Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 8

Vifaa vya Kutusaidia Kuhubiri​—Kuchapisha Machapisho kwa Ajili ya Watu Ulimwenguni Pote

Vifaa vya Kutusaidia Kuhubiri​—Kuchapisha Machapisho kwa Ajili ya Watu Ulimwenguni Pote

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Yehova anaendelea kutupatia vifaa tunavyohitaji ili kuwafundisha watu kutoka kila taifa, kabila, na lugha

1, 2. (a) Katika karne ya kwanza, ni nini kilichosaidia kueneza habari njema katika Milki yote ya Roma? (b) Tuna uthibitisho gani unaoonyesha kwamba Yehova anatuunga mkono? (Ona pia sanduku “ Habari Njema Katika Lugha Zaidi ya 670.”)

WATU waliotembelea Yerusalemu hawakuamini kile walichokuwa wakisikia. Wagalilaya walikuwa wakizungumza kwa ufasaha lugha za kigeni, na ujumbe waliokuwa wakitangaza uliwavutia wasikilizaji wao. Ilikuwa Pentekoste 33 W.K., na wanafunzi walikuwa wamepokea kimuujiza zawadi ya kuzungumza katika lugha mbalimbali, jambo hilo lilithibitisha kwamba Mungu alikuwa akiwaunga mkono. (Soma Matendo 2:1-8, 12, 15-17.) Habari njema ambazo walihubiri siku hiyo ziliwafikia watu wa malezi mbalimbali na baadaye zilisambaa katika Milki yote ya Roma.—Kol. 1:23.

2 Leo, watumishi wa Mungu hawazungumzi kimuujiza lugha mbalimbali. Hata hivyo, wanahubiri katika lugha nyingi zaidi kuliko ilivyokuwa katika karne ya kwanza kwa kuwa wanatafsiri ujumbe wa Ufalme katika lugha zaidi ya 670. (Mdo. 2:9-11) Watu wa Mungu wamechapisha machapisho mengi sana na katika lugha nyingi sana hivi kwamba ujumbe wa Ufalme umepenya katika kila pembe ya dunia. * Huo pia ni uthibitisho wa kutosha kwamba Yehova anamtumia Mfalme Yesu Kristo kuelekeza kazi yetu ya kuhubiri. (Mt. 28:19, 20) Tunapopitia baadhi ya vifaa ambavyo tumetumia kutimiza kazi hii katika miaka 100 iliyopita, ona jinsi ambavyo Mfalme ametuzoeza hatua kwa hatua tupendezwe na watu na kutuchochea tuwe walimu wa Neno la Mungu.—2 Tim. 2:2.

Mfalme Anawapa Watumishi Wake Vifaa vya Kupandia Mbegu za Kweli

3. Kwa nini tunatumia vifaa mbalimbali katika kazi yetu ya kuhubiri?

3 Yesu alilinganisha “neno la ufalme” na mbegu, na moyo wa mtu akaulinganisha na udongo. (Mt. 13:18, 19) Kama vile mkulima anavyoweza kutumia vifaa mbalimbali kulainisha udongo na kuutayarisha ili aweze kupanda mbegu, watu wa Yehova wametumia vifaa mbalimbali ambavyo vimewasaidia kutayarisha mioyo ya mamilioni ya watu kukubali ujumbe wa Ufalme. Baadhi ya vifaa hivyo vilitumiwa kwa muda mfupi. Vifaa vingine, kama vile vitabu na magazeti vinaendelea kufanya kazi muhimu. Tofauti na mbinu nyingi za mawasiliano zilizotajwa katika sura iliyotangulia, vifaa vyote vinavyozungumziwa hapa vimewasaidia wahubiri wa Ufalme kuzungumza na watu uso kwa uso.—Mdo. 5:42; 17:2, 3.

Karakana ya kutengeneza gramafoni na vifaa vya sauti, Toronto, Kanada

4, 5. Hotuba zilizorekodiwa zilitumiwaje, lakini zilikuwa na upungufu gani?

4 Hotuba zilizorekodiwa. Katika miaka ya 1930 hadi miaka ya 1940, wahubiri walitumia hotuba za Biblia zilizorekodiwa ambazo zilichezwa kwenye gramafoni. Kila rekodi ilicheza kwa muda usiozidi dakika tano. Nyakati nyingine rekodi hizo zilikuwa na vichwa vifupi, kama vile “Utatu,” “Toharani,” na “Ufalme.” Rekodi hizo zilitumiwaje? Ndugu Clayton Woodworth, Jr., aliyebatizwa mwaka wa 1930 nchini Marekani, alisema hivi: “Nilibeba gramafoni iliyokuwa ndani ya sanduku dogo, ilikuwa na springi iliyokazwa, pia ilikuwa na kifaa fulani chenye sindano kwenye ncha ambacho kingeweza kung’olewa na kurudishwa, kifaa hicho kilipaswa kuwekwa mahali panapofaa kwenye santuri ili iweze kucheza vizuri. Nilipokaribia mlango fulani, ningefungua sanduku na kuweka kifaa hicho chenye sindano juu ya santuri, kisha ningepiga hodi. Mwenye nyumba akifungua mlango, ningesema hivi, ‘Nina ujumbe muhimu ambao ningependa usikie.’” Waliitikiaje? Ndugu Woodworth, anasema, “Mara nyingi watu walikubali kusikiliza ujumbe huo. Nyakati nyingine, walikataa na kufunga mlango. Na mara chache, walifikiri nilikuwa nikiuza gramafoni.”

Kufikia mwaka wa 1940, zaidi ya hotuba 90 zilikuwa zimerekodiwa na zaidi ya santuri milioni moja zilikuwa zimetengenezwa

5 Kufikia mwaka wa 1940, zaidi ya hotuba 90 zilikuwa zimerekodiwa na santuri zaidi ya milioni moja zilikuwa zimetengenezwa. John E. Barr, ambaye alikuwa painia nchini Uingereza wakati huo na baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema hivi: “Katika miaka ya 1936 hadi 1945, gramafoni ilikuwa mwandamani wangu wa kawaida. Kwa kweli, siku hizo ningejihisi mpweke ikiwa nisingekuwa nayo. Ilitia sana moyo kusikia sauti ya Ndugu Rutherford mlangoni, ungehisi ni kana kwamba yupo pamoja nawe. Hata hivyo, gramafoni haingeweza kufundisha watu kwa njia inayofaa kwa kuwa haingeweza kugusa mioyo ya watu.”

6, 7. (a) Kadi za ushuhuda zilikuwa na manufaa na upungufu gani? (b) Ni katika njia gani Yehova ‘ameweka maneno katika vinywa vyetu’?

6 Kadi za ushuhuda. Kuanzia mwaka wa 1933, wahubiri walitiwa moyo kutumia kadi za ushuhuda wanapohubiri mlango kwa mlango. Kadi ya ushuhuda ilikuwa na ukubwa wa sentimeta 7.6 kwa sentimeta 12.7. Ilikuwa na ujumbe mfupi wa Biblia na maelezo kuhusu machapisho yanayotegemea Biblia ambayo mwenye nyumba angeweza kupata. Mhubiri angempa mwenye nyumba kadi hiyo na kumwomba aisome. “Nilifurahia kutumia kadi ya ushuhuda katika huduma,” akasema Lilian Kammerud, ambaye baadaye alitumikia akiwa mmishonari nchini Puerto Riko na Argentina. Kwa nini alifurahia? Alisema hivi: “Wengi wetu hatungeweza kutoa utangulizi mzuri. Hivyo ilinisaidia kujua jinsi ya kuwafikia watu.”

Kadi ya ushuhuda (Kiitaliano)

7 Ndugu David Reusch, ambaye alibatizwa mwaka wa 1918, alisema hivi, “Kadi za ushuhuda ziliwasaidia akina ndugu kwa kuwa wengi wao walihisi hawangeweza kutoa ujumbe kwa njia inayofaa.” Hata hivyo, kifaa hicho kilikuwa na upungufu wake. Ndugu Reusch alieleza hivi: “Nyakati nyingine watu walidhani kwamba hatuwezi kusema. Kwa njia fulani, wengi wetu hatukuwa na uwezo wa kuongea. Lakini Yehova alikuwa akitutayarisha ili tuwahubirie watu tukiwa wahudumu wake. Hivi karibuni angetia maneno yake katika vinywa vyetu kwa kutufundisha jinsi ya kutumia Maandiko mlangoni. Yehova alitimiza hilo kupitia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ambayo ilianza katika miaka ya 1940.”—Soma Yeremia 1:6-9.

8. Unaweza kumruhusu Kristo akuzoeze kwa njia gani?

8 Vitabu. Tangu mwaka wa 1914, watu wa Yehova wamechapisha vitabu mbalimbali zaidi ya 100 vinavyozungumzia Biblia. Baadhi ya vitabu hivyo viliandikwa hasa ili kuwazoeza wahubiri wawe wahudumu stadi. Anna Larsen, anayeishi Denmark, ambaye amekuwa mhubiri kwa miaka 70 hivi, anasema: “Yehova alitusaidia tuwe wahubiri stadi kupitia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na vitabu vilivyotumiwa katika shule hiyo. Nakumbuka kitabu cha kwanza kuchapishwa kwa kusudi hilo kilikuwa Theocratic Aid to Kingdom Publishers (Msaada wa Kitheokrasi kwa Wahubiri wa Ufalme) kilichotolewa katika mwaka wa 1945. Kisha katika mwaka wa 1946 kitabu “Equipped for Every Good Work,” (Tumeandaliwa kwa Ajili ya Kila Kazi Njema) kikachapishwa. Sasa tunatumia kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kilichochapishwa mwaka wa 2001.” Kwa kweli, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na vitabu hivyo vimetusaidia sana kwa kuwa Yehova “ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu.” (2 Kor. 3:5, 6) Je, umejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Je, unabeba kitabu Shule ya Huduma kwenye mkutano kila juma na kufuatana na mwangalizi wa shule anapokirejelea? Ikiwa unafanya hivyo, utakuwa unamruhusu Kristo akuzoeze kuwa mwalimu bora.—2 Kor. 9:6; 2 Tim. 2:15.

9, 10. Vitabu vimetimiza sehemu gani katika kazi ya kupanda na kumwagilia maji mbegu za kweli?

9 Yehova ametusaidia pia kwa kuliongoza tengenezo lake lichapishe vitabu ambavyo vinawasaidia wahubiri kufafanua mafundisho ya msingi ya Biblia. Kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele kilikuwa na matokeo mazuri sana. Kilichapishwa kwa mara ya kwanza katika mwaka wa 1968 na kikawavutia watu wengi. Huduma ya Ufalme ya Novemba 1968 ilisema hivi: “Kuna uhitaji mkubwa sana wa kitabu Kweli hivi kwamba katika mwezi wa Septemba kiwanda cha Sosaiti huko Brooklyn kiliongeza zamu moja ya usiku.” Huduma hiyo iliendelea kusema hivi: “Pindi fulani mwezi wa Agosti idadi ya vitabu vilivyohitajiwa ilizidi vile vilivyokuwa akibani kwa zaidi ya nakala milioni moja na nusu!” Kufikia mwaka wa 1982, nakala zaidi ya milioni 100 za kitabu hicho zilikuwa zimechapishwa katika lugha 116. Kwa miaka 14, tangu mwaka wa 1968 hadi mwaka wa 1982, kitabu Kweli kilisaidia kuwe na ongezeko la wahubiri wa Ufalme zaidi ya milioni moja. *

10 Kitabu kingine cha kujifunzia Biblia ambacho kimekuwa na matokeo mazuri, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilitolewa katika mwaka wa 2005. Tayari nakala milioni 200 hivi zimechapishwa katika lugha 256! Kumekuwa na matokeo gani? Katika kipindi cha miaka saba tu, kuanzia mwaka wa 2005 hadi 2012, watu milioni 1.2 wamekuwa wahubiri wa habari njema. Katika kipindi hichohicho, idadi ya watu tunaowafundisha Biblia imeongezeka kutoka milioni 6 hivi hadi zaidi ya milioni 8.7. Pasipo shaka, Yehova anabariki jitihada zetu za kupanda na kumwagilia maji mbegu za kweli ya Ufalme.—Soma 1 Wakorintho 3:6, 7.

11, 12. Kulingana na maandiko yaliyoonyeshwa, magazeti yetu yalikusudiwa kuwafikia watu gani?

11 Magazeti. Mwanzoni, gazeti Mnara wa Mlinzi liliandikwa hasa kwa ajili ya “kundi dogo,” wale walio na “mwito wa mbinguni.” (Luka 12:32; Ebr. 3:1) Oktoba 1, 1919, tengenezo la Yehova lilitoa gazeti lingine, ambalo lilikusudiwa kuwavutia wasomaji tofauti, yaani, watu wote. Gazeti hilo lilikuja kupendwa sana na Wanafunzi wa Biblia na watu wote hivi kwamba kwa miaka mingi lilisambazwa sana kuliko gazeti Mnara wa Mlinzi. Lilipoanza kuchapishwa gazeti hilo liliitwa The Golden Age. Katika mwaka wa 1937, jina hilo lilibadilishwa na kuwa Consolation. Kisha, katika mwaka wa 1946, lilianza kujulikana kama Amkeni!

12 Kwa makumi ya miaka, mtindo na muundo wa gazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! umebadilika, lakini kusudi lake ni lilelile, yaani, kuutangaza Ufalme wa Mungu na kujenga imani katika Biblia. Leo, Mnara wa Mlinzi linachapishwa katika matoleo mawili—toleo la funzo na toleo la watu wote. Toleo la funzo limeandaliwa kwa ajili ya “watumishi wa nyumbani,” yaani, “kundi ndogo” na wale “kondoo wengine.” * (Mt. 24:45; Yoh. 10:16) Toleo la watu wote limeandaliwa hasa kwa ajili ya wale ambao bado hawajui kweli lakini wanamheshimu Mungu na Biblia. (Mdo. 13:16) Amkeni! hukazia fikira wale ambao hawajui mengi kuhusu Biblia na Mungu wa kweli, Yehova.—Mdo. 17:22, 23.

13. Unaona jambo gani lenye kutokeza kuhusu magazeti yetu? (Zungumzia chati “ Machapisho Yaliyovunja Rekodi za Ulimwengu.”)

13 Kufikia mwanzoni mwa mwaka wa 2014, kila mwezi zaidi ya nakala milioni 44 za Amkeni! na milioni 46 hivi za Mnara wa Mlinzi zilichapishwa. Amkeni! lilitafsiriwa katika lugha 100 hivi, na Mnara wa Mlinzi, katika zaidi ya lugha 200, na hilo lilifanya yawe magazeti yanayotafsiriwa na kusambazwa kwa wingi zaidi ulimwenguni pote! Mafanikio hayo hayapaswi kutushangaza. Magazeti hayo yana ujumbe ambao Yesu alisema ungehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.—Mt. 24:14.

14. Ni jitihada gani ambazo tumefanya, na kwa nini?

14 Biblia. Katika mwaka wa 1896, Ndugu Russell na washiriki wenzake walibadili jina la shirika walilotumia kuchapisha machapisho ili jina Biblia litiwe ndani, hivyo shirika hilo likaja kujulikana kama Watch Tower Bible and Tract Society. Badiliko hilo lilifaa kwa sababu sikuzote Biblia imekuwa kifaa kikuu kinachotumiwa kueneza habari njema kuhusu Ufalme. (Luka 24:27) Kupatana na jina la kisheria la shirika hilo, watumishi wa Mungu wamejitahidi sana kusambaza Biblia na kuwatia moyo watu waisome. Kwa mfano, katika mwaka wa 1926, Tafsiri ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ya The Emphatic Diaglott, ya Benjamin Wilson ilichapishwa katika viwanda vyetu vya uchapishaji. Kuanzia mwaka wa 1942, tulichapisha na kusambaza nakala 700,000 hivi za Biblia nzima ya King James Version. Miaka miwili tu baadaye, tulianza kuchapisha tafsiri ya American Standard Version, ambayo hutumia jina la Yehova mara 6,823. Kufikia mwaka wa 1950, tulikuwa tumesambaza zaidi ya nakala 250,000.

15, 16. (a) Kwa nini unaithamini Tafsiri ya Ulimwengu Mpya? (Zungumzia sanduku “ Kuharakisha Kazi ya Kutafsiri Biblia.”) (b) Unawezaje kumruhusu Yehova aguse moyo wako?

15 Katika mwaka wa 1950, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikiwa nzima ilitolewa katika buku moja mwaka wa 1961. Tafsiri hiyo humheshimu Yehova kwa kulirudisha jina lake mahali ambapo lilipatikana katika maandishi ya awali ya Kiebrania. Pia, jina la Mungu linapatikana mara 237 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Ili kuhakikisha kwamba ni sahihi na inasomeka kwa urahisi, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imefanyiwa marekebisho mara nyingi, na marekebisho ya karibuni zaidi yalifanywa mwaka wa 2013. Kufikia mwaka wa 2013, zaidi ya nakala milioni 201 za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya zilikuwa zimechapishwa ikiwa nzima au sehemu katika lugha 121.

16 Watu wameitikiaje wanapoipata Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha yao? Mwanaume fulani anayeishi nchini Nepal alisema hivi: “Watu wengi walisema kwamba ilikuwa vigumu kuielewa tafsiri ya zamani ya Kinepali kwa sababu ilitumia lugha ngumu. Lakini sasa tunaweza kuielewa Biblia vizuri sana kwa sababu inatumia lugha ya kawaida.” Alipoanza kusoma tafsiri ya Kisango, mwanamke mmoja katika Jamhuri ya Afrika ya Kati alianza kulia na kusema, “Hii ndiyo lugha inayogusa moyo wangu.” Kama mwanamke huyo, kila mmoja wetu anaweza kumruhusu Yehova aguse moyo wake kwa kusoma Neno lake kila siku.—Zab. 1:2; Mt. 22:36, 37.

Kuthamini Vifaa na Mazoezi Ambayo Tumepata

17. Unaweza kuonyeshaje kwamba unathamini vifaa na mazoezi unayopata, na utapata matokeo gani ukifanya hivyo?

17 Je, unathamini vifaa na mazoezi ambayo Mfalme Yesu Kristo ametupatia hatua kwa hatua? Je, unatenga wakati wa kusoma machapisho ambayo yametolewa na tengenezo la Mungu, na je, unayatumia kuwasaidia wengine? Ikiwa unafanya hivyo, utaelewa hisia za Dada Opal Betler, ambaye alibatizwa Oktoba 4, 1914. Opal alisema hivi: “Katika miaka yote, mimi na mume wangu [Edward] tulitumia gramafoni na kadi za ushuhuda. Tulihubiri nyumba kwa nyumba tukitumia vitabu, vijitabu, na magazeti. Tulishiriki katika kampeni za kuhubiri na maandamano ya kutangaza habari, na kusambaza trakti. Baadaye tulizoezwa kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia katika nyumba za watu wanaopendezwa. Tumekuwa na maisha yenye shughuli nyingi na yenye furaha.” Yesu aliahidi kwamba raia wake wangekuwa na kazi nyingi ya kupanda, kuvuna, na kushangilia pamoja. Opal na wengine wengi wamethibitisha maneno hayo kuwa kweli.—Soma Yohana 4:35, 36.

18. Tuna pendeleo gani?

18 Huenda watu wengi ambao kwa sasa si watumishi wa Mfalme wakawaona watu wa Mungu kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Mdo. 4:13) Lakini hebu fikiria! Mfalme amewafanya watu wake ambao wanaonekana kuwa wa kawaida wawe na uwezo mkubwa sana wa kuchapisha machapisho mengi sana. Baadhi ya machapisho hayo yametafsiriwa na kusambazwa kwa wingi sana ulimwenguni! Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba ametuzoeza na kutuchochea kutumia vifaa hivyo kueneza habari njema kwa watu wa mataifa yote. Ni pendeleo kubwa sana kushirikiana pamoja na Kristo katika kazi ya kupanda mbegu za kweli na kukusanya wanafunzi!

^ fu. 2 Katika miaka kumi tu iliyopita, watu wa Yehova wamechapisha machapisho yanayotegemea Biblia zaidi ya bilioni 20. Isitoshe, Tovuti yetu, jw.org, sasa inatembelewa na zaidi ya watu bilioni 2.7 ulimwenguni pote wanaotumia Intaneti.

^ fu. 9 Machapisho mengine yanayotegemea Biblia ambayo yamewasaidia wahubiri kufundisha kweli ya Biblia ni The Harp of God (kilichochapishwa mwaka wa 1921), “Let God Be True” (kilichochapishwa mwaka wa 1946), Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani (kilichochapishwa mwaka wa 1982), na Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele (kilichochapishwa mwaka wa 1995).

^ fu. 12 Ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2013, ukurasa wa 23, fungu la 13, linalozungumzia uelewaji mpya kuhusu wale wanaofanyiza “watumishi wa nyumbani.”