan. 4:25; Lu. 21:24) Hata ikiwa wakati huo ndugu zetu hawakuelewa kabisa mambo yote kuhusu mwaka huo uliotiwa alama, walitangaza mupaka sehemu za mbali mambo ambayo walijua kuhusu mwaka huo. Kweli ya Biblia ambayo walitangaza wakati huo inaendelea kuwa na matokeo mupaka wakati wetu.

11, 12. (a) Ndugu Russell aliwasifu nani kuhusu mambo aliyokuwa anafundisha? (b) Ni nini inaonyesha kwamba kazi ambayo ndugu Russell na wenzake walifanya katika miaka fulani mbele ya mwaka wa 1914 ilikuwa ya maana sana?

11 Iwe ndugu Russell ao ndugu wenzake waaminifu, hakuna aliyejipiga kifua kwamba yeye ndiye aliyekuwa wa kwanza kuvumbua na kuelewa mafundisho hayo ya kweli ya Biblia. Ndugu Russell aliwasifu sana wengine walioanza kutafuta kweli mbele yake. Na zaidi sana, alimusifu Yehova Mungu ambaye anafundisha watu Wake mafundisho ambayo wanahitaji kujua, na anawafundisha wakati wanahitaji kujua mafundisho hayo. Bila shaka, Yehova alibariki bidii za ndugu Russell na wenzake za kutenganisha kweli na mafundisho ya uongo. Kadiri miaka ilipita, walizidi kuonekana tofauti na dini zingine ambazo zilijidai kuwa za Kikristo.

Ndugu Russell na wenzake walikuwa wanatetea mafundisho ya kweli

12 Kazi ya wanaume hao waaminifu ya kutetea kweli katika miaka fulani mbele ya mwaka wa 1914 ilikuwa ya ajabu kabisa! Gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 1 Mwezi 11, 1917, lilipozungumuzia kazi iliyofanyika mbele ya mwaka huo, lilisema hivi: “Leo mamilioni ya watu wametoka katika utumwa wa woga. Wameingizwa katika utumwa huo kupitia mafundisho ya moto wa milele na mafundisho mengine ya uongo. . . . Kumepita miaka zaidi ya 40 tangu ile Kweli iliyo kama mawimbi ya bahari ilianza kuongezeka, inazidi kuongezeka na itaendelea kuongezeka mupaka wakati itajaa dunia yote. Maadui wa ile Kweli watajaribu kuizuia ili isienee katika dunia yote. Lakini kazi ya watu hao ni kama mutu anayejaribu kuzuia mawimbi ya bahari kwa kutumia kifagio cha kawaida tu.”

13, 14. (a) Ni nini inaonyesha kwamba ‘mujumbe’ alitayarisha njia kwa ajili ya Masiya-Mufalme? (b) Tunaweza kujifunza nini juu ya ndugu zetu hao walioishi kumepita miaka zaidi ya 100?

13 Fikiria jambo hili: Tungeweza kusema kwamba watu wa Mungu walikuwa wametayarishwa kuhusu mwanzo wa kuwapo kwa Kristo ikiwa hawangejua kutofautisha Yesu na Baba yake, Yehova? Bila shaka hapana! Ao tungeweza kusema kwamba watu walikuwa wametayarishwa ikiwa hawangejua kwamba zawadi ya kutokufa inapewa tu watu wadogo, ni kusema, wafuasi wa Kristo, wala mutu hapewe zawadi hiyo kwa bure? Vilevile hawangekuwa wametayarishwa ikiwa waliamini kwamba Mungu anawatesa watu katika moto wa milele bila kupumuzika! Inaonekana wazi kwamba ‘mujumbe’ alitayarisha njia kwa ajili ya Masiya-Mufalme!

14 Basi tuseme nini juu yetu leo? Tunaweza kujifunza nini juu ya ndugu zetu hao walioishi kumepita miaka zaidi ya 100? Sisi pia tunapaswa kusoma na kujifunza Neno la Mungu kwa bidii. (Yoh. 17:3) Watu wa ulimwengu wanapenda sana vitu vya kimwili, kwa hiyo, wanaendelea kuwa na njaa ya kiroho. Sisi tusiwe hivyo, ni vizuri hamu yetu ya kula chakula cha kiroho iongezeke zaidi na zaidi!—Soma 1 Timotheo 4:15.

