Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 5

Mfalme Anaufunua Ufalme

Mfalme Anaufunua Ufalme

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Watu wa Mungu wanaelewa kweli muhimu kuhusu Ufalme, watawala wake, raia wake, na pia uhitaji wa kuwa washikamanifu

1, 2. Ni katika njia gani Yesu alikuwa kiongozi mwenye hekima?

HEBU wazia kwamba mtu fulani mwenye uzoefu anakuongoza unapotalii jiji zuri na linalopendeza sana. Jiji hilo ni geni kwako na kwa watalii wenzako, hivyo mnasikiliza kwa makini sana kila neno la kiongozi huyo. Nyakati fulani, wewe na watalii wenzako mnakuwa na msisimko wa kutaka kujua kuhusu vitu fulani katika jiji hilo ambavyo bado hamjaviona. Hata hivyo, unapomuuliza yule anayewaongoza kuhusu vitu hivyo, hasemi jambo lolote, anasubiri hadi wakati unaofaa ufike, mara nyingi mnapokaribia tu kuona kitu fulani ndipo anasema. Baada ya muda, unavutiwa sana na hekima yake, kwa kuwa anawaambia jambo mnalohitaji kujua wakati unaofaa wa kujua jambo hilo.

2 Hali ya Wakristo wa kweli inafanana na ya watalii hao. Tunajifunza kwa hamu kuhusu jiji lenye kupendeza zaidi kuliko majiji yote, “jiji lililo na misingi ya kweli,” yaani, Ufalme wa Mungu. (Ebr. 11:10) Yesu alipokuwa duniani, yeye binafsi aliwaongoza wafuasi wake kwenye ujuzi wa kina kuhusu Ufalme huo. Je, alijibu maswali yao yote na kuwaambia kila kitu kuhusu Ufalme huo kwa wakati mmoja? Hapana. Alisema hivi: “Bado nina mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili kwa sasa.” (Yoh. 16:12) Akiwa kiongozi mwenye hekima zaidi, Yesu hakuwalemea kamwe wanafunzi wake kwa kuwapa ujuzi ambao hawangeuelewa wakati huo.

3, 4. (a) Yesu ameendeleaje kuwafundisha watu waaminifu kuhusu Ufalme wa Mungu? (b) Tutachunguza nini katika sura hii?

3 Yesu alisema maneno yaliyoandikwa kwenye Yohana 16:12 katika usiku wake wa mwisho duniani. Baada ya kifo chake, angeendeleaje kuwafundisha watu waaminifu kuhusu Ufalme wa Mungu? Aliwahakikishia hivi mitume wake: “Roho ya ile kweli . . . atawaongoza ninyi ndani ya kweli yote.” * (Yoh. 16:13) Tunaweza kuifananisha roho takatifu na kiongozi mwenye subira. Roho hiyo ndiyo njia ambayo Yesu anaitumia kuwafundisha wafuasi wake jambo lolote wanalohitaji kujua kuhusu Ufalme wa Mungu—kwa wakati unaofaa wanapohitaji kujua jambo hilo.

4 Acheni sasa tuchunguze jinsi ambavyo roho takatifu ya Yehova imekuwa ikiwaongoza Wakristo wanyofu kwenye ujuzi mwingi zaidi kuhusu Ufalme huo. Kwanza, tutachunguza jinsi tulivyopata jibu la swali hili: Ufalme wa Mungu ulianza kutawala lini? Kisha, tutachunguza utambulisho na tumaini la watawala wa Ufalme huo na raia wake. Mwishowe, tutaona jinsi ambavyo wafuasi wa Kristo walielewa vizuri zaidi kuhusu uhitaji wa kuwa washikamanifu kwa Ufalme.

Kuelewa Mwaka Muhimu

5, 6. (a) Wanafunzi wa Biblia walikuwa na maoni gani yasiyo sahihi kuhusu kusimamishwa kwa Ufalme na mavuno? (b) Kwa nini maoni hayo yasiyo sahihi hayapaswi kutufanya tutilie shaka kwamba Yesu alikuwa akiwaongoza wafuasi wake?

5 Kama tulivyoona katika Sura ya 2 ya kitabu hiki, kwa makumi ya miaka Wanafunzi wa Biblia walitaja waziwazi kwamba unabii muhimu wa Biblia ungetimia katika mwaka wa 1914. Hata hivyo, wakati huo waliamini kwamba kuwapo kwa Kristo kulianza mwaka wa 1874, na kwamba alianza kutawala mbinguni mwaka wa 1878, na kuwa Ufalme haungesimamishwa kikamili hadi Oktoba 1914. Mavuno yangeanza mwaka wa 1874 na kumalizika mwaka wa 1914 wakati ambapo watiwa-mafuta wangekusanywa na kwenda mbinguni. Je, maoni hayo yasiyo sahihi yanatufanya tutilie shaka kwamba Yesu alikuwa akiwaongoza watu hao waaminifu kupitia roho takatifu?

6 Bila shaka hapana! Hebu fikiria tena mfano tuliozungumzia mwanzoni mwa sura hii. Je, maswali na maoni ya watalii kuhusu vitu ambavyo hawajaviona bado yangetokeza shaka kwamba kiongozi wao hategemeki? Hapana! Vivyo hivyo, ingawa nyakati fulani watu wa Mungu wanajaribu kuelewa habari fulani kuhusu kusudi la Yehova kabla ya wakati wa roho takatifu kuwaongoza kuzielewa kweli hizo, ni wazi kwamba Yesu anawaongoza. Hivyo, watu waaminifu wako tayari kusahihishwa na kwa unyenyekevu wao hurekebisha maoni yao.—Yak. 4:6.

7. Watu wa Mungu waliangaziwa nuru gani za kiroho?

7 Miaka iliyofuata mwaka wa 1919, watu wa Mungu waliangaziwa nuru zaidi za kiroho. (Soma Zaburi 97:11.) Katika mwaka wa 1925, gazeti Mnara wa Mlinzi lilikuwa na makala ya kihistoria yenye kichwa “Kuzaliwa kwa Taifa.” Ilitoa uthibitisho wa Kimaandiko wenye kusadikisha kwamba Ufalme wa Kimasihi ulikuwa umezaliwa mwaka wa 1914, na hilo likatimiza mfano wa kiunabii wa mwanamke wa kimbingu wa Mungu akizaa mtoto, kama ilivyoandikwa kwenye Ufunuo sura ya 12. * Makala hiyo iliendelea kueleza kwamba mateso na taabu iliyowapata watu wa Yehova wakati wa miaka ya vita ilikuwa ishara inayoonyesha wazi kwamba Shetani alikuwa ametupwa chini kutoka mbinguni, “akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufu. 12:12.

8, 9. (a) Umuhimu wa Ufalme wa Mungu ulikaziwaje? (b) Tutachunguza maswali gani?

8 Ufalme ni muhimu kadiri gani? Katika mwaka wa 1928, gazeti Mnara wa Mlinzi lilianza kukazia kwamba Ufalme ulikuwa jambo muhimu sana kuliko wokovu wa mtu binafsi kwa msingi wa fidia. Bila shaka, Yehova atautumia Ufalme wa Kimasihi kulitakasa jina lake, kutetea enzi yake kuu, na kutimiza makusudi yake yote kuhusiana na wanadamu.

9 Ni nani wangetawala pamoja na Kristo katika Ufalme huo? Ni nani wangekuwa raia wa Ufalme huo hapa duniani? Na wafuasi wa Kristo wanapaswa kufanya kazi gani?

Kazi ya Kuvuna Yaelekezwa Zaidi kwa Watiwa-Mafuta

10. Kwa muda mrefu watu wa Mungu wameelewa nini kuhusu wale 144,000?

10 Miongo kadhaa kabla ya mwaka wa 1914, tayari Wakristo wa kweli walielewa kwamba wafuasi waaminifu wa Kristo 144,000 ndio ambao wangetawala pamoja naye mbinguni. * Wanafunzi hao wa Biblia waliona kwamba idadi hiyo ni halisi na hao 144,000 walianza kuchaguliwa katika karne ya kwanza W.K.

11. Wale watakaokuwa washiriki wa bibi-arusi wa Kristo walielewaje mgawo wao wakiwa duniani?

11 Hata hivyo, wale watakaokuwa washiriki wa bibi-arusi wa Kristo walipewa kazi gani ya kufanya wakiwa wangali duniani? Waliona kwamba Yesu alikuwa amekazia sana umuhimu wa kazi ya kuhubiri na aliihusianisha na kipindi cha mavuno. (Mt. 9:37; Yoh. 4:35) Kama tulivyoona katika Sura ya 2, kwa muda fulani waliamini kwamba kipindi cha mavuno kingedumu kwa miaka 40, na kufikia mwisho wake wakati watiwa-mafuta watakapokusanywa na kwenda mbinguni. Hata hivyo, kwa kuwa kazi iliendelea baada ya ile miaka 40 kwisha, ufafanuzi zaidi ulihitajika. Sasa tunajua kwamba majira ya mavuno—majira ya kutenganisha ngano na magugu, yaani, kutenganisha Wakristo waaminifu watiwa-mafuta na Wakristo wa uwongo—yalianza mwaka wa 1914. Wakati ulikuwa umefika wa kukazia fikira kazi ya kukusanya idadi iliyobaki ya jamii hiyo ya kimbingu!

Mwaka wa 1914 ulikuwa mwanzo wa majira ya mavuno (Ona fungu la 11)

12, 13. Mfano wa Yesu wa mabikira kumi na talanta umetimiaje katika siku za mwisho?

12 Kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, Kristo aliendelea kumwongoza mtumwa mwaminifu na mwenye busara akazie umuhimu wa kazi ya kuhubiri. Alikuwa amempa mgawo huo katika karne ya kwanza. (Mt. 28:19, 20) Pia, alitaja sifa ambazo wafuasi wake watiwa-mafuta wangehitaji kuwa nazo ili kutimiza utume huo wa kuhubiri. Jinsi gani? Katika mfano wake wa mabikira kumi, alionyesha kwamba watiwa-mafuta wangepaswa kukesha, kubaki macho kiroho, ikiwa walitaka kufikia lengo lao kuu la kushiriki katika sherehe kubwa ya harusi huko mbinguni, wakati Yesu atakapoungana na “bibi-arusi” wake, wale 144,000. (Ufu. 21:2) Kisha, katika mfano wake wa talanta, Yesu alifundisha kwamba watumishi wake watiwa-mafuta wangekuwa na bidii ya kufanya kazi ya kuhubiri ambayo alikuwa amewapa.—Mt. 25:1-30.

13 Katika karne moja iliyopita, watiwa-mafuta wamekuwa macho na wenye bidii. Bila shaka, watathawabishwa sana kwa sababu ya kukesha! Hata hivyo, je, kazi kubwa ya mavuno ingehusisha tu kukusanywa kwa watawala wenzi wa Kristo waliosalia duniani?

Ufalme Unawakusanya Raia Wake wa Duniani!

14, 15. Kitabu The Finished Mystery kilizungumzia vikundi gani vinne?

14 Kwa miaka mingi wanaume na wanawake waaminifu wamekuwa na hamu kubwa ya kujua kuhusu “umati mkubwa” (“mkutano mkubwa,” Union Version) unaotajwa katika Ufunuo 7:9-14. Haishangazi kwamba kabla ya kufika kwa wakati wa Kristo kufunua utambulisho wa kundi hilo kubwa, mambo mengi sana ambayo yalisemwa kuhusu kundi hilo yalikuwa tofauti sana na kweli zilizo wazi, na rahisi kueleweka tunazozijua na kuzipenda leo.

15 Katika mwaka wa 1917, kitabu The Finished Mystery kilieleza kwamba kuna “viwango au aina mbili za wokovu wa Kimbingu, na kuna viwango au aina mbili za wokovu wa kidunia.” Ni nani ambao walifanyiza vikundi hivyo vinne vya watu wenye matumaini hayo tofauti ya wokovu? Kwanza, kulikuwa na wale 144,000, ambao wangetawala na Kristo. Pili, kulikuwa na mkutano mkubwa. Siku hizo, ilieleweka kwamba hawa ni wale Wakristo ambao bado walikuwa wakishirikiana na makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo. Walikuwa na kiasi fulani cha imani lakini haikutosha kuwafanya wawe na msimamo imara wa kufuatia utimilifu. Kwa hiyo, wangepewa vyeo vya chini huko mbinguni. Kuhusu duniani, ilidhaniwa kwamba kile kikundi cha tatu kingefanyizwa na “wakuu wa kale,” yaani, watu waaminifu kama vile Abrahamu, Musa, na wengine, nao wangekuwa na mamlaka juu ya kile kikundi cha nne, yaani, wanadamu wote.

16. Ni nuru gani ya kiroho iliyoangazwa katika mwaka wa 1923 na 1932?

16 Roho takatifu iliwaongozaje wafuasi wa Kristo kwenye uelewaji ambao tunauthamini sana leo? Iliwaongoza hatua kwa hatua, kupitia mfuatano wa nuru ya kiroho iliyoangazwa. Mapema katika mwaka wa 1923, gazeti Mnara wa Mlinzi lilitaja kikundi ambacho hakikuwa na tamaa ya kwenda mbinguni ambacho kingeishi duniani chini ya utawala wa Kristo. Mnamo 1932, Mnara wa Mlinzi lilizungumza kuhusu Yonadabu (Yehonadabu), ambaye alishikamana na Yehu, mfalme wa Israeli aliyetiwa mafuta na Mungu ili kumuunga mkono katika vita dhidi ya ibada ya uwongo. (2 Fal. 10:15-17) Makala hiyo ilisema kwamba katika siku za kisasa kuna jamii ya watu ambao wanafananishwa na Yonadabu, na ikaongezea kusema kwamba Yehova angeiokoa jamii hiyo ya watu “kutoka katika taabu ya Har–Magedoni” ili waishi hapa duniani.

17. (a) Katika mwaka wa 1935, ni nuru gani ya kiroho iliangaza zaidi? (b) Uelewaji mpya kuhusu mkutano mkubwa ulikuwa na matokeo gani kwa Wakristo waaminifu? (Ona sanduku “ Sababu Kubwa ya Kuwa na Furaha.”)

17 Katika mwaka wa 1935 nuru ya kiroho iliangaza zaidi. Katika kusanyiko lililofanywa huko Washington, D.C., mkutano mkubwa ulitambulishwa kuwa jamii ya kidunia, hao ndio wale kondoo wanaotajwa katika mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi. (Mt. 25:33-40) Mkutano huo mkubwa ungekuwa sehemu ya “kondoo wengine,” ambao Yesu alisema hivi kuwahusu: “Hao pia nitawaleta.” (Yoh. 10:16) Wakati msemaji J.  F. Rutherford, aliposema: “Tafadhali, nyote mlio na tumaini la kuishi milele duniani simameni,” zaidi ya nusu ya wasikilizaji walisimama! Kisha akatangaza hivi, “Tazameni! Mkutano mkubwa!” Watu wengi walifurahi sana kuelewa tumaini lao la wakati ujao.

18. Wafuasi wa Kristo wamekaziaje fikira huduma, na wamepata matokeo gani?

18 Tangu wakati huo, Kristo amewaongoza watu wake ili wakazie fikira kazi ya kukusanya wale watakaokuwa washiriki wa umati huo mkubwa ambao utatoka katika dhiki kuu wakiwa hai na salama. Mwanzoni, kazi ya kukusanya haikuonekana kuwa kubwa. Ndugu Rutherford alieleza hivi wakati fulani: “Inaonekana kwamba ‘mkutano mkubwa’ hautakuwa mkubwa sana.” Bila shaka, sasa tunajua jinsi ambavyo Yehova amebariki kwa kiasi kikubwa kazi ya kuvuna tangu wakati huo! Chini ya mwongozo wa Yesu na roho takatifu, watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wamekuwa kama vile tu Yesu alivyotabiri—“kundi moja” wakitumikia chini ya “mchungaji mmoja.”

Ndugu Rutherford hakujua kwamba washiriki wa umati mkubwa wangekuja kuwa wengi sana (Kushoto kwenda kulia: Nathan H. Knorr, Joseph F. Rutherford, na Hayden C. Covington)

19. Tunaweza kushiriki jinsi gani katika kuongeza idadi ya umati mkubwa?

19 Idadi kubwa ya watu waaminifu wataishi milele katika dunia itakayokuwa paradiso, wakiwa chini ya utawala wa Kristo na watawala wenzake 144,000. Je, haichangamshi moyo kuchunguza jinsi ambavyo Kristo amewaongoza watu wa Mungu kuelewa waziwazi tumaini hilo la Kimaandiko la wakati ujao? Tuna pendeleo la pekee sana kuwajulisha watu tunaokutana nao katika huduma kuhusu tumaini hilo! Acheni tujitahidi kuhubiri kadiri tuwezavyo ili idadi ya umati mkubwa iendelee kuongezeka, wakipaaza sauti kubwa hata zaidi kulisifu jina la Yehova!—Soma Luka 10:2.

Idadi ya umati mkubwa inaendelea kuongezeka

Uhitaji wa Kuwa Washikamanifu kwa Ufalme

20. Tengenezo la Shetani limefanyizwa na mifumo gani, na ushikamanifu wa Kikristo unahusika jinsi gani?

20 Kadiri watu wa Mungu walivyoendelea kujifunza kuhusu Ufalme, ndivyo pia walivyohitaji kuelewa kikamili maana ya kuwa washikamanifu kwa serikali hiyo ya mbinguni. Kwa sababu hiyo, katika mwaka wa 1922, gazeti Mnara wa Mlinzi lilieleza kwamba kuna matengenezo mawili, tengenezo la Yehova na tengenezo la Shetani. Tengenezo la Shetani limefanyizwa na mfumo wa kibiashara, kidini, na kisiasa. Wale ambao ni washikamanifu kwa Ufalme wa Mungu ulio chini ya Kristo hawapaswi kulegeza ushikamanifu wao kwa kujihusisha isivyofaa na sehemu yoyote ya tengenezo la Shetani. (2 Kor. 6: 17) Hilo linamaanisha nini?

21. (a) Ni katika njia gani mtumwa mwaminifu amewaonya watu wa Mungu kuhusu biashara kubwa? (b) Katika mwaka wa 1963, gazeti Mnara wa Mlinzi lilifunua nini kuhusu “Babiloni Mkubwa”?

21 Chakula cha kiroho kinachotolewa na mtumwa mwaminifu kimekuwa kikifunua kwa ukawaida ufisadi wa biashara kubwa na kuwaonya watu wa Mungu wasishawishiwe na ufuatiliaji wa vitu vya kimwili ambao umeenea sana. (Mt. 6: 24) Vivyo hivyo, machapisho yetu yameendelea kufunua waziwazi sehemu ya kidini ya tengenezo la Shetani. Katika mwaka wa 1963, gazeti Mnara wa Mlinzi lilionyesha wazi kwamba “Babiloni Mkubwa” hawakilishi tu dini zinazodai kuwa za Kikristo bali pia milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. Hivyo, kama vile tutakavyochunguza kwa kina katika Sura ya 10 ya kitabu hiki, watu wa Mungu katika kila nchi na utamaduni wamesaidiwa ‘kutoka kwake,’ wakijisafisha na kuyaacha mazoea yote ya dini ya uwongo.—Ufu. 18:2, 4.

22. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, wengi wa watu wa Mungu walielewaje himizo lililo kwenye Waroma 13:1?

22 Hata hivyo, vipi kuhusu sehemu ya kisiasa ya tengenezo la Shetani? Je, Wakristo wa kweli wangeshiriki katika vita na mizozo ya mataifa? Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba wafuasi wa Kristo hawakupaswa kuua wanadamu wenzao. (Mt. 26:52) Hata hivyo, wengi wao walielewa kwamba himizo lililo kwenye Waroma 13:1 kuhusu kuzitii “mamlaka zilizo kubwa” lilimaanisha kwamba walipaswa kujiunga na jeshi, kuvaa sare za jeshi, na hata kubeba silaha; lakini, wakiamriwa kumuua adui, walipaswa kupiga risasi hewani.

23, 24. Tulielewa jinsi gani andiko la Waroma 13:1 wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, na wafuasi wa Kristo waliongozwa kwenye uelewaji gani sahihi zaidi?

23 Wakati tu Vita vya Pili ya Ulimwengu vilipokuwa vikianza katika mwaka wa 1939, gazeti Mnara wa Mlinzi lilikuwa na makala iliyozungumzia kwa kina suala la kutounga mkono upande wowote. Makala hiyo ilionyesha waziwazi kwamba Wakristo hawakupaswa kushiriki kwa njia yoyote ile katika vita na mizozo ya mataifa ya ulimwengu wa Shetani. Mwongozo huo ulikuja kwa wakati uliofaa kwelikweli! Wafuasi wa Kristo walilindwa dhidi ya hatia kubwa sana ya damu ambayo mataifa yalipata katika vita hivyo. Hata hivyo, kuanzia mwaka wa 1929, machapisho yetu yalikuwa pia yameeleza kwamba mamlaka zilizo kubwa zinazotajwa kwenye Waroma 13:1 hazikurejelea watawala wa ulimwengu, badala yake zilirejelea Yehova na Yesu. Uelewaji sahihi zaidi bado ulihitajika.

24 Katika mwaka wa 1962, roho takatifu iliwaongoza wafuasi wa Kristo kwenye uelewaji huo sahihi, wakati makala muhimu zilizozungumzia andiko la Waroma 13:1-7 zilipochapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15 na Desemba 1. Hatimaye, watu wa Mungu wakaelewa vizuri kanuni ya ujitiisho wa kadiri ambao Yesu alikuwa amefunua katika maneno yake yanayojulikana sana: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Luka 20:25) Sasa Wakristo wa kweli wanaelewa kuwa mamlaka zilizo kubwa ni serikali za ulimwengu huu na kwamba Wakristo wanapaswa kujitiisha chini yake. Hata hivyo, ujitiisho huo ni wa kadiri. Serikali za ulimwengu zinapotuamuru tusimtii Yehova Mungu, tunajibu kama mitume: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Mdo. 5:29) Katika Sura ya 13 na ya 14 ya kitabu hiki, tutajifunza mengi zaidi kuhusu jinsi ambavyo watu wa Mungu wamefuata kanuni ya Kikristo ya kutounga mkono upande wowote.

Ni pendeleo kubwa sana kuwaambia wengine kuhusu tumaini la uzima wa milele linalotajwa katika Biblia!

25. Kwa nini unathamini jinsi ambavyo roho takatifu imewaongoza watu wa Mungu kupata uelewaji kuhusu Ufalme wa Mungu?

25 Hebu fikiria mambo yote ambayo wafuasi wa Kristo wamefundishwa kuhusu Ufalme katika karne moja iliyopita. Tumejifunza Ufalme wa Mungu ulisimamishwa wakati gani huko mbinguni na umuhimu wake. Tunaelewa vizuri matumaini mawili ambayo watu waaminifu wamepewa, tumaini la kwenda mbinguni na tumaini la kuishi duniani. Pia, tunajua jinsi tunavyoweza kuonyesha ushikamanifu kwa Ufalme wa Mungu na wakati uleule kujitiisha kwa kadiri chini ya serikali za ulimwengu. Hebu jiulize, ‘Je, ningejua kweli hizo muhimu ikiwa Yesu Kristo hangemwongoza mtumwa wake mwaminifu azielewe na kisha kuzifundisha?’ Kwa kweli, ni pendeleo kubwa sana kuongozwa na Kristo na roho takatifu!

^ fu. 3 Kulingana na kitabu kimoja, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ongoza” katika mstari huo linamaanisha “kuonyesha njia.”

^ fu. 7 Kabla ya wakati huo, ilieleweka kwamba maono hayo yalihusu vita kati ya dini ya kipagani ya Milki ya Roma dhidi ya Kanisa Katoliki.

^ fu. 10 Mnamo Juni 1880, gazeti Zion’s Watch Tower lilidokeza kwamba wale 144,000 wangekuwa Wayahudi wa asili waliogeuka na kuwa Wakristo kufikia mwaka wa 1914. Hata hivyo, mwishoni mwa mwaka wa 1880, uelewaji mwingine ulichapishwa ambao unakaribiana sana na ule ambao tumekuwa nao sikuzote tangu wakati huo.