Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 3

Yehova Anafunua Kusudi Lake

Yehova Anafunua Kusudi Lake

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Yehova anafunua hatua kwa hatua uelewaji wa kusudi lake, lakini anafanya hivyo kwa wale tu wanaomwogopa

1, 2. Yehova amefunuaje kusudi lake kwa ajili ya wanadamu?

WAZAZI wenye upendo huwahusisha watoto wao katika mazungumzo yanayohusu mambo ya familia. Hata hivyo, wanatumia busara inapohusu kiasi cha habari wanazowaambia watoto wao. Wanawafunulia watoto wao habari ambazo wanafikiri kwamba wamekomaa vya kutosha kuzielewa.

2 Vivyo hivyo, Yehova amefunua hatua kwa hatua kusudi lake kwa ajili ya wanadamu. Lakini amefanya hivyo tu wakati unaofaa ulipofika. Hebu tuchunguze kifupi jinsi ambavyo Yehova amefunua kweli kuhusu Ufalme katika historia yote ya wanadamu.

Kwa Nini Ufalme Unahitajika?

3, 4. Je, Yehova alipanga mapema maisha ya wanadamu? Eleza.

3 Mwanzoni, Ufalme wa Kimasihi haukuwa sehemu ya kusudi la Yehova. Kwa nini? Kwa sababu Yehova hakupanga mapema maisha ya wanadamu; aliwaumba wanadamu wakiwa na uhuru wa kuchagua. Hivyo, aliwaambia Adamu na Hawa kusudi lake kwa ajili ya wanadamu: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwa. 1:28) Pia, Yehova alitaka waheshimu viwango vyake vya mema na mabaya. (Mwa. 2:16, 17) Adamu na Hawa wangeweza kuchagua kubaki wakiwa washikamanifu. Ikiwa wao na wazao wao wangefanya hivyo, hatungehitaji Ufalme unaotawaliwa na Kristo ili utimize kusudi la Mungu. Leo, ulimwengu mzima ungekuwa umejaa wanadamu wakamilifu wanaomwabudu Yehova.

4 Uasi wa Shetani, Adamu, na Hawa haukumfanya Yehova atupilie mbali kusudi lake la kuifanya dunia ijae wanadamu wakamilifu. Badala yake, Yehova alibadili njia yake ya kutimiza kusudi hilo. Kusudi lake si kama treni ambalo ni lazima lipite katika reli fulani hususa ili lifike mwisho wa safari yake, na linaweza kuacha reli kwa sababu ya utendaji wa watu. Yehova anapotaja kusudi lake, hakuna nguvu yoyote ulimwenguni inayoweza kumzuia kulitimiza. (Soma Isaya 55:11.) Ikiwa jambo fulani linatishia kuzuia njia ambayo Yehova anatumia kutimiza kusudi lake, Yeye hutumia njia nyingine. * (Kut. 3:14, 15) Anapoona inafaa, Yehova huwajulisha watumishi wake washikamanifu njia hiyo mpya ambayo atatumia kutimiza kusudi lake.

5. Yehova alitendaje uasi ulipotokea Edeni?

5 Ili kushughulikia uasi uliotokea Edeni, Yehova alikusudia kusimamisha Ufalme. (Mt. 25:34) Ilipoonekana kana kwamba hakuna tumaini kwa wanadamu, Yehova alianza kufunua njia ambayo angetumia kuwarudishia wanadamu ukamilifu na kuondoa madhara yote ambayo yamesababishwa na jitihada za Shetani za kunyakua mamlaka ambazo hazikufanikiwa. (Mwa. 3:14-19) Hata hivyo, Yehova hakufunua habari zote kuhusu Ufalme kwa wakati mmoja.