‘Mutoke Kwake, Watu Wangu’

15. Wanafunzi wa Biblia walifikia kuelewa nini hatua kwa hatua? (Soma pia maelezo mengine.)

15 Wanafunzi wa Biblia walifundisha kwamba ni lazima kuachana kabisa na dini za ulimwengu. Katika mwaka wa 1879, gazeti Munara wa Mulinzi lilizungumuzia “dini ya Babiloni.” Je, lilizungumuza juu ya mapapa? Ao juu ya Kanisa Katoliki la Roma? Kwa miaka mingi dini za Kiprotestanti zilikuwa zimefundisha kwamba Babiloni inayotajwa katika unabii wa Biblia ni Kanisa Katoliki. Lakini, Wanafunzi wa Biblia walifikia polepole kuelewa kwamba dini zote zinazojidai kuwa za Kikristo zimo pia katika “Babiloni” wa siku zetu. Sababu gani waliamini hivyo? Kwa sababu dini hizo zote zinafundisha mafundisho ya uongo kama tulivyoona hapo juu. Kadiri miaka ilivyopita, vichapo vyetu vilionyesha wazi kwamba watu walio na moyo muzuri wanapaswa kutoka katika dini za Babiloni.

16, 17. (a) Ni musaada gani kitabu L’Aurore du Millénium Buku la 3 na gazeti Munara wa Mulinzi vilitolea watu ili kuwasaidia watoke katika dini za uongo? (b) Ni jambo gani lilipunguza uzito wa maonyo yaliyotelewa mwanzoni? (Soma maelezo mengine.)

16 Kwa mufano, katika mwaka wa 1891, kitabu ‘L’Aurore du Millénium’ katika Buku lake la 3, kilionyesha kwamba Mungu amekataa Babiloni wa siku hizi. Kitabu hicho kilisema hivi: “Makanisa yote ya dini zinazojidai kuwa za Kikristo yamekataliwa na Mungu.” Kitabu hicho kilisema tena kwamba kila mutu ambaye “hakubaliane na mafundisho ya uongo na matendo ya Babiloni anaombwa kuanzia sasa kuachana kabisa na Babiloni.”

17 Katika Mwezi wa 1, 1900, gazeti Munara wa Mulinzi liliwashauri wote ambao majina yao yalikuwa bado kufutwa katika vitabu vya dini zao na ambao waliendelea kusema hivi ili kutetea mwenendo wao: “Ninakubaliana kabisa na ile kweli, na ninahuzuria mara mojamoja kwenye kanisa langu.” Gazeti hilo liliuliza: “Lakini ni sawa kabisa kuwa muguu moja ndani na muguu mwingine katika Babiloni? Huo ndio utii ambao Mungu anaomba . . . na utii kama huo unaweza kweli kukubaliwa naye na kumupendeza? Hapana kabisa. Wakati mutu anaingia katika dini fulani anafanya agano mbele ya watu wote, na anapaswa kutimiza mambo yote ambayo agano hilo linaomba mupaka wakati . . . atajulisha mbele ya watu wote kwamba yeye si muamini tena wa dini hiyo.” Kadiri miaka ilivyopita, ujumbe huo ukawa wenye nguvu zaidi na zaidi. Watumishi wa Yehova wanapaswa kukata kabisa urafiki wote na dini za uongo.

18. Sababu gani ilikuwa jambo la lazima watu watoke katika Babiloni Mukubwa?

18 Ikiwa maonyo ya kutoka katika Babiloni Mukubwa hayakuwa yametolewa kwa ukawaida, je, wakati Kristo alifanywa kuwa Mufalme, angeweza kukuta kikundi cha watu wenye kutayarishwa, ni kusema, watumishi wake watiwa-mafuta hapa duniani? Bila shaka hapana. Kwa sababu ni Wakristo tu waliotoka katika utumwa wa Babiloni ndio wangeweza kumuabudu Yehova “kwa roho na kweli.” (Yoh. 4:24) Sisi pia leo tumeazimia kuachana kabisa na dini za uongo? Kwa hiyo, tuendelee basi kutii ile amri inayosema: ‘Mutoke kwake, watu wangu’!—Soma Ufunuo 18:4.

