Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 10

Mfalme Anawasafisha Watu Wake Kiroho

Mfalme Anawasafisha Watu Wake Kiroho

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Sababu ambazo zilimfanya Yesu awasafishe na kuwatakasa wafuasi wake kiroho na jinsi alivyofanya hivyo

1-3. Yesu alifanya nini alipopata hekalu likichafuliwa?

YESU aliliheshimu sana hekalu la Yerusalemu kwa sababu alijua kile kilichowakilishwa na hekalu hilo. Kwa muda mrefu hekalu hilo lilikuwa kitovu cha ibada ya kweli duniani. Lakini ibada hiyo, yaani, ibada ya Mungu mtakatifu, Yehova—lazima iwe safi na takatifu. Hivyo basi, wazia jinsi Yesu alivyohisi alipokuja hekaluni Nisani 10, 33 W.K., na kupata likichafuliwa. Ni nini kilichokuwa kikifanyika hekaluni?—Soma Mathayo 21:12, 13.

2 Katika Ua wa Mataifa, wafanyabiashara wenye pupa na wale waliokuwa wakibadili pesa walikuwa wakiwapunja waabudu waliokuja kumtolea Yehova dhabihu hekaluni. * Yesu ‘aliwafukuza wale wote waliokuwa wakiuza na kununua katika hekalu, na kuzipindua meza za wale waliokuwa wakibadili pesa.’ (Linganisha na Nehemia 13:7-9.) Aliwashutumu wanaume hao wenye ubinafsi kwa kuifanya nyumba ya Baba yake kuwa “pango la wanyang’anyi.” Kwa kufanya hivyo, Yesu alionyesha kwamba aliliheshimu hekalu na kile kilichowakilishwa na hekalu hilo. Ibada ya Baba yake ilipaswa kuwa safi!

3 Karne nyingi baadaye, baada ya kuwekwa rasmi kuwa Mfalme wa Kimasihi, Yesu alilitakasa tena hekalu. Hekalu hilo linahusisha wale wote wanaotaka kumwabudu Yehova kwa njia anayoikubali. Hivyo basi, ni hekalu gani alilolitakasa?

Kuwatakasa “Wana wa Lawi”

4, 5. (a) Wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu walisafishwa na kutakaswa jinsi gani kuanzia mwaka wa 1914 hadi mapema mwaka wa 1919? (b) Je, huo ndio ulikuwa mwisho wa kusafishwa na kutakaswa kwa watu wa Mungu? Eleza.

4 Kama tulivyoona katika Sura ya 2 ya kitabu hiki, baada ya kuwekwa kuwa Mfalme mwaka wa 1914, Yesu alikuja na Baba yake kukagua hekalu la kiroho, yaani, mpango wa ibada safi. * Matokeo ya ukaguzi huo ni kwamba Mfalme aliona kuwa Wakristo watiwa-mafuta, yaani, “wana wa Lawi,” walihitaji kusafishwa na kutakaswa. (Mal. 3:1-3) Kuanzia mwaka wa 1914 hadi mapema mwaka wa 1919, Yehova akiwa Msafishaji, aliruhusu watu wake wapitie majaribu na hali ngumu ambayo iliwasafisha na kuwatakasa. Inafurahisha kwamba watiwa-mafuta hao waliibuka kutoka katika majaribu hayo makali wakiwa wametakaswa, na tayari kumuunga mkono Mfalme wa Kimasihi!

5 Je, huo ndio ulikuwa mwisho wa kusafishwa na kutakaswa kwa watu Mungu? Hapana. Katika kipindi chote cha siku za mwisho, Yehova kupitia Mfalme wa Kimasihi ameendelea kuwasaidia wafuasi wake wawe safi ili wabaki katika hekalu la kiroho. Katika sura mbili zinazofuata, tutaona jinsi ambavyo amewasafisha kiadili na kitengenezo. Lakini kwanza, acheni tuzungumzie jinsi ambavyo amewatakasa watu wake kiroho. Inaimarisha imani kuchunguza yale ambayo Yesu amefanya—iwe kupitia njia zinazoonekana waziwazi au zisizoonekana—ili kuwasaidia wafuasi wake wawe safi kiroho.

“Jiwekeni Safi”

6. Amri za Yehova kwa Wayahudi waliokuwa uhamishoni zinatusaidiaje kuelewa maana ya kuwa safi kiroho?

6 Usafi wa kiroho unamaanisha nini? Ili kujibu swali hilo, acheni kwanza tuchunguze maneno ambayo Yehova aliwaambia Wayahudi waliokuwa uhamishoni walipokuwa karibu kutoka Babiloni katika karne ya sita K.W.K. (Soma Isaya 52:11.) Wayahudi hao walikuwa wakirudi Yerusalemu ili kujenga upya hekalu na kurudisha ibada ya kweli. (Ezra 1:2-4) Yehova alitaka watu wake waache kila kitu kilichohusiana na dini ya Babiloni. Ona kwamba aliwapa amri kadhaa: “Msiguse kitu chochote kilicho najisi,” “tokeni katikati yake,” na “jiwekeni safi.” Ibada safi ya Yehova haipaswi kamwe kuchafuliwa na ibada ya uwongo. Hivyo, tunapaswa kukata shauri gani? Kuwa safi kiroho kunamaanisha kujitenga na mafundisho na mazoea ya dini ya uwongo.

7. Yesu ametumia njia gani kuwasaidia wafuasi wake kuwa safi kiroho?

7 Muda mfupi baada ya kuwekwa rasmi kuwa Mfalme, Yesu aliweka rasmi njia inayotambuliwa waziwazi ambayo ameitumia kuwasaidia wafuasi wake wawe safi kiroho. Njia hiyo ni mtumwa mwaminifu na mwenye busara, ambaye Kristo alimweka rasmi mwaka wa 1919. (Mt. 24:45) Kufikia mwaka huo, Wanafunzi wa Biblia tayari walikuwa wameyaacha mafundisho mengi ya dini za uwongo. Lakini bado walihitaji kusafishwa zaidi kiroho. Kupitia mtumwa wake mwaminifu, Kristo aliwafunulia wafuasi wake hatua kwa hatua sherehe na mazoea ambayo walihitaji kuacha. (Met. 4:18) Acheni tuchunguze baadhi ya sherehe na mazoea hayo.

Je, Wakristo Wanapaswa Kusherehekea Krismasi?

8. Kwa muda mrefu Wanafunzi wa Biblia walijua jambo gani kuhusu Krismasi, lakini hawakuona uhitaji gani?

8 Kwa muda mrefu Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba Krismasi ilikuwa na chanzo cha kipagani na kwamba Yesu hakuzaliwa Desemba 25. Gazeti Zion’s Watch Tower la Desemba 1881 lilisema hivi: “Mamilioni ya wapagani walibadilishwa na kuwa Wakristo. Hata hivyo badiliko hilo lilikuwa kwa jina tu kwa kuwa makasisi wa kipagani walianza kuitwa makasisi wa Kikristo na sikukuu za kipagani zikaanza kuitwa kwa majina ya kikristo—Krismasi ikiwa mojawapo ya sikukuu hizo.” Katika mwaka wa 1883, gazeti Mnara wa Mlinzi lilikuwa na makala yenye kichwa “Yesu Alizaliwa Lini?” ambayo ilifafanua kwamba Yesu alizaliwa mwanzoni mwa Oktoba hivi. * Hata hivyo, wakati huo Wanafunzi wa Biblia hawakuona uhitaji wa kuacha kusherehekea Krismasi. Hata washiriki wa familia ya Betheli ya Brooklyn waliendelea kuisherehekea. Hata hivyo, baada ya mwaka wa 1926, mambo yalianza kubadilika. Kwa nini?

9. Wanafunzi wa Biblia walikuja kutambua nini kuhusu Krismasi?

9 Baada ya kuchunguza jambo hilo kwa kina na kwa uangalifu, Wanafunzi wa Biblia walikuja kutambua kwamba chanzo na mazoea yanayoambatana na Krismasi yanamvunjia Mungu heshima. Makala yenye kichwa “Chanzo cha Krismasi,” iliyokuwa katika gazeti The Golden Age la Desemba 14, 1927, ilieleza kwamba Krismasi ni sikukuu ya kipagani, inayokazia anasa, na inahusisha ibada ya sanamu. Makala hiyo ilionyesha wazi kwamba Kristo hakuamuru watu washerehekee sikukuu hiyo na kisha ikamalizia kwa kusema hivi waziwazi: “Kwa kuwa ulimwengu, mwili wenye dhambi, na Ibilisi anataka watu waiendeleze na kuadhimisha Krismasi . . . hiyo ni sababu ya kutosha kwa wale ambao wamejitoa kabisa kumtumikia Yehova kutosherehekea sikukuu hiyo.” Haishangazi kwamba familia ya Betheli haikusherehekea Krismasi mwezi huo wa Desemba—na haijasherehekea tena!

10. (a) Ni ufafanuzi gani kamili kuhusu Krismasi uliotolewa Desemba 1928? (Ona pia sanduku “ Krismasi, Chanzo na Kusudi Lake.”) (b) Watu wa Mungu walionywa jinsi gani kuhusu sikukuu na sherehe nyingine ambazo walipaswa kuziepuka? (Ona sanduku “ Sikukuu na Sherehe Nyingine Zafichuliwa.”)

10 Mwaka uliofuata, Wanafunzi wa Biblia walipata ufafanuzi kamili kuhusu Krismasi. Desemba 12, 1928, Ndugu Richard H. Barber, aliyefanya kazi katika makao makuu, alitoa hotuba kupitia redio ambayo ilifunua waziwazi vyanzo vichafu vya sikukuu hiyo. Watu wa Mungu waliitikiaje mwelekezo huo ulio wazi kutoka makao makuu? Akikumbuka wakati ambao familia yake iliacha kusherehekea Krismasi, Ndugu Charles Brandlein alisema hivi: “Je, tulisikitika kuacha mambo hayo ya kipagani? La hasha! . . . Ilikuwa kama kuvua nguo chafu sana na kuitupa.” Akiwa na maoni kama hayo,  Henry A. Cantwell, ambaye baadaye alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko alisema hivi: “Tulifurahi kuacha jambo fulani ili kuonyesha kwamba tunampenda Yehova.” Wafuasi washikamanifu wa Kristo walikuwa tayari kufanya mabadiliko yaliyohitajika ili wasishiriki katika sherehe iliyotokana na ibada chafu. *Yoh. 15:19; 17:14.

11. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamuunga mkono Mfalme wa Kimasihi?

11 Wanafunzi hao waaminifu wa Biblia walituwekea mfano mzuri sana! Tunapotafakari mfano wao, inafaa tujiulize: ‘Ninaonaje mwongozo tunaopata kutoka kwa mtumwa mwaminifu? Je, ninakubali na kufuata yale ambayo ninajifunza?’ Tunapotii kwa hiari tunaonyesha kwamba tunamuunga mkono Mfalme wa Kimasihi anayemtumia mtumwa mwaminifu kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.—Mdo. 16:4, 5.

Je, Wakristo Watumie Msalaba?

Nembo ya msalaba na taji (Ona fungu la 12 na 13)

12. Kwa miaka mingi, Wanafunzi wa Biblia walikuwa na maoni gani kuhusu msalaba?

12 Kwa miaka mingi, Wanafunzi wa Biblia waliuona msalaba kuwa alama inayokubalika ya Ukristo. Bila shaka, hawakuona kwamba msalaba unapaswa kuabudiwa kwa sababu walijua ni kosa kuabudu sanamu. (1 Kor. 10:14; 1 Yoh. 5:21) Mapema mwaka wa 1883, gazeti Mnara wa Mlinzi lilieleza wazi kwamba “ibada zote za sanamu ni chukizo kwa Mungu.” Hata hivyo, mwanzoni, Wanafunzi wa Biblia hawakuona ubaya wowote kutumia msalaba kwa njia walizofikiri kwamba zinafaa. Kwa mfano, walivaa pini zenye msalaba na taji kama beji za kuwatambulisha. Kwa maoni yao, pini hizo zilionyesha kwamba ikiwa wangekuwa waaminifu mpaka kifo, wangepokea taji la uzima. Kuanzia mwaka wa 1891, alama ya msalaba na taji ilionekana kwenye ukurasa wa mbele wa gazeti Mnara wa Mlinzi.

13. Wafuasi wa Kristo walipata uelewaji gani kuhusu matumizi ya msalaba? (Ona pia sanduku “ Wafunuliwa Hatua kwa Hatua Kuhusu Matumizi ya Msalaba.”)

13 Nembo ya msalaba na taji ilipendwa sana na Wanafunzi wa Biblia. Hata hivyo, kuanzia mwishoni mwa miaka ya 1920, wafuasi wa Kristo walifunuliwa hatua kwa hatua uelewaji kuhusu matumizi ya msalaba. Akikumbuka kusanyiko lililofanywa Detroit, Michigan, Marekani mwaka wa 1928, Ndugu Grant Suiter, ambaye baadaye alitumikia katika Baraza Linaloongoza alisema hivi: “Katika kusanyiko hilo ilifafanuliwa kwamba nembo ya msalaba na taji haikuhitajika wala kukubalika.” Kwa miaka michache iliyofuata, uelewaji zaidi ulifunuliwa. Ilikuwa wazi kwamba msalaba hauna nafasi katika ibada safi na iliyotakaswa kiroho.

14. Watu wa Mungu waliitikiaje ufafanuzi uliotolewa hatua kwa hatua kuhusu msalaba?

14 Watu wa Mungu waliitikiaje walipopata ufafanuzi uliotolewa hatua kwa hatua kuhusu msalaba? Je, waliendelea kutumia nembo ya msalaba na taji ambayo waliipenda sana? “Tuliacha kuitumia tulipotambua kile ilichokuwa ikiwakilisha,” akasema Lela Roberts ambaye amemtumikia Yehova kwa miaka mingi. Dada mwingine mwaminifu, Ursula Serenco, anaeleza hisia za wengi anaposema: “Tulikuja kutambua kwamba kile tulichoona kuwa kinawakilisha kifo cha Bwana wetu na ujitoaji wetu wa Kikristo kilikuwa alama ya kipagani. Kupatana na Methali 4:18, tulishukuru kwamba njia ilikuwa ikiendelea kung’aa.” Wafuasi washikamanifu wa Kristo hawakutaka kushiriki katika mazoea machafu ya dini za uwongo!

15, 16. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tumeazimia kudumisha nyua za kidunia za hekalu la kiroho la Yehova zikiwa safi?

15 Tumeazimia vivyo hivyo leo. Tunatambua kwamba Kristo amekuwa akitumia njia inayotambuliwa waziwazi, yaani, mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara, kuwasaidia watu wake kuendelea kuwa safi kiroho. Hivyo, tunapoonywa kupitia chakula cha kiroho tunachopata kuhusu sherehe, mazoea, au desturi ambazo zimechafuliwa na dini ya uwongo, tunatii na kuziacha haraka. Kama ilivyokuwa kwa ndugu na dada zetu ambao waliishi siku za mapema za kuwapo kwa Kristo, tumeazimia kudumisha nyua za kidunia za hekalu la Yehova la kiroho zikiwa safi.

16 Katika kipindi chote cha siku za mwisho, Kristo pia amekuwa akifanya mambo mengi tusiyoyaona ili kuyalinda makutaniko ya watu wa Yehova dhidi ya watu ambao wanaweza kuyachafua kiroho. Amefanya hivyo jinsi gani? Acheni tuone.

Kutenganisha “Waovu Kutoka Katikati ya Waadilifu”

17, 18. Katika mfano wa wavu wa kukokota, ni nini kinachomaanishwa na (a) kushusha wavu wa kukokota, (b) “kukusanya samaki wa kila aina,” (c) kukusanya walio wazuri ndani ya vyombo, na (d) kuwatupilia mbali samaki wasiofaa?

17 Mfalme Yesu Kristo anaendelea kuyalinda makutaniko ya watu wa Mungu duniani kote. Katika njia ambazo hatuwezi kuzielewa kikamili, Kristo na malaika wamekuwa wakifanya kazi ya kutenganisha. Yesu aliifafanua kazi hiyo katika mfano wake wa wavu wa kukokota. (Soma Mathayo 13:47-50.) Mfano huo unamaanisha nini?

Wavu wa kukokota unawakilisha kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme kwa wanadamu wote ambao wanafananishwa na bahari (Ona fungu la 18)

18 Kushusha “wavu wa kukokota . . . ndani ya bahari.” Wavu wa kukokota unawakilisha kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme kwa wanadamu wote ambao wanafananishwa na bahari. “Kukusanya samaki wa kila aina.” Habari njema inawavutia watu wa aina zote—wale wanaochukua hatua na kuwa Wakristo wa kweli, na pia wengi ambao mwanzoni wanaweza kuonyesha kwamba wanapendezwa lakini hawachukui msimamo upande wa ibada safi. * Kukusanya “walio wazuri ndani ya vyombo.” Wanyofu wanakusanywa kwenye makutaniko yanayofananishwa na vyombo, ambamo wanaweza kumtolea Yehova ibada safi. Kuwatupilia mbali samaki “wasiofaa.” Katika kipindi chote cha siku za mwisho, Kristo na malaika wamekuwa wakitenganisha “waovu kutoka katikati ya waadilifu.” * Matokeo ni kwamba wote ambao hawana mioyo minyofu, yaani, wale ambao huenda hawataki kuacha mazoea au mafundisho ya uwongo, hawajaruhusiwa kuchafua makutaniko. *

19. Unahisije kuhusu yale ambayo Kristo amekuwa akifanya ili kulinda usafi wa watu wa Mungu na usafi wa ibada ya kweli?

19 Je, haichangamshi moyo kujua kwamba Mfalme wetu Yesu Kristo anawalinda wote ambao wako chini ya utunzaji wake? Na je, haifariji kujua kwamba anasafisha na kulinda ibada ya kweli na waabudu wa kweli, kwa bidii ileile aliyokuwa nayo aliposafisha hekalu katika karne ya kwanza W.K.? Tunashukuru sana kwamba Kristo amekuwa akilinda usafi wa kiroho wa watu wa Mungu na usafi wa ibada ya kweli! Tunaweza kuonyesha kwamba tunamuunga mkono Mfalme na Ufalme wake kwa kuepuka kabisa dini ya uwongo.

^ fu. 2 Wayahudi kutoka maeneo mengine waliokuja hekaluni walipaswa kulipia kodi ya hekalu ya kila mwaka kwa kutumia aina fulani ya sarafu, na wale waliobadili pesa waliwatoza malipo fulani ili kuwabadilishia sarafu hizo. Kwa kuongezea, huenda wageni hao walihitaji kununua wanyama kwa ajili ya kutoa dhabihu. Yesu aliwaita wafanyabiashara hao “wanyang’anyi,” labda kwa sababu walitoza malipo ya juu kupita kiasi kwa ajili ya huduma zao.

^ fu. 4 Watu wa Yehova duniani wanamwabudu katika nyua za kidunia za hekalu lake kuu la kiroho.

^ fu. 8 Makala hiyo ilionyesha kuwa fundisho la kwamba Yesu alizaliwa wakati wa majira ya baridi kali “halipatani na simulizi la wachungaji wakiwa nje na makundi yao.”—Luka 2:8.

^ fu. 10 Katika barua yake ya Novemba 14, 1927, Ndugu Frederick W. Franz aliandika hivi: “Hatutasherehekea Krismasi mwaka huu. Familia ya Betheli imeamua kutosherehekea Krismasi tena.” Miezi michache baadaye katika barua ya Februari 6, 1928, Ndugu Franz aliandika: “Hatua kwa hatua Bwana anatusafisha kutokana na makosa ya tengenezo la Kibabiloni la Ibilisi.”

^ fu. 18 Kwa mfano, katika mwaka wa 2013, kulikuwa na kilele cha wahubiri 7,965,954 ilhali watu 19,241,252 walihudhuria Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo.

^ fu. 18 Kutenganishwa kwa samaki wazuri na samaki wasiofaa ni tofauti na kutenganishwa kwa kondoo na mbuzi. (Mt. 25:31-46) Kutenganishwa kwa kondoo na mbuzi au hukumu ya mwisho, kunafanywa wakati wa dhiki kuu inayokuja. Kabla ya wakati huo, wote walio kama samaki wasiofaa wanaweza kumrudia Yehova na kukusanywa katika makutaniko yanayofananishwa vyombo.—Mal. 3:7.

^ fu. 18 Mwishowe, kwa njia ya mfano wasiofaa watatupwa katika tanuru ya moto, yaani, wataharibiwa.