Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 6

Watu Wanaohubiri​—Wahudumu Wanajitoa kwa Hiari

Watu Wanaohubiri​—Wahudumu Wanajitoa kwa Hiari

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Mfalme anakusanya jeshi la wahubiri

1, 2. Ni kazi gani kubwa ambayo Yesu alitabiri, na ni swali gani muhimu linalozuka?

MARA nyingi viongozi wa kisiasa hutoa ahadi ambazo hawazitimizi. Hata wale walio na nia nzuri huenda wasiweze kutimiza ahadi zao. Jambo la kupendeza ni kwamba Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo, hutimiza ahadi zake sikuzote.

2 Baada ya kuwekwa kuwa Mfalme katika mwaka wa 1914, Yesu alikuwa tayari kutimiza unabii aliotoa miaka 1,900 hivi mapema. Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alitabiri: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Utimizo wa maneno hayo ungekuwa sehemu ya ishara ya kuwapo kwake katika mamlaka ya Kifalme. Hata hivyo, swali muhimu linazuka: Mfalme angewezaje kukusanya jeshi la wahubiri waliojitoa kwa hiari katika siku za mwisho—wakati ambapo watu wangekuwa wenye ubinafsi, wasio na upendo, na wasiopenda mambo ya kidini? (Mt. 24:12; 2 Tim. 3:1-5) Tunahitaji kujua jibu la swali hilo kwa sababu linawahusu Wakristo wote wa kweli.

3. Yesu alikuwa na uhakika gani, na kwa nini?

3 Hebu soma tena maneno ya kinabii ya Yesu. Je, maneno “itahubiriwa” yanaonyesha kwamba alikuwa na uhakika? Ndiyo! Yesu alikuwa na uhakika kwamba katika siku za mwisho kungekuwa na watu wanaomuunga mkono kwa hiari. Kwa nini alikuwa na uhakika huo? Alijifunza kutoka kwa Baba yake. (Yoh. 12:45; 14:9) Alipokuwa mbinguni, Yesu alijionea mwenyewe kwamba Yehova ana uhakika kuwa waabudu wake watajitoa kwa hiari. Acheni tuone jinsi ambavyo Yehova alionyesha uhakika huo.

“Watu Wako Watajitoa kwa Hiari”

4. Yehova aliwaalika Waisraeli wategemeze kazi gani, nao waliitikiaje?

4 Kumbuka kilichotokea Yehova alipomwagiza Musa ajenge maskani au hema ambalo lingekuwa kituo cha ibada cha taifa la Israeli. Kupitia Musa, Yehova aliwaalika watu wote wategemeze kazi hiyo. Musa aliwaambia hivi: “Toeni mchango kwa ajili ya Yehova. Kila mtu mwenye moyo wenye nia na aulete.” Matokeo yakawa nini? Watu “walimletea matoleo ya hiari asubuhi kwa asubuhi.” Walitoa michango mingi hivi kwamba “wakazuiliwa wasilete”! (Kut. 35:5; 36:3, 6) Waisraeli hao walithibitisha kwamba Yehova hakukosea kwa kuwa na uhakika nao.

5, 6. Kulingana na Zaburi 110:1-3, Yehova na pia Yesu walitarajia waabudu wa kweli waonyeshe roho gani katika wakati wa mwisho?

5 Je, Yehova alitarajia waabudu wake wawe na roho hiyo ya kujitoa kwa hiari katika siku za mwisho? Ndiyo! Zaidi ya miaka 1,000 kabla ya Yesu kuzaliwa duniani, Yehova alimwongoza Daudi aandike kuhusu wakati ambapo Masihi angeanza kutawala. (Soma Zaburi 110:1-3.) Yesu, Mfalme aliyetawazwa karibuni, angekuwa na maadui ambao wangempinga. Hata hivyo, angekuwa pia na watu wengi wanaomuunga mkono. Watu hao hawangelazimishwa kumtumikia Mfalme. Hata watoto miongoni mwao wangejitoa kwa hiari na kuwa umati mkubwa sana ambao kwa kufaa unaweza kulinganishwa na matone ya umande ambayo huifunika ardhi wakati wa mapambazuko. *

Wale wanaounga mkono Ufalme kwa hiari ni kama matone mengi ya umande (Ona fungu la 5)

6 Yesu alijua kwamba unabii ulio kwenye Zaburi 110 ulimhusu yeye. (Mt. 22:42-45) Kwa hiyo, alikuwa na kila sababu ya kuwa na uhakika kwamba atakuwa na watu watakaomuunga mkono kwa ushikamanifu na ambao watajitoa kwa hiari kuhubiri habari njema duniani kote. Mambo hakika ya kihistoria yanaonyesha nini? Je, kweli Mfalme huyo amekusanya jeshi la wahubiri wanaojitoa kwa hiari katika siku hizi za mwisho?

“Pendeleo na Wajibu Wangu Ni Kutangaza Ujumbe Huo”

7. Baada ya kutawazwa kuwa Mfalme, Yesu alichukua hatua gani ili kuwatayarisha wale wanaomuunga mkono kwa ajili ya kazi iliyokuwa mbele yao?

7 Muda mfupi baada ya kutawazwa kuwa Mfalme, Yesu alichukua hatua ili kuwatayarisha wafuasi wake kwa ajili ya kazi kubwa ambayo ilipaswa kufanywa. Kama tulivyoona katika Sura ya 2, alifanya kazi ya kukagua na kusafisha kuanzia mwaka wa 1914 hadi mwanzoni mwa mwaka wa 1919. (Mal. 3:1-4) Kisha, katika mwaka wa 1919, alimweka rasmi mtumwa mwaminifu ili awaongoze wafuasi wake. (Mt. 24:45) Hasa kuanzia wakati huo na kuendelea, mtumwa huyo alianza kutoa chakula cha kiroho kupitia hotuba kwenye makusanyiko na machapisho ambayo yamekuwa yakikazia tena na tena kwamba kila Mkristo anapaswa kuhubiri.

8-10. Makusanyiko yalichocheaje kazi ya kuhubiri? Toa mfano. (Ona pia sanduku “ Makusanyiko ya Zamani Yaliyochochea Kazi ya Kuhubiri.”)

8 Hotuba za makusanyiko. Wakiwa na hamu ya kupata mwongozo, Wanafunzi wa Biblia walikusanyika Cedar Point, Ohio, Marekani, kuanzia Septemba 1 hadi 8, 1919, kwa ajili ya kusanyiko la kwanza tangu Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kwisha. Siku ya pili ya kusanyiko hilo, Ndugu Rutherford alisema hivi waziwazi katika hotuba yake: “Utume wa Mkristo duniani . . . ni kutangaza ujumbe wa ufalme wa Bwana.”

9 Kusanyiko hilo lilifikia kilele chake siku tatu baadaye wakati Ndugu Rutherford alipotoa hotuba yenye kichwa, “Hotuba kwa Wafanyakazi Wenzi,” ambayo ilichapishwa kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi chini ya kichwa “Kuutangaza Ufalme.” Alisema hivi: “Anapokuwa ametulia, ni kawaida kwa Mkristo kujiuliza, Kwa nini niko duniani? Jibu lake linapaswa kuwa, Kwa fadhili, Bwana ameniweka niwe balozi wake ili niwapelekee watu ujumbe wa upatanisho ambao Mungu amenipa, na pendeleo na wajibu wangu ni kutangaza ujumbe huo.”

10 Wakati wa hotuba hiyo ya kihistoria, Ndugu Rutherford alitangaza kwamba gazeti jipya, The Golden Age (sasa linaitwa Amkeni!), litachapishwa ili kutumiwa kuwaelekeza watu kwenye Ufalme ambao ndio tumaini pekee la wanadamu. Kisha akauliza ni nani wangependa kushiriki kugawanya gazeti hilo. Ripoti moja kuhusu kusanyiko hilo ilisema hivi: “Watu wengi walikubali. Wahudhuriaji wote 6,000 walisimama na kuonyesha kwamba walikuwa tayari kushiriki katika kazi hiyo.” * Ni wazi kwamba Mfalme alikuwa na watu waliomuunga mkono kwa hiari na walikuwa tayari kutangaza Ufalme wake!

11, 12. Gazeti Mnara wa Mlinzi la mwaka wa 1920 lilisema kazi ambayo Yesu alitabiri ingefanywa wakati gani?

11 Machapisho. Kupitia gazeti Mnara wa Mlinzi, umuhimu wa kazi ambayo Yesu alitabiri, yaani, kuhubiri habari njema ya Ufalme, ulifafanuliwa wazi. Hebu tuchunguze mifano kadhaa kuanzia mapema miaka ya 1920.

12 Ni ujumbe gani ambao ungetangazwa ili kutimiza Mathayo 24:14? Kazi hiyo ingefanywa wakati gani? Makala yenye kichwa “Injili ya Ufalme” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1920 ilieleza hivi kuhusu ujumbe huo: “Habari njema inahusu mwisho wa mfumo wa kale wa mambo na kusimamishwa kwa ufalme wa Masihi.” Makala hiyo ilionyesha wazi wakati ambapo ujumbe huo ungehubiriwa kwa kusema: “Ujumbe huo lazima utangazwe kati ya kile kipindi cha vita vikuu [Vita vya Kwanza vya Ulimwengu] na wakati wa ile ‘dhiki kuu.’” Hivyo makala hiyo ilisema: “Sasa ndio wakati . . . wa kutangaza hii habari njema kotekote katika dini zinazodai kuwa za Kikristo.”

13. Gazeti Mnara wa Mlinzi la mwaka wa 1921 liliwachocheaje Wakristo watiwa-mafuta wajitoe kwa hiari?

13 Je, watu wa Mungu wangelazimishwa kufanya kazi ambayo Yesu alikuwa ametabiri? Hapana. Makala, “Iweni Wenye Moyo Mkuu,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1921 iliwahimiza Wakristo watiwa-mafuta wajitoe kwa hiari. Kila mmoja alitiwa moyo ajiulize: “Je, naliona kuwa pendeleo kubwa na pia wajibu wangu kushiriki katika kazi hii?” Makala hiyo iliendelea kusema: “Tuna uhakika kwamba mnapoliona [kuwa pendeleo kushiriki katika kazi hiyo] mtakuwa kama Yeremia, ambaye moyoni mwake neno la Bwana lilikuwa ‘kama moto unaowaka ambao umefungiwa ndani ya mifupa [yake],’ likimchochea hivi kwamba hangeweza kujizuia kusema.” (Yer. 20:9) Kitia-moyo hicho kinaonyesha kwamba Yehova na Yesu wanawaamini wale wanaounga mkono Ufalme kwa ushikamanifu.

14, 15. Katika mwaka wa 1922, gazeti Mnara wa Mlinzi liliwahimiza Wakristo watiwa-mafuta watumie njia gani kuwafikia watu?

14 Wakristo wa kweli wangetumia njia gani kuwafikishia wengine ujumbe wa Ufalme? Makala fupi lakini yenye nguvu iliyokuwa na kichwa, “Utumishi Ni wa Lazima,” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1922, iliwahimiza Wakristo watiwa-mafuta wawe na “bidii ya kuwapelekea watu machapisho na kuzungumza nao kwenye nyumba zao, na kutoa ushahidi kwamba ufalme wa mbinguni uko karibu.”

15 Ni wazi kwamba kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, Kristo amemtumia mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara kukazia tena na tena kwamba pendeleo na wajibu wa Mkristo duniani ni kutangaza ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, Wanafunzi wa Biblia wa mapema waliitikiaje walipotiwa moyo washiriki katika kazi ya kutangaza Ufalme?

“Waaminifu Watajitolea”

16. Baadhi ya wazee waliitikiaje wazo la kwamba kila mtu alipaswa kushiriki katika huduma?

16 Katika miaka ya 1920 na 1930, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walipinga wazo la kwamba Wakristo wote watiwa-mafuta wanapaswa kushiriki katika huduma. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1927 lilieleza hali ilivyokuwa: “Leo kuna wale ambao wana cheo cha uzee katika kanisa [kutaniko] . . . wanaokataa kuwatia moyo ndugu zao washiriki katika utumishi, nao wenyewe wanakataa kushiriki katika utumishi. . . . Wanapuuza pendekezo la kwenda mlango kwa mlango ili kuwapelekea watu ujumbe kumhusu Mungu, Mfalme wake na ufalme wake.” Makala hiyo ilisema hivi waziwazi: “Wakati umefika kwa waaminifu kuwatia alama watu hao na kuwaepuka, na kuwaambia kwamba hatutawapa tena watu hao cheo cha uzee.” *

17, 18. Watu wengi kutanikoni waliitikiaje mwongozo uliotolewa na makao makuu, na mamilioni ya watu wameitikiaje katika miaka 100 iliyopita?

17 Kwa kupendeza, wengi kutanikoni walitii kwa moyo wote mwongozo huo kutoka makao makuu. Waliliona kuwa pendeleo kuwaambia watu kuhusu ujumbe wa Ufalme. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1926, lilieleza hivi: “Waaminifu watajitolea . . . kuwaambia watu ujumbe huu.” Waaminifu hao walitimiza maneno ya kinabii yaliyo kwenye Zaburi 110:3 na wakathibitisha kwamba wanamuunga mkono kwa hiari Mfalme wa Kimasihi.

18 Katika miaka 100 iliyopita, mamilioni ya watu wamejitoa kwa hiari kufanya kazi ya kutangaza Ufalme. Katika sura chache zinazofuata, tutazungumzia jinsi ambavyo wamehubiri, yaani, mbinu na vifaa ambavyo wametumia, na matokeo ambayo wamepata. Hata hivyo, acheni kwanza tuzungumzie sababu ambayo imewafanya mamilioni washiriki kwa hiari katika kazi hii ya kuhubiri kuhusu Ufalme licha ya kuishi katika ulimwengu wenye ubinafsi. Tunapochunguza sababu hizo, inafaa tujiulize, ‘Kwa nini mimi huwaambia wengine habari njema?’

“Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme”

19. Kwa nini tunatii shauri la Yesu kwamba ‘tuendelee kuutafuta kwanza ufalme’?

19 Yesu aliwashauri wafuasi wake ‘waendelee kuutafuta kwanza ufalme.’ (Mt. 6:33) Kwa nini tunatii shauri hilo? Kimsingi, ni kwa sababu tunatambua umuhimu wa Ufalme, yaani, Ufalme ndio utakaotumiwa hasa kutimiza kusudi la Mungu. Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, roho takatifu imefunua hatua kwa hatua kweli zenye kusisimua kuhusu Ufalme. Kweli hizo muhimu za Ufalme zinapogusa mioyo yetu, tunachochewa kuutafuta kwanza Ufalme huo.

Kama mwanaume anayepata hazina iliyofichwa anavyojawa na shangwe, Wakristo hufurahi kwamba wamepata kweli ya Ufalme (Ona fungu la 20)

20. Mfano wa Yesu kuhusu hazina iliyofichwa unaonyeshaje kwamba wafuasi wake wangetii shauri lake la kuendelea kuutafuta kwanza Ufalme?

20 Yesu alijua jinsi ambavyo wafuasi wake wangetii shauri la kuutafuta kwanza Ufalme. Fikiria mfano wake wa hazina iliyofichwa. (Soma Mathayo 13:44.) Anapofanya kazi zake za kawaida shambani, mtu anayetajwa katika mfano huo anapata hazina iliyofichwa na mara moja anatambua thamani yake. Anafanya nini? “Kwa sababu ya shangwe aliyo nayo, anaenda na kuuza vitu alivyo navyo na kulinunua shamba hilo.” Tunajifunza nini? Tunapopata kweli ya Ufalme na kutambua thamani yake, kwa shangwe tutadhabihu jambo lolote lile ili kutanguliza mambo ya Ufalme maishani mwetu. *

21, 22. Wale wanaounga mkono Ufalme kwa ushikamanifu huonyeshaje kwamba wanautafuta kwanza Ufalme? Toa mfano.

21 Wale wanaounga mkono Ufalme kwa ushikamanifu huonyesha kwa matendo, na si kwa maneno tu, kwamba wanautafuta kwanza Ufalme. Wanatumia maisha yao, uwezo wao, na mali zao katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Wengi wamejidhabihu mambo mengi ili waingie katika utumishi wa wakati wote. Wahubiri hao wanaojitoa kwa hiari wamejionea wenyewe kwamba Yehova huwabariki wale wanaoutafuta kwanza Ufalme. Fikiria mfano ufuatao wa mapainia wa zamani.

22 Avery na Lovenia Bristow walikuwa makolpota (mapainia) kusini mwa Marekani katika miaka ya mwishoni mwa 1920. Miaka mingi baadaye, Lovenia alisema hivi: “Mimi na Avery tumefurahia sana kufanya upainia pamoja kwa miaka mingi. Mara nyingi hatukujua tutapata wapi pesa za petroli au chakula. Lakini sikuzote Yehova alitupa kile tulichohitaji. Hatukuacha upainia. Sikuzote tulipata mahitaji yetu ya lazima.” Lovenia alikumbuka kwamba siku moja walipokuwa wakitumikia jijini Pensacola, Florida, hawakuwa na pesa za kutosha kununua chakula. Lakini waliporudi nyumbani, walipata mifuko miwili iliyojaa chakula mlangoni pamoja na barua iliyosema, “Tunawapenda, Kutaniko la Pensacola.” * Lovenia alisema hivi kuhusu miaka mingi aliyotumikia akiwa painia: “Yehova hatuachi kamwe. Hatutamaushi tunapomtegemea.”

23. Unaionaje kweli ya Ufalme ambayo umepata, na umeazimia kufanya nini?

23 Sisi sote hatuwezi kuhubiri kwa kiwango kilekile. Hali zetu zinatofautiana. Hata hivyo, sote tunaliona kuwa pendeleo kutangaza habari njema kwa nafsi yote. (Kol. 3:23) Kwa kuwa tunathamini sana kweli ya Ufalme tuliyopata, tuko tayari, naam, tuna hamu ya kujidhabihu kwa vyovyote vile ili tutumikie kwa kadiri tuwezavyo. Je, hilo ndilo azimio lako?

24. Ni jambo gani kubwa ambalo Ufalme umetimiza katika siku za mwisho?

24 Katika karne moja iliyopita, kwa kweli Mfalme amekuwa akitimiza unabii aliotoa kwenye Mathayo 24:14. Na amefanya hivyo bila kuwalazimisha wafuasi wake. Baada ya kutoka katika ulimwengu huu wenye ubinafsi, wafuasi wake wamejitoa kwa hiari ili kuhubiri. Kazi yao ya kuhubiri inayofanywa duniani kote ni sehemu ya ishara ya kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme, na ni mojawapo ya mambo makubwa ambayo Ufalme umetimiza katika siku za mwisho.

^ fu. 5 Katika Biblia, umande unahusianishwa na wingi.—Mwa. 27:28; Mika 5:7.

^ fu. 10 Kijitabu To Whom the Work Is Entrusted (Kwa Wale Waliokabidhiwa Kazi) kilieleza hivi: “Gazeti The Golden Age litatumiwa katika kampeni ya kupeleka ujumbe wa ufalme nyumba kwa nyumba. . . . baada ya kutoa ujumbe huo, nakala ya The Golden Age inapaswa kuachwa katika kila nyumba, iwe mtu ameandikisha gazeti hilo au la.” Kwa miaka mingi baada ya hapo, akina ndugu walitiwa moyo wawatolee watu maandikisho ya The Golden Age na Mnara wa Mlinzi. Kuanzia Februari 1, 1940, watu wa Yehova walitiwa moyo wawaachie watu magazeti hayo na waripoti magazeti waliyowaachia watu.

^ fu. 16 Wakati huo, wazee walichaguliwa kwa kupigiwa kura na kutaniko. Kwa hiyo, kutaniko lingekataa kuwapigia kura wanaume waliopinga kazi ya kuhubiri. Badiliko la kuacha kuwachagua wazee kwa njia ya kura na kuanza kuwaweka rasmi kitheokrasi litazungumziwa katika Sura ya 12.

^ fu. 20 Yesu alifundisha jambo hilohilo katika mfano wake kuhusu mwanabiashara anayesafiri kutafuta lulu moja ya thamani kubwa. Anapoipata, mwanabiashara huyo anauza vitu vyote alivyo navyo na kuinunua. (Mt. 13:45, 46) Pia, mifano yote miwili inatufundisha kwamba tunaweza kujifunza kweli ya Ufalme katika njia mbalimbali. Wengine hupata kweli hiyo bila kutarajia; hali wengine huitafuta. Lakini hata iwe tulipata kweli kwa njia gani, tuko tayari kujidhabihu ili tuutangulize Ufalme maishani.

^ fu. 22 Makutaniko yaliitwa mashirika.