Mikusanyiko kwa Ajili ya Ibada

19, 20. Ni mashauri gani gazeti Munara wa Mulinzi lilitoa ili kuwatia moyo watu wa Mungu wakusanyike pamoja ili kumuabudu Mungu?

19 Wanafunzi wa Biblia walifundisha kwamba mahali ambapo inawezekana, Wakristo wanapaswa kukusanyika pamoja ili kumuabudu Mungu. Wakristo wa kweli wanatambua kwamba kutoka katika dini za uongo hakutoshe. Ni jambo la maana sana kufanya yale yanayoombwa na ibada ya kweli. Tangu wakati gazeti Munara wa Mulinzi lilianza kutokea, liliwatia moyo wasomaji kukusanyika pamoja ili kumuabudu Mungu. Kwa mufano, katika Mwezi wa 7, 1880, ndugu Russell alitoa ripoti kuhusu safari aliyofanya ili kutoa hotuba mbalimbali. Alifasiria namna mikutano mingi iliyofanywa ilikuwa yenye kutia moyo. Kisha, aliwatia moyo wasomaji watume karte ao barua fupi ili kuonyesha maendeleo yao; barua ao karte fulani ingeweza kutolewa katika gazeti Munara wa Mulinzi. Sababu gani aliwatia moyo wafanye hivyo? Alisema hivi: “Mufanye hivyo ili sisi wote tujue . . . namna Bwana anawabariki; na ikiwa munaendelea kukusanyika pamoja na wale walio na imani kama yenu, imani isiyolinganishwa na kitu chochote.”

Charles Russell na kikundi cha kwanza cha Wanafunzi wa Biblia katika muji wa Copenhagen, huko Danemark, katika mwaka wa 1909

20 Katika mwaka wa 1882, habari moja ambayo ilitokea katika gazeti Munara wa Mulinzi ilikuwa na kichwa “Tukusanyike Pamoja.” Habari hiyo iliwatia moyo Wakristo wakusanyike pamoja “ili kujengana, kutiana moyo na kutiana nguvu.” Ilisema hivi: “Ni jambo la lazima kufanya hivyo hata ikiwa kati yenu hakuna mutu aliyesoma masomo mengi ao aliye na kipawa fulani. Kila mumoja wenu alete Biblia yake, karatasi, na kalamu, na mufaidike kadiri inavyowezekana wakati wengine wanapotoa musaada kwa njia ya Konkordansi ya Biblia. Muchague habari munayopenda kuzungumuzia; muombe roho takatifu iwaongoze ili kuelewa habari hiyo. Kisha musome, mufikiri, na mulinganishe andiko moja na andiko lingine. Kwa kufanya hivyo, bila shaka, mutaongozwa katika kweli.”

21. Ni mufano gani muzuri kutaniko la muji wa Allegheny, Pennsylvania, liliwekea ndugu wengine kuhusu kukusanyika na kuhusu uchungaji?

21 Makao makubwa ya Wanafunzi wa Biblia yalikuwa katika muji wa Allegheny, huko Pennsylvania, États-Unis. Ndugu hao waliwekea wengine mufano muzuri kwa kukusanyika pamoja ili kutii shauri lililoongozwa na roho ya Mungu, linalopatikana katika andiko la Waebrania 10:24, 25. (Soma.) Kisha miaka mingi, ndugu Charles Capen ambaye alikuwa amekwisha kuzeeka, alikumbuka namna alikuwa anahuzuria mikutano hiyo alipokuwa angali mutoto mudogo. Aliandika hivi: “Ningali nakumbuka andiko moja kati ya maandiko yaliyokuwa kwenye ukuta wa jumba la kusanyiko. ‘Bwana wenu ni mumoja, Kristo; na ninyi wote ni ndugu.’ Kila mara nilikumbuka andiko hilo: hakuna viongozi wala watu wa kawaida kati ya watu wa Yehova.” (Mt. 23:8) Ndugu Capen alikumbuka pia namna mikutano hiyo ilikuwa yenye kuchochea na yenye kutia moyo sana. Pia, alikumbuka bidii ya ndugu Russell ya kulisha kila ndugu katika kutaniko.

22. Namna gani watu waaminifu walionyesha kwamba walikubali kitia moyo juu ya kuhuzuria mikutano ya Kikristo, na mufano wao unaweza kutufundisha nini?

