Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 11

Usafi wa Maadili​—Unaonyesha Utakatifu wa Mungu

Usafi wa Maadili​—Unaonyesha Utakatifu wa Mungu

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Jinsi ambavyo Mfalme amewafundisha watu wake kuheshimu viwango vya Mungu vya maadili

Hebu wazia ukiingia katika lango linaloelekea kwenye ua wa nje wa hekalu kuu la kiroho la Yehova

1. Ezekieli aliona jambo gani linalotustaajabisha?

UNGEHISIJE ikiwa ungeona jambo kama lile aliloona nabii Ezekieli karne 25 hivi zilizopita? Hebu wazia: Unakaribia jengo kubwa la hekalu linalong’aa. Malaika mwenye nguvu yuko hapo kukuonyesha eneo hilo tukufu! Unapanda ngazi saba zinazoelekea kwenye moja kati ya malango matatu. Malango hayo yanakustaajabisha sana. Yana kimo cha meta 30 hivi. Katika miingilio yake, unaona vyumba vya walinzi. Kuna nguzo zenye umbo la mitende mirefu.—Eze. 40:1-4, 10, 14, 16, 22; 41:20.

2. (a) Hekalu la kiroho linawakilisha nini? (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Vitu vilivyo kwenye miingilio ya hekalu vinatufundisha nini?

2 Hayo ni maono ya hekalu la kiroho. Ezekieli alilifafanua kwa kina sana hivi kwamba maelezo yake yanajaza sura ya 40 hadi 48 za kitabu chake cha unabii. Hekalu hilo linawakilisha mpango wa Yehova wa ibada safi. Kila sehemu ya hekalu hilo inatufundisha jambo fulani kuhusu ibada yetu katika siku hizi za mwisho. * Malango marefu yanamaanisha nini? Yanatukumbusha kwamba wote wanaoingia katika mpango wa Yehova wa ibada safi lazima waishi kulingana na viwango vya juu na vinyoofu vya Mungu. Hata ile michongo ya miti ya mitende inaonyesha jambo hilo, kwa sababu nyakati nyingine katika Biblia mitende inawakilisha unyoofu. (Zab. 92:12) Namna gani vyumba vya walinzi? Kwa kweli, wale wanaoshindwa kuheshimu viwango vya Mungu hawaruhusiwi kuingia katika mpango huu mzuri wa ibada safi unaoongoza kwenye uhai.—Eze. 44:9.

3. Kwa nini wafuasi wa Kristo wamehitaji kuendelea kusafishwa?

3 Maono ya Ezekieli yametimizwaje? Kama tulivyoona katika Sura ya 2 ya kitabu hiki, Yehova alimtumia Kristo kuwasafisha watu wake kwa njia ya kipekee kuanzia mwaka wa 1914 hadi mapema mwaka wa 1919. Je, kusafishwa huko kulikoma wakati huo? Hapana! Kwa karne yote iliyopita, Kristo ameendelea kuhakikisha kwamba viwango vitakatifu vya Yehova kuhusu mwenendo vinafuatwa. Hivyo wafuasi wake wamehitaji kuendelea kusafishwa. Kwa nini? Kwa sababu Kristo amekuwa akikusanya wafuasi wake kutoka katika ulimwengu huu uliopotoka kimaadili na Shetani hajaacha kamwe kujaribu kuwarudisha tena kwenye upotovu wa maadili. (Soma 2 Petro 2:20-22.) Acheni tuchunguze maeneo matatu ambayo Wakristo wa kweli wamekuwa wakisafishwa hatua kwa hatua. Kwanza, tutazungumzia jinsi tulivyosafishwa kuhusiana na maadili, kisha maandalizi muhimu ya kulifanya kutaniko liendelee kubaki likiwa safi, na mwishowe mpango wa familia.

Kusafishwa Kimaadili Kadiri Miaka Ilivyopita

4, 5. Kwa muda mrefu Shetani ametumia mbinu gani, na amepata mafanikio gani?

4 Sikuzote watu wa Yehova wamekuwa makini kuhusiana na mwenendo safi kiadili. Hivyo, wamefuata maagizo yaliyo wazi kuhusu maadili. Fikiria mifano michache.

