Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 9

Matokeo ya Kuhubiri​—“Mashamba . . . Ni Meupe kwa Ajili ya Kuvunwa”

Matokeo ya Kuhubiri​—“Mashamba . . . Ni Meupe kwa Ajili ya Kuvunwa”

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Yehova amekuza mbegu za kweli ya Ufalme

1, 2. (a) Kwa nini wanafunzi wanashangaa? (b) Yesu anazungumza kuhusu mavuno gani?

WANAFUNZI wanashangaa. Yesu amewaambia hivi: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” Wanatazama upande ambao Yesu anawaonyesha, lakini hawaoni mashamba meupe, bali ya kijani—rangi ya shayiri zilizoanza tu kumea. Labda wanajiuliza, ‘Anazungumzia mavuno gani?’ Kwani ‘itapita miezi kadhaa kabla ya mavuno kuanza.’—Yoh. 4: 35.

2 Hata hivyo, Yesu hazungumzi kuhusu mavuno halisi. Badala yake, anatumia nafasi hiyo kuwafundisha wanafunzi wake mambo mawili muhimu kuhusu mavuno ya kiroho, yaani, kuvuna watu. Ni mambo gani hayo? Ili kupata jibu la swali hilo, acheni tuchunguze simulizi hilo kwa kina zaidi.

Wachochewa Kutenda na Wanaahidiwa Shangwe

3. (a) Ni nini ambacho huenda kilimfanya Yesu aseme: “Mashamba . . . ni meupe kwa ajili ya kuvunwa”? (Ona maelezo ya chini.) (b) Yesu alifafanuaje maneno yake?

3 Mazungumzo ya Yesu na wanafunzi wake yalifanyika mwishoni mwa mwaka wa 30 W.K., karibu na mji wa Samaria ulioitwa Sikari. Wanafunzi wake walipokuwa katika mji huo, Yesu alibaki nyuma kwenye kisima fulani ambako alimweleza mwanamke mmoja kweli za kiroho, na mwanamke huyo alielewa mara moja umuhimu wa mafundisho ya Yesu. Wanafunzi wa Yesu waliporudi, mwanamke huyo alifanya haraka kwenda Sikari ili akawaambie jirani zake mambo yenye kustaajabisha aliyokuwa amejifunza. Ripoti yake iliamsha upendezi mkubwa, na majirani wake wengi walifanya haraka kwenda katika kisima hicho ili wakamwone Yesu. Huenda ni katika pindi hiyo—Yesu alipotazama mbali kwenye mashamba na kuona umati wa Wasamaria ukija—alisema: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” * Kisha, ili kufafanua kwamba hakumaanisha mavuno halisi, bali mavuno ya kiroho, Yesu aliongezea hivi: ‘Mvunaji . . . anakusanya matunda kwa ajili ya uzima wa milele.’—Yoh. 4:5-30, 36.

4. (a) Yesu alifundisha mambo gani mawili kuhusu mavuno? (b) Tutachunguza maswali gani?

4 Yesu alifundisha mambo gani mawili muhimu kuhusu mavuno ya kiroho? Jambo la kwanza, kazi hiyo inapaswa kufanywa haraka. Maneno yake “mashamba . . . ni meupe kwa ajili ya kuvunwa” yalikusudiwa kuwachochea wafuasi wake kutenda. Ili kukazia kwamba wanafunzi wake wanapaswa kutenda kwa uharaka, Yesu aliongezea hivi: “Tayari mvunaji anapokea mshahara.” Naam, tayari mavuno yalikuwa yameanza na hakukuwa na wakati wa kukawia! Jambo la pili, wafanyakazi ni wenye shangwe. Yesu alisema wapandaji na wavunaji ‘watashangilia pamoja.’ (Yoh. 4:35b, 36) Kama vile Yesu alivyoshangilia alipoona kwamba “wengi wa Wasamaria . . . walimwamini,” ndivyo pia wanafunzi wake wangepata shangwe kubwa wakifanya kazi ya kuvuna kwa nafsi yote. (Yoh. 4:39-42) Kisa hicho kilichotokea katika karne ya kwanza kina umuhimu mkubwa sana kwetu kwa sababu kinaonyesha mambo yanayotokea leo wakati wa yale mavuno makubwa sana ya kiroho. Mavuno hayo ya siku za kisasa yalianza lini? Ni nani wanaoshiriki katika mavuno hayo? Kumekuwa na matokeo gani?

Mfalme Wetu Anaongoza Katika Mavuno Makubwa Sana

5. Ni nani anayeongoza katika kazi ya mavuno ya ulimwenguni pote, na maono ya Yohana yanaonyeshaje kwamba kazi hiyo inapaswa kufanywa haraka?

5 Katika maono ya mtume Yohana, Yehova anafunua kwamba alimpa Yesu mgawo wa kuongoza katika kazi ya kuvuna watu ulimwenguni pote. (Soma Ufunuo 14:14-16.) Katika maono hayo, Yesu anatajwa akiwa na taji na mundu. “Taji la dhahabu juu ya kichwa [cha Yesu]” linaonyesha kwamba yeye ni Mfalme anayetawala. “Mundu mkali mkononi mwake” unaonyesha jukumu lake akiwa Mvunaji. Yehova anakazia kwamba kazi hiyo inapaswa kufanywa haraka, anaposema hivi kupitia malaika: “Mavuno ya dunia yameiva kabisa.” Kwa kweli, “saa imekuja ya kuvuna” na hakuna wakati wa kukawia! Kwa kutii amri ya Mungu, Yesu ‘anatia ndani mundu wake,’ nayo dunia inavunwa, yaani, watu wa dunia wanavunwa. Maono hayo yenye kusisimua yanatukumbusha tena kwamba “mashamba . . . ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” Je, maono hayo yanatusaidia kutambua mavuno hayo ya ulimwenguni pote yalianza lini? Ndiyo!

6. (a) “Majira ya mavuno” yalianza lini? (b) “Mavuno ya dunia” yalianza lini? Fafanua.

6 Kwa kuwa maono ya Yohana kwenye Ufunuo sura ya 14 yanamwonyesha Yesu, Mvunaji, akiwa amevaa taji (mstari wa 14), hivyo basi tayari alikuwa amewekwa rasmi kuwa Mfalme katika mwaka wa 1914. (Dan. 7:13, 14) Muda fulani baada ya hapo, Yesu anaamriwa aanze kuvuna (mstari wa 15). Mfuatano huo wa matukio unaonekana katika mfano wa Yesu kuhusu mavuno ya ngano, ambapo anasema: “Mavuno ni umalizio wa mfumo wa mambo.” Hivyo, matukio yote mawili, yaani, majira ya mavuno na umalizio wa mfumo huu wa mambo yalianza wakati uleule, mwaka wa 1914. Baadaye “katika majira ya mavuno,” uvunaji wa ngano ulianza. (Mt. 13:30, 39) Leo, kwa kuwa tunajua yaliyotukia huko nyuma, tunaweza kuona kwamba mavuno yalianza miaka kadhaa baada ya Yesu kuanza kutawala akiwa Mfalme. Kwanza, kuanzia mwaka wa 1914 hadi mwanzoni mwa mwaka wa 1919, Yesu alifanya kazi ya kuwasafisha wafuasi wake watiwa-mafuta. (Mal. 3:1-3; 1 Pet. 4:17) Kisha, katika mwaka wa 1919, “mavuno ya dunia” yakaanza. Bila kukawia, Yesu alimtumia mtumwa mwaminifu aliyewekwa rasmi karibuni ili awasaidie ndugu zetu waone uharaka wa kazi ya kuhubiri. Fikiria yale yaliyotokea.

7. (a) Ni uchunguzi gani uliowasaidia ndugu zetu kuona uharaka wa kazi ya kuhubiri? (b) Ndugu zetu walitiwa moyo wafanye nini?

7 Mnamo Julai 1920, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema hivi: “Baada ya kuchunguza Maandiko imeonekana wazi kwamba kanisa limepewa pendeleo kubwa la kutangaza ujumbe kuhusu ufalme.” Kwa mfano, maneno ya kinabii ya Isaya yaliwasaidia akina ndugu waone kwamba habari za Ufalme zilipaswa kutangazwa ulimwenguni pote. (Isa. 49:6; 52:7; 61:1-3) Hawakujua jinsi ambavyo kazi hiyo ingetimizwa, lakini waliamini kwamba Yehova angewafungulia njia. (Soma Isaya 59:1.) Kwa sababu ya uelewaji huo ulio wazi kuhusu uharaka wa kazi ya kuhubiri, ndugu zetu walitiwa moyo waongeze bidii yao ya kuhubiri. Akina ndugu waliitikiaje?

8. Katika mwaka wa 1921, ndugu zetu walielewa mambo gani mawili kuhusu kazi ya kuhubiri?

8 Mnamo Desemba 1921, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema hivi: “Umekuwa mwaka wenye matokeo sana kuliko yote; na idadi kubwa sana ya watu imesikia ujumbe wa kweli katika mwaka wa 1921 kuliko miaka mingine iliyopita.” Gazeti hilo liliongezea: “Bado kuna mengi ya kufanya. . . . Acheni tuyafanye tukiwa na moyo wenye shangwe.” Ona kwamba akina ndugu walielewa mambo mawili muhimu kuhusu kazi ya kuhubiri ambayo Yesu alikuwa ameyakazia kwa mitume wake: Kazi inapaswa kufanywa haraka, na wafanyakazi ni wenye shangwe.

9. (a) Katika mwaka wa 1954, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema nini kuhusu kazi ya mavuno, na kwa nini? (b) Kumekuwa na ongezeko gani la wahubiri ulimwenguni pote katika kipindi cha miaka 50 iliyopita? (Ona chati “ Ongezeko la Ulimwenguni Pote.”)

9 Katika miaka ya 1930, baada ya akina ndugu kuelewa kwamba umati mkubwa wa kondoo wengine ungekubali ujumbe wa Ufalme, kazi ya kuhubiri ikaongezeka zaidi. (Isa. 55:5; Yoh. 10:16; Ufu. 7:9) Kukawa na matokeo gani? Idadi ya wale wanaohubiri ujumbe wa Ufalme ikaongezeka kutoka watu 41,000 katika mwaka wa 1934 hadi 500,000 katika mwaka wa 1953! Gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1954, lilikata shauri hili: “Ni roho ya Yehova na nguvu za Neno lake zimetimiza kazi hii kubwa sana ya mavuno inayofanywa ulimwenguni pote.” *Zek. 4:6.

ONGEZEKO LA ULIMWENGUNI POTE

Nchi

1962

1987

2013

Australia

15,927

46,170

66,023

Brazili

26,390

216,216

756,455

 Ufaransa

18,452

96,954

124,029

Italia

6,929

 149,870

247,251

Japani

2,491

120,722

 217,154

Mexico

27,054

222,168

772,628

Nigeria

33,956

133,899

344,342

Filipino

36,829

101,735

181,236

Marekani

289,135

780,676

1,203,642

Zambia

30,129

67,144

162,370

ONGEZEKO LA IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA

1950

234,952

1960

646,108

1970

1,146,378

1980

1,371,584

1990

3,624,091

2000

4,766,631

2010

8,058,359

Matokeo ya Mavuno —Yalitabiriwa kwa Njia Iliyo Wazi

10, 11. Katika mfano wa mbegu ya haradali, ni sehemu gani za ukuzi wa mbegu ambazo zinakaziwa?

10 Katika mifano yake kuhusu Ufalme, Yesu alitabiri kwa njia iliyo wazi kuhusu matokeo ya kazi ya mavuno. Acheni tuchunguze ule mfano wa mbegu ya haradali na ule wa chachu. Tutachunguza hasa jinsi ambavyo mifano hiyo imetimizwa katika wakati wa mwisho.

11 Mfano wa mbegu ya haradali. Mtu fulani anapanda mbegu ya haradali. Kisha mbegu hiyo inakua na kuwa mti ambao ndege hupata makao. (Soma Mathayo 13:31, 32.) Ni sehemu gani za ukuzi wa mbegu zinazokaziwa katika mfano huo? (1) Kiwango cha ukuzi kinastaajabisha. “Mbegu ndogo zaidi kuliko zote” inamea na kuwa mti wenye “matawi makubwa.” (Marko 4:31, 32) (2) Ukuzi ni hakika. “Baada ya [mbegu hiyo] kupandwa, humea.” Yesu hasemi, “Huenda ikamea.” Hapana, anasema: “Humea.” Hakuna kitu chochote kinachoweza kuzuia ukuzi wake. (3) Mti huo uliokua unawavutia wageni na unaandaa makao. “Ndege wa mbinguni huja” na “kupata makao chini ya kivuli chake.” Sehemu hizo tatu zinahusianaje na mavuno ya kiroho leo?

12. Mfano wa mbegu ya haradali unahusianaje na kazi ya mavuno leo? (Ona pia chati “ Ongezeko la Idadi ya Mafunzo ya Biblia.”)

12 (1) Kiwango cha ukuzi: Mfano huo unakazia ukuzi wa ujumbe wa Ufalme na kutaniko la Kikristo. Tangu mwaka wa 1919, wafanyakazi wa mavuno wenye bidii wamekuwa wakikusanywa katika kutaniko la Kikristo lililopangwa upya. Wakati huo, idadi ya wafanyakazi ilikuwa ndogo, lakini ikaongezeka haraka. Kwa kweli, tangu miaka ya 1900 hadi leo, idadi hiyo imeongezeka kwa kasi sana. (Isa. 60:22) (2) Uhakikisho: Ukuzi wa kutaniko la Kikristo hauwezi kuzuiwa. Ingawa mbegu hiyo ndogo ilikabili upinzani mwingi, iliendelea kukua. (Isa. 54:17) (3) Makao: “Ndege wa mbinguni” ambao wanapata makao katika mti huo wanawakilisha mamilioni ya watu wenye mioyo minyofu kutoka nchi 240 hivi ambao wameukubali ujumbe wa Ufalme na kuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo. (Eze. 17:23) Wakiwa katika kutaniko wanapata chakula cha kiroho, wanaburudishwa, na kulindwa.—Isa. 32:1, 2; 54:13.

Mfano wa mbegu ya haradali unaonyesha kwamba wale walio ndani ya kutaniko la Kikristo ndio wanaofurahia makao na ulinzi (Ona fungu la 11, 12)

13. Mfano wa chachu unakazia sehemu gani za ukuzi?

13 Mfano wa chachu. Baada ya mwanamke kuongeza kiasi fulani cha chachu kwenye tonge la unga, chachu hiyo inachachusha tonge lote. (Soma Mathayo 13:33.) Ni sehemu gani za ukuzi zinazokaziwa katika mfano huo? Acheni tuzungumzie sehemu mbili. (1) Ukuzi unasababisha mabadiliko. Chachu inaenea ‘mpaka tonge lote linachacha.’ (2) Ukuzi unaenea kote. Chachu hiyo inachachusha ‘vipimo vyote vitatu vikubwa vya unga,’ yaani, tonge lote. Sehemu hizo mbili zinahusianaje na mavuno ya kiroho leo?

14. Mfano wa chachu unahusianaje na kazi ya mavuno leo?

14 (1) Mabadiliko: Chachu inawakilisha ujumbe wa Ufalme, na tonge la unga linawakilisha wanadamu. Kama vile chachu inavyosababisha mabadiliko kwenye unga baada ya kuchanganywa pamoja na unga, ndivyo ujumbe wa Ufalme unavyosababisha mabadiliko katika mioyo ya watu wanapokubali ujumbe huo. (Rom. 12:2) (2) Kuenea kote: Kuenea kwa chachu kunawakilisha kuenea kwa ujumbe wa Ufalme. Chachu inapochanganywa na unga inaenea kila mahali kwenye tonge lote. Vivyo hivyo, ujumbe wa Ufalme umeenea “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Kuenea kwa chachu kunaonyesha pia kwamba hata katika maeneo ambayo kazi yetu imepigwa marufuku, ujumbe wa Ufalme utaenea, hata ingawa huenda utendaji wetu wa kuhubiri katika sehemu hizo za dunia usionekane waziwazi.

15. Maneno yaliyo kwenye Isaya 60:5, 22 yametimizwaje? (Ona pia masanduku “ Yehova Alifanya Iwezekane,” kwenye ukurasa wa 93, na “ Jinsi Ambavyo ‘Mnyonge’ Amekuwa ‘Taifa Lenye Nguvu,’” kwenye ukurasa wa 96-97.)

15 Miaka 800 hivi kabla Yesu hajatoa mifano hiyo, Yehova, kupitia nabii Isaya, alitabiri kwa lugha rahisi kuhusu kuenea kwa mavuno ya kiroho katika siku zetu, na shangwe ambayo ingesababishwa na kazi hiyo ya kuvuna. * Yehova anaeleza kwamba watu “kutoka mbali” wanamiminika katika tengenezo lake. Akizungumza na “mwanamke,” ambaye leo anawakilishwa na watiwa-mafuta ambao wangali duniani, anasema hivi: “Utaona na hakika ung’ae, na moyo wako kwa kweli utatetemeka na kupanuka, kwa sababu mali za bahari zitajielekeza kwako; mali za mataifa zitakuja kwako.” (Isa. 60:1, 4, 5, 9) Maneno hayo ni kweli kabisa! Leo, watumishi wa Yehova ambao wamemtumikia kwa muda mrefu, kwa kweli wanang’aa kwa shangwe wanapoona jinsi ambavyo idadi ya wahubiri wa Ufalme katika nchi zao imeongezeka kutoka watu wachache tu hadi maelfu ya watu.

Sababu Inayowafanya Watumishi Wote wa Yehova Washangilie

16, 17. Ni sababu gani moja inayofanya ‘mpandaji na mvunaji washangilie pamoja’? (Ona pia sanduku “ Jinsi Trakti Mbili Zilivyogusa Mioyo ya Watu Wawili Huko Amazoni.”)

16 Utakumbuka kwamba Yesu aliwaambia mitume wake: ‘Mvunaji anakusanya matunda kwa ajili ya uzima wa milele, ili mpandaji na mvunaji wapate kushangilia pamoja.’ (Yoh. 4:36) ‘Tunashangiliaje pamoja’ katika mavuno ya ulimwenguni pote? Tunafanya hivyo katika njia kadhaa. Acheni tuchunguze njia tatu.

17 Kwanza, tunashangilia kuona jukumu la Yehova katika kazi ya mavuno. Tunapohubiri ujumbe wa Ufalme, tunapanda mbegu. (Mt. 13:18, 19) Tunapomsaidia mtu awe mwanafunzi wa Kristo, tunavuna matunda. Na sisi sote tunakuwa na shangwe kubwa sana tunapoona kwa kustaajabu jinsi ambavyo Yehova anasababisha mbegu ya Ufalme ‘kuota na kukua na kuwa ndefu.’ (Marko 4:27, 28) Baadhi ya mbegu tunazotawanya huota na kukua baadaye na zinavunwa na wengine. Huenda umewahi kujionea jambo alilojionea Joan, dada Mkristo kutoka Uingereza ambaye alibatizwa miaka 60 iliyopita. Alisema hivi: “Nimekutana na watu walioniambia kwamba mimi nilipanda mbegu kwenye mioyo yao wakati nilipowahubiria miaka mingi iliyopita. Pasipo mimi kujua, Mashahidi wengine baadaye walijifunza nao Biblia na kuwasaidia wawe watumishi wa Yehova. Ninashangilia kwamba mbegu niliyoipanda ilikua na ikavunwa.”—Soma 1 Wakorintho 3:6,  7.

18. Ni sababu gani ya kuwa na shangwe inayotajwa kwenye 1 Wakorintho 3:8?

18 Pili, tunaendelea kuwa wafanyakazi wenye shangwe tunapokumbuka kwamba Paulo alisema: “Kila mtu atapokea thawabu yake mwenyewe kulingana na kazi yake mwenyewe.” (1 Kor. 3:8) Thawabu inatolewa kulingana na kazi, na si kulingana na matokeo ya kazi hiyo. Uhakika huo ni kitia moyo kwelikweli kwa wale wanaohubiri katika maeneo ambayo ni watu wachache sana hukubali habari njema! Machoni pa Mungu, kila Shahidi ambaye anashiriki kwa moyo wote katika kazi ya kupanda ‘anazaa matunda mengi’ na hivyo ana sababu ya kushangilia.—Yoh. 15:8; Mt. 13:23.

19. (a) Unabii wa Yesu ulio kwenye Mathayo 24:14 unahusianaje na shangwe yetu? (b) Tunapaswa kukumbuka nini hata ikiwa sisi binafsi hatufanikiwi kumfanya mtu kuwa mwanafunzi?

19 Tatu, tunashangilia kwamba kazi yetu inatimiza unabii. Fikiria jibu ambalo Yesu aliwapa mitume wake walipomuuliza: “Nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Yesu aliwaambia kwamba sehemu moja ya ishara hiyo ingekuwa kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Je, alikuwa akizungumza kuhusu kazi ya kufanya wanafunzi? La hasha! Alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:3, 14) Hivyo, kazi ya kuhubiri Ufalme, yaani, kupanda mbegu, ni sehemu ya ile ishara. Kwa hiyo, tunapohubiri habari njema ya Ufalme, tunakumbuka kwamba hata kama hatufanikiwi kumfanya mtu kuwa mwanafunzi, tunafanikiwa kutoa “ushahidi.” * Naam, hata iwe watu wanaitikia au la, tunashiriki kutimiza unabii wa Yesu na tumepewa pendeleo la kutumikia tukiwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Hiyo ni sababu nzuri kama nini ya kushangilia!

“Tokea Maawio ya Jua Hata Machweo Yake”

20, 21. (a) Maneno ya Malaki 1:11 yanatimizwa jinsi gani? (b) Kuhusu kazi ya mavuno, umeazimia kufanya nini, na kwa nini?

20 Katika karne ya kwanza, Yesu aliwasaidia mitume wake waone kwamba kazi ya kuhubiri ilipaswa kufanywa haraka. Kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, Yesu amewasaidia wanafunzi wake wa siku hizi kuelewa ukweli huohuo. Kwa sababu hiyo, watu wa Mungu wameongeza utendaji wao. Kwa kweli, kazi ya mavuno imesonga bila kuzuiwa. Kama ilivyotabiriwa na nabii Malaki, leo kazi ya kuhubiri inafanywa “tokea maawio ya jua hata machweo yake.” (Mal. 1:11 UV) Naam, tokea maawio hadi machweo, yaani, tokea mashariki hadi magharibi, hata wawe wapi katika pembe zote za dunia, wapandaji na wavunaji wanafanya kazi na kushangilia pamoja. Na tokea maawio hadi machweo, yaani, kutoka asubuhi hadi jioni, au siku nzima, tunafanya kazi tukiwa na hisi ya uharaka.

21 Leo, tunapotazama nyuma zaidi ya miaka 100 hivi iliyopita na kuona jinsi ambavyo kikundi kidogo cha watumishi wa Mungu kimekua na kuwa “taifa hodari,” mioyo yetu kwa kweli ‘inatetemeka na kupanuka’ kwa shangwe. (Isa. 60:5, 22) Shangwe hiyo na upendo wetu kwa Yehova, “Bwana wa mavuno,” na umchochee kila mmoja wetu aendelee kushiriki katika kuyakamilisha mavuno hayo makubwa sana kuwahi kufanywa!—Luka 10:2.

^ fu. 3 Huenda maneno ya Yesu kuhusu ‘mashamba kuwa meupe’ yalirejelea kanzu nyeupe ambazo huenda zilivaliwa na umati wa Wasamaria ambao Yesu aliuona ukiwakaribia.

^ fu. 9 Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu miaka hiyo na makumi ya miaka iliyofuata, tunakutia moyo usome ukurasa wa 425-520 wa kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu ambacho kinasimulia yale ambayo kazi ya mavuno ilitimiza kutoka mwaka wa 1919 hadi 1992.

^ fu. 15 Kwa habari zaidi kuhusu unabii huu wenye kupendeza, ona kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote II, ukurasa wa 303-320.

^ fu. 19 Tayari Wanafunzi wa Biblia wa mapema waliielewa kweli hiyo muhimu. Gazeti Zion’s Watch Tower la Novemba 15, 1895 lilisema hivi: “Ikiwa ngano kidogo tu inaweza kukusanywa, basi ushahidi kuhusu kweli unaweza kutolewa kwa kiasi kikubwa. . . . Wote wanaweza kuhubiri injili.”