22 Watu waaminifu walifuata mufano huo na walikubali maagizo waliyopewa. Makutaniko yalianzishwa katika miji mingine, kama vile muji wa Ohio na Michigan, na kisha mahali pote katika Amerika ya Kaskazini na katika inchi zingine. Fikiria jambo hili: Watumishi waaminifu wangelikuwa wametayarishwa kabisa kuhusu kuwapo kwa Kristo ikiwa hawakuwa wamezoezwa kutii shauri la Biblia la kukusanyika pamoja ili kumuabudu Mungu? Bila shaka hapana! Tuseme nini juu yetu leo? Tunapaswa kuwa wenye kuazimia kuhuzuria mikutano kwa ukawaida, tunapaswa kila wakati kutafuta wakati wa kumuabudu Mungu pamoja na kujengana kiroho.

Kuhubiri kwa Bidii

23. Gazeti Munara wa Mulinzi lilisema nini ili kuonyesha wazi kwamba kila mutiwa-mafuta anapaswa kuhubiri ile kweli?

23 Wanafunzi wa Biblia walifundisha kwamba watiwa-mafuta wote wanapaswa kuwa wahubiri wa ile kweli. Katika mwaka wa 1885, gazeti Munara wa Mulinzi lilisema hivi: “Tusisahau kwamba kila mutu aliyetiwa mafuta, alitiwa mafuta ili kuhubiri (Isa. 61:1), na aliitwa kwa ajili ya huduma.” Katika mwaka wa 1888, habari moja katika gazeti Munara wa Mulinzi ilikazia hivi: “Kazi yetu inajulikana wazi . . . Tukiona kazi hiyo kuwa si ya lazima na kutoa visababu, hilo litaonyesha kabisa kwamba sisi ni watumishi wavivu na wasiopenda kazi, na hilo litaonyesha kwamba hatustahili kuwa watiwa-mafuta.”

24, 25. (a) Ndugu Russell na wenzake waliwatia ndugu moyo kuhubiri, zaidi ya hilo walifanya tena nini? (b) Namna gani kolportere mumoja alizungumuzia kazi yake wakati hakukukuwa na motokari kama leo?

24 Ndugu Russell na wenzake walitia ndugu moyo kuhubiri, lakini walifanya pia zaidi. Walianza pia kuchapisha trakte ambazo ziliitwa Trakte za Wanafunzi wa Biblia, kisha ziliitwa Teolojia ya Zamani (zilichapishwa mara ine kwa mwaka). Wasomaji wa Munara wa Mulinzi walitumiwa trakte hizo ili kuzigawanyia watu bila malipo.

Ni vizuri kila mumoja wetu ajiulize hivi, ‘Kazi ya kuhubiri ndio kazi ya maana sana katika maisha yangu?’

25 Wale waliojitoa katika utumishi wa wakati wote waliitwa wakolportere. Ndugu Charles Capen, tuliyezungumuzia hapo mwanzoni, alikuwa kati yao. Kisha miaka fulani alikumbuka hivi: “Nilitumia karte iliyotengenezwa na Biro ya Uchunguzi wa Jiolojia ya Serikali ya Amerika ili kujua eneo langu na kuhubiri eneo hilo la Pennsylvania. Karte zilikuwa zinaonyesha barabara zote, na hilo lilinisaidia kufikia sehemu zote za kila eneo kwa miguu. Wakati fulani nilikuwa ninatembea eneo hilo mwendo wa siku tatu ili kuchukua maombi ya watu kuhusu mabuku ya kitabu Étude des Écritures. Kisha nilikuwa ninalipa feza ili kutumia farasi ao motokari ya kukokotwa na farasi, ili niweze kuwapelekea watu vitabu hivyo. Mara nyingi nilipitisha usiku pamoja na watu wenye kuishi katika mashamba yao. Siku hizo, watu walitumia njia hiyo ili kusafiri, kwa sababu hakukuwa na mitokari mingi kama leo.”

Ndugu huyu ambaye ni kolportere, alichapa “Karte ya Vipindi vya Matukio” kwenye motokari ambayo ilikokotwa na farasi

26. (a) Sababu gani watu wa Mungu walipaswa kufanya kazi ya kuhubiri ili wawe wenye kutayarishwa kwa ajili ya utawala wa Kristo? (b) Ni maulizo gani ni vizuri kila mumoja ajiulize?