Yehova Anaanza Kufunua Kweli Kuhusu Ufalme

6. Yehova aliahidi nini, lakini hakufunua nini?

6 Katika unabii wa kwanza, Yehova aliahidi kwamba “uzao” fulani ungemponda nyoka. (Soma Mwanzo 3:15.) Hata hivyo, utambulisho wa yule atakayekuwa uzao huo na uzao wa nyoka haukufunuliwa wakati huo. Kwa kweli, kwa miaka 2,000 hivi, Yehova hakufunua habari zaidi kuhusu jambo hilo. *

7. Kwa nini Yehova alimchagua Abrahamu, na hilo linatufundisha jambo gani muhimu?

7 Hatimaye, Yehova alimchagua Abrahamu kuwa yule ambaye uzao ulioahidiwa ungekuja kupitia kwake. Abrahamu alichaguliwa kwa sababu ‘alisikiliza sauti ya Yehova.’ (Mwa. 22:18) Tunajifunza jambo fulani muhimu sana katika kisa hiki—Yehova anafunua kusudi lake kwa wale tu wanaomwogopa na kumheshimu.—Soma Zaburi 25:14.

8, 9. Yehova aliwafunulia Abrahamu na Yakobo mambo gani kuhusu uzao ulioahidiwa?

8 Alipokuwa akizungumza na rafiki yake Abrahamu kupitia malaika, Yehova alifunua kwa mara ya kwanza jambo hili muhimu sana kuhusu ule uzao ulioahidiwa: Angekuwa mwanadamu. (Mwa. 22:15-17; Yak. 2:23) Lakini mwanadamu huyo angemponda nyoka jinsi gani? Nyoka alikuwa nani? Mambo ambayo yangefunuliwa baadaye yangejibu maswali hayo.

9 Yehova aliamua kwamba uzao ulioahidiwa ungekuja kupitia mjukuu wa Abrahamu, Yakobo, mwanaume aliyekuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. (Mwa. 28:13-22) Kupitia Yakobo, Yehova alifunua kwamba Yule Aliyeahidiwa angetokea katika ukoo wa Yuda, mwana wa Yakobo. Yakobo alitabiri kwamba mzao huyo wa Yuda angepokea “fimbo ya enzi,” fimbo ambayo iliwakilisha mamlaka ya kifalme, na ‘vikundi vya watu vingemtii yeye.’ (Mwa. 49:1, 10) Kupitia unabii huo, Yehova alionyesha kwamba Yule Aliyeahidiwa angekuwa mtawala, mfalme.

10, 11. Kwa nini Yehova aliwafunulia Daudi na Danieli kusudi lake?

10 Karibu miaka 650 baada ya Yuda kufa, Yehova alimfunulia Mfalme Daudi, wa ukoo wa Yuda, habari zaidi kuhusu kusudi lake. Yehova alimwona Daudi kuwa “mtu anayekubalika kwa moyo wake.” (1 Sam. 13:14; 17:12; Mdo. 13:22) Kwa kuwa Daudi alimwogopa na kumheshimu Mungu, Yehova aliamua kufanya agano pamoja naye na kumwahidi kwamba mmoja wa wazao wake angetawala milele.—2 Sam. 7:8, 12-16.

11 Miaka 500 hivi baadaye, Yehova alimtumia nabii Danieli kufunua mwaka hususa ambao Mtiwa-Mafuta, au Masihi, angetokea duniani. (Dan. 9:25) Yehova alimwona Danieli kuwa “mtu mwenye kutamanika sana.” Kwa nini? Kwa sababu Danieli alimheshimu sana Yehova na alimtumikia daima.—Dan. 6:16; 9:22, 23.

12. Danieli aliambiwa afanye nini, na kwa nini?

12 Ingawa Yehova aliwatumia manabii waaminifu kama Danieli kuandika habari nyingi kuhusu uzao ulioahidiwa, yaani Masihi, wakati wa Yehova wa kuwafunulia watumishi wake maana kamili ya mambo ambayo roho yake iliwaongoza kuandika haukuwa umefika. Kwa mfano, baada ya kupewa maono yanayohusiana na kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu, Danieli aliambiwa atie muhuri unabii huo hadi wakati uliowekwa na Yehova. Wakati huo, ujuzi wa kweli ungekuwa “mwingi.”—Dan. 12:4.

Yehova aliwatumia wanaume waaminifu kama Danieli kuandika habari nyingi kuhusu Ufalme wa Kimasihi

Yesu Anafunua Kusudi la Mungu

13. (a) Ni nani aliyekuwa uzao ulioahidiwa? (b) Yesu alifunuaje habari zaidi kuhusu unabii ulioandikwa katika Mwanzo 3:15?

13 Yehova alimtambulisha waziwazi Yesu kuwa ndiye uzao ulioahidiwa, mzao wa Daudi ambaye angetawala akiwa Mfalme. (Luka 1:30-33; 3:21, 22) Yesu alipoanza huduma yake, ni kana kwamba nuru iliwaangazia watu ili waelewe kusudi la Mungu. (Mt. 4:13-17) Kwa mfano, Yesu aliondoa shaka zozote kuhusu utambulisho wa yule “nyoka” anayetajwa kwenye Mwanzo 3:14, 15, alipomwita Ibilisi “muuaji” na “baba ya uwongo.” (Yoh. 8:44) Katika ufunuo aliompa Yohana, Yesu alimtambulisha “yule nyoka wa zamani” kuwa “yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani.” * (Soma Ufunuo 1:1; 12:9.) Katika ufunuo huohuo, Yesu anaonyesha jinsi ambavyo yeye mwenyewe, akiwa ule uzao ulioahidiwa, atatimiza unabii uliotolewa Edeni na kumponda kabisa Shetani.—Ufu. 20: 7-10.

14-16. Je, ni mara zote Wakristo wa karne ya kwanza walielewa kikamili maana ya kweli ambazo Yesu alifunua? Eleza.

14 Kama tulivyoona katika Sura ya 1 ya kitabu hiki, Yesu alizungumza sana kuhusu Ufalme. Hata hivyo, si kila mara aliwafunulia wanafunzi wake habari zote walizotaka kujua. Hata alipozungumzia jambo fulani hususa, ilichukua muda mrefu, nyakati nyingine hata karne nyingi, kwa wafuasi wa Kristo kuelewa kikamili kweli ambazo Bwana wao alikuwa amewafunulia. Fikiria mifano michache.

15 Katika mwaka wa 33 W.K., Yesu alieleza wazi kwamba watawala ambao watamsaidia Mfalme wa Ufalme wa Mungu wangechaguliwa kutoka duniani na kufufuliwa wakiwa viumbe wa roho mbinguni. Hata hivyo, wanafunzi wake, hawakuelewa mara moja ufunuo huo. (Dan. 7:18; Yoh. 14:2-5) Katika mwaka huohuo, Yesu alitumia mifano kuonyesha kwamba Ufalme haungesimamishwa hadi muda mrefu upite baada ya yeye kwenda mbinguni. (Mt. 25:14, 19; Luka 19:11, 12) Wanafunzi hawakuelewa wazo hilo muhimu sana na ndiyo sababu baada ya Yesu kufufuliwa walimuuliza hivi: “Je, unarudishia Israeli ufalme wakati huu?” Hata hivyo, Yesu aliamua kutofunua habari zaidi wakati huo. (Mdo. 1:6, 7) Pia, Yesu alifundisha kwamba kungekuwa na “kondoo wengine,” ambao hawangekuwa sehemu ya “kundi dogo” la watawala wenzake. (Yoh. 10:16; Luka 12:32) Wafuasi wa Kristo hawakuelewa kikamili ni nani watakaofanyiza makundi hayo mawili hadi miaka kadhaa baada ya Ufalme kusimamishwa katika mwaka wa 1914.

16 Yesu angewaambia wanafunzi wake mambo mengi alipokuwa duniani, lakini alijua kwamba hawangeweza kuyastahimili. (Yoh. 16:12) Bila shaka, ujuzi mwingi kuhusu Ufalme ulifunuliwa katika karne ya kwanza. Hata hivyo, huo haukuwa wakati wa ujuzi huo kuwa mwingi.

Ujuzi wa Kweli Unakuwa Mwingi “Wakati wa Mwisho”

17. Tunapaswa kufanya nini ili kuelewa kweli kuhusu Ufalme, lakini ni nini kingine kinachohitajiwa?

17 Yehova alimwahidi Danieli kwamba “wakati wa mwisho,” wengi ‘wangeenda huku na huku, na ujuzi wa kweli’ kuhusu kusudi la Mungu ungekuwa mwingi. (Dan. 12:4) Wale wanaotaka ujuzi huo ni lazima wajitahidi sana kuupata. Kitabu kimoja kinasema kwamba kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa “kwenda huku na huku” hutoa wazo la mtu anayekichunguza kitabu kwa makini sana na kwa ukamili. Hata hivyo, haidhuru tunachunguza Biblia kwa ukamili kadiri gani, hatuwezi kuelewa kwa usahihi kweli kuhusu Ufalme isipokuwa Yehova atusaidie kuzielewa.—Soma Mathayo 13:11.

18. Wale wanaomwogopa Yehova wameonyeshaje imani na unyenyekevu?

18 Kama vile Yehova alivyofunua hatua kwa hatua kweli kuhusu Ufalme kabla ya mwaka wa 1914, anaendelea kufanya vivyo hivyo wakati huu wa mwisho. Kama vile Sura ya 4 na ya 5 za kitabu hiki zitakavyoonyesha, kwa miaka 100 iliyopita, watu wa Mungu wamelazimika kurekebisha uelewaji wao mara kadhaa. Je, jambo hilo linamaanisha kwamba hawana utegemezo wa Yehova? La hasha! Yeye huwategemeza. Kwa nini? Kwa sababu wale wanaomwogopa Yehova wameonyesha sifa mbili anazopenda—imani na unyenyekevu. (Ebr. 11:6; Yak. 4:6) Watumishi wa Yehova wana imani kwamba ahadi zote zilizo katika Neno la Mungu zitatimia. Wanaonyesha unyenyekevu wanapokubali kwamba hawakuelewa kikamili jinsi ambavyo ahadi hizo zingetimizwa. Mtazamo huo wa unyenyekevu unaonyeshwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1925, ambalo lilisema hivi: “Tunajua kwamba Bwana ndiye mfafanuzi wa mambo, na kwamba atawafafanulia watu wake Neno lake kwa njia nzuri na kwa wakati wake mwenyewe.”

“Bwana . . . atawafafanulia watu wake Neno lake kwa njia nzuri na kwa wakati wake mwenyewe”

19. Yehova ameturuhusu kuelewa nini sasa, na kwa nini?

19 Ufalme uliposimamishwa mwaka wa 1914, watu wa Mungu hawakuwa na ujuzi kamili kuhusu jinsi ambavyo unabii mbalimbali uliohusiana na Ufalme ungetimizwa. (1 Kor. 13:9, 10, 12) Kwa kuwa tuna tamaa ya kuona ahadi za Mungu zikitimia, pindi fulani tumekata shauri kimakosa. Kwa miaka mingi, hekima ya maneno yaliyotajwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi lililonukuliwa kwenye fungu lililotangulia imeonekana wazi. Makala hiyo ilieleza hivi: “Inaonekana kuwa inafaa kukata shauri kwamba, hatuwezi kuelewa unabii hadi uwe umetimia au unaendelea kutimia.” Sasa kwa kuwa tuko mwishoni kabisa mwa wakati wa mwisho, unabii mwingi kuhusu Ufalme umetimia na unaendelea kutimia. Kwa kuwa watu wa Mungu ni wanyenyekevu na wako tayari kurekebishwa, Yehova ameruhusu tuelewe kikamili zaidi kusudi lake. Ujuzi wa kweli umekuwa mwingi!

Marekebisho ya Uelewaji Yanawajaribu Watu wa Mungu

20, 21. Marekebisho ya uelewaji yaliwaathirije Wakristo wa karne ya kwanza?

20 Yehova anaporekebisha uelewaji wetu wa kweli, mioyo yetu hujaribiwa. Je, imani na unyenyekevu utatuchochea kukubali mabadiliko? Wakristo walioishi katikati ya karne ya kwanza walikabili jaribu kama hilo. Kwa mfano, hebu wazia ukiwa Mkristo Myahudi na unaishi wakati huo. Unaiheshimu sana Sheria ya Musa na unajivunia kuwa Mwisraeli. Sasa unapokea barua kutoka kwa mtume Paulo zilizoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu zikieleza kwamba watu hawako tena chini ya Sheria, na kwamba Yehova amewakataa Waisraeli wa asili na badala yake anakusanya Waisraeli wa kiroho ambao wanafanyizwa na Wayahudi na Watu wa Mataifa. (Rom. 10:12; 11:17-24; Gal. 6:15, 16; Kol. 2:13, 14) Wewe ungefanya nini?

21 Wakristo wanyenyekevu walikubali ufafanuzi wa Paulo ulioongozwa na roho, na Yehova aliwabariki. (Mdo. 13:48) Wengine walikasirishwa na marekebisho hayo na walitaka kushikilia uelewaji wao wa zamani. (Gal. 5:7-12) Ikiwa hawangebadili maoni yao, basi watu hao wangepoteza nafasi ya kutawala pamoja na Kristo.—2 Pet. 2:1.

22. Unahisije kuhusu marekebisho ya uelewaji wetu kuhusu makusudi ya Mungu?

22 Katika miaka ya hivi karibuni, Yehova amerekebisha uelewaji wetu kuhusu Ufalme. Kwa mfano, ametusaidia tuelewe vizuri zaidi ni wakati gani wale watakaokuwa raia wa Ufalme watatenganishwa na watu wasioitikia habari njema, kama vile kondoo na mbuzi wanavyotenganishwa. Pia, ametufundisha kuhusu wakati ambapo idadi kamili ya wale 144,000 itatimia, maana ya mifano ambayo Yesu alitoa kuhusu Ufalme, na ni wakati gani mtiwa-mafuta wa mwisho atafufuliwa na kuishi mbinguni. * Wewe unatendaje unapopata marekebisho hayo? Je, imani yako inaimarishwa? Je, unaona marekebisho hayo kuwa uthibitisho wa kwamba Yehova anaendelea kuwaelimisha watu wake wanyenyekevu? Habari zifuatazo katika kitabu hiki zitaimarisha zaidi uhakika wako kwamba Yehova anaendelea kufunua kusudi lake hatua kwa hatua kwa wale wanaomwogopa.

^ fu. 4 Jina la Mungu linatokana na kitenzi cha Kiebrania kinachomaanisha “kuwa.” Hivyo, jina la Yehova linaweza kumaanisha yeye ni Mtimizaji wa ahadi zake. Ona sanduku lenye kichwa “Maana ya Jina la Mungu,” kwenye ukurasa wa 43.

^ fu. 6 Ingawa leo kipindi hicho cha wakati huenda kikaonekana kuwa kirefu, tunapaswa kukumbuka kwamba wanadamu walikuwa wakiishi miaka mingi sana wakati huo; kulikuwa na watu wanne kutoka Adamu hadi Abrahamu ambao maisha yao yalipishana. Maisha ya Adamu yalipishana na maisha ya Lameki, baba ya Noa. Maisha ya Lameki yalipishana na maisha ya Shemu, mwana wa Noa. Maisha ya Shemu yalipishana na maisha ya Abrahamu.—Mwa. 5:5, 31; 9:29; 11:10, 11; 25:7.

^ fu. 13 Jina “Shetani” linapatikana mara 18 katika Maandiko ya Kiebrania. Hata hivyo, jina “Shetani” linapatikana zaidi ya mara 30 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa kufaa, Maandiko ya Kiebrania hayakumzungumzia sana Shetani badala yake yalikazia zaidi kumtambulisha Masihi. Masihi alipowasili, alimfunua Shetani waziwazi, na jambo hilo limeandikwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

^ fu. 22 Ili kupata maelezo zaidi kuhusu baadhi ya marekebisho hayo ya uelewaji, ona makala zifuatazo katika gazeti Mnara wa Mlinzi: Oktoba 15, 1995, ukurasa wa 23-28; Januari 15, 2008, ukurasa wa 20-24; Julai 15, 2008, ukurasa wa 17-21; Julai 15, 2013, ukurasa wa 9-14.