Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 10

Mufalme Anasafisha Wafuasi Wake Kiroho

Mufalme Anasafisha Wafuasi Wake Kiroho

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Sababu gani na namna gani Yesu amesafisha na kutakasa wafuasi wake kiroho

1-3. Yesu alifanya nini wakati alikuta watu wako wanachafua hekalu?

YESU alikuwa anaheshimu sana hekalu la Yerusalemu kwa sababu alijua kwamba ibada ya Yehova ilikuwa inafanyika humo. Kwa miaka mingi, ni hapo ibada ya kweli ilikuwa inafanyika hapa duniani. Lakini kwa sababu Yehova ni Mungu mutakatifu, iliomba ibada hiyo iwe safi na yenye kutakata. Kwa hiyo, wazia namna Yesu alijisikia siku ile alifika kwenye hekalu hilo, na kukuta watu wako wanalichafua; ilikuwa tarehe 10 Mwezi wa Nisani, 33. Ni mambo gani watu walikuwa wanafanya ili kulichafua?—Soma Mathayo 21:12, 13.

2 Katika Uwanja wa Watu wa Mataifa, wafanyabiashara na wabadilisha-feza wenye pupa walikuwa wanajipatia faida isiyo ya haki kwa kupunja wale ambao walikuwa wanakuja kuabudu na kumutolea Yehova sadaka. * Yesu ‘aliwafukuza wale wote waliokuwa wakiuzisha na kununua katika hekalu, na kuzipindua meza za wale ambao walikuwa wanabadilisha feza.’ (linganisha na Nehemia 13:7-9.) Yesu anaonyesha wazi ubaya wa watu hao wenye kutafuta faida yao wenyewe kwa sababu wanageuza nyumba ya Baba yake kuwa ‘pango la wanyanganyi.’ Kwa kufanya hivyo, Yesu alionyesha kwamba aliheshimu hekalu na vilevile ibada ambayo ilikuwa inafanyika ndani. Ibada ambayo watu walimutolea Baba yake ilipaswa kuwa safi!

3 Kisha miaka mingi, Yesu aliwekwa kuwa Masiya-Mufalme, na kisha kupewa cheo hicho, alisafisha tena hekalu. Hekalu hilo linahusu kila mutu ambaye anapenda kumuabudu Yehova katika njia ambayo inakubalika naye leo. Kwa hiyo, ni hekalu gani ambalo alisafisha tena?

Kuwatakasa “Wana wa Lawi”

4, 5. (a) Namna gani wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu walitakaswa na kusafishwa kuanzia mwaka wa 1914 mupaka mwanzo-mwanzo wa mwaka wa 1919? (b) Huo ndio ulikuwa mwisho wa kutakaswa na kusafishwa kwa watu wa Mungu? Fasiria.

4 Kama vile tuliona katika Sura ya 2, kisha Yesu kuwekwa kuwa Mufalme katika mwaka wa 1914, alikuja pamoja na Baba yake ili kuchunguza hekalu la kiroho, ni kusema, mipango ambayo Yehova alikamata kwa ajili ya ibada safi. * Kisha uchunguzi huo, Mufalme aliona kwamba Wakristo watiwa-mafuta, ni kusema, “wana wa Lawi” walipaswa kutakaswa na kusafishwa. (Mal. 3:1-3) Kuanzia mwaka wa 1914 mupaka mwanzo-mwanzo wa mwaka wa 1919, Musafishaji, ni kusema, Yehova, aliacha watu wake wapate majaribu mengi na magumu mbalimbali ili watakaswe na kuwa safi. Jambo lenye kufurahisha ni kwamba, Wakristo watiwa-mafuta walitoka katika majaribu hayo ambayo yalikuwa kama moto, wakiwa safi. Hali hiyo iliwafanya wakuwe na hamu sana ya kuonyesha kwamba wanamuunga mukono Masiya-Mufalme!

5 Huo ndio ulikuwa mwisho wa kutakaswa na kusafishwa kwa watu wa Mungu? Hapana. Katika siku hizi za mwisho, Yehova ameendelea kusafisha watu wake kupitia Masiya-Mufalme, ili wabaki katika hekalu la kiroho. Katika sura mbili ambazo zinafuata, tutajifunza namna Yesu ameendelea kuwasafisha wafuasi wake ili wawe na mwenendo safi na wafuate utaratibu wa tengenezo. Acha kwanza tuzungumuzie kazi ya kusafisha kiroho. Ni jambo lenye kutia imani nguvu kuchunguza mambo ambayo Yesu amefanya ili kusaidia wafuasi wake kuwa safi kiroho. Mambo fulani yamefanyika kwa njia yenye kuonekana wazi, lakini mengine yamefanyika bila kuonekana.

Muendelee Kuwa “Safi”

6. Kuwa safi kiroho kunamaanisha nini kulingana na sheria ambayo Yehova aliwapatia Wayahudi waliokuwa Babiloni katika uhamisho?

6 Kuwa safi kiroho kunamaanisha nini? Ili kujibu ulizo hilo, acha tuchunguze maneno ambayo Yehova aliwaambia Wayahudi ambao walipelekwa katika uhamisho, Babiloni, na ambao walikuwa karibu kurudi kwao katika miaka ya 500 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. (Soma Isaya 52:11.) Sababu ya kwanza ambayo iliwafanya Wayahudi hao warudishwe kwao Yerusalemu ni hii: kujenga hekalu na kuanzisha tena ibada safi. (Ezra 1:2-4) Yehova alipenda watu wake watoke na waachane na kila fundisho ao desturi ya dini za Babiloni. Ona mufululizo wa sheria ambao aliwapatia: ‘Musiguse kitu chochote kilicho najisi [ao kichafu],’ ‘mutoke katikati yake,’ na ‘mujiweke [muendelee kuwa] safi.’ Ibada safi ya Yehova haipaswe kuchafuliwa na ibada ya uongo. Kwa hiyo, tunaweza kusema nini? Kuwa safi kiroho kunamaanisha kuachana kabisa na desturi zote na mafundisho ya dini za uongo.

7. Ni kupitia njia gani Yesu amesaidia wafuasi wake kuwa safi kiroho?

7 Muda kidogo tu kisha kuwekwa kuwa Mufalme, Yesu alianzisha njia ambayo inajulikana wazi na ambayo kupitia hiyo amesaidia wafuasi wake kuwa safi kiroho. Njia hiyo ni mutumwa mwaminifu na mwenye busara, ambaye Kristo aliweka katika mwaka wa 1919. (Mt. 24:45) Kufikia mwaka huo, Wanafunzi wa Biblia, walikuwa wamejisafisha kwa kuachana na mafundisho fulani ya dini za uongo. Hata hivyo, walipaswa tena kusafishwa kiroho. Kupitia mutumwa wake mwaminifu, Kristo alifunulia wafuasi wake hatua kwa hatua sikukuu na desturi mbalimbali ambazo walipaswa kuachana nazo. (Met. 4:18) Acha tuchunguze mifano fulani.

Wakristo Wanapaswa Kufanya Sikukuu ya Noeli?

8. Tangu zamani Wanafunzi wa Biblia walielewa nini kuhusu Noeli, lakini, wakati huo ni jambo gani hawakuona kuwa ni lazima kufanya?

8 Tangu zamani, Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba Noeli ilianzishwa na wapagani na kwamba Yesu hakuzaliwa tarehe 25 Mwezi wa 12. Gazeti Munara wa Mulinzi la Mwezi wa 12, 1881, lilisema hivi: “Mamilioni ya watu wametoka katika dini za Kipagani na kuingizwa katika kanisa. Lakini mabadiliko ambayo walifanya ilikuwa zaidi sana ya jina tu, kwa sababu makuhani wa kipagani walibadilisha jina na kuwa makasisi (ao mapadri) wa kikristo. Na sikukuu za kipagani zilichukua majina ya kikristo: moja ya sikukuu hizo ni Noeli.” Katika mwaka wa 1883, gazeti Munara wa Mulinzi lilikuwa na habari “Yesu Alizaliwa Wakati Gani?” habari hiyo ilionyesha kwamba Yesu alizaliwa mwanzo wa Mwezi wa 10 hivi.[3] Hata hivyo, wakati huo, Wanafunzi wa Biblia hawakuona kwamba ilikuwa lazima kuacha kufanya sikukuu hiyo ya Noeli. Hata ndugu wa Beteli ya Brooklyn waliendelea kufanya sikukuu hiyo. Lakini, kisha mwaka wa 1926, mambo yalianza kubadilika. Sababu gani?

9. Wanafunzi wa Biblia walifikia kuelewa nini kuhusu Noeli?

9 Kisha kuchunguza sana na kwa uangalifu jambo hilo, Wanafunzi wa Biblia walifikia kuelewa kwamba chanzo cha Noeli na desturi zake hazimuletee Mungu heshima. Gazeti L’Âge d’Or la tarehe 14 Mwezi wa 12, 1927 lilikuwa na habari “Noeli Ilitoka Wapi?” Habari hiyo ilionyesha kwamba Noeli ni sikukuu ya kipagani ambayo inakazia sana mambo ya raha na ibada ya sanamu. Habari hiyo ilionyesha wazi kwamba Kristo hakuagiza wafuasi wake wafanye sikukuu ya Noeli. Na ilimalizia kwa kusema hivi juu ya Noeli: “Kwa sababu ulimwengu, tamaa ya mwili, na Shetani wanapenda sikukuu hiyo iendelee kufanywa, sababu hizo zinatosha na zinapaswa kuwachochea wale wote ambao walijitoa kwa Yehova kwa moyo wao wote, wachukie sikukuu hiyo.” Kwa hiyo, si jambo la kushangaza ikiwa katika mwezi wa 12 mwaka huo, familia ya Beteli haikufanya sikukuu hiyo. Na mupaka sasa!

10. (a) Katika Mwezi wa 12, 1928, ni maelezo gani yalitolewa kuhusu Noeli? (Soma pia kisanduku  “Noeli Ilitoka Wapi na Sababu Gani Ilianzishwa.) (b) Ni maonyo gani watu wa Mungu walipewa kuhusu sikukuu zingine ambazo walipaswa kuepuka? (Soma kisanduku  Chanzo cha Sikukuu Zingine.)

10 Mwaka ambao ulifuata, Wanafunzi wa Biblia walipata tena maelezo mengi zaidi juu ya Noeli. Katika Mwezi wa 12, 1928, Ndugu Richard H. Barber, aliyekuwa anatumikia kwenye makao makubwa, alitoa hotuba kwenye radio ambayo ilifunua wazi kwamba sikukuu hiyo chafu ilianzishwa na wapagani. Ndugu walifanya nini wakati walipata muongozo wa mutumwa mwaminifu? Ndugu Charles Brandlein anakumbuka wakati yeye na familia yake waliacha kufanya sikukuu ya Noeli. Alisema hivi: “Hatukuhuzunika hata kidogo kuachana na sikukuu hiyo ya kipagani. . . . Ilikuwa kama vile kuondoa vazi ambalo lilichafuliwa na kulitupilia mbali.” Ndugu Henry A. Cantwell ambaye kisha alikuwa mwangalizi wa muzunguko, alionyesha pia mawazo yaleyale. Alisema hivi: “Tulifurahi kuona kwamba tuliweza kuachana na jambo fulani ili kuonyesha kwamba tunamupenda Yehova.” Wafuasi waaminifu wa Kristo walikuwa tayari kufanya mabadiliko ambayo yaliombwa na walikusudia kutojiingiza kwa njia yoyote katika sikukuu ambayo ilitokana na ibada ambayo ilichafuliwa. *​—Yoh. 15:19; 17:14.

11. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tunaunga mukono Masiya-Mufalme?

11 Kwa kweli, Wanafunzi wa Biblia hao waaminifu ni mufano muzuri kwetu! Wakati tunafikiria mufano wao ni vizuri kila mutu ajiulize: ‘Ninakubali muongozo ambao unatoka kwa mutumwa mwaminifu? Ninafurahia muongozo huo na ninatumia katika maisha yangu yale ambayo ninajifunza?’ Kuwa tayari kutii kutaonyesha kwamba tunaunga mukono Masiya-Mufalme, ambaye anatumia mutumwa mwaminifu ili kutupatia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.​—Mdo. 16:4, 5.

Wakristo Wanapaswa Kutumia Musalaba?

Alama ya taji yenye kuwa na musalaba (Ona fungu la 12 na la 13)

12. Kwa miaka mingi, namna gani Wanafunzi wa Biblia waliuona musalaba?

12 Kwa miaka mingi, Wanafunzi wa Biblia waliona musalaba kuwa alama yenye kukubaliwa ambayo inatambulisha dini ya Kikristo. Hata hivyo, walielewa kabisa kwamba musalaba haupaswe kuabudiwa, kwa sababu walijua kwamba ni vibaya kuabudu sanamu. (1 Kor. 10:14; 1 Yoh. 5:21) Mwanzo-mwanzo wa mwaka wa 1883, gazeti Munara wa Mulinzi lilionyesha waziwazi kwamba “kila ibada ya sanamu ni chukizo kwa Mungu.” Hata hivyo, hapo mwanzo, Wanafunzi wa Biblia hawakuona ubaya wowote wa kutumia musalaba kwa njia ambayo inafaa. Kwa mufano, kwenye mavazi walikuwa wanajivunia kuvaa taji yenye kuwa na musalaba ili kujitambulisha. Walifikiri alama hiyo ilimaanisha tu kwamba ikiwa wanabaki waaminifu mupaka kufa watapokea taji la uzima. Kuanzia mwaka wa 1891, alama ya taji yenye kuwa na musalaba ilionekana kwenye jalada la gazeti Munara wa Mulinzi.

13. Ni mwangaza gani wafuasi wa Kristo walipata kuhusu matumizi ya musalaba? (Soma pia kisanduku  “Tuliendelea Kupata Mwangaza Kuhusu Musalaba.”)

13 Wanafunzi wa Biblia walipenda sana kuwa na alama hiyo yenye musalaba. Lakini kuanzia mwisho-mwisho wa miaka ya 1920, walipata mwangaza hatua kwa hatua kuhusu matumizi ya musalaba. Ndugu Grant Suiter, ambaye kisha alitumikia katika Baraza Lenye Kuongoza, alikumbuka habari ambayo ilitolewa kwenye mukusanyiko wa Detroit, Michigan, Amerika. Alisema hivi: “Kwenye mukusanyiko huo ilionyeshwa wazi kuwa si lazima kuitumia alama ya taji yenye kuwa na musalaba, na pia kwamba ni chukizo na haikubaliwe.” Katika miaka fulani ambayo ilifuata kulitolewa mafasirio mengine zaidi kuhusu musalaba. Ilionyeshwa wazi kwamba musalaba haukuwa na nafasi katika ibada safi na yenye kutakata kiroho.

14. Watu wa Mungu walifanya nini wakati walipata mwangaza kuhusu musalaba?

14 Watu wa Mungu walifanya nini wakati walipata mwangaza huo ambao ulizidi kuongezeka kuhusu musalaba? Waliendelea kutumia alama ya taji yenye kuwa na musalaba, ambayo walikuwa wanapenda sana? Dada Lela Roberts ambaye alimutumikia Yehova kwa miaka mingi, alisema hivi: “Wakati tulijua kwamba ni alama ya kipagani, tuliachana nayo bila kusita.” Dada mwengine mwaminifu anayeitwa Ursula Serenco, alionyesha mawazo ya ndugu wengi kuhusu musalaba. Alisema hivi: “Tulifikia kutambua kwamba alama ambayo tulipenda sana na kufikiri kuwa inaonyesha kifo cha Bwana wetu, na kwamba ni alama ambayo inaonyesha kujitoa kwa Mukristo, ilikuwa kabisa alama ya kipagani. Kulingana na andiko la Methali 4:18, tulifurahi kuona kwamba nuru inayongaa sana ilizidi kuongezeka.” Wafuasi waaminifu wa Kristo walipenda kuachana kabisa na desturi chafu za dini ya uongo!

15, 16. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tumeazimia kufanya uwanja wa hekalu la kiroho la Yehova hapa duniani uendelee kuwa safi?

15 Leo, tunaunga mukono azimio la Wakristo hao. Tunatambua kwamba Kristo ameendelea kutumia njia ambayo inaonekana wazi, ni kusema, mutumwa mwaminifu na mwenye busara, ili kusaidia watu wa Mungu waendelee kuwa safi kiroho. Kwa hiyo, wakati chakula cha kiroho ambacho tunapata kinatuonya kuhusu sikukuu fulani, desturi fulani ao tabia ambazo zimechafuliwa na dini ya uongo, tutatii bila kukawia. Kama vile ndugu na dada zetu ambao waliishi katika miaka ya mwanzo-mwanzo ya kuwapo kwa Kristo, tumeazimia kufanya viwanja vya hekalu la kiroho la Yehova hapa duniani viendelee kuwa safi.

16 Pia katika siku hizi za mwisho, Kristo ameendelea kufanya mambo fulani ambayo hayaonekane kwa macho yetu ili kulinda makutaniko ya watu wa Yehova yasiambukizwe na watu wabaya. Amefanya hivyo namna gani? Acha tuone.

Kutenganisha “Waovu Kutoka Katikati ya Waadilifu”

17, 18. Katika mufano wa wavu inamaanisha nini: (a) kushusha wavu ndani ya bahari? (b) “kukusanya samaki wa kila aina?” (c) kukusanya samaki walio wazuri ndani ya vyombo?, na (d) kutupa mbali samaki wasiofaa?

17 Mufalme Yesu Kristo anaendelea kukesha na kulinda makutaniko ya watu wa Mungu duniani pote. Kwa njia ambazo hazionekane kwa macho yetu, Kristo na malaika wameendelea kufanya kazi ya kutenganisha watu. Yesu alizungumuzia kazi hiyo katika mufano wake wa wavu. (Soma Mathayo 13:47-50.) Mufano huo unamaanisha nini?

TWavu unafananisha kazi ya kuhubiri Ufalme ambayo inafanyika katika bahari inayofananisha wanadamu (Ona fungu la 18)

18 Kushusha “wavu . . . ndani ya bahari.” Wavu unafananisha kazi ya kuhubiri Ufalme ambayo inafanyika katika bahari, ambayo inafananisha wanadamu. “Kukusanya samaki wa kila aina.” Habari njema inavuta watu wa kila aina, ni kusema, wale wote ambao wanachukua hatua ya kuwa Wakristo wa kweli, na vilevile wale ambao mwanzoni wanaonyesha kupendezwa, lakini wanakosa kushikamana kabisa na ibada safi. * Kukusanya samaki “walio wazuri ndani ya vyombo.” Watu wenye mioyo mizuri wanakusanywa katika vyombo ambavyo vinafananisha makutaniko, ambamo wanaweza kumutolea Yehova ibada safi. Kutupa mbali samaki “wasiofaa.” Katika siku hizi za mwisho, Kristo na malaika wameendelea kuwatenganisha “waovu kutoka katikati ya waadilifu [ao wenye haki].” * Ndio sababu, wale watu wasio na mioyo mizuri, ni kusema, wale ambao wanakataa kuachana na desturi ao imani yao ya uongo hawaruhusiwe kuchafua makutaniko. *

19 Unajisikia namna gani unapofikiria mambo ambayo Kristo amefanya ili kulinda usafi wa watu wa Mungu na usafi wa ibada ya kweli?

19 Hauone kwamba ni jambo lenye kutia moyo kujua kwamba Mufalme wetu, Yesu Kristo analinda wafuasi wake? Hauone kwamba ni jambo lenye kutia moyo kuona kwamba bidii yake kwa ajili ya ibada ya kweli na kwa ajili ya waabudu wa kweli ni ileile ambayo alionyesha kwa kusafisha hekalu wakati alikuwa hapa duniani? Sisi ni wenye shukrani sana kuona kwamba Kristo ameendelea kufanya kazi ya kulinda watu wa Mungu na usafi wa kiroho wa ibada ya kweli! Tunaweza kuonyesha kwamba tunaunga mukono Mufalme na Ufalme wake kwa kuepuka kabisakabisa uhusiano wowote na dini ya uongo.

^ fu. 2 Wayahudi ambao walikuja Yerusalemu kutoka mbali walipaswa kutumia feza za mahali hapo ili kulipa kodi ya hekalu ya kila mwaka. Kwa hiyo, wabadilisha-feza waliwaomba malipo ili kubadilisha feza zao katika feza ambazo ziliombwa. Tena, walihitaji kuuza wanyama ili kutoa sadaka. Yesu aliita wafanyabiashara hao ‘wanyanganyi’ kwa sababu inaonekana kwamba waliuzisha kwa bei kali na waliomba malipo kwa sababu ya kazi mbalimbali ambazo walikuwa wanafanya.

^ fu. 4 Watu wa Yehova hapa duniani wanamuabudu Yehova katika viwanja vya duniani vya hekalu kubwa la kiroho.

^ fu. 10 Habari hii ilionyesha kwamba tarehe ambayo inafikiriwa kuwa ndio wakati Yesu alizaliwa ni kipindi cha baridi kali. Tarehe hiyo “haipatane na habari ambayo inasema kwamba wachungaji walikuwa inje pamoja na wanyama wao.”—Lu. 2:8.

^ fu. 18 Ndugu Frederick W. Franz, katika barua yake mwenyewe ya tarehe 14 Mwezi wa 11, 1927, aliandika hivi: “Katika mwaka huu hatutakuwa na sikukuu ya Noeli. Ndugu wa Beteli wameamua kwamba hawatafanya tena sikukuu ya Noeli.” Pia katika barua yake ya tarehe 6 Mwezi wa 2, 1928, ambayo aliandika kisha miezi kidogo, Ndugu Franz aliandika hivi: “Hatua kwa hatua, Bwana ameendelea kutusafisha ili tusichafuliwe na udanganyifu wa tengenezo la Babiloni ambalo linaongozwa na Ibilisi.”

^ fu. 18 Kwa mufano, katika mwaka wa 2013, tulikuwa wahubiri 7 965 254, lakini wale ambao walihuzuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo walikuwa 19 241 252.

^ fu. 18 Mufano wa kutenganisha samaki wazuri na samaki wabaya ni tofauti na mufano wa kutenganisha kondoo na mbuzi. (Mt. 25:31-46) Kazi ya kutenganisha ao hukumu ya mwisho ya kondoo na mbuzi itafanyika wakati wa ile ziki kubwa ambayo inakuja. Mupaka sasa, wote walio kama samaki wabaya wanaweza kumurudilia Yehova na kukusanywa katika vyombo ambavyo vinafananisha makutaniko.—Mal. 3:7.

Kwa mwisho, watu wasio na mioyo mizuri watatupwa kwa njia ya mufano katika tanuru ya moto unaowaka, ni kusema, kuharibiwa kabisa.