26 Bila shaka, ili kuhubiri hivyo kwa juhudi, iliomba mutu awe na bidii na asiwe mwoga. Tungeweza kusema kwamba Wakristo wa kweli walikuwa wametayarishwa kwa ajili ya utawala wa Kristo ikiwa hawangefundishwa kwamba kazi ya kuhubiri ni ya maana kabisa? Jibu ni hapana! Zaidi ya hilo, katika siku zilizokuwa mbele, kazi hiyo ndio ingekuwa alama ya maana sana yenye kuonyesha kuwapo kwa Kristo. (Mt. 24:14) Watu wa Mungu walipaswa kuwa wametayarishwa ili kufanya kazi hiyo yenye kuokoa uzima kuwa ya maana sana katika maisha yao. Kwa hiyo, ni vizuri kila mumoja wetu ajiulize hivi: ‘Kazi ya kuhubiri ndio kazi ya maana sana katika maisha yangu? Ninajiima mambo mengine ili niweze kufanya kabisa kazi hiyo?’

Kuzaliwa kwa Ufalme wa Mungu!

27, 28. Mutume Yohana aliona nini katika maono, na Shetani na mashetani wake walifanya nini wakati wa kuzaliwa kwa Ufalme?

27 Kisha ule mwaka wa maana sana ulifika, ni kusema, mwaka wa 1914. Kama vile tuliona mwanzoni mwa sura hii, hakuna mwanadamu aliyejionea tukio hilo nzuri sana lililotokea mbinguni. Lakini, mutume Yohana alionyeshwa katika maono jambo lililotokea mbinguni. Alionyeshwa jambo hilo kwa njia ya ishara ao alama. Yohana aliona “ishara [alama] kubwa” mbinguni. Aliona ‘mwanamuke’ wa Mungu, ni kusema, tengenezo la Mungu la viumbe vya kiroho mbinguni. Mwanamuke huyo alikuwa na mimba na alizaa mutoto mwanaume. Mutoto huyo wa mufano ambaye tunazungumuzia, karibuni ‘atachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma.’ Wakati mutoto huyo anazaliwa ‘anachukuliwa mupaka kwa Mungu na mupaka kwenye kiti chake [mutoto] cha ufalme.’ Sauti kubwa katika mbingu inasema hivi: “Sasa kumekuwa na wokovu na nguvu na Ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake.”​—Ufu. 12:1, 5, 10.

28 Bila shaka, Yohana aliona katika maono kuzaliwa kwa Ufalme wa Masiya. Tukio hilo lilikuwa tukio nzuri sana, lakini halikumufurahisha kila mutu. Shetani na mashetani wake walipigana na malaika waaminifu ambao waliongozwa na Mikaeli, ao Kristo. Matokeo yalikuwa hivi: ‘Yule nyoka mukubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayoikaliwa, akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.’​—Ufu. 12:7, 9.

Katika mwaka wa 1914, Wanafunzi wa Biblia walianza kutambua alama ya kuwapo kwa Kristo kusikoonekana

29, 30. Kisha kuzaliwa kwa Ufalme wa Masiya, mambo yalibadilika namna gani (a) duniani? (b) mbinguni?

29 Miaka mingi mbele ya mwaka wa 1914, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamesema kwamba kipindi cha musukosuko kingeanza katika mwaka huo uliotiwa alama. Lakini, hata hivyo, hawakujua ni kwa kadiri gani mambo hayo yangetimia sawasawa kama vile walisema. Yohana aliona katika maono kwamba Shetani angeanza hata kuchochea sana mambo ya wanadamu: ‘Kwa sababu hiyo mufurahi, enyi mbingu na nyinyi munaokaa ndani! Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, mwenye hasira kali, [kwa sababu] anajua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.’ (Ufu. 12:12) Katika mwaka wa 1914, vita ya kwanza ya ulimwengu ilitokea na alama ya kuwapo kwa Kristo katika Ufalme ilianza kutimia katika ulimwengu wote. Zile “siku za mwisho” za ulimwengu huu muovu zilianza wakati huo.​—2 Tim. 3:1.

