Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA 7

Njia Mbalimbali Zilizotumiwa Ili Kuhubiri​—Kutumia Kila Njia Ili Kuhubiria Watu

Njia Mbalimbali Zilizotumiwa Ili Kuhubiri​—Kutumia Kila Njia Ili Kuhubiria Watu

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Watu wa Mungu wanatumia kila njia ili kuhubiria vikundi vikubwa vya watu kadiri inavyowezekana

1, 2. (a) Yesu alitumia ufundi gani ili kuhubiria watu wengi? (b) Namna gani wanafunzi wake waaminifu walifuata mufano wake, na sababu gani?

YESU anapatikana pembeni ya bahari na watu wengi wanamuzunguka. Anapanda katika mashua na anaomba wanafunzi wake wapeleke mashua hiyo mbali kidogo na inchi kavu. Sababu gani anafanya hivyo? Anajua kwamba kuwa juu ya maji kutaongeza sauti yake na kwa hiyo watu wengi wanaweza kusikia ujumbe wake vizuri zaidi.—Soma Marko 4:1, .

2 Katika miaka ya mbele ya kuzaliwa kwa Ufalme na kisha, wanafunzi waaminifu wa Kristo walifuata mufano wake. Walitumia ufundi mupya uliotokea ili kuhubiria vikundi vikubwa vya watu habari njema ya Ufalme. Kwa sababu wanaongozwa na Mufalme, watu wa Mungu wanaendelea kufanya upya njia zao za kuhubiri, wanapatanisha njia hizo na hali na pia wanatumia tekinolojia mupya kadiri inawezekana. Tunapenda watu wengi wasikie habari njema kadiri inawezekana mbele ya mwisho kuja. (Mt. 24:14) Kwa hiyo, acha sasa tuzungumuzie njia fulani ambazo tumetumia ili kuhubiria watu, hata kama wanaishi wapi. Wewe pia fikiria njia ambazo unaweza kutumia ili kuiga imani ya wale waliotangaza habari njema katika miaka ya mwanzo-mwanzo.

Kuhubiria Vikundi Vikubwa vya Watu

3. Sababu gani maadui wa ile kweli walikasirika kuhusu matumizi yetu ya magazeti ya ulimwengu?

3 Kutumia magazeti ya ulimwengu. Kuanzia mwaka wa 1879, Ndugu Russell na wenzake walikuwa wanachapisha gazeti Munara wa Mulinzi, ili kuhubiria watu wengi ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, miaka kumi mbele ya mwaka wa 1914, ilionekana kwamba Kristo alikuwa ameongoza mambo ili watu wengi zaidi wapate kusikia habari njema. Kuanzia mwaka wa 1903, matukio mbalimbali yalifuatana. Katika mwaka huo, Dr. Ephraim Llewellyn Eaton, musemaji wa kikundi cha mapastere wa Kiprotestanti katika Pennsylvania, aliomba kuwe na mabishano mbele ya watu wengi kati yake na Ndugu Charles Taze Russell juu ya mafundisho fulani ya Biblia. Katika barua ambayo alimuandikia Russell, Eaton aliandika hivi: “Nimefikiri kwamba mabishano mbele ya watu wengi juu ya mafundisho fulani ambayo wewe na mimi hatusikilizane . . . yatawapendeza sana watu wengi.” Russell na wenzake walifikiri pia kwamba watu wengi watapendezwa na jambo hilo. Kwa hiyo, walipanga kwamba mabishano hayo yachapishwe katika gazeti lenye kusifiwa sana, ni kusema, The Pittsburgh Gazette. Watu walipenda sana kusoma habari katika magazeti, na kwa sababu hotuba za Russell zilifasiria kweli ya Biblia kwa njia iliyo wazi na yenye kusadikisha sana, waandikaji wa magazeti waliomba kuandika hotuba za Russell na kuzitolea watu kila juma. Bila shaka, jambo hilo liliwakasirisha sana maadui wa ile kweli!

Kufikia mwaka wa 1914, magazeti ya ulimwengu zaidi ya 2000 yalikuwa yanachapisha hotuba za ndugu Russell

4, 5. Ndugu Russell alionyesha sifa gani, na namna gani ndugu walio na mamlaka katika tengenezo leo, wanaweza kumuiga?

4 Bila kukawia, magazeti mengi ya ulimwengu yalipenda kuandika hotuba za Russell. Katika mwaka wa 1908, gazeti Munara wa Mulinzi liliandika kwamba hotuba za ndugu Russell zilichapishwa “kwa ukawaida katika magazeti 11 ya ulimwengu.” Hata hivyo, ndugu ambao wanajua vizuri faida ya magazeti walimushauri ndugu Russell afikirie kuhamisha biro ya Sosaiti ambayo ilipatikana Pittsburgh na kuipeleka kwenye muji ambao unajulikana sana. Huko, magazeti mengi ya ulimwengu yangeweza kuandika habari mbalimbali zinazotegemea Biblia. Kisha kufikiria shauri hilo na mambo mengine, Russell alihamishia biro ya Sosaiti katika muji wa Brooklyn, New York, katika mwaka wa 1909. Matokeo yalikuwa namna gani? Kisha tu kuhama kwa miezi fulani, magazeti ya ulimwengu 400 hivi yalikuwa yanachapisha hotuba za ndugu Russell, na magazeti mengine yaliendelea kuongezwa kwenye hesabu hiyo. Kufikia wakati Ufalme ulianza kutawala katika mwaka wa 1914, magazeti ya ulimwengu zaidi ya 2000 katika luga ine yalikuwa yanachapisha hotuba za ndugu Russell na habari zingine zenye kutegemea Biblia!

5 Kwa sababu mambo yaliendelea vizuri hivyo, hilo linatupatia somo gani? Ndugu walio na mamlaka fulani katika tengenezo la Mungu leo, watafanya vizuri kuiga unyenyekevu wa ndugu Russell. Wakati wanataka kuchukua maamuzi mazito, ni vizuri wafikirie mashauri ya wengine.​—Soma Methali 15:22.

6. Namna gani mafundisho ya kweli ambayo yalichapishwa katika gazeti la ulimwengu yalimusaidia dada Ora?

6 Mafundisho ya kweli juu ya Ufalme, ambayo yalichapishwa katika magazeti hayo ya ulimwengu yalibadilisha maisha ya watu. (Ebr. 4:12) Tuchukue mufano wa dada Ora Hetzel, ambaye alibatizwa mwaka wa 1917, yeye ni mumoja wa watu wengi ambao walijifunza kweli kwa mara ya kwanza kupitia habari kama hizo zilizotolewa katika magazeti. Dada Ora anaeleza hivi: “Kisha kuolewa, nilienda kumutembelea mama yangu katika muji wa Rochester, Minnesota. Wakati nilifika, nilimukuta iko anakata kwenye gazeti habari ambazo ziliandikwa kwenye gazeti fulani la ulimwengu. Habari hizo zilikuwa ni hotuba za ndugu Russell. Mama yangu alinifasiria mambo aliyojifunza kupitia habari hizo.” Kuanzia hapo, dada Ora alikubali mafundisho ya kweli, na kwa miaka 60 hivi, aliendelea kuwa muhubiri mwaminifu wa Ufalme wa Mungu.

7. Ni sababu gani ziliwafanya ndugu waliokuwa wanaongoza wafikirie upya ikiwa wataendelea kutumia magazeti ya ulimwengu ili kutangaza habari njema?

7 Katika mwaka wa 1916, mambo mawili makubwa yaliwafanya ndugu waliokuwa wanaongoza wafikirie upya ikiwa wataendelea kutumia magazeti ya ulimwengu ili kutangaza habari njema. Jambo la kwanza ni kwamba Vita Kubwa ya Ulimwengu ilikuwa inawaka moto, na kwa hiyo, wachapishaji wa magazeti walikuwa na magumu ya kupata vyombo vya kazi wakati huo. Katika mwaka wa 1916, ripoti iliyotoka Uingereza kwenye biro yetu yenye kuangalia habari zetu ambazo zinachapishwa katika magazeti, ilionyesha magumu hayo kwa kusema hivi: “Kuna magazeti zaidi ya 30 tu ambayo yanachapisha Hotuba za Ndugu Russell kwa wakati huu. Inaonekana wazi kwamba hesabu hiyo itapunguka sana kwa sababu ya kupanda sana kwa bei ya karatasi.” Jambo la pili ilikuwa ni kifo cha Ndugu Russell kilichotokea tarehe 31 Mwezi wa 10, 1916. Kwa hiyo, gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 12, 1916, lilitangaza hivi: “Kwa sababu Ndugu Russell amekufa, hotuba [zilizokuwa zinachapishwa katika magazeti ya ulimwengu] hazitaendelea tena kuchapishwa.” Hata kama njia hiyo ya kuhubiri ilifikia mwisho, njia zingine, kama vile kutumia filme ya “Foto-Drama ya Uumbaji,” ziliendelea kuwa na matokeo mazuri.

8. Ni kazi gani ilifanyika ili kutayarisha filme ya “Foto-Drama ya Uumbaji”?

8 Kutumia filme. Ndugu Russell na wenzake walitumika karibu miaka tatu ili kutayarisha filme iliyoitwa “Foto-Drama ya Uumbaji,” ambayo ilianza kuonyeshwa mwaka wa 1914. (Met. 21:5) Foto-Drama hiyo, ilikuwa filme ya ufundi mupya ambayo ilikuwa na picha zenye kutikisika zilizoambatanishwa na sauti zilizorekodiwa, na ilitumia pia slaidi (vioo vidogo-vidogo) zenye picha za rangi ambazo zilichorwa kwa ufundi wa mikono na ambazo zilikuwa na picha ambazo hazitikisike. Ndugu wengi walicheza hadisi mbalimbali za Biblia na walipigwa picha ambazo zilitumiwa ili kutayarisha filme hiyo. Ilifanyika hivyo pia kwa wanyama. Ripoti fulani ya mwaka wa 1913 ilisema hivi: “Sehemu kubwa ya wanyama waliokuwa katika mashamba ya wanyama walipigwa picha ili kutokeza picha zenye kutikisika za wanyama na kufanyiza hivyo sehemu kubwa ya habari ya Noa.” Ni ndugu na dada wenye ufundi wa kuchora, wa Uingereza, Amerika, Paris na Philadelphie, ndio walitengeneza kwa mikono kila picha ya zile mamia ya picha zenye rangi ambazo zilichorwa kwenye slaidi na ambazo zilitumiwa kwa kuonyesha filme ya Foto-Drama ya Uumbaji.

9. Sababu gani ndugu walikubali kutumia feza nyingi na wakati mwingi ili kutayarisha filme ya “Foto-Drama”?

9 Sababu gani ndugu walikubali kutumia feza nyingi na wakati mwingi hivyo ili kutayarisha filme hiyo ya “Foto-Drama”? Azimio ambalo lilichukuliwa kwenye mikusanyiko iliyofuatana ya mwaka wa 1913 linatoa jibu. Azimio hilo lilisema hivi: “Magazeti ya Amerika yanatumia picha za kuchorwa na zenye kuchekesha ili kubadilisha mawazo ya watu, na jambo hilo linafanikiwa kwa namna ya ajabu. Kwa sababu picha hizo zenye kutikisika zinapendwa sana na watu na kwa sababu tunapaswa kujiambatanisha na hali, mambo hayo yameonyesha kwamba picha hizo ni za maana sana. Na kwa sababu sisi ni wahubiri wenye kusonga mbele na walimu wa madarasa [makutaniko] ya Biblia, tunaamini kwamba kutumia picha kama hizo zenye kutikisika na zenye kuchorwa kwenye slaidi itakuwa njia yenye kuzaa matunda na yenye kufaa kwetu sisi watangazaji wa injili na waalimu.”

Kuonyesha filme ya “Foto-Drama”

10. Filme ya “Foto-Drama” ilionyeshwa katika inchi gani mbalimbali?

10 Katika mwaka wa 1914, filme ya “Foto-Drama” ilionyeshwa katika miji 80 kila siku. Katika Amerika na Kanada, karibu watu milioni 8 waliona filme hiyo. Filme hiyohiyo ilionyeshwa katika Ujerumani, Australia, Danemark, Finlande, Nouvelle-Zélande, Norvège, Suède, Suisse, Uingereza. Foto-Drama iliyofupishwa, yenye hotuba iliyorekodiwa na muziki tu, na picha zenye hazitikisike, ilionyeshwa katika miji midogo-midogo. Filme hiyo iliyofupishwa iliitwa “Eureka Drama,” haikuomba feza nyingi ili kuitayarisha na ilikuwa mwepesi kubeba. Kufikia mwaka wa 1916, iwe “Foto-Drama” ao “Eureka Drama” ilikuwa imetafsiriwa katika luga ya Kifaransa, Kiarmenia, Kidanwa-Norvegia, Kijerumani, Kigiriki, Kiitalia, Kipolishi, Kihispania, na Kiswidi.

Katika mwaka wa 1914, filme “Foto-Drama” ilionyeshwa katika chumba chenye kujaa watu

11, 12. Filme ya “Foto-Drama” ilimusaidia namna gani kijana mumoja, na alituachia mufano gani muzuri?

11 “Foto-Drama” iliyotafsiriwa katika luga ya Kifaransa ilimusaidia sana kijana mumoja wa miaka 18 aliyeitwa Charles Rohner. Alisema hivi: “Ilionyeshwa katika muji wangu wa Colmar, Alsace, Ufaransa. Kuanzia mwanzo, nilishangaa sana kuona namna filme hiyo ilifundisha kweli ya Biblia kwa njia iliyo wazi kabisa.”

12 Matokeo ya jambo hilo ni kwamba Charles alibatizwa na katika mwaka wa 1922 alianza kazi ya utumishi wa wakati wote. Moja ya mugawo wake wa kwanza ilikuwa kusaidia kuonyesha filme “Foto-Drama” kwa vikundi vingi vya watu katika Ufaransa. Wakati Charles anazungumuza juu ya mugawo wake, yeye anasema hivi: “Nilikuwa na mugawo wa kazi mbalimbali: kucheza chombo cha muziki kinachoitwa fidla (violon), kuwa mutumishi anayeangalia mambo ya feza na vichapo. Nilipewa pia kazi ya kuwaambia watu wakae kimya mbele ya programu kuanza. Wakati wa kupumuzika, tulikuwa tunawatolea watu vichapo. Kila ndugu ao dada alipewa mugawo wa kugawanyia watu vichapo katika sehemu fulani ya jumba la kuonyeshea filme. Kila mumoja alikuwa na vichapo vingi katika mikono ili kumutolea kila mutu anayepatikana katika sehemu ambayo alipewa. Zaidi ya hilo, kwenye kila mulango wa jumba hilo, kulikuwa na meza zenye kujaa vichapo.” Katika mwaka wa 1925, Charles aliitwa kwenye Beteli ya Brooklyn, New York. Wakati alifika huko, alipewa daraka la kuongoza kikundi cha wapiga-muziki cha radio mupya ya WBBR. Kisha kufikiria mufano wa ndugu Charles, kila mumoja wetu anaweza kujiuliza hivi: ‘Mimi niko tayari kukubali kila mugawo ambao ninaweza kupewa ili kusaidia katika kutangaza ujumbe wa Ufalme?’—Soma Isaya 6:8.

13, 14. Namna gani radio ilitumiwa ili kutangaza habari njema? (Soma pia kisanduku “ Programu za Radio WBBR” na “ Mukusanyiko Ambao Utaendelea Kukumbukwa.”)

13 Kutumia radio. Katika mwaka wa 1920 mupaka mwaka wa 1930, kazi ya kutumia “Foto-Drama” ilianza kupunguka. Lakini matumizi ya radio ilitokea, na ilionekana kuwa njia ya maana ya kutangaza habari njema ya Ufalme. Tarehe 16 Mwezi wa 4, 1922, Ndugu Rutherford alitoa hotuba kwa njia ya radio katika Metropolitan Opera ya Philadelphia, Pennsylvania. Ilikuwa ni mara yake ya kwanza kufanya hivyo katika muji huo. Inasemekana kwamba watu 50 000 hivi, walisikiliza hotuba yake yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Hata Kidogo.” Kisha, katika mwaka wa 1923, programu ya mukusanyiko ilitolewa kwa njia ya radio kwa mara ya kwanza. Zaidi ya kutumia radio za kibiashara, ndugu waliokuwa wanaongoza waliamua kwamba ingekuwa jambo la hekima tuwe na kituo chetu wenyewe cha radio, ambacho kilijengwa Staten Island, New York, na kiliandikishwa kisheria kwa jina la WBBR. Radio hiyo ilianza kutangaza habari tarehe 24 Mwezi wa 2, 1924.

Katika mwaka wa 1922, ilisemekana kwamba watu 50000 hivi, walisikiliza kupitia radio hotuba iliyosema “Mamilioni ya Watu Wanaoishi Leo Hawatakufa Hata Kidogo”

14 Ili kufasiria kusudi la radio WBBR, gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 1 Mwezi wa 12, 1924, lilisema hivi: “Tunaamini kwamba radio ni njia isiyotumia feza nyingi na ni njia yenye matokeo mazuri ambayo hatujapata kutumia ili kutangaza ujumbe wa ile kweli.” Kisha gazeti hilo liliongeza hivi: “Ikiwa Bwana anaona kwamba inafaa tujenge vituo vingine vya radio ili kutangaza ile kweli, atatupatia feza kulingana na wema wake.” (Zab. 127:1) Kufikia mwaka wa 1926, watu wa Yehova walikuwa na vituo sita vya radio. Vituo viwili vilikuwa Amerika: radio WBBR katika New York na radio NENO karibu ya Chicago. Vituo vingine ine vilikuwa katika inchi ya Kanada: katika muji wa Alberta, wa British Columbia, wa Ontario, na wa Saskatchewan.

15, 16. (a) Katika Canada viongozi wa dini walifikia kufanya nini kuhusu matumizi yetu ya radio? (b) Namna gani hotuba ambazo zilitolewa kwa njia ya radio na kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba vilisaidiana?

15 Viongozi wa dini zinazojidai kuwa za Kikristo walitambua matumizi yetu ya radio ili kutangaza kweli ya Biblia. Ndugu Albert Hoffman, ambaye alizoea kazi iliyokuwa inafanywa kwa njia ya radio ya Saskatchewan, Kanada, alisema hivi: “Watu zaidi na zaidi walianza kujua Wanafunzi wa Biblia [leo Mashahidi wa Yehova]. Ushahidi mukubwa sana ulikuwa umetolewa mupaka mwaka wa 1928, wakati viongozi wa dini waliwachochea sana viongozi wa serikali na kufanya radio zote ambazo zinatumiwa na Wanafunzi wa Biblia katika Kanada kunyanganywa vikaratasi vyao vya serikali vinavyowaruhusu kutumia radio.”

16 Hata kama radio zetu katika Kanada zilifungwa, hotuba zenye kutegemea Biblia ziliendelea kutolewa kupitia radio za kibiashara. (Mt. 10:23) Ili kufanya programu za radio hizo ziwe na matokeo mazuri zaidi, gazeti Munara wa Mulinzi na gazeti L’Âge d’Or (leo Amuka!) yalionyesha liste ya radio za kibiashara ambazo zinatangaza ile kweli ya Biblia ili wahubiri wanaoenda nyumba kwa nyumba waweze kutia watu moyo wasikilize hotuba zenye kutegemea Biblia kupitia radio za mahali ambako wanaishi. Matokeo yalikuwa namna gani? Kichapo Le Bulletin cha Mwezi wa 1, 1931, kilisema hivi: “Kazi ya radio imekuwa kichocheo kabisa kwa ndugu katika kazi yao ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Ripoti nyingi ambazo zimetufikia kwenye biro zimeonyesha kwamba watu wanasikiliza hotuba za ndugu Rutherford kupita radio, na kwa sababu hiyo, wako tayari kabisa kukamata vitabu ambavyo tunawatolea.” Kichapo Le Bulletin kilifasiria kwamba kazi ya radio na kazi ya nyumba kwa nyumba ni “njia mbili kubwa za kuhubiri ambazo tengenezo la Bwana linatumia.”

17, 18. Hata ikiwa hali zilibadilika, namna gani radio iliendelea kufanya kazi?

17 Katika mwaka wa 1930 mupaka mwaka wa 1940, upinzani ulitokea ili kutukataza tusitumie radio za kibiashara. Kwa hiyo, mwisho wa mwaka wa 1937, watu wa Yehova walijipatanisha na hali ambazo zilikuwa zimebadilika. Waliachana na radio za kibiashara na walikazia zaidi mahubiri ya nyumba kwa nyumba. * Hata hivyo, radio iliendelea kufanya kazi ya maana sana ili kueneza ujumbe wa Ufalme katika maeneo fulani ya mbali ao maeneo ambayo ni vigumu kufikiwa kwa sababu ya hali za kisiasa za inchi. Kwa mufano, kuanzia mwaka wa 1951 mupaka mwaka wa 1991, radio iliyopatikana katika Berlin ya Mangaribi, Ujerumani, ilitangaza kwa ukawaida hotuba za Biblia. Kwa hiyo, wale walioishi katika maeneo ya Ujerumani ya Mashariki wangeweza kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Kuanzia mwaka wa 1961, kwa miaka zaidi ya 30, radio ya taifa la Suriname, Amerika ya Kusini, iliendelea kuwa na programu ya dakika 15 kila juma ili kutangaza mafundisho mbalimbali ya kweli ya Biblia. Kuanzia mwaka wa 1969 mupaka mwaka wa 1977, tengenezo lilitolea watu kwa njia ya radio programu zaidi ya 350 zilizorekodiwa. Habari hizo zilitolewa kwa mufululizo katika kichwa “Kila Andiko Linafaa.” Katika Amerika, radio 291, ambazo zilipatikana katika maeneo 48 (ambayo ni inchi ndogo-ndogo za Amerika), ziliendelea kutangaza programu hizo. Katika mwaka wa 1996, radio ya Apia, muji mukubwa wa inchi ya Pasifiki ya Kusini ya taifa la Samoa, ilitangaza kila juma programu iliyokuwa na kichwa “Maulizo Yako Juu ya Biblia Yanajibiwa.”

18 Wakati tulikaribia mwaka wa 2 000, radio haikukuwa tena chombo cha maana sana katika kutangaza habari njema. Ufundi mwingine wa kitekinolojia ulitokea ambao umefanya iwezekane kuwafikia watu wengi kuliko zamani.

19, 20. Sababu gani watumishi wa Yehova wana adresi ya Internete jw.org, na jambo hilo limekuwa na matokeo gani mazuri? (Soma pia kisanduku “ JW.ORG.”)

19 Internete. Katika mwaka wa 2013, watu karibu miliare 3, ni kusema, karibu watu 40 juu ya 100 katika dunia walitumia Internete. Inakadiriwa kwamba watu miliare 2 hivi, wanatumia vyombo kama vile telefone na vifaa vingine vyenye kuwa na Internete. Hesabu hiyo inaendelea kuongezeka, na ongezeko hilo ni kubwa zaidi katika Afrika ambako watu wanatumia sana Internete kupitia vyombo kama vile telefone. Afrika ina zaidi ya watu milioni 90 ambao wamefanya uandikisho ili kutumia Internete kwa njia ya telefone. Maendeleo hayo yamebadilisha kabisa njia ambayo watu wengi wanatumia ili kupata habari.

20 Kuanzia mwaka wa 1997, watu wa Yehova wameanza pia kutumia njia hiyo ya kupashana habari inayotumiwa na watu wengi. Katika mwaka wa 2013, adresi yetu ya Internete jw.org inapatikana katika luga 300 hivi, na habari zinazotegemea Biblia zimetiwa humo, ambazo watu wanaweza kuchukua katika luga zaidi ya 520. Kila siku, zaidi ya watu 750 000 wanafungua adresi yetu ya Internete. Zaidi ya kutazama video mbalimbali, kila mwezi watu wanapakua zaidi ya vitabu milioni 3, magazeti milioni 4, na nyimbo ao usomaji mwingi wa kusikiliza milioni 22.

21. Habari ya Sina imekufundisha nini?

21 Adresi yetu ya Internete imekuwa njia yenye matokeo sana ili kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu, hata katika inchi ambako kazi yetu inakatazwa. Kwa mufano, mwanzoni mwa mwaka wa 2013, mutu fulani anayeitwa Sina alipata adresi yetu jw.org na akaita kwa njia ya telefone ndugu kwenye makao makubwa yanayopatikana Amerika. Mutu huyo alikuwa anapenda kujua mengi juu ya Biblia. Sababu gani hilo lilikuwa jambo la ajabu? Sina amezaliwa katika familia ya Kiislamu na anaishi katika kijiji cha mbali sana katika inchi ambako kazi ya Mashahidi wa Yehova inakatazwa. Kwa sababu aliita, mipango ilichukuliwa ili Sina ajifunze Biblia mara mbili kwa juma na ndugu fulani wa Amerika. Funzo hilo liliongozwa kwa kutumia ufundi wa video kwenye Internete.

Kufundisha Kila Mutu Kipekee

22, 23. (a) Njia ambazo zimetumiwa ili kuhubiria vikundi vikubwa vya watu, zimechukua nafasi ya mahubiri ya nyumba kwa nyumba? (b) Namna gani Mufalme amebariki nguvu zetu?

22 Kati ya njia hizo ambazo tumetumia ili kuhubiria vikundi vikubwa vya watu, kama vile magazeti ya ulimwengu, filme ya “Foto-Drama,” programu za radio, na Internete, hakuna njia inayokusudiwa kuchukua nafasi ya mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Sababu gani tunasema hivyo? Kwa sababu watu wa Yehova wamejifunza kupitia mufano ambao Yesu alituachia. Yeye hakuhubiria tu vikundi vikubwa vya watu; alifikiria pia kumusaidia kila mutu kipekee. (Lu. 19:1-5) Yesu alizoeza pia wanafunzi wake kufanya hivyo, na aliwapatia ujumbe wa kuhubiria watu. (Soma Luka 10:1, 8-11.) Kama vile tulizungumuzia katika Sura ya 6, ndugu ambao walikuwa wanaongoza wakati huo, waliendelea kutia moyo kila mutumishi wa Yehova kuzungumuza na kila mutu kipekee.—Mdo. 5:42; 20:20.

23 Kisha miaka 100 tangu kuzaliwa kwa Ufalme, wahubiri zaidi ya milioni 7 na nusu wanafanya kazi ya kufundisha wengine makusudi ya Mungu kwa bidii. Bila shaka, Mufalme amebariki njia mbalimbali ambazo tumetumia ili kutangaza Ufalme. Kama vile sura inayofuata itaonyesha, Mufalme ametupatia pia vyombo tunavyohitaji ili kutangaza habari njema kwa kila taifa, kabila, na luga.—Ufu. 14:6.

^ fu. 17 Katika mwaka wa 1957, ndugu ambao walikuwa wanaongoza waliamua kufunga kituo cha mwisho cha vituo vya radio ya WBBR katika New York.