5 Mwenendo mpotovu kingono. Yehova alikusudia uhusiano wa kingono kati ya wenzi wa ndoa uwe safi na wafurahie. Shetani anatumia zawadi hiyo nzuri kuwashawishi watu wa Yehova waitumie kwa njia isiyofaa na hivyo waharibu uhusiano wao pamoja na Mungu. Shetani alifanikiwa kutumia mbinu hiyo katika siku za Balaamu na kukawa na matokeo mabaya, na amekuwa akiitumia sana katika siku hizi za mwisho kuliko wakati mwingine wowote.—Hes. 25:1-3, 9; Ufu. 2:14.

6. Ni nadhiri gani iliyochapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi, nayo ilikuwa na kusudi gani, na kwa nini baadaye iliacha kutumiwa? (Ona pia maelezo ya chini.)

6 Ili kupinga jitihada za Shetani, gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1908, lilichapisha nadhiri ambayo ilitia ndani ahadi hii: “Nyakati zote na mahali popote, nitajiendesha kwa njia inayofaa kuelekea watu wa jinsia tofauti iwe ni hadharani au faraghani.” * Wengi waliiweka nadhiri hiyo ingawa haikuwa lazima, na wakapeleka majina yao yachapishwe kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi. Miaka mingi baadaye, ilionekana kwamba ingawa nadhiri hiyo iliwasaidia wengi wakati huo, ilianza kuchukuliwa kidesturi; kwa hiyo ikaacha kutumiwa. Hata hivyo, viwango vyake vya juu vya maadili vilifuatwa sikuzote.

7. Katika mwaka wa 1935, gazeti Mnara wa Mlinzi lilizungumzia tatizo gani, na lilikazia jambo gani?

7 Shetani alizidisha mashambulizi yake. Toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1935, lilizungumzia waziwazi tatizo lililokuwa likienea miongoni mwa watu wa Mungu. Baadhi ya watu wa Mungu walifikiri kwamba maadamu wanashiriki katika huduma haidhuru ikiwa hawafuati viwango vya Yehova vya maadili katika maisha yao ya kibinafsi. Gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema hivi waziwazi: “Kila mtu anapaswa kukumbuka kwamba kushiriki tu katika kazi ya kutoa ushahidi si ndilo takwa pekee kwa Mkristo. Mashahidi wa Yehova ni wawakilishi wake, na ni wajibu wao kumwakilisha Yehova na ufalme wake kwa njia inayofaa.” Kisha makala hiyo ilitoa shauri lililo wazi kuhusu ndoa na maadili, na hivyo kuwasaidia watu wa Mungu ‘kuukimbia uasherati.’—1 Kor. 6:18.

8. Kwa nini gazeti Mnara wa Mlinzi limekazia tena na tena maana kamili ya neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa mwenendo mpotovu kingono?

8 Katika miaka ya karibuni zaidi, gazeti Mnara wa Mlinzi limekazia tena na tena maana sahihi ya neno linalotumiwa katika Maandiko ya Kigiriki kuhusu mwenendo mpotovu kingono—por·neiʹa. Neno hilo halimaanishi tu kufanya ngono. Badala yake, por·neiʹa inatia ndani matendo mengi mapotovu kiadili, kwa ujumla inahusisha matendo yote machafu yanayofanywa katika nyumba za makahaba. Hivyo wafuasi wa Kristo wamelindwa dhidi ya wimbi la upotovu wa maadili kingono ambalo limewafunika watu wengi leo.—Somo Waefeso 4:17-19.

9, 10. (a) Gazeti Mnara wa Mlinzi lilizungumzia suala gani kuhusu maadili mwaka wa 1935? (b) Biblia inafundisha nini kuhusu matumizi ya pombe?

9 Kutumia kileo kupita kiasi. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1935, lilizungumzia suala lingine kuhusu maadili: “Imeonekana kwamba baadhi ya watu wa Mungu wanashiriki katika utumishi wa shambani na kufanya kazi nyingine za tengenezo wakiwa wametumia [pombe]. Maandiko yanaruhusu kutumia pombe chini ya hali gani? Je, ingefaa kutumia pombe hivi kwamba inaathiri utumishi wako katika tengenezo la Bwana?”

10 Jibu lilionyesha maoni yaliyosawazika ya Neno la Mungu kuhusu pombe. Biblia haikatazi kutumia divai na aina nyingine za pombe kwa kiasi, lakini inashutumu vikali ulevi. (Zab. 104:14, 15; 1 Kor. 6:9, 10) Inapohusu kushiriki katika utumishi mtakatifu wakiwa wametumia kileo, kwa muda mrefu watumishi wa Mungu wamekumbushwa tena na tena kuhusu kisa cha wana wa Haruni, ambao waliuawa na Mungu kwa sababu ya kutoa moto haramu kwenye madhabahu ya Mungu. Muda mfupi baadaye, simulizi hilo linafunua kile ambacho huenda kilisababisha wanaume hao kufanya jambo hilo lisilofaa, kwa kuwa Mungu alitoa sheria iliyowakataza makuhani wote kutumia kileo wanapotoa utumishi wao mtakatifu. (Law. 10:1, 2, 8-11) Wakifuata kanuni hiyo leo, wafuasi wa Kristo wanaepuka kutumia kileo wanaposhiriki katika utumishi mtakatifu.

11. Watu wa Mungu wamenufaikaje kwa kupata uelewaji zaidi kuhusu uraibu wa kileo?

11 Katika miaka ya karibuni zaidi, wafuasi wa Kristo wamenufaika kwa kupata uelewaji zaidi kuhusu uraibu wa kileo, au kutumia kileo kupita kiasi. Kupitia chakula cha kiroho kinachotolewa kwa wakati unaofaa, watu wengi wamesaidiwa kukabiliana vizuri na hali hiyo na kudhibiti tena maisha yao. Wengine wamesaidiwa kushinda tatizo hilo kabisa. Hatupaswi kuruhusu matumizi mabaya ya kileo yaharibu heshima, familia na, zaidi ya yote, pendeleo letu la kushiriki katika ibada safi ya Yehova.

“Hatuwezi kuwazia Bwana wetu akinuka moshi wa tumbaku au akiweka kitu chochote kichafu mdomoni mwake.”—C. T. Russell

12. Watumishi wa Kristo walikuwa na maoni gani kuhusu matumizi ya tumbaku hata kabla ya siku za mwisho kuanza?

12 Matumizi ya tumbaku. Watumishi wa Kristo walianza kupinga matumizi ya tumbaku hata kabla ya siku za mwisho kuanza. Miaka mingi iliyopita, Charles Capen, ndugu mzee, anakumbuka kilichotukia alipokutana na Charles Taze Russell kwa mara ya kwanza mwishoni mwa karne ya 19. Capen, ambaye alikuwa na umri wa miaka 13 wakati huo, pamoja na ndugu zake watatu walikuwa kwenye ngazi katika jengo lililoitwa Bible House huko Allegheny, Pennsylvania. Russell alipokuwa akipita aliwauliza: “Ninyi vijana mnavuta sigara? Kuna harufu ya sigara hapa.” Walimwambia kwamba hawakuwa wakivuta sigara. Kwa hakika jambo hilo lilionyesha wazi maoni yake kuhusu sigara. Katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1895, Ndugu Russell alielezea andiko la 2 Wakorintho 7:1, akisema: “Kwa maoni yangu, Mkristo anayetumia tumbaku kwa njia yoyote ile, hamletei Mungu utukufu wala kujifaidi yeye mwenyewe. . . . Hatuwezi kuwazia Bwana wetu akinuka moshi wa tumbaku au akiweka kitu chochote kichafu mdomoni mwake.”

13. Katika mwaka wa 1973, watu wa Mungu walipata uelewaji gani kuhusu maadili?

13 Katika mwaka wa 1935, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba tumbaku ni “jani chafu” na likasema kwamba mtu yeyote ambaye angetafuna au kuvuta tumbaku hangeendelea kuwa mshiriki wa familia ya Betheli au kutumikia akiwa mwakilishi wa tengenezo la Mungu akiwa painia au mhudumu anayesafiri. Mwaka wa 1973, watu wa Mungu walipata uelewaji zaidi kuhusu maadili. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 1 lilieleza kwamba Shahidi wa Yehova hangeendelea kuwa na msimamo mzuri katika kutaniko ikiwa angeendelea kuwa na zoea hilo hatari, chafu, na lisilo la upendo. Wale wote ambao walikataa kuacha matumizi mabaya ya tumbaku walipaswa kutengwa na ushirika. * Kristo alikuwa amechukua hatua nyingine muhimu ili kuwasafisha wafuasi wake.

14. Mungu ana maoni gani kuhusu damu, na zoea la kutia damu mishipani lilikujaje kuwa jambo la kawaida?

14 Matumizi mabaya ya damu. Katika siku za Noa, Mungu alisema kwamba ni kosa kula damu. Alirudia jambo hilo katika Sheria yake kwa taifa la Israeli, na pia aliliamuru kutaniko la Kikristo “kujiepusha . . . na damu.” (Mdo. 15:20, 29; Mwa. 9:4; Law. 7:26) Haishangazi kwamba katika siku zetu Shetani ametafuta mbinu ya kuwashawishi watu wengi wasitii sheria hiyo ya Mungu. Katika karne ya 19, madaktari walikuwa wakifanya majaribio ya kuwatia watu damu mishipani, lakini baada ya wataalamu kugundua aina za damu, zoea hilo lilienea sana. Katika mwaka wa 1937, damu ilianza kukusanywa na kuhifadhiwa katika benki za damu, na pia Vita vya Pili vya Ulimwengu vilichangia sana matumizi hayo ya damu. Muda si muda, kutia damu mishipani kukawa jambo la kawaida ulimwenguni pote.

15, 16. (a) Mashahidi wa Yehova walichukua msimamo gani kuhusu kutiwa damu mishipani? (b) Ni msaada gani ambao wafuasi wa Kristo wamepata kuhusu kutiwa damu mishipani na matibabu yasiyohusisha damu, na kumekuwa na matokeo gani?

15 Mapema mwaka wa 1944, gazeti Mnara wa Mlinzi lilionyesha kwamba kutiwa damu mishipani ni njia nyingine ya kula damu. Mwaka uliofuata, msimamo huo wa Kimaandiko ulifafanuliwa na kukaziwa zaidi. Kufikia mwaka wa 1951, orodha ya maswali na majibu ilichapishwa ili kuwasaidia watu wa Mungu kujua jinsi ya kushughulika na wataalamu wa tiba. Ulimwenguni pote, wafuasi waaminifu wa Kristo walichukua msimamo thabiti, mara nyingi walikabiliana na dharau, uhasama, na hata mateso. Hata hivyo, Kristo aliendelea kuliongoza tengenezo lake liandae msaada uliohitajiwa. Broshua na makala zilizofanyiwa utafiti wa kina zilichapishwa.

16 Katika mwaka wa 1979, baadhi ya wazee walianza kutembelea hospitali ili kuwasaidia madaktari kuelewa vizuri msimamo wetu kuhusu damu, sababu za Kimaandiko, na matibabu mengine yasiyohusisha damu. Katika mwaka wa 1980, wazee katika majiji 39 nchini Marekani walipata mazoezi maalumu kwa ajili ya kazi hiyo. Baada ya muda, Baraza Linaloongoza lilikubali Halmashauri za Uhusiano na Hospitali zianzishwe ulimwenguni pote. Je, jitihada hizo zimefanikiwa kadiri wakati ulivyopita? Leo, makumi ya maelfu ya wataalamu wa tiba—kutia ndani madaktari wanaofanya upasuaji, madaktari, wataalamu wa unusukaputi—wanashirikiana na Mashahidi ambao ni wagonjwa, wakiheshimu uamuzi wetu wa kutibiwa bila kutiwa damu mishipani. Hospitali nyingi zinatoa matibabu yasiyohusisha damu, baadhi ya hospitali hizo hata zinaona matibabu hayo kuwa bora kabisa. Je, si jambo linalotia moyo kuona jinsi ambavyo Yesu amewalinda wafuasi wake dhidi ya jitihada za Shetani za kuwachafua?—Soma Waefeso 5:25-27.

Hospitali nyingi zinatoa matibabu yasiyohusisha damu, baadhi ya hospitali hizo hata zinaona matibabu hayo kuwa bora kabisa

17. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini jinsi ambavyo Kristo amekuwa akiwasafisha wafuasi wake?

17 Inafaa tujiulize, ‘Je, tunathamini jinsi ambavyo Kristo amekuwa akiwasafisha wafuasi wake, akitufundisha kufuata viwango vya juu vya maadili vya Yehova?’ Ikiwa ndivyo, acheni basi tukumbuke kwamba siku zote Shetani anatafuta njia ya kututenganisha na Yehova na Yesu kwa kutufanya tusiheshimu viwango vya Mungu vya maadili. Ili kutulinda na ushawishi huo, kwa upendo tengenezo la Yehova limeendelea kutuonya na kutukumbusha kuhusu upotovu wa maadili wa ulimwengu huu. Na tuwe macho, tukubali, na tutii mashauri tunayopokea.—Met. 19:20.

Kulilinda Kutaniko Dhidi ya Shutuma za Kimaadili

18. Maono ya Ezekieli yanatukumbusha jambo gani lililo wazi kuhusu wale wanaovunja kimakusudi viwango vya Mungu?

18 Sehemu ya pili ya usafishaji wa kimaadili inahusisha hatua zinazochukuliwa ili kulinda usafi wa kutaniko. Inasikitisha kwamba si wote ambao wanakubali viwango vya Yehova na kujiweka wakfu kwa Mungu hushikilia kwa ushikamanifu uamuzi wao. Mwishowe baadhi yao hubadili uamuzi wao na kuvunja kimakusudi viwango hivyo. Watu hao wanapaswa kuchukuliwa hatua gani? Tunaweza kupata jibu katika maono ya Ezekieli ya hekalu la kiroho lililozungumziwa mwanzoni mwa sura hii. Kumbuka yale malango marefu. Katika kila mwingilio, kulikuwa na vyumba vya walinzi. Walinzi wangelinda hekalu, huenda ili kumzuia mtu yeyote ambaye “hajatahiriwa moyoni” asiingie. (Eze. 44:9) Hicho ni kikumbusho kilicho wazi kwamba ibada safi ni pendeleo wanalopewa wale tu wanaojitahidi kuishi kulingana na viwango safi vya mwenendo vya Yehova. Vivyo hivyo leo, si kila mtu ana pendeleo la kushirikiana na Wakristo katika ibada safi.

19, 20. (a) Kristo amewasaidiaje hatua kwa hatua wafuasi wake kurekebisha jinsi ya kushughulikia visa vya dhambi nzito? (b) Ni sababu gani tatu zinazofanya wakosaji wasiotubu watengwe na ushirika?

19 Huko nyuma katika mwaka wa 1892, gazeti Mnara wa Mlinzi lilieleza kwamba “ni wajibu wetu kuwatenga Wakristo ambao, wanakataa waziwazi au kwa njia isiyo wazi kwamba Kristo alijitoa mwenyewe kuwa fidia . . . kwa ajili ya wote.” (Soma 2 Yohana 10.) Mwaka wa 1904, kitabu The New Creation kilieleza kwamba wote wanaoendelea kujihusisha katika mwenendo mbaya wanalihatarisha kutaniko. Wakati huo, kutaniko zima lingehusika katika kushughulikia visa vya dhambi nzito na kutoa hukumu. Hata hivyo, jambo hilo lilitokea mara chache. Mwaka wa 1944, gazeti Mnara wa Mlinzi lilionyesha kwamba ndugu wenye madaraka tu ndio waliopaswa kushughulikia visa hivyo. Katika mwaka wa 1952, utaratibu wa Kimaandiko wa kushughulikia mambo ya kihukumu ulichapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi, ukifafanua kwamba sababu ya msingi ya kuwatenga na ushirika wale wasiotubu ni kulinda usafi wa kutaniko.

20 Kwa miaka mingi tangu wakati huo, Kristo amewasaidia wafuasi wake kuelewa na kurekebisha njia ya kushughulikia makosa mazito. Wazee Wakristo wanazoezwa kushughulikia mambo ya kihukumu kwa njia ya Yehova, wakionyesha haki na rehema kwa usawaziko. Leo tunaona waziwazi angalau sababu tatu za kuchukua hatua za kumtenga na ushirika wa kutaniko mkosaji asiyetubu: (1) ili jina la Yehova lisishutumiwe, (2) ili kulinda kutaniko lisichafuliwe na matokeo ya dhambi nzito, na (3) ili kumsaidia mkosaji atubu ikiwezekana.

21. Mpango wa kutenga na ushirika umekuwa na manufaa gani kwa watu wa Mungu?

21 Je, unaona jinsi ambavyo mpango wa kutenga na ushirika umekuwa wenye manufaa kwa wafuasi wa Kristo leo? Katika Israeli la kale, mara nyingi wakosaji wangekuwa na uvutano mbaya kwa taifa hilo, nyakati fulani hata walikuwa wengi kuliko wale waliompenda Yehova na kutaka kufanya yaliyo sawa. Hivyo, mara nyingi taifa hilo lililetea suto jina la Yehova na kupoteza kibali cha Mungu. (Yer. 7:23-28) Lakini leo, Yehova hashughuliki na taifa fulani hususa, anashughulika na wanaume na wanawake wa kiroho. Kwa kuwa wakosaji wasiotubu wanaondolewa katikati yetu, Shetani hapati nafasi ya kuwatumia kuendelea kuliharibu kutaniko na viwango vyake safi. Badala yake, uvutano wao unapunguzwa. Hivyo, tukiwa kikundi, tunahakikishiwa kwamba tutaendelea kupata kibali cha Yehova. Kumbuka kwamba Yehova aliahidi hivi: “Hakuna silaha itakayofanywa juu yako itakayofanikiwa.” (Isa. 54:17) Je, tunawaunga mkono kwa ushikamanifu wazee, ambao wana daraka zito la kushughulikia visa vya hukumu?

Kumtukuza Yeye Ambaye Kila Familia Hupata Jina Kutokana Naye

22, 23. Kwa nini tunawathamini Wakristo wenzetu walioishi mapema katika karne ya 20, lakini ni nini kinachoonyesha kwamba usawaziko kuhusu familia ulihitajika?

22 Sehemu ya tatu ambayo wafuasi wa Kristo wamefaidika kwa kuendelea kusafishwa inahusiana na ndoa na maisha ya familia. Je, maoni yetu kuhusu familia yamerekebishwa kadiri miaka ilivyopita? Ndiyo. Kwa mfano, tunaposoma kuhusu watumishi wa Mungu walioishi mapema katika karne ya 20, tunavutiwa sana na jinsi ambavyo walijidhabihu. Tunathamini sana kwamba walitanguliza utumishi mtakatifu katika maisha yao. Pamoja na hayo, tunaweza kuona kwamba usawaziko ulihitajika. Jinsi gani?

23 Lilikuwa jambo la kawaida kwa akina ndugu kwenda kuhubiri au kufanya kazi ya kusafiri mbali na familia zao kwa miezi mingi mfululizo. Nyakati nyingine, machapisho yetu yalikazia sana useja kuliko hata Maandiko yalivyoukazia, wakati huohuo hakukuwa na habari nyingi kuhusu jinsi ya kuimarisha ndoa za Kikristo. Je, bado wafuasi wa Kristo wana maoni kama hayo leo? Hapana!

Migawo ya Kitheokrasi haipaswi kuingilia wajibu wa kifamilia

24. Kristo aliwasaidiaje watu wake waaminifu kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu ndoa na familia?

24 Leo, migawo ya Kitheokrasi haipaswi kuingilia wajibu wa kifamilia. (Soma 1 Timotheo 5:8.) Zaidi ya hilo, Kristo amehakikisha kwamba wafuasi wake waaminifu duniani wanaendelea kupata habari nyingi za Kimaandiko zilizosawazika kuhusu ndoa na maisha ya familia. (Efe. 3:14, 15) Katika mwaka wa 1978, Kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha kilichapishwa. Miaka 18 hivi baadaye, kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia kikachapishwa. Zaidi ya hayo, gazeti Mnara wa Mlinzi limechapisha makala nyingi ambazo zimekusudiwa kuwasaidia wenzi wa ndoa watumie kanuni za Maandiko katika ndoa zao.

25-27. Kwa miaka mingi, mahitaji ya watoto wa umri tofauti-tofauti yametoshelezwa jinsi gani?

25 Vipi kuhusu watoto na vijana? Kwa miaka mingi, mahitaji yao yametoshelezwa. Tangu zamani, tengenezo la Yehova limewaandalia machapisho mazuri watoto wenye umri tofauti-tofauti. Wakati fulani machapisho hayo yalikuwa machache lakini sasa yanapatikana kwa wingi sana. Kwa mfano, kuanzia mwaka wa 1919 hadi mwaka wa 1921 gazeti The Golden Age lilikuwa na makala Funzo la Biblia kwa Vijana.” Baada ya hapo, broshua The Golden Age ABC ilichapishwa mwaka wa 1920 na kitabu Children katika mwaka wa 1941. Katika miaka ya 1970, vitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu, Kupata Faida Zote za Ujana Wako, na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia vilitolewa. Katika mwaka wa 1982, mfululizo wa makala “Vijana Huuliza” ulianza kuchapishwa katika gazeti Amkeni!, makala hizo zilitumiwa katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa mwaka wa 1989.

Broshua Masomo Yangu ya Biblia ilipokelewa kwa shangwe katika kusanyiko hili nchini Ujerumani

26 Leo, tuna mabuku mawili ya karibuni zaidi ya Vijana Huuliza, wakati huohuo mfululizo huo unaendelea kuwekwa katika Tovuti yetu ya jw.org. Pia tuna kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Tovuti yetu ina habari nyingi kwa ajili ya vijana, zinazotia ndani kadi za wahusika katika Biblia, mazoezi ya kujifunza Biblia kwa ajili watoto wenye umri mkubwa na mdogo, video, hadithi za Biblia zilizochorwa, na pia masomo ya Biblia kwa ajili ya watoto wasiozidi umri wa miaka mitatu. Ni wazi kwamba maoni ya Kristo kuhusu vijana hayajabadilika tangu wakati alipowakumbatia watoto wachanga katika karne ya kwanza. (Marko 10:13-16) Anataka vijana miongoni mwetu wahisi wanapendwa na wanalishwa vizuri kiroho.

27 Pia Yesu anataka watoto walindwe dhidi ya madhara. Kadiri ulimwengu huu unavyozidi kupotoka kimaadili, ndivyo visa vya kuwatendea watoto vibaya vinazidi kuenea. Hivyo, habari zilizo wazi na zinazoeleweka zimechapishwa ili kuwasaidia wazazi wawalinde watoto wao dhidi ya matendo hayo mabaya. *

28. (a) Kama ilivyoonyeshwa katika maono ya Ezekieli ya hekalu, ni lazima tufanye nini ikiwa tunataka kushiriki katika ibada safi? (b) Umeazimia kufanya nini?

28 Je, si jambo lenye kusisimua kutafakari jinsi ambavyo Kristo ameendelea kuwasafisha wafuasi wake, kuwazoeza kuheshimu viwango vya juu vya maadili vya Yehova, kuishi kupatana navyo, na kufaidika? Fikiria tena kuhusu hekalu ambalo Ezekieli aliona katika maono. Kumbuka malango marefu. Ni kweli kwamba hilo si hekalu halisi, bali la kiroho. Hata hivyo, je, tunaliona kuwa halisi? Tunaingia ndani yake, si tu kwa kwenda Jumba la Ufalme, kufungua Biblia au kupiga hodi mlangoni tunapokuwa katika huduma. Hayo ni mambo ambayo tunaweza kuona. Mnafiki anaweza kufanya mambo yote hayo pasipo kuingia kamwe katika hekalu la Yehova. Hata hivyo, tukifanya mambo hayo na wakati huohuo tuishi kulingana na viwango vya Yehova vya juu zaidi vya maadili na kushiriki katika ibada safi tukiwa na mtazamo unaofaa, tutakuwa tumeingia na kutumikia mahali hapo patakatifu zaidi, yaani, mpango wa ibada safi ya Yehova Mungu! Acheni tuendelee kuthamini pendeleo hilo bora. Acheni siku zote tuendelee kufanya yote tunayoweza ili tuonyeshe utukufu wa Yehova kwa kushikilia viwango vyake vya uadilifu!

^ fu. 2 Katika mwaka wa 1932, Buku la 2 la kitabu Vindication lilionyesha kwanza kwamba unabii wa Biblia unaohusu kurudishwa kwa watu wa Mungu katika nchi yao ulitimizwa katika siku zetu kwa Waisraeli wa kiroho, na si Waisraeli wa kimwili. Unabii huo unazungumzia kurudishwa kwa ibada safi. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1999, lilieleza kwamba maono ya Ezekieli kuhusu hekalu ni mojawapo ya unabii unaozungumzia kurudishwa kwa ibada safi na kwa hiyo unatimizwa kwa njia muhimu kiroho katika siku za mwisho.

^ fu. 6 Nadhiri hiyo haikuruhusu mwanaume na mwanamke kuwa peke yao ndani ya chumba isipokuwa mlango uwe wazi kabisa—au ikiwa wao ni wenzi wa ndoa au wana uhusiano wa karibu sana wa kifamilia. Kwa miaka kadhaa, nadhiri hiyo ilisomwa kila siku ikiwa sehemu ya programu ya Ibada ya Asubuhi Betheli.

^ fu. 13 Matumizi mabaya ya tumbaku yanatia ndani kuivuta, kuitafuna, au kulima kwa ajili ya matumizi kama hayo.

^ fu. 27 Kwa mfano, ona sura ya 32 ya kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu; pia ona ukurasa wa 3-11 wa gazeti Amkeni! la Oktoba 2007.