30 Hata hivyo, kulikuwa na furaha mbinguni. Shetani na mashetani wake walifukuzwa mbinguni, kwa milele. Tunasoma hivi: ‘Kwa sababu hiyo mufurahi, enyi mbingu na nyinyi munaokaa ndani!’ (Ufu. 12:12) Kwa sababu Yesu alimaliza kusafisha mbingu na aliwekwa kuwa Mufalme, Ufalme wa Masiya ulikuwa sasa tayari kutenda kwa faida ya watu wa Mungu hapa duniani. Ulichukua hatua gani? Kama vile tuliona mwanzoni mwa sura hii, Kristo ambaye ni ‘mujumbe wa agano’ angeanza kwanza kusafisha watu wa Mungu hapa duniani. Hilo lingetimia namna gani?

Kipindi cha Kujaribiwa

31. Nabii Malaki alitabiri nini juu ya kipindi cha kusafishwa, na unabii huo ulianza kutimia mwaka gani? (Soma pia maelezo mengine.)

31 Nabii Malaki alitabiri kwamba kusafishwa huko haingekuwa jambo mwepesi. Aliandika hivi: ‘Ni nani atakayestahimili [atakayevumilia] siku ya kuja kwake, na ni nani atakayesimama wakati atakapoonekana? Kwa maana atakuwa kama moto wa musafishaji na kama sabuni ya wafuaji wa nguo.’ (Mal. 3:2) Ni ajabu! Maneno hayo yalitimizwa kama yalivyosemwa. Kuanzia mwaka wa 1914, watu wa Mungu duniani waliendelea kupambana na majaribu mengi na magumu mbalimbali. Wakati Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilikuwa inawaka moto, Wanafunzi wa Biblia waliteswa vikali na walifungwa.

32. Ni muvurugo gani uliingia katika tengenezo katika mwaka wa 1916 ambao uliumiza sana watu wa Mungu?

32 Muvurugo uliingia pia katika tengenezo. Katika mwaka wa 1916, Ndugu Russell alikufa mwenye umri wa miaka 64 tu. Watu wengi wa Mungu walihuzunika sana. Kifo chake kilifunua kwamba wengi walikuwa wanaheshimu mwanadamu kupita kiasi. Hata ikiwa Ndugu Russell hakukubali hata kidogo heshima kama hiyo, wengi walikuwa wanaonyesha hali ya kumuabudu. Wengi walifikiri kwamba kifo chake ndicho kilikuwa mwisho wa ufunuo wa ile kweli, ufunuo unaofanyika hatua kwa hatua. Tena wengi waliingiwa na chuki na hawakuweza tena kusonga mbele. Hali hiyo pia ilifanya kuwe na uasi-imani ambao ulitokeza mugawanyiko katika tengenezo.

33. Namna gani kukosa kutimia kwa matumaini fulani ilikuwa jaribu kwa watu wa Mungu?

33 Jaribu lingine lilitokea wakati matumaini ambayo Wanafunzi wa Biblia walikuwa nayo hayakutimia. Gazeti Munara wa Mulinzi lilionyesha wazi kwamba Nyakati za Mataifa zingefikia mwisho katika mwaka wa 1914. Hata hivyo, ndugu hawakuelewa vizuri ni nini ingefanyika kabisa katika mwaka huo. (Lu. 21:24) Walifikiri kwamba katika mwaka wa 1914, Kristo angepeleka bibi-arusi wake, ni kusema, Wakristo watiwa-mafuta, mbinguni ili kutawala pamoja naye. Matumaini hayo hayakutimia. Kisha, katika mwaka wa 1917, gazeti Munara wa Mulinzi lilitangaza kwamba miaka 40 ya mavuno ingepaswa kumalizika katika mwaka wa 1918 (pengine kuanzia mwezi wa 4 mupaka mwezi wa 6). Lakini kazi ya kuhubiri habari njema iliendelea kuzaa matunda, haikumalizika katika mwaka huo. Kisha gazeti likasema kwamba kazi ya mavuno ilikuwa imekwisha kabisa na kwamba ni kipindi cha kukusanya mavuno ndicho kiliendelea. Wengi walivunjika moyo na waliacha kumutumikia Yehova.

34. Ni jaribu gani lingine lenye kuvunja moyo lilitokea katika mwaka wa 1918, na sababu gani viongozi wengi wa dini walifikiri watu wa Mungu “wamekufa”?

34 Jaribu lingine lenye kuvunja moyo lilitokea katika mwaka wa 1918. Ndugu J. F. Rutherford, aliyechukua nafasi ya Ndugu C. T. Russell ya kuongoza kazi ya watu wa Mungu, alifungwa na ndugu wengine saba ambao walikuwa wanasimamia kazi. Walihukumiwa bila haki na kufungwa miaka mingi kwenye gereza kubwa la serikali ya États-Unis, Atlanta, Georgia. Kwa wakati fulani ilionekana kama kazi ya watu wa Mungu imesimama. Wakubwa wengi wa dini zinazojidai kuwa za Kikristo walifurahi. Walifikiri hivi: Kwa sababu “viongozi” hao wamefungwa, makao makubwa yao katika Brooklyn yamefungwa, na kazi yao ya kuhubiri inashambuliwa vikali katika Amerika na Ulaya, basi wale Wanafunzi wa Biblia wenye kutusumbua “wamekufa.” Kwa hiyo, hawatakuwa tena hatari kwetu. (Ufu. 11:3, 7-10) Walijidanganya kabisa!

Kipindi cha Kurudishwa Tena Kwenye Uzima!

35. Sababu gani Yesu aliacha wafuasi wake wateseke, na alifanya nini ili kuwasaidia?

35 Maadui wa ile kweli hawakujua hata kidogo kwamba Yesu aliacha watu wake wateseke kwa sababu Yehova alikuwa sasa anaketi ‘kama musafishaji na mutakasaji wa feza.’ (Mal. 3:3) Yehova na Mwana wake walijua vizuri kwamba wale walio waaminifu wangeokoka majaribu hayo yaliyo kama moto. Kwa hiyo wangetakaswa na kuwa safi ili wastahili zaidi kumutumikia Mufalme. Katika miezi ya mwanzo ya mwaka wa 1919, ilionekana wazi kwamba roho ya Mungu ilikuwa imefanya jambo ambalo maadui wa watu wake walifikiri kuwa haliwezekane. Watumishi wake waaminifu walirudishwa tena kwenye uzima! (Ufu. 11:11) Inaonekana kwamba wakati huo, Yesu alitimiza alama ya maana sana ya siku za mwisho. Alimutia ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara,’ ni kusema, kikundi kidogo cha wanaume watiwa-mafuta, ili aongoze watu wake na kuwatolea chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.—Mt. 24:45-47.

36. Ni nini inaonyesha kwamba watu wa Mungu walirudishwa tena kwenye uzima kiroho?

36 Tarehe 26 Mwezi wa 3, 1919, Ndugu Rutherford na wenzake walifunguliwa. Bila kukawia mukusanyiko mukubwa ambao ulifanywa Mwezi wa 9 ulitayarishwa. Mipango ilichukuliwa ili kuwe na gazeti la pili zaidi ya Munara wa Mulinzi, na lingeitwa L’Âge d’Or (leo Amuka!). Gazeti hilo lilipaswa kutumiwa katika mahubiri. Katika mwaka huohuo, kulitokea kichapo Le Bulletin kwa mara ya kwanza, leo ni buku la mukutano Utumishi na Maisha ya Mukristo. Tokea hapo kichapo hicho kimekuwa na mapendekezo yanayotuchochea katika kazi ya kuhubiri. Bila shaka, kuanzia mwaka wa 1919 kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba imetiwa pa nafasi ya kwanza.

37. Katika miaka iliyofuata mwaka wa 1919, namna gani wengine walionyesha kwamba wao si waaminifu?

37 Kazi ya kuhubiri habari njema iliendelea kusafisha wafuasi wa Kristo, kwa sababu wale waliokuwa na majivuno na kiburi hawakufurahia kufanya kazi hiyo inayoomba unyenyekevu. Wale waliokataa kuhubiri walijitenga na watumishi walio waaminifu. Katika miaka iliyofuata mwaka wa 1919, wale wasio waaminifu walianza kuwasema vibaya watumishi waaminifu wa Yehova, na kuwachafua. Walijiunga hata na wale waliokuwa wanawatesa watumishi waaminifu wa Yehova.

38. Kila baraka na ushindi mbalimbali wa wafuasi wa Kristo hapa duniani ni ushuhuda wa nini kwetu?

38 Ijapokuwa hao wafuasi wa Kristo walishambuliwa, waliendelea kubarikiwa na kuwa na nguvu kiroho. Kuanzia hapo, kila baraka na ushindi waliokuwa wanapata, ni ushuhuda kwetu kwamba Ufalme wa Mungu unatawala! Ikiwa wanadamu hao wasio wakamilifu, ambao walikuwa kikundi kidogo, waliendelea kumushinda Shetani na ulimwengu wake muovu, ni kwa sababu Mungu aliwategemeza na kuwabariki. Alifanya hivyo kupitia Mwana wake na Ufalme wa Masiya!​—Soma Isaya 54:17.

Ndugu Rutherford anatoa hotuba yenye kuchochea kwenye mukusanyiko mukubwa, miezi fulani tu kisha kufunguliwa kwake

39, 40. (a) Kitabu hiki kitazungumuzia sehemu gani fulani? (b) Kujifunza kitabu hiki kutakuletea faida gani?

39 Katika sura inayofuata tutachunguza mambo ambayo Ufalme wa Mungu umetimiza duniani katika kipindi cha miaka 100 hivi, tangu kuzaliwa kwa ufalme huo mbinguni. Kila sehemu ya kitabu hiki itazungumuzia sehemu fulani ya kazi ya Ufalme inayotimizwa duniani. Kila sura, kila kisanduku cha kurudilia mambo, vitamusaidia kila mumoja wetu aone kwamba Ufalme si jambo la kuwazia tu. Katika sura za mwisho, tutazungumuzia namna mambo yatakuwa wakati Ufalme utakuja hivi karibuni kuharibu watu waovu na kufanya dunia kuwa paradiso. Kujifunza kitabu hiki kutakuletea faida gani?

40 Shetani anapenda usiwe na imani katika Ufalme wa Mungu. Lakini Yehova yeye anapenda imani yako iwe nguvu ili iweze kukulinda na kukufanya ubaki nguvu kiroho. (Efe. 6:16) Kwa hiyo, tunakutia moyo ujifunze kitabu hiki kwa bidii. Uendelee kujiuliza, ‘Ninauona Ufalme wa Mungu kuwa jambo la kweli kabisa?’ Ikiwa unauona Ufalme kuwa jambo la kweli kabisa, bila shaka, hilo litakufanya utegemeze Ufalme huo kwa uaminifu na kwa bidii, na ukuwe hapo siku ile kila mutu ataona kwa macho yake kwamba Ufalme wa Mungu si jambo la kuwazia tu na kwamba unatawala!

Ukitaka kujua mengi juu ya Grew, Stetson, na Storrs, soma kitabu Mashahidi wa Yehova​—Wapiga Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa 45, 46.

Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba ni lazima kutoka katika dini za uongo zilizofanya urafiki na ulimwengu. Hata hivyo, kwa miaka mingi waliendelea kuwaona kama ndugu wa Kikristo watu ambao, ijapokuwa hawakuwa Wanafunzi wa Biblia, walisema kwamba wanaamini zabihu ya ukombozi na ambao walijidai kwamba walijitoa kwa Mungu.

Jambo moja ambalo lilipunguza uzito wa maonyo hayo, ni kwamba maonyo hayo yalikuwa yanazungumuzia tu kundi ndogo la Kristo: watu 144000. Katika Sura ya 5 ya kitabu hiki tutaona kwamba mbele ya mwaka wa 1935, Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba ‘mukutano mukubwa’ unaozungumuziwa katika andiko la Ufunuo 7:9, 10 (tafsiri ya King James), utatia ndani waamini wengi wa dini zinazojidai kuwa za Kikristo, na kwamba wangebarikiwa kwa kuwa kikundi cha pili huko mbinguni, kwa sababu mwishoni wangejiunga na Kristo.

Katika Mwezi wa 9, 1920, gazeti L’Âge d’Or lilikuwa na habari ya pekee iliyozungumuzia kwa kirefu mateso makali ya kinyama na yenye kuchukiza sana katika inchi ya Canada, Uingereza, Ujerumani, na Étas-Unis. Ni kweli kwamba miaka mingi mbele ya vita ya kwanza ya ulimwengu kulikuwa na mateso, lakini yakilinganishwa na hayo yalikuwa madogo tu.

Kwa miaka mingi gazeti Munara wa Mulinzi lilikuwa linatolewa ili kuwajenga tu Wakristo wa kundi ndogo.