Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 12

Tengenezo Linalomtumikia “Mungu wa Amani”

Tengenezo Linalomtumikia “Mungu wa Amani”

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Yehova anawapanga watu wake kitengenezo hatua kwa hatua

1, 2. Gazeti Zion’s Watch Tower lilifanyiwa marekebisho gani mnamo Januari 1895, na akina ndugu waliitikiaje badiliko hilo?

MWANAFUNZI wa Biblia mwenye bidii, John A. Bohnet, alifurahi sana alipopata gazeti Zion’s Watch Tower la Januari 1895. Gazeti hilo lilikuwa na jalada jipya kabisa—picha ya mnara mrefu wa taa ukiangaza anga lenye giza kwenye bahari iliyochafuka. Tangazo lililochapishwa katika gazeti hilo kuhusu muundo huo mpya lilikuwa na kichwa “Sura Yetu Mpya.”

2 Ndugu Bohnet alivutiwa sana na jalada hilo hivi kwamba alimwandikia barua Ndugu Russell. Aliandika hivi: “Ninafurahi kuona gazeti Mnara wa Mlinzi likipendeza sana. Ni maridadi sana.” Mwanafunzi mwingine mwaminifu wa Biblia, John H. Brown aliandika hivi kuhusu jalada hilo: “Linavutia sana. Mnara huo unasimama kwenye msingi imara huku mawimbi na dhoruba zikiupiga.” Jalada hilo jipya lilikuwa ndilo badiliko la kwanza ambalo ndugu zetu waliona mwaka huo—lakini huo ulikuwa mwanzo tu. Mwezi wa Novemba, walifahamishwa kuhusu badiliko lingine kubwa. Kwa kupendeza, lilihusu tena bahari yenye dhoruba.

3, 4. Ni tatizo gani lililozungumziwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1895, na ni badiliko gani kubwa lilitangazwa?

3 Makala ndefu iliyochapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1895, lilifunua wazi tatizo lililokuwa kama mawimbi yenye dhoruba ambalo lilikuwa likivuruga amani ya shirika, au tengenezo, la Wanafunzi wa Biblia. Akina ndugu walikuwa wakizozana kuhusu ni nani aliyepaswa kuwa kiongozi wa kutaniko. Ili kuwasaidia akina ndugu kujua walichohitaji kufanya ili kutatua roho hiyo ya ushindani inayosababisha migawanyiko, makala hiyo ilifananisha tengenezo na meli. Kisha ikakubali waziwazi kwamba ndugu waliokuwa wakiongoza hawakuwa wamelitayarisha tengenezo lililo kama meli kustahimili dhoruba kali. Walipaswa kufanya nini?

4 Makala hiyo ilisema kwamba nahodha mzuri huhakikisha kwamba meli ina vitu vinavyoweza kutumiwa kuokoa uhai na mabaharia wako tayari kufunga milango ya kushukia ndani ya meli wanapoona dhoruba ikija. Vivyo hivyo, ndugu waliokuwa wakiongoza katika tengenezo walipaswa kuhakikisha kwamba makutaniko yote yametayarishwa kukabiliana na hali zilizo kama dhoruba kali. Ili kutimiza hilo, makala hiyo ilitangaza badiliko kubwa sana. Iliagiza kwamba “katika kila kutaniko, wazee wachaguliwe” haraka iwezekanavyo ili “‘wasimamie’ kundi.”—Mdo. 20:28.

5. (a) Kwa nini mpango wa kwanza wa kuwa na wazee ulikuwa hatua muhimu? (b) Tutazungumzia maswali gani?

5 Mpango huo wa kwanza wa kuwa na wazee ulikuwa hatua muhimu katika kuanzishwa kwa utaratibu uliopaswa kufuatwa kutanikoni. Uliwasaidia ndugu zetu kukabiliana na misukosuko iliyosababishwa na Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Kwa makumi ya miaka iliyofuata, marekebisho mengine ya kitengenezo yaliwasaidia watu wa Mungu kumtumikia Yehova vizuri zaidi. Ni unabii gani wa Biblia uliotabiri kuhusu marekebisho hayo? Ni mabadiliko gani ya kitengenezo ambayo umejionea? Yamekunufaishaje?

“Nitaweka Amani Kuwa Waangalizi Wako”

6, 7. (a) Andiko la Isaya 60:17 linamaanisha nini? (b) Kutajwa kwa “waangalizi” na “wagawa-kazