Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA 5

Mufalme Anafunua Kweli Mbalimbali Juu ya Ufalme

Mufalme Anafunua Kweli Mbalimbali Juu ya Ufalme

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Watu wa Mungu wanafikia kuelewa mafundisho ya kweli na ya maana juu ya Ufalme, juu ya wale ambao watatawala katika Ufalme, juu ya wale ambao watakuwa raia, na pia juu ya mambo ambayo mutu anapaswa kufanya ili kuonyesha kwamba anashikamana na Ufalme

1, 2. Sababu gani tunasema kwamba Yesu ni kiongozi mwenye hekima?

WAZIA munatembelea muji fulani mukubwa sana na wenye kuvutia. Munatembezwa na mutu mwenye kujua muji huo vizuri. Kwa sababu ni mara yenu ya kwanza kufika katika muji huo, munasikiliza kwa uangalifu kila neno ambalo mutu huyo anasema. Wakati fulani, munashangaa kwa furaha kuona mambo fulani ya muji huo ambayo ni mapya kwenu. Wakati munamuuliza mutu anayewatembeza juu ya mambo kama hayo, anawaomba muvumilie kidogo. Na wakati unaofaa anawatolea maelezo ambayo ni ya lazima kwenu. Anafanya hivyo wakati tu munaanza kuona vizuri mambo muliuliza. Bila shaka, mutapendezwa zaidi na zaidi na hekima yake kwa sababu anawaelezea mambo munapenda kujua kwa wakati unaofaa.

2 Sisi Wakristo wa kweli tuko kama watu hao ambao wanatembezwa katika muji. Tunafurahia sana kujifunza juu ya muji muzuri zaidi kuliko miji mingine yote. ‘Muji ulio na misingi ya kweli,’ ni kusema, Ufalme wa Mungu. (Ebr. 11:10) Wakati Yesu alikuwa hapa duniani, aliwasaidia wafuasi wake kujua mambo mengi juu ya Ufalme. Hata hivyo, je, Yesu aliwaambia mara moja kila jambo ambalo walipenda kujua juu ya Ufalme? Hapana. Yeye alisema hivi: ‘Ningali na mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamuwezi kuyastahimili [ao kuyavumilia] kwa sasa.’ (Yoh. 16:12) Kwa sababu Yesu ni kiongozi mwenye hekima kuliko viongozi wote, hakuwatolea wanafunzi wake ujuzi unaopita uwezo wao wakati huo.

3, 4. (a) Namna gani Yesu aliendelea kufundisha wafuasi wake waaminifu juu ya Ufalme wa Mungu? (b) Ni mambo gani tatu tutazungumuzia katika sura hii?

3 Maneno hayo ambayo tunasoma katika andiko la Yohana 16:12, ni maneno Yesu alisema katika usiku wa mwisho wa maisha yake hapa duniani. Kisha kufa kwake, namna gani angeendelea kufundisha wafuasi wake waaminifu juu ya Ufalme wa Mungu? Aliwaahidia mitume wake hivi: “Roho ya ile kweli, atawaongoza ninyi ndani ya kweli yote.” * (Yoh. 16:13) Kwa hiyo, tunaweza kulinganisha roho takatifu na kiongozi muvumilivu. Yesu anatumia roho takatifu ili kufundisha wafuasi wake kila jambo ambalo wanapenda kujua juu ya Ufalme wa Mungu. Anafanya hivyo kwa wakati unaofaa.

4 Tuzungumuzie sasa namna roho takatifu ya Yehova imekuwa ikiwaongoza Wakristo wenye mioyo mizuri katika ujuzi mwingi wa ile kweli juu ya Ufalme. Kwanza, tutachunguza namna gani tulifikia kuelewa ni wakati gani Ufalme ulianza kutawala. Pili, tutachunguza ni nani watatawala katika Ufalme na wana tumaini gani, na ni nani watakuwa raia (wale ambao watatawaliwa) na wana tumaini gani. Na tatu, tutaona namna gani wafuasi wa Kristo walifikia kuelewa vizuri mambo ambayo wanapaswa kufanya ili kuonyesha kwamba wanashikamana na Ufalme.

Mwaka wa Maana Sana

5, 6. (a) Ni mawazo gani yenye makosa ambayo Wanafunzi wa Biblia walikuwa nayo juu ya Ufalme kuanza kutawala na juu ya wakati wa kipindi cha mavuno? (b) Mawazo yenye makosa kama hayo, yanapaswa kutufanya tuwe na mashaka kwamba Yesu haongoze wafuasi wake? Fasiria jibu lako

5 Katika Sura ya 2, tuliona kwamba kwa miaka mingi Wanafunzi wa Biblia walifundisha kwamba mwaka wa 1914 utakuwa mwaka wa maana sana ili kutimiza unabii wa Biblia. Hata hivyo, wakati huo waliamini kwamba kuwapo kwa Kristo kulikuwa kumeanza katika mwaka wa 1874, na kwamba alianza kutawala mbinguni katika mwaka wa 1878. Tena waliamini kwamba Ufalme utaanza kabisakabisa kutawala katika Mwezi wa 10, 1914. Waliamini pia kwamba kipindi cha mavuno kilikuwa kimeanza mwaka wa 1874 na kingemalizika mwaka wa 1914, na waliamini kwamba mwisho wa kipindi hicho watiwa-mafuta wangechukuliwa na kuenda mbinguni. Je, mawazo yenye makosa kama hayo, yanapaswa kutufanya tuwe na mashaka kwamba Yesu hakuwa anaongoza watu hao waaminifu kupitia roho takatifu?

6 Hapana kabisa! Fikiria tena mufano wetu katika fungu la kwanza. Kwa sababu wale ambao wanatembezwa wanawazia na kuuliza mbele ya wakati mambo fulani, hiyo ndio sababu ya kuwa na mashaka na kufikiri kwamba kiongozi wao si mutu wa kutumainiwa? Ni vigumu kufikiri hivyo! Vilevile, hata ikiwa wakati fulani, watu wa Mungu wanajikaza kuelewa mambo fulani juu ya kusudi la Yehova mbele roho takatifu iwaongoze katika kweli yote, hilo halimaanishe kwamba Yesu hawaongoze. Watu hao waaminifu wako tayari kurekebishwa, na kubadilisha mawazo yao kwa unyenyekevu.​—Yak. 4:6.

7. Watu wa Mungu walibarikiwa kwa kupata miangaza gani ya kiroho?

7 Kisha mwaka wa 1919, watu wa Mungu walibarikiwa kwa kupata zaidi na zaidi nuru ya kiroho. (Soma Zaburi 97:11.) Katika mwaka wa 1925, habari fulani ya pekee ilitolewa katika gazeti Munara wa Mulinzi ambayo ilikuwa na kichwa “Kuzaliwa kwa Taifa.” Habari hiyo ilitoa ushuhuda wenye kusadikisha wa Maandiko kwamba Ufalme wa Masiya umezaliwa tangu mwaka wa 1914, ili kutimiza unabii ulioandikwa katika Ufunuo sura ya 12. Katika unabii huo, tengenezo la Mungu linafananishwa na mwanamuke anayezaa mutoto mwanaume. * Habari hiyo ilionyesha pia kwamba mateso na magumu ambayo yaliwapata watu wa Yehova katika miaka hiyo ya vita, ilikuwa ni alama ya kwamba Shetani alikuwa ametupwa duniani. Kwa hiyo, ‘alikuwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.’​—Ufu. 12:12.

8, 9. (a) Namna gani Ufalme wa Mungu ulikaziwa kuwa jambo la maana sana? (b) Ni maulizo gani tutachunguza?

8 Sababu gani Ufalme ni jambo la maana sana? Katika mwaka wa 1928, gazeti Munara wa Mulinzi lilianza kukazia kwamba Ufalme ni jambo la maana zaidi kuliko hata wokovu wa mutu kupitia zabihu ya ukombozi. Kwa kweli, ni kupitia Ufalme wa Masiya ndio Yehova atalitakasa jina lake, na kutetea utawala wake mukubwa, na pia kutimiza makusudi yake yote kuhusu wanadamu.

9 Ni nani watatawala na Kristo katika Ufalme huo? Ni nani ambao watakuwa raia wa Ufalme huo hapa duniani? Na wafuasi wa Kristo wangepaswa kufanya kazi gani?

Kukusanywa kwa Watiwa-Mafuta

10. Watu wa Mungu walikuwa wamekwisha kuelewa nini juu ya wale 144000?

10 Miaka mingi mbele ya mwaka wa 1914, Wakristo wa kweli walikuwa wamekwisha kuelewa kwamba wafuasi wa Kristo 144000 ndio watatawala naye mbinguni. * Wanafunzi hao wa Biblia walielewa kwamba hesabu hiyo haikuwa ya mufano na kwamba wafuasi hao walianza kukusanywa wakati wa mitume.

11. Namna gani wale ambao watakuwa bibi-arusi wa Kristo walielewa hatua kwa hatua kazi ambayo walipaswa kufanya wakati wangali hapa duniani?

11 Kwa hiyo, wale ambao watakuwa bibi-arusi wa Kristo wangefanya kazi gani wakati wangali duniani? Walielewa kwamba Yesu alikazia kazi ya kuhubiri na alionyesha kwamba kazi hiyo itafanyika katika kipindi cha mavuno. (Mt. 9:37; Yoh. 4:35) Katika Sura ya 2, tuliona kwamba wakati fulani Wanafunzi wa Biblia walifundisha kuwa kipindi cha mavuno kitachukua miaka 40, na kwamba mwisho wa kipindi hicho watiwa-mafuta wangechukuliwa na kuenda mbinguni. Lakini, kisha miaka hiyo 40, kazi ya mavuno iliendelea, kwa hiyo, iliomba kuwe na mafasirio mapya. Leo, tunaelewa kabisa kwamba kipindi cha mavuno kilianza katika mwaka 1914. Ilikuwa ni kipindi cha kutenganisha ngano na magugu, ni kusema, kutenganisha Wakristo watiwa-mafuta waaminifu na Wakristo wa uongo. Wakati ulikuwa umefika ili kukazia kukusanywa kwa mabaki ya wale ambao wana tumaini la kuenda mbinguni!

Kipindi cha mavuno kilianza mwaka wa 1914

(Soma fungu la 11)

12, 13. Katika siku za mwisho, namna gani mufano wa Yesu kuhusu mabikira kumi na ule mufano wa talanta imetimizwa?

12 Kuanzia mwaka wa 1919, Kristo aliendelea kuongoza mutumwa mwaminifu na mwenye busara ili akazie kazi ya kuhubiri. Yesu alikuwa amekazia kazi hiyo wakati alikuwa duniani. (Mt. 28:19, 20) Alizungumuzia pia sifa ambazo wafuasi wake watiwa-mafuta wangepaswa kuonyesha ili kutimiza kazi hiyo ya kuhubiri. Namna gani alionyesha hilo? Yesu alitoa mufano wa mabikira kumi. Katika mufano huo alionyesha kwamba watiwa-mafuta walipaswa kuendelea kukesha na kuwa macho kiroho ili kufikia muradi wao wa maana sana, ni kusema, kuwa katika karamu kubwa ya ndoa huko mbinguni. Karamu hiyo itafanyika wakati Kristo ataungana na “bibi-arusi” wake, ni kusema, watu 144000. (Ufu. 21:2) Kisha, Yesu alitoa mufano wa talanta. Katika mufano huo, alifundisha kwamba wafuasi wake watiwa-mafuta watatumika kwa bidii ili kutimiza kazi ya kuhubiri ambayo aliwapatia.—Mt. 25:1-30.

13 Katika miaka 100 iliyopita, Wakristo watiwa-mafuta wamejionyesha kuwa macho na wenye bidii. Bila shaka, Wakristo hao watapewa zawadi yao kwa sababu wameendelea kuwa macho. Hata hivyo, kazi hiyo kubwa ya mavuno ingekusanya tu mabaki ya wale 144000 ambao watatawala pamoja na Kristo?

Kukusanywa kwa Raia wa Ufalme!

14, 15. Ni vikundi gani ine vilizungumuziwa katika kitabu Le mistère de Dieu accompli?

14 Kwa miaka mingi, wanaume na wanawake waaminifu walikuwa wanapenda sana kujua juu ya ‘umati mukubwa’ (‘mukutano mukubwa,’ Union Version) unaotajwa katika Ufunuo 7:9-14. Kwa hiyo, si jambo la kushangaza kwamba mbele ya Kristo kufunua ni nani wanafanyiza kikundi hicho kikubwa, mambo mengi ambayo yalisemwa juu ya watu hao ni tofauti na kweli iliyo wazi na rahisi ambayo tunajua na tunapenda leo.

15 Katika mwaka wa 1917, kitabu Le mystère accompli kilisema kwa kukazia kwamba kuna “aina mbili ao namna mbili ya wokovu kwa wale wataenda mbinguni. Na kwamba kuna aina mbili ao namna mbili ya wokovu kwa wale watabaki duniani.” Kulingana na kitabu hicho ni nani wangefanyiza vikundi hivyo ine vya watu wenye kuwa na matumaini hayo tofauti ya wokovu? Kikundi cha kwanza, ni wale 144000, ambao watatawala pamoja na Kristo. Kikundi cha pili, ni ule mukutano mukubwa. Wakati huo, ndugu walifikiri kwamba hao ni Wakristo ambao wangali katika dini ambazo zinajidai kuwa za Kikristo, na ambao wana imani kidogo, ambayo haiwasaidie kuchukua musimamo imara wa ushikamanifu. Kwa hiyo, wangepewa vyeo vya chini mbinguni. Juu ya wale ambao wangepata wokovu duniani, kitabu hicho kilionyesha kwamba kikundi cha tatu, ni “watu wa zamani walioheshimiwa,” ni kusema, watu waaminifu kama vile Abrahamu, Musa, na wengine. Wao wangepaswa kuwa na vyeo vya mamlaka juu ya kikundi cha ine, ni kusema, wanadamu wengine.

16. Katika mwaka wa 1923 na mwaka wa 1932, watu wa Mungu walipata miangaza gani ya kiroho?

16 Namna gani roho takatifu iliwaongoza wafuasi wa Kristo kwenye ujuzi ambao tunafurahia leo? Jambo hilo lilifanyika hatua kwa hatua kupitia habari-mufululizo ambazo zilikuwa nuru ya kiroho. Miezi ya mwanzo wa mwaka wa 1923, gazeti Munara wa Mulinzi lilikazia uangalifu juu ya kikundi cha watu wasiokuwa na tumaini la kuenda mbinguni na ambao wataishi duniani na kutawaliwa na Kristo. Katika mwaka wa 1932, gazeti Munara wa Mulinzi lilizungumuza juu ya Yonadabu (Yehonadabu), ambaye alishikamana na mutiwa-mafuta wa Mungu, ni kusema, Mufalme wa Israeli Yehu, ili kumuunga mukono katika vita ya kumaliza ibada ya uongo. (2 Fal. 10:15-17) Habari hiyo ilisema kwamba wakati wetu kuna kikundi cha watu ambao wako kama Yonadabu. Na habari hiyo ilisema pia kwamba Yehova atalinda watu wa kikundi hiki ili waweze “kupita ziki ya Har-magedoni” na kuishi hapa duniani.

17. (a) Katika mwaka wa 1935, ndugu walipata mwangaza gani wa kiroho? (b) Namna gani ndugu walionyesha kwamba walifurahi sana wakati walipata maelezo juu ya mukutano mukubwa? (Soma kisanduku “ Mwishowe Tulipata Kitulizo Kabisa.”)

17 Katika mwaka wa 1935, ndugu walipata mwangaza mupya wa kiroho. Kwenye mukusanyiko ambao ulifanyika Washington, D.C., wahuzuriaji walijulishwa kwamba mukutano mukubwa ni kikundi cha watu ambao wataishi duniani. Wao ndio kondoo ambao Yesu anazungumuzia katika mufano wake wa kondoo na mbuzi. (Mt. 25:33-40) Mukutano mukubwa unapaswa kuwa sehemu ya “kondoo wengine” ambao Yesu alisema juu yao hivi: “Hao pia nitawaleta.” (Yoh. 10:16) Wakati ndugu Joseph F. Rutherford, aliuliza: “Wale wote ambao wana tumaini la kuishi milele duniani, tafazali, munaweza kusimama?” Wengi kati ya wahuzuriaji walisimama. Naye akasema: “Mutazame! Ule mukutano mukubwa!” Wengi walifurahia kabisa kusikia sasa juu ya tumaini lao la wakati ujao.

18. Katika kazi ya kuhubiri, wafuasi wa Kristo walitumia nguvu zao juu ya kufanya nini, na walipata matokeo gani?

18 Tangu wakati huo, Kristo ameendelea kuwaongoza wafuasi wake kutumia nguvu zao ili kukusanya watu ambao ni wa mukutano mukubwa ambao watapita wazima na salama ile ziki kubwa. Mwanzoni, ilionekana kwamba watu wa mukutano mukubwa ambao watakusanywa hawatakuwa wengi kabisa. Hata siku fulani, ndugu Rutherford alisema hivi: “Inaonekana kwamba ‘mukutano mukubwa’ hautakuwa mukubwa kabisa kama tunavyowazia.” Kwa kweli, leo tunaona namna Yehova amebariki kazi ya mavuno tangu wakati huo! Kwa uongozi wa Yesu na roho takatifu, watiwa-mafuta na wenzao, wale “kondoo wengine” wametimiza kabisa maneno ambayo Yesu alisema. Wamekuwa “kundi moja” ambalo linatumika pamoja na ambalo linaongozwa na ‘muchungaji mumoja.’

Ndugu Rutherford hakuweza kufikiria kama umati mukubwa ungekuwa mukubwa kama ulivyo leo (Kuanzia kushoto: Nathan H. Knorr, Joseph F. Rutherford, na Hayden C. Covington)

19. Tunaweza kufanya nini ili sisi pia tuunge mukono kazi ya kukusanya mukutano mukubwa?

19 Watu wengi waaminifu wataishi milele katika paradiso duniani, watatawaliwa na Kristo pamoja na wale 144000. Haufurahi kabisa kuona namna Kristo ameongoza watu wa Mungu kwenye tumaini la wakati ujao ambalo linapatana na Biblia na ambalo liko wazi kabisa? Ni pendeleo kabisa kuhubiria wengine juu ya tumaini hilo! Kwa hiyo, acha tuwe watendaji kadiri hali yetu inaturuhusu, ili kufanya hesabu ya watu wa mukutano mukubwa iendelee kuongezeka zaidi, na hivyo, sauti ya kulitukuza jina la Yehova iwe kubwa zaidi kuliko wakati uliopita!​—Soma Luka 10:2.

Hesabu ya umati mukubwa inaendelea kuongezeka

Mutu Anapaswa Kufanya Nini Ili Kuonyesha Kwamba Anashikamana na Ufalme?

20. Taja sehemu zinazofanyiza tengenezo la Shetani, na Wakristo washikamanifu hawapaswe kufanya nini?

20 Wakati watu wa Mungu waliendelea kujifunza juu ya Ufalme, iliomba pia waelewe kabisa sababu gani wanapaswa kushikamana na serikali ya mbinguni. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1922, gazeti Munara wa Mulinzi lilionyesha wazi kwamba kuna matengenezo mawili ambayo yanafanya kazi: Tengenezo la Yehova na tengenezo la Shetani. Lile la Shetani linafanyizwa na sehemu ya kibiashara, ya kidini na ya kisiasa (politike). Wote ambao wanaongozwa na Kristo na ambao wanashikamana na Ufalme wa Mungu hawapaswe kuvunja ushikamanifu wao kwa kujiingiza katika sehemu yoyote ya tengenezo la Shetani. (2 Kor. 6:17) Hilo linamaanisha nini?

21. (a) Namna gani mutumwa mwaminifu ameendelea kuwaonya watu wa Mungu juu ya mashirika makubwa-makubwa ya kibiashara? (b) Katika mwaka wa 1963, gazeti Munara wa Mulinzi lilionyesha kwamba ‘Babiloni Mukubwa’ ni nini?

21 Mutumwa mwaminifu ameendelea kutoa chakula cha kiroho ambacho kinaonyesha wazi udanganyifu wa mashirika makubwa-makubwa ya kibiashara. Na anawaonya watu wa Mungu kuepuka mutego wa kupenda sana vitu vya kimwili. (Mt. 6:24) Pia, vichapo vyetu vimeendelea kusaidia watu waone wazi kabisa ubaya wa dini ambazo ni sehemu ya tengenezo la Shetani. Katika mwaka wa 1963, gazeti Munara wa Mulinzi lilionyesha wazi kwamba ‘Babiloni Mukubwa’ ni dini zote za uongo za duniani pote, na dini zote ambazo zinajidai kuwa za Kikristo. Kwa hiyo, wakati tutajifunza Sura ya 10 ya kitabu hiki, utaona namna watu wa Mungu wa inchi mbalimbali na desturi zote wamesaidiwa ‘kutoka katika [Babiloni Mukubwa],’ wamekuwa safi kwa sababu wameachana kabisa na mafundisho ao matendo ya dini za uongo.—Ufu. 18:2, 4.

22. Wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, namna gani watu wengi wa Mungu walielewa andiko la Waroma 13:1?

22 Sasa tuseme nini juu ya siasa ambayo pia ni sehemu ya tengenezo la Shetani? Wakristo wa kweli wanaweza kujiingiza katika vita mbalimbali na ugomvi wa mataifa? Wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba wafuasi wa Kristo hawapaswe kuua wanadamu wenzao. (Mt. 26:52) Hata hivyo, wengi wao walielewa kama maneno kutii “mamlaka zilizo kubwa” ambayo yanapatikana katika andiko la Waroma 13:1 yaliwaruhusu kujiunga na jeshi, kuvaa mavazi ya askari, na hata kuchukua silaha; lakini wakati waliombwa kuua adui, wangepaswa kupiga masasi katika hewa.

23, 24. Wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, namna gani tulielewa andiko la Waroma 13:1, na namna gani wafuasi wa Kristo waliongozwa ili kuelewa andiko hilo vizuri?

23 Katika mwaka wa 1939, wakati Vita ya Pili ya Ulimwengu ilianza kuenea, gazeti Munara wa Mulinzi lilizungumuzia kwa njia iliyo wazi kwamba Wakristo hawapaswe kujiingiza katika mambo ya vita. Habari ya gazeti hilo ilionyesha wazi kwamba wafuasi wa Kristo hawapaswe kwa njia yoyote kujiingiza katika vita mbalimbali na ugomvi wa mataifa ya ulimwengu wa Shetani. Huo ulikuwa uongozi ambao ulitolewa kwa wakati unaofaa kabisa! Kwa kufuata uongozi huo, wafuasi wa Kristo walilindwa ili wasiwe na deni ya damu, deni mbaya sana ambayo mataifa walijipatia kwa sababu ya kujiingiza katika vita hiyo. Hata hivyo, kuanzia mwaka wa 1929, vichapo vyetu vilionyesha kwamba mamlaka zilizo kubwa ambazo zinazungumuziwa katika andiko la Waroma 13:1 haikuwa viongozi wa serikali, lakini ni Yehova na Yesu. Lakini, iliomba waelewe andiko hilo vizuri zaidi.

24 Katika mwaka wa 1962, roho takatifu iliwaongoza wafuasi wa Kristo kuelewa vizuri zaidi andiko hilo. Mwaka huo habari za pekee ambazo zilizungumuzia andiko la Waroma 13:1-7 zilitolewa katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 11 na wa tarehe 1 Mwezi wa 12. Mwishowe, watu wa Mungu walifikia kuelewa vizuri kanuni ambayo inaonyesha kwamba utii wao kwa wakubwa wenye mamlaka wa ulimwengu ni wa mipaka kulingana na maneno ya Yesu ambayo yanajulikana sana. Maneno hayo ni haya: ‘Mumulipe Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mumulipe Mungu vitu vya Mungu.’ (Lu. 20:25) Leo, Wakristo wa kweli wanaelewa kwamba mamlaka zilizo kubwa ni wakubwa wenye mamlaka wa ulimwengu huu, na kwamba Wakristo wanapaswa kuwatii. Lakini, utii huo ni wa mipaka. Wakati wakubwa wenye mamlaka wanatukataza kumutii Yehova Mungu, hapo tutajibu kama mitume: ‘Lazima tumutii Mungu kuwa mutawala kuliko wanadamu.’ (Mdo. 5:29) Katika Sura ya 13 na ya 14 ya kitabu hiki, tutajifunza zaidi namna watu wa Mungu walitumikisha kanuni ambayo inaomba Wakristo kutojiingiza katika mambo ya vita ao ya siasa.

Ni pendeleo kabisa kuhubiria watu tumaini la uzima wa milele linalopatikana katika Biblia!

25. Sababu gani wewe unafurahia namna roho takatifu inatuongoza ili kuelewa kweli juu ya Ufalme wa Mungu?

25 Fikiria mambo yote ambayo wafuasi wa Kristo wamefundishwa juu ya Ufalme miaka 100 iliyopita. Tumejifunza ni wakati gani Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mbinguni na sababu gani Ufalme huo ni jambo la maana sana. Tumeelewa vizuri kwamba kuna matumaini mawili kwa ajili ya watu waaminifu: tumaini la kuenda mbinguni na tumaini la kuishi hapa duniani. Pia tunajua mambo tunapaswa kufanya ili kuonyesha kwamba tunashikamana na Ufalme wa Mungu, na wakati huohuo kuonyesha utii wenye mipaka kwa wakubwa wenye mamlaka wa ulimwengu huu. Ujiulize, ‘Kama Yesu hangeongoza mutumwa wake mwaminifu kuelewa mafundisho hayo ya kweli na kuyafundisha, mimi mwenyewe ningeyaelewa?’ Tumebarikiwa sana kuwa na Kristo na pia roho takatifu ili kutuongoza!

^ fu. 3 Kitabu kimoja kinasema kwamba, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kuongoza” katika andiko hilo linamaanisha “kuonyesha njia.”

^ fu. 7 Mbele ya hapo, walifikiri kwamba andiko hilo la Ufunuo lilionyesha vita kati ya utawala wa dini ya kipagani ya Roma na utawala wa dini ya Katoliki ya Roma ambao unaongozwa na papa.

^ fu. 10 Katika Mwezi wa 6, 1880, gazeti Munara wa Mulinzi lilionyesha kwamba wale watu 144000 wangekuwa Wayahudi wa kimwili ambao wangekuwa Wakristo mbele ya mwaka wa 1914. Lakini, kisha, katika mwaka wa 1880, habari ilitolewa ambayo inalingana sana na namna tunavyoelewa jambo hilo leo.