Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 7

Mbinu za Kuhubiri​—Kutumia Kila Njia Ili Kuwafikia Watu

Mbinu za Kuhubiri​—Kutumia Kila Njia Ili Kuwafikia Watu

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Watu wa Mungu wanatumia mbinu mbalimbali za kuhubiri ili kuwafikia watu wengi kadiri iwezekanavyo

1, 2. (a) Yesu alitumia mbinu gani ili kuzungumza na umati? (b) Wanafunzi waaminifu wa Kristo walifuataje mfano wake, na kwa nini?

UMATI unakusanyika na kumzunguka Yesu kwenye ufuo wa bahari, hivyo anaamua kupanda mashua na kusonga mbali kidogo. Kwa nini? Anajua kwamba mawimbi ya maji yangekuza sauti yake na watu wengi wangesikia vizuri ujumbe wake.—Soma Marko 4:1, 2.

2 Karibu na wakati wa kuzaliwa kwa Ufalme, wanafunzi waaminifu wa Kristo walifuata mfano wake na kutumia mbinu mpya ili kueneza habari njema za Ufalme kwa watu wengi sana. Chini ya mwongozo wa Mfalme, watu wa Mungu wanaendelea kubuni njia mpya na kuzitumia kadiri hali zinavyobadilika na tekinolojia mpya kutokea. Tunataka kuwafikia watu wengi iwezekanavyo kabla mwisho haujafika. (Mt. 24:14) Chunguza baadhi ya mbinu ambazo tumetumia kuwafikia watu mahali popote walipo. Pia, fikiria jinsi unavyoweza kuiga imani ya wale wote walioeneza habari njema katika siku za mapema.

Kuwafikia Watu Wengi

3. Kwa nini kutumia magazeti ya habari kuliwakasirisha maadui wa ile kweli?

3 Magazeti ya habari. Ndugu Russell na wenzake walikuwa wakichapisha gazeti Mnara wa Mlinzi tangu mwaka wa 1879, na hivyo kuwapelekea watu wengi ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, kwa miaka kumi kabla ya mwaka wa 1914, inaonekana kwamba Kristo aliongoza mambo ili habari njema ziwafikie watu wengi zaidi. Mfuatano wa matukio ulianza mwaka wa 1903. Mwaka huo, Dakt. E.  L.  Eaton, msemaji wa kikundi cha wahudumu wa Kiprotestanti huko Pennsylvania, alimwalika Charles Taze Russell katika mijadala kuhusu mafundisho ya Biblia. Katika barua yake kwa Russell, Eaton aliandika: “Nimefikiria kwamba mjadala wa hadharani kuhusu baadhi ya maswali ambayo mimi na wewe tunatofautiana . . . utawanufaisha sana watu wote.” Russell na wenzake walifikiri watu wangenufaika, hivyo wakapanga mijadala hiyo ichapishwe katika gazeti maarufu la habari The Pittsburgh Gazette. Kwa kuwa makala hizo zilipendwa sana na Russell alifafanua kweli za Biblia kwa njia ya wazi na yenye kusadikisha sana, basi gazeti hilo liliamua kuchapisha hotuba za Russell kila juma. Lazima jambo hilo liliwakasirisha sana maadui wa ile kweli!

Kufikia mwaka wa 1914, zaidi ya magazeti 2,000 yalikuwa yakichapisha hotuba za Russell

4, 5. Russell alionyesha sifa gani, na wale walio na madaraka wanaweza kuigaje mfano wake?

4 Punde si punde, magazeti mengi ya habari yalitaka kuchapisha hotuba za Russell. Kufikia mwaka wa 1908, gazeti Mnara wa Mlinzi liliripoti kwamba hotuba hizo zilikuwa zikichapishwa “kwa ukawaida katika magazeti kumi na moja.” Hata hivyo, akina ndugu wanaofahamu vizuri magazeti ya habari walimshauri Russell kwamba ikiwa atahamisha ofisi za Sosaiti kutoka Pittsburgh hadi kwenye jiji lililojulikana zaidi, magazeti mengi yangechapisha makala hizo zinazozungumzia Biblia. Baada ya kufikiria kwa uzito ushauri huo na mambo mengine, Russell alihamishia ofisi Brooklyn, New York, mwaka wa 1909. Kulikuwa na matokeo gani? Miezi kadhaa tu baada ya kuhamia Brooklyn, magazeti 400 yalikuwa yakichapisha hotuba za Russell, na idadi hiyo ikazidi kuongezeka. Kufikia wakati Ufalme uliposimamishwa mwaka wa 1914, zaidi ya magazeti 2,000 katika lugha nne yalikuwa yakichapisha hotuba na makala za Russell!

5 Matukio hayo yanatufundisha jambo gani muhimu? Wale wote walio na madaraka katika tengenezo la Mungu leo inafaa waige unyenyekevu wa Russell. Katika njia gani? Wanapofanya maamuzi muhimu, wafikirie ushauri wa wengine.—Soma Methali 15:22.

6. Kweli zilizochapishwa katika gazeti zilibadili jinsi gani maisha ya mwanamke fulani?

6 Kweli hizo za Ufalme zilizochapishwa katika magazeti zilibadili maisha ya watu. (Ebr. 4:12) Kwa mfano, Ora Hetzel, aliyebatizwa mwaka wa 1917, alikuwa miongoni mwa wengi waliojifunza kweli kwa mara ya kwanza kupitia makala hizo. Ora alisema hivi: “Baada ya kuolewa, nilienda kumtembelea mama yangu aliyeishi Rochester, Minnesota. Nilipofika, nilimkuta anakata makala kutoka kwenye gazeti la habari. Makala hizo zilikuwa hotuba za Russell. Mama alinieleza mambo aliyojifunza kutokana na makala hizo.” Ora alikubali kweli alizojifunza na kwa miaka sitini hivi alitangaza kwa uaminifu Ufalme wa Mungu.

7. Kwa nini wale waliokuwa wakiongoza walifikiria tena ikiwa ingefaa kuendelea kutumia magazeti?

7 Katika mwaka wa 1916, matukio mawili makubwa yalifanya akina ndugu waliokuwa wakiongoza wafikirie tena ikiwa ingefaa kuendelea kutumia magazeti ya habari kueneza habari njema. Kwanza, vile Vita Vikuu ambavyo vilikuwa vikiendelea wakati huo vilifanya iwe vigumu kupata vifaa vya uchapishaji. Mwaka wa 1916, ripoti kutoka idara yetu ya magazeti nchini Uingereza, ilisema: “Kuna zaidi ya magazeti 30 tu kwa sasa yanayochapisha Hotuba hizo. Hivi karibuni huenda idadi hiyo ikapungua zaidi kwa sababu ya kuongezeka kwa bei ya karatasi.” Tukio la pili lilikuwa kifo cha Ndugu Russell Oktoba 31, 1916. Hivyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1916, lilitangaza hivi: “Kwa sababu Ndugu Russell amekufa, hotuba zake hazitachapishwa tena [katika magazeti ya habari].” Ingawa mbinu hiyo ya kuhubiri haikuendelea kutumiwa, mbinu nyingine kama vile, “Photo-Drama of Creation,” ziliendelea kufanikiwa sana.

8. Ni mambo gani yaliyohusika katika kutengeneza sinema ya “Photo-Drama of Creation”?

8 Maonyesho ya picha. Russell na wenzake walitumia miaka mitatu hivi kutayarisha sinema ya “Photo-Drama of Creation,” iliyotolewa mwaka wa 1914. (Met. 21:5) Sinema hiyo ilitayarishwa kwa kutumia mbinu mpya ya kuunganisha picha, sauti zilizorekodiwa, na slaidi za vioo zenye rangi. Mamia ya watu waliigiza masimulizi ya Biblia ambayo yalirekodiwa kwenye sinema hiyo, na hata wanyama walitumiwa. Ripoti moja ya mwaka wa 1913 inasema: “Wanyama wengi kutoka mojawapo ya bustani kubwa za wanyama walitumiwa kwenye onyesho la Noa katika sinema hiyo ya kihistoria.” Mamia ya slaidi za vioo ambazo zilitumiwa katika sinema hiyo zilipakwa rangi na wasanii kutoka London, New York, Paris, na Philadelphia.

9. Kwa nini muda mwingi na pesa nyingi zilitumiwa kutengeneza sinema ya “Photo-Drama”?

9 Kwa nini muda mwingi na pesa nyingi zilitumika ili kutengeneza sinema ya “Photo-Drama”? Azimio lililopitishwa katika makusanyiko yaliyofanywa mwaka wa 1913 lilieleza hivi: “Kwa kuwa magazeti ya habari ya Marekani yamefanikiwa sana kushawishi watu kwa kutumia vibonzo na michoro, na pia kwa kuwa sinema hizo zinapendwa sana na zinaweza kuwasilisha habari mpya katika njia mbalimbali, manufaa yake yameonekana wazi. Kwa hiyo, tunaamini kabisa kwamba sisi tukiwa wahubiri na walimu wa madarasa ya Biblia, tuna sababu za kutosha kukubali kwamba sinema na slaidi zinazotumia projekta ni mbinu inayofaa na yenye matokeo sana kwa ajili ya waeneza-evanjeli na walimu.”

Juu: Chumba cha projecta ya “Photo-Drama”; Chini: Slaidi za “Photo-Drama”

10. Sinema ya “Photo-Drama” ilionyeshwa katika maeneo mengi kadiri gani?

10 Katika mwaka wa 1914, sinema ya “Photo-Drama” ilionyeshwa katika majiji 80 kila siku. Watu milioni nane hivi nchini Marekani na Kanada waliona sinema hiyo. Mwaka huohuo, sinema ya “Photo-Drama” ilionyeshwa Australia, Denmark, Finland, New Zealand, Norway, Sweden, Uingereza, Ujerumani, na Uswisi. Sinema iliyofupishwa ambayo ilikuwa na sauti pekee ilitengenezwa ili ionyeshwe kwenye miji midogo. Sinema hiyo iliyoitwa “Eureka Drama”—haikuhitaji pesa nyingi kuitengeneza na ilikuwa rahisi kuisafirisha. Kufikia mwaka wa 1916, sinema zote, yaani, “Photo-Drama” na “Eureka Drama” zilikuwa zimetafsiriwa katika Kiarmenia, Kifaransa, Kigiriki, Kihispania, Kiitaliano, Kijerumani, Kipolandi, Kiswedi, na mchanganyiko wa Kinorwei na Kidenmarki.

Katika mwaka wa 1914, sinema ya “Photo-Drama” ilionyeshwa katika majumba yaliyojaa watu

11, 12. Sinema ya “Photo-Drama” ilikuwa na matokeo gani kwa kijana mmoja, na alituwekea mfano gani?

11 Tafsiri ya Kifaransa ya sinema “Photo-Drama” ilimgusa sana kijana mwenye umri wa miaka 18 aliyeitwa Charles Rohner. Charles anasema hivi: “Ilionyeshwa kwenye mji nilioishi—Colmar, Alsace, Ufaransa. Kuanzia mwanzo wa sinema hiyo, nilivutiwa sana na jinsi kweli za Biblia zilivyofafanuliwa kwa njia yenye kueleweka.”

12 Matokeo yake ni kwamba Charles alibatizwa na mwaka wa 1922 akaanza utumishi wa wakati wote. Mmoja kati ya migawo yake ya kwanza ulikuwa kuonyesha sinema ya “Photo-Drama” nchini Ufaransa. Akieleza kazi alizofanya, Charles anasema: “Nilipewa kazi kadhaa—kucheza ala ya fidla, kuwa mtumishi wa hesabu, na kuwa mtumishi wa vitabu. Pia, nilipewa mgawo wa kuwaomba wasikilizaji wanyamaze kabla ya programu kuanza. Wakati wa mapumziko tuligawa machapisho. Kila ndugu au dada aligawiwa sehemu fulani ya ukumbi. Kila mmoja alibeba machapisho mkononi na kumpa kila mtu katika sehemu yake. Kwa kuongezea, kwenye mwingilio wa ukumbi kulikuwa na meza zilizojaa machapisho.” Mwaka wa 1925, Charles alialikwa kutumikia Betheli ya Brooklyn, New York. Akiwa huko, alipewa mgawo wa kuongoza okestra kwa ajili ya kituo kipya cha redio kilichoitwa WBBR. Baada ya kuchunguza mfano wa Ndugu Rohner, tunaweza kujiuliza hivi, ‘Je, niko tayari kukubali mgawo wowote ili kusaidia kueneza ujumbe wa Ufalme?’—Soma Isaya 6:8.

13, 14. Redio zilitumiwaje kueneza habari njema? (Ona pia masanduku “ Vipindi Kwenye Kituo cha WBBR” na “ Kusanyiko la Kihistoria.”)

13 Redio. Katika miaka ya 1920, kazi ya “Photo-Drama” ilianza kupungua, lakini redio ikaibuka kuwa njia muhimu ya kueneza habari njema ya Ufalme. Aprili 16, 1922, Ndugu Rutherford alitoa hotuba yake ya kwanza kupitia redio akiwa kwenye Nyumba ya Opera ya Metropolitan huko Philadelphia, Pennsylvania. Inakadiriwa kwamba watu 50,000 walisikia hotuba hiyo yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Kisha mwaka wa 1923, kwa mara ya kwanza sehemu ya programu ya kusanyiko ilitangazwa kwenye redio. Mbali na kutumia vituo vya redio vya kulipia, ndugu waliokuwa wakiongoza waliamua kwamba lingekuwa jambo la busara kujenga kituo chetu wenyewe. Kituo hicho kilijengwa katika Kisiwa cha Staten, New York, na kusajiliwa kwa jina WBBR. Matangazo ya kwanza kabisa yalirushwa hewani Februari 24, 1924.

 Katika mwaka wa 1922, inakadiriwa kwamba watu 50,000 walisikia hotuba yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe” iliyotolewa kupitia redio

14 Likizungumzia kusudi la WBBR, gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1924, lilisema: “Tunaamini kwamba kati ya mbinu zote ambazo zimewahi kutumiwa, redio ndiyo njia isiyogharimu pesa nyingi na yenye matokeo mazuri zaidi katika kueneza ujumbe wa kweli.” Kisha likaongeza hivi: “Ikiwa Bwana anaona inafaa kujenga vituo vingine vya redio kwa ajili ya kueneza kweli, atatoa pesa kwa njia yake mwenyewe.” (Zab. 127:1) Kufikia mwaka wa 1926, watu wa Yehova walimiliki vituo sita vya redio. Vituo viwili vilikuwa nchini Marekani—WBBR jijini New York na WORD karibu na Chicago. Vile vingine vinne vilikuwa nchini Kanada, huko Alberta, British Columbia, Ontario, na Saskatchewan.

15, 16. (a) Viongozi wa kidini nchini Kanada waliitikiaje matangazo yetu ya redio? (b) Hotuba za redioni na kazi ya nyumba kwa nyumba zilitegemezana jinsi gani?

15 Viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo waliona jitihada hizo za kueneza kweli za Biblia kupitia vituo vya redio. Albert Hoffman, aliyeshiriki kufanya kazi katika kituo cha redio huko Saskatchewan, Kanada, alisema hivi: “Watu wengi walianza kuwafahamu Wanafunzi wa Biblia [kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo]. Ushahidi mzuri sana ulitolewa hadi mwaka wa 1928, wakati viongozi wa kidini waliposhinikiza maofisa wa serikali na vituo vyote vya redio vya Wanafunzi wa Biblia nchini Kanada vikanyang’anywa leseni.”

16 Licha ya kufungwa kwa vituo vyetu vya redio nchini Kanada, hotuba za Biblia ziliendelea kutangazwa kupitia vituo vya redio vya kulipia. (Mt. 10:23) Ili hotuba hizo ziwafikie watu wengi sana, magazeti Mnara wa Mlinzi na The Golden Age (sasa Amkeni!) yalikuwa na orodha ya vituo vyote vilivyotangaza kweli za Biblia ili wahubiri wanapohubiri mlango kwa mlango wawatie watu moyo wasikilize hotuba hizo kupitia vituo hivyo. Kulikuwa na matokeo gani? Bulletin (sasa Huduma Yetu ya Ufalme) ya Januari 1931 ilisema: “Redio imewachochea sana akina ndugu kuhubiri mlango kwa mlango. Tumepokea ripoti nyingi zinazosema kwamba watu wengi wamesikiliza na, baada ya kusikia hotuba zilizotolewa na Ndugu  Rutherford, walikuwa tayari kuchukua vitabu ambavyo tuliwapa.” Bulletin ilisema kwamba redio na kazi ya nyumba kwa nyumba ndiyo “mbinu mbili kuu zilizotumiwa na tengenezo la Bwana.”

17, 18. Ingawa hali zilibadilika, redio ziliendeleaje kuwa sehemu muhimu ya kutangaza ujumbe wa Ufalme?

17 Katika miaka ya 1930, upinzani dhidi ya matangazo yetu katika vituo vya redio vya kulipia uliongezeka. Kwa hiyo mwishoni mwa mwaka wa 1937, watu wa Yehova walibadilikana kulingana na hali. Waliacha kutumia vituo vya redio na wakakazia fikira huduma ya nyumba kwa nyumba. * Hata hivyo, redio iliendelea kuwa sehemu muhimu katika kueneza ujumbe wa Ufalme katika maeneo ya mbali na sehemu ambazo hazingeweza kufikiwa kwa sababu za kisiasa. Kwa mfano, kuanzia mwaka wa 1951 hadi 1991, kituo kimoja huko Berlin Magharibi, Ujerumani, kilitangaza kwa ukawaida hotuba za Biblia ili wale walioishi katika ile iliyoitwa Ujerumani Mashariki waweze kusikia ujumbe wa Ufalme. Kuanzia mwaka wa 1961 na kwa zaidi ya miaka 30 baadaye, kituo cha redio cha kitaifa huko Suriname, Amerika Kusini, kilikuwa na kipindi cha dakika 15 kila juma ili kueneza kweli za Biblia. Kuanzia mwaka wa 1969 hadi 1977, tengenezo lilirekodi hotuba zaidi ya 350 katika mfululizo wenye kichwa, “Andiko Lote Ni Lenye Faida.” Nchini Marekani vituo vya redio 291, katika majimbo 48, vilirusha hewani hotuba hizo. Mwaka wa 1996, kituo cha redio huko Apia, mji mkuu wa Samoa, Pasifiki Kusini, kilikuwa na kipindi cha kila juma kilichoitwa “Maswali Yako ya Biblia Yajibiwa.”

18 Mwishoni mwa karne ya 20, redio haikuwa tena njia kuu ya kueneza habari njema. Hata hivyo, teknolojia nyingine ilitokea ambayo ilifanya iwe rahisi kuwafikia watu wengi zaidi.

19, 20. Kwa nini watu wa Yehova walianzisha Tovuti ya jw.org, na imekuwa na matokeo gani? (Ona pia sanduku “ JW.ORG.”)

19 Intaneti. Kufikia mwaka wa 2013, zaidi ya watu bilioni 2.7, yaani, karibu asilimia 40 ya watu ulimwenguni pote, walikuwa wameunganishwa na Intaneti. Kulingana na makadirio fulani, watu bilioni mbili hivi wanaweza kutumia Intaneti kupitia simu na kompyuta ndogo za mkononi. Idadi hiyo inaendelea kuongezeka ulimwenguni pote, lakini kwa sasa Afrika ndilo bara ambalo idadi ya watu wanaotumia Intaneti inaongezeka kwa kasi, kwa kuwa watu zaidi ya milioni 90 wana vifaa vinavyoweza kuunganishwa na Intaneti. Maendeleo hayo yamebadili kabisa namna watu wanavyopata habari.

20 Kuanzia mwaka wa 1997, watu wa Yehova walianza kutumia mbinu hiyo ya mawasiliano. Mwaka wa 2013, Tovuti ya jw.org ilipatikana katika lugha 300 hivi, na habari zinazotegemea Biblia zingeweza kupakuliwa katika zaidi ya lugha 520. Kila siku, zaidi ya watu 750,000 hutembelea tovuti hiyo. Isitoshe, kila mwezi, mbali na kutazama video, watu hupakua vitabu zaidi ya milioni 3, magazeti milioni 4, na rekodi za kusikiliza milioni 22.

21. Umejifunza nini kutokana na kisa cha Sina?

21 Tovuti hiyo imekuwa njia bora sana ya kueneza habari njema za Ufalme wa Mungu hata katika nchi ambazo kazi yetu imezuiliwa. Kwa mfano, mapema mwaka wa 2013, mwanaume anayeitwa Sina alitembelea tovuti ya jw.org na akapiga simu kwenye makao makuu yaliyoko Marekani, akiomba habari zaidi kuhusu Biblia. Kwa nini hilo halikuwa jambo la kawaida? Sina anatoka katika familia ya Waislamu na anaishi katika kijiji cha mbali katika nchi ambayo kazi ya Mashahidi wa Yehova imezuiliwa vikali. Matokeo ni kwamba mipango ilifanywa ili Sina ajifunze Biblia mara mbili kwa juma pamoja na Shahidi fulani huko Marekani. Funzo hilo lilifanywa kupitia huduma za video katika Intaneti.

Kumfundisha Mtu Mmoja-Mmoja

22, 23. (a) Je, mbinu zilizotumiwa kuwafikia watu wengi zaidi zimechukua mahali pa huduma ya mlango kwa mlango? (b) Mfalme amebariki jinsi gani jitihada zetu?

22 Mbinu zote ambazo tumetumia ili kuwafikia watu wengi zaidi, kama vile magazeti, sinema ya “Photo-Drama,” vipindi vya redio, na Tovuti, hazikukusudiwa zichukue mahali pa huduma ya mlango kwa mlango. Kwa nini? Kwa sababu watu wa Yehova wamejifunza kutokana na kielelezo kilichowekwa na Yesu. Yesu hakuhubiria umati pekee, bali alikazia fikira kumsaidia mtu mmoja-mmoja. (Luka 19:1-5) Yesu pia aliwazoeza wanafunzi wake kufanya vivyo hivyo, na akawapa ujumbe watakaohubiri. (Soma Luka 10:1, 8-11.) Kama tulivyojifunza kwenye Sura ya 6, sikuzote wale wanaoongoza wamewatia moyo watumishi wa Yehova wazungumze na watu ana kwa ana.—Matendo 5:42; 20:20.

23 Miaka mia moja baada ya Ufalme kuzaliwa, zaidi ya wahubiri milioni 7.9 wanashiriki kwa bidii kuwafundisha watu kuhusu makusudi ya Mungu. Pasipo shaka, Mfalme amebariki mbinu zote ambazo tumetumia kuutangaza Ufalme. Kama sura ifuatayo itakavyoonyesha, ametupatia pia vifaa tunavyohitaji ili kueneza habari njema kwa kila taifa, kabila, na lugha.—Ufu. 14:6.

^ fu. 17 Katika mwaka wa 1957, ndugu waliokuwa wakiongoza waliamua kufunga kituo cha redio cha WBBR huko New York. Hicho ndicho kituo kilichokuwa kimebaki.