Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 4

Yehova Analikweza Jina Lake

Yehova Analikweza Jina Lake

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Watu wa Mungu wanalipa jina la Mungu heshima inayostahili

1, 2. Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inalikweza jina la Mungu katika njia gani?

JUMANNE asubuhi, Desemba 2, 1947, kikundi kidogo cha akina ndugu watiwa-mafuta katika Betheli ya Brooklyn, New York, kilianza kazi kubwa. Ilikuwa kazi ngumu, lakini kwa miaka 12 waliifanya bila kuchoka. Hatimaye, Jumapili, Machi 13, 1960, walimaliza kutafsiri maandishi ya mwisho ya tafsiri mpya ya Biblia. Miezi mitatu baadaye, Juni 18, 1960, Ndugu Nathan Knorr alitangaza kutolewa kwa buku la mwisho la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa watu waliohudhuria kusanyiko huko Manchester, Uingereza. Msemaji alieleza hisia za wote waliohudhuria aliposema hivi: ‘Leo ni siku ya shangwe kwa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote!’ Jambo la pekee na lenye kufurahisha kuhusu tafsiri hiyo mpya ni kwamba imetumia jina la Mungu mara nyingi.

Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa mwaka wa 1950 katika Kusanyiko la Ongezeko la Kitheokrasi (Kushoto: Yankee Stadium, Jiji la New York; kulia: Ghana)

2 Tafsiri nyingi za Biblia hazitumii jina la Mungu. Hata hivyo, watumishi watiwa-mafuta wa Yehova walipinga mbinu za Shetani za kufuta jina la Mungu kutoka katika kumbukumbu la wanadamu. Utangulizi wa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyotolewa siku hiyo ulisema hivi: “Jambo kuu katika tafsiri hii ni kwamba imelirudisha jina la Mungu mahali pake panapofaa.” Kwa kweli, Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia jina la Mungu, Yehova, zaidi ya mara 7,000. Tafsiri hiyo imelikweza jina la Baba yetu wa mbinguni, Yehova, kwa njia ya pekee sana!

3. (a) Ndugu zetu walitambua nini kuhusu maana ya jina la Mungu? (b) Tunapaswa kuelewaje andiko la Kutoka 3:13, 14? (Ona sanduku “ Maana ya Jina la Mungu.”)

3 Miaka ya mapema, Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba jina la Mungu linamaanisha “Mimi niko ambaye niko.” (Kut. 3:14, Union Version) Kwa hiyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1926, lilisema hivi: “Jina Yehova linamaanisha . . . Yeye ambaye hana mwanzo wala mwisho.” Hata hivyo, kabla ya watafsiri wa Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kuanza kazi yao, Yehova alikuwa amewasaidia watu wake watambue kwamba jina lake halimaanishi tu hana mwanzo wala mwisho, bali jambo muhimu zaidi ni kwamba yeye ni Mungu mwenye kusudi na anayetenda ili kutimiza kusudi hilo. Walijifunza kwamba jina Yehova kihalisi humaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Ndiyo, alisababisha ulimwengu na pia viumbe wenye akili wawepo, na anaendelea kusababisha mapenzi na kusudi lake litimie. Kwa nini basi ni muhimu jina la Mungu likwezwe, nasi tunaweza kushiriki jinsi gani katika kulikweza?

Kutakaswa kwa Jina la Mungu

4, 5. (a) Tunaomba nini tunaposali: “Jina lako na litakaswe”? (b) Mungu atalitakasa jina lake lini na jinsi gani?

4 Yehova anataka jina lake likwezwe. Kwa kweli, kusudi lake kuu ni kulitakasa jina lake, kama inavyoonekana wazi katika ombi la Yesu la kwanza katika sala yake ya kielelezo: “Jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Tunaomba nini tunaposali, “Jina lako na litakaswe”?

5 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 1 ya kitabu hiki, ombi hili “Jina lako na litakaswe” ni kati ya maombi matatu yaliyotajwa kwenye sala ya kielelezo ya Yesu ambayo yanahusiana na kusudi la Yehova. Yale mengine mawili ni: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke.” (Mt. 6:10) Hivyo, kama vile tunavyomwomba Yehova achukue hatua ili kusababisha Ufalme wake uje na mapenzi yake yatendeke, ndivyo pia tunamwomba Yehova achukue hatua ya kulitakasa jina lake. Kwa maneno mengine, tunamwomba Yehova achukue hatua ya kuliondolea jina lake suto ambayo limeletewa tangu uasi katika Edeni. Yehova atajibu jinsi gani sala hiyo? Anasema hivi: “Nami hakika nitalitakasa jina langu kuu, ambalo lilikuwa likitiwa unajisi katikati ya mataifa.” (Eze. 36:23; 38:23) Wakati wa Har–Magedoni, Yehova atakapoondoa uovu wote, atalitakasa jina lake mbele ya uumbaji wote.

6. Tunaweza kushiriki jinsi gani kulitakasa jina la Mungu?

6 Katika historia yote, Yehova amewaruhusu watumishi wake washiriki kulitakasa jina lake. Ni kweli kwamba hatuwezi kulifanya jina la Mungu liwe takatifu kuliko lilivyo. Tayari jina hilo ni takatifu kabisa. Kwa hiyo, tunawezaje kulitakasa? Isaya anasema hivi: “Yehova wa majeshi—yeye Ndiye mnayepaswa kuona kuwa mtakatifu.” Na Yehova alisema hivi kuhusu watu wake: “Watalitakasa jina langu . . . , nao watamheshimu Mungu wa Israeli.” (Isa. 8:13; 29:23) Hivyo, tunalitakasa jina la Mungu kwa kuliona kuwa tofauti na majina mengine na kulikweza juu ya majina yote, na kwa kuwasaidia wengine walione kuwa takatifu. Tunaonyesha kwamba tunaliogopa na kuliheshimu jina la Mungu kwa kumtambua Yehova kuwa Mtawala wetu na kumtii kutoka moyoni.—Met. 3:1; Ufu. 4:11.

Wanatayarishwa Kulibeba na Kulikweza Jina la Mungu

7, 8. (a) Kwa nini ilichukua muda mrefu kwa watu wa Mungu kulibeba jina lake? (b) Tutachunguza nini sasa?

7 Watumishi wa Mungu katika nyakati za kisasa wametumia jina la Mungu katika machapisho yao tangu miaka ya 1870. Kwa mfano, gazeti Zion’s Watch Tower la Agosti 1879 na kitabu cha nyimbo Songs of the Bride kilichochapishwa mwaka huohuo, kilitaja jina Yehova. Hata hivyo, inaonekana kwamba kabla Yehova hajaruhusu watu wake waitwe kwa jina lake takatifu hadharani, alihakikisha kwamba walitimiza matakwa ya pendeleo hilo kubwa. Yehova aliwatayarishaje Wanafunzi hao wa Biblia kwa ajili ya kulibeba jina lake?

8 Tunapotazama nyuma mwishoni mwa miaka ya 1800 na mwanzoni mwa miaka ya 1900, tunaona jinsi ambavyo Yehova aliwasaidia watu wake kuelewa vizuri kweli muhimu zinazohusiana na jina lake. Acheni tuchunguze kweli tatu kati ya hizo.

9, 10. (a) Kwa nini makala za mapema za Mnara wa Mlinzi zilimkazia fikira zaidi Yesu? (b) Ni badiliko gani lililofanywa kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, na kulikuwa na matokeo gani? (Ona pia sanduku “ Jinsi Ambavyo Gazeti Mnara wa Mlinzi Limelikweza Jina la Mungu.”)

9 Kwanza, watumishi wa Yehova walikuja kuwa na maoni yanayofaa kuhusu umuhimu wa jina la Mungu. Wanafunzi waaminifu wa Biblia walioishi katika miaka ya mapema waliona mpango wa fidia kuwa fundisho kuu la Biblia. Hiyo ndiyo sababu gazeti Mnara wa Mlinzi lilimkazia fikira zaidi Yesu. Kwa mfano, katika mwaka wa kwanza wa kuchapishwa kwa gazeti hilo, lilitaja jina Yesu mara kumi zaidi ya jina Yehova. Likizungumzia miaka ya mapema ya Wanafunzi wa Biblia, gazeti Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1976, lilisema kwamba ‘walimkazia fikira Yesu kupita kiasi.’ Lakini kadiri wakati ulivyopita, Yehova aliwasaidia kutambua heshima ambayo Biblia inalipa jina la Mungu. Jambo hilo liliwaathirije Wanafunzi wa Biblia? Hasa kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, makala hiyohiyo ya Mnara wa Mlinzi ilisema kwamba “walianza kumheshimu zaidi Yehova, Baba wa kimbingu wa Masihi.” Kwa kweli, katika miaka kumi iliyofuata baada ya mwaka wa 1919, gazeti Mnara wa Mlinzi lilitaja jina la Mungu zaidi ya mara 6,500!

10 Kwa kulikazia fikira kwa njia inayofaa jina Yehova, akina ndugu walionyesha kwamba wanalipenda jina la Mungu. Kama Musa, waliazimia ‘kulitangaza jina la Yehova.’ (Kum. 32:3; Zab. 34:3) Hivyo, kama alivyoahidi katika Maandiko, Yehova aliona jinsi walivyolipenda jina lake, naye akawaonyesha kibali.—Zab. 119:132; Ebr. 6:10.

11, 12. (a) Machapisho yetu yalibadilika jinsi gani muda mfupi baada ya mwaka wa 1919? (b) Yehova alikuwa akivuta uangalifu wa watumishi wake kwenye kazi gani, na kwa nini?

11 Pili, Wakristo wa kweli walielewa vizuri kazi ambayo Mungu aliwapa. Muda mfupi baada ya mwaka wa 1919, ndugu watiwa-mafuta waliowaongoza watu wa Mungu walichochewa na roho takatifu kuchunguza unabii wa Isaya. Baadaye, habari zilizokuwa katika machapisho yetu zilianza kukazia jambo tofauti. Kwa nini badiliko hilo lilikuwa ‘chakula kwa wakati unaofaa’?—Mt. 24:45.

12 Kabla ya mwaka wa 1919, gazeti Mnara wa Mlinzi halikuwahi kuzungumzia kwa kina maneno haya ya Isaya: “‘Ninyi ni mashahidi wangu,’ asema Yehova, ‘mtumishi wangu ambaye nimemchagua.’” (Soma Isaya 43:10-12.) Hata hivyo, muda mfupi baada ya mwaka wa 1919, machapisho yetu yalianza kukazia fikira andiko hilo, yakiwatia moyo watiwa-mafuta wote washiriki katika kazi ambayo Yehova alikuwa amewapa, yaani, kutoa ushahidi kumhusu. Kwa kweli, kuanzia mwaka wa 1925 hadi mwaka wa 1931, sura ya 43 ya kitabu cha Isaya ilizungumziwa katika matoleo 57 ya Mnara wa Mlinzi, na katika kila toleo maneno ya Isaya yalihusianishwa na Wakristo wa kweli. Ni wazi kwamba katika miaka hiyo, Yehova alikuwa akivuta uangalifu wa watumishi wake kwenye kazi ambayo walipaswa kufanya. Kwa nini alifanya hivyo? Kwa njia fulani, alitaka “wajaribiwe juu ya kufaa kwanza.” (1 Tim. 3:10) Kabla ya kustahili kulibeba jina la Mungu, Wanafunzi wa Biblia walihitaji kumthibitishia Yehova kwa matendo yao kwamba kwa kweli walikuwa mashahidi wake.—Luka 24:47, 48.

13. Neno la Mungu linafunuaje suala muhimu zaidi linalopaswa kutatuliwa?

13 Tatu, watu wa Yehova walikuja kuelewa umuhimu wa kutakaswa kwa jina la Mungu. Katika miaka ya 1920, watu wa Yehova walitambua kwamba kutakaswa kwa jina la Mungu ndilo suala muhimu zaidi ambalo linapaswa kutatuliwa. Neno la Mungu linafunuaje kweli hiyo muhimu? Fikiria mifano miwili. Ni sababu gani kuu iliyomfanya Mungu awakomboe Waisraeli kutoka Misri? Yehova alisema hivi: “Ili nifanye jina langu litangazwe katika dunia yote.” (Kut. 9:16) Na kwa nini Yehova alilionyesha rehema taifa la Israeli lilipomwasi? Yehova alisema hivi tena: “Nami nikachukua hatua kwa ajili ya jina langu mwenyewe ili lisitiwe unajisi mbele ya macho ya mataifa.” (Eze. 20:8-10) Wanafunzi wa Biblia walijifunza nini kutokana na masimulizi hayo na mengine yaliyo katika Biblia?

14. (a) Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1920, watu wa Mungu walitambua nini? (b) Uelewaji wa kina ambao Wanafunzi wa Biblia walipata ulikuwa na matokeo gani katika kazi ya kuhubiri? (Ona pia sanduku “ Sababu Kuu ya Kuhubiri.”)

14 Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1920, watu wa Mungu walitambua maana ya maneno ambayo Isaya alikuwa amesema miaka 2,700 hivi mapema. Alisema hivi kumhusu Yehova: “Hivyo uliwaongoza watu wako ili ujifanyie mwenyewe jina zuri.” (Isa. 63:14) Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba suala muhimu zaidi lilikuwa kutakaswa kwa jina la Mungu na si wokovu wa mtu binafsi. (Isa. 37:20; Eze. 38:23) Mwaka wa 1929, kitabu Prophecy kilifafanua kweli hiyo kwa kusema: “Jina la Yehova ndilo suala muhimu zaidi mbele ya viumbe wote.” Uelewaji huo uliorekebishwa uliwachochea watumishi wa Mungu kutoa ushahidi kumhusu Yehova na kuliondolea jina hilo lawama.

15. (a) Kufikia miaka ya 1930, ndugu zetu walikuwa na maoni gani? (b) Wakati ulikuwa umefika wa kufanya nini?

15 Kufikia mwanzoni mwa miaka ya 1930, ndugu zetu walikuwa na maoni yanayofaa kuhusu umuhimu wa jina la Mungu, walielewa vizuri kazi ambayo Mungu alikuwa amewapa, na walielewa kwa kina suala muhimu linalopaswa kutatuliwa. Sasa wakati ulikuwa umefika wa Yehova kuwapa watumishi wake pendeleo la kulibeba jina lake hadharani. Ili kuelewa jinsi ambavyo jambo hilo lilifanyika, acheni tuchunguze matukio fulani yaliyopita.

Yehova Anawachukua “Watu kwa Ajili ya Jina Lake”

16. (a) Yehova hulikweza jina lake kwa njia gani kuu? (b) Nyakati za kale, ni nani kwanza waliotumikia wakiwa watu kwa ajili ya jina la Mungu?

16 Njia kuu ambayo Yehova analikweza jina lake ni kwa kuwa na watu wanaolibeba jina lake hapa duniani. Kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. na kuendelea, Waisraeli wakiwa taifa walimwakilisha Yehova wakiwa watu wake. (Isa. 43:12) Hata hivyo, walishindwa kutimiza sehemu yao katika agano lao pamoja na Mungu, hivyo katika mwaka wa 33 W.K., walipoteza uhusiano wao wa pekee pamoja na Yehova. Muda mfupi baadaye, Yehova ‘alielekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.’ (Mdo. 15:14) Watu hao waliotoka tu kuchaguliwa walikuja kujulikana kama “Israeli wa Mungu,” na walitia ndani wafuasi wa Kristo watiwa-mafuta kutoka katika mataifa mbalimbali.—Gal. 6:16.

17. Shetani alifaulu kutumia njama gani?

17 Karibu mwaka wa 44 W.K., wanafunzi wa Kristo “kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.” (Mdo. 11:26) Mwanzoni, jina hilo lilikuwa la pekee kwa sababu lilirejelea Wakristo wa kweli tu. (1 Pet. 4:16) Hata hivyo, kama mfano wa Yesu wa ngano na magugu unavyoonyesha, Shetani alifaulu katika njama yake ya kuwafanya Wakristo wote wa uwongo waitwe kwa jina hilo la pekee. Kwa sababu hiyo, kwa karne nyingi Wakristo wa kweli hawangeweza kutofautishwa na Wakristo wa uwongo. Lakini jambo hilo lilianza kubadilika wakati wa “majira ya mavuno,” ambayo yalianza mwaka wa 1914. Kwa nini? Kwa sababu malaika walianza kutenganisha Wakristo wa uwongo na Wakristo wa kweli.—Mt. 13:30, 39-41.

18. Ni nini kilichowasaidia ndugu zetu kuona uhitaji wa kuwa na jina jipya?

18 Baada ya mtumwa mwaminifu kuwekwa rasmi mwaka wa 1919, Yehova aliwasaidia watu wake kutambua kazi ambayo alikuwa amewapa. Mara moja, waliona kwamba kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba iliwatofautisha na Wakristo wote wa uwongo. Baada ya kutambua jambo hilo, haikuchukua muda mrefu wakagundua kwamba jina “Wanafunzi wa Biblia” halikuwatofautisha kwa njia inayofaa. Kusudi lao kuu maishani halikuwa kujifunza Biblia tu bali kutoa ushahidi kumhusu Mungu na kuheshimu na kulikweza jina lake. Kwa hiyo, ni jina gani ambalo lingefaana na kazi ambayo walikuwa wakifanya? Swali hilo lilijibiwa mwaka wa 1931.

Programu ya kusanyiko, 1931

19, 20. (a) Ni azimio gani lenye kusisimua lililotolewa kwenye kusanyiko mwaka wa 1931? (b) Ndugu zetu waliitikiaje walipoanza kuitwa kwa jina jipya?

19 Mnamo Julai 1931, Wanafunzi wa Biblia 15,000 hivi waliwasili Columbus, Ohio, Marekani, kwa ajili ya kusanyiko. Walipoona programu ya kusanyiko, wengi walishangazwa na herufi mbili kubwa J na W zilizokuwa zimeandikwa kwenye ukurasa wa mbele wa programu. Wahudhuriaji walijiuliza, ‘Herufi hizo zinamaanisha nini?’ Wengine walijaribu kukisia maana ya herufi hizo. Kisha, Jumapili Julai 26, Ndugu Joseph Rutherford alitoa azimio hili lenye maneno yenye nguvu: “Twataka tujulikane na kuitwa kwa jina hili, yaani, Mashahidi wa Yehova.” Baada tu ya azimio hilo, wote waliohudhuria walielewa maana ya zile herufi zilizokuwa zikiwatatanisha. Zilimaanisha Jehovah’s Witnesses (Mashahidi wa Yehova), jina la Kimaandiko linalotegemea andiko la Isaya 43:10.

20 Wahudhuriaji waliitikia azimio hilo kwa shangwe na makofi mengi. Kupitia redio, makofi hayo yalisikika katika sehemu nyingi za dunia! Ernest na Naomi Barber nchini Australia walikumbuka hivi: “Makofi yalipoanza kupigwa huko Marekani, akina ndugu katika jiji la Melbourne walisimama kwa shangwe na kuanza kupiga makofi pia. Hatutasahau kamwe siku hiyo!” *

Jina la Mungu Linakwezwa Ulimwenguni Pote

21. Jina jipya lilichocheaje kazi ya kuhubiri?

21 Kuitwa kwa jina la Kimaandiko, Mashahidi wa Yehova, kuliwachochea watumishi wa Mungu wawe na bidii ya kuhubiri. Edward na Jessie Grimes, wenzi wa ndoa mapainia huko Marekani, ambao walihudhuria kusanyiko la mwaka wa 1931 huko Columbus, walisema hivi: “Tulitoka nyumbani tukiwa Wanafunzi wa Biblia, lakini tulirudi tukiwa Mashahidi wa Yehova. Tulifurahi kwa sababu sasa tulikuwa na jina ambalo lilitusaidia kutukuza jina la Mungu wetu.” Baada ya kusanyiko hilo, Mashahidi fulani walitumia mbinu mpya ili kutimiza jambo hilo. Ili kujitambulisha kwa wenye nyumba, waliwapa kadi iliyokuwa na ujumbe huu: “Mimi ni shahidi wa YEHOVA, ninahubiri kuhusu Ufalme wa YEHOVA Mungu wetu.” Naam, watu wa Mungu walijivunia kulibeba jina Yehova, nao walikuwa tayari kutangaza maana ya jina hilo kwa mapana na marefu.—Isa. 12:4.

“Tulitoka nyumbani tukiwa Wanafunzi wa Biblia, lakini tulirudi tukiwa Mashahidi wa Yehova”

22. Ni nini kinachothibitisha kwamba watu wa Yehova wana utambulisho wa pekee?

22 Miaka mingi imepita tangu Yehova alipowaongoza ndugu zetu watiwa-mafuta kukubali jina hilo la pekee. Tangu wakati huo, je, Shetani amefaulu kufunika utambulisho wa watu wa Mungu? Je, amefaulu kufanya iwe vigumu kwa watu kutambua tofauti kati yetu na dini nyingine? La hasha! Badala yake, utambulisho wetu wa pekee tukiwa mashahidi wa Mungu unaonekana wazi kuliko wakati mwingine wowote. (Soma Mika 4:5; Malaki 3:18.) Kwa kweli, tumehusianishwa sana na jina la Mungu hivi kwamba mtu yeyote anapotumia sana jina hilo, anatambuliwa kuwa Shahidi wa Yehova. Badala ya kufunikwa na dini za uwongo zilizo kama milima, ibada ya kweli ya Yehova ‘imewekwa imara juu ya kilele cha milima.’ (Isa. 2:2) Leo, ibada ya Yehova pamoja na jina lake takatifu, limekwezwa kwelikweli.

23. Kulingana na Zaburi 121:5, ni kweli gani muhimu kumhusu Yehova ambayo inatuimarisha sana?

23 Tunaimarishwa sana kujua kwamba Yehova atatulinda dhidi ya mashambulizi ya Shetani ya sasa na ya wakati ujao! (Zab. 121:5) Tuna sababu nzuri kuhisi kama mtunga-zaburi alivyohisi alipoandika: “Lenye furaha ni taifa ambalo Mungu wake ni Yehova, watu ambao amewachagua wawe urithi wake.”—Zab. 33:12.

^ fu. 20 Ona Sura ya 7, ukurasa wa 72-74, kwa habari zaidi kuhusu matumizi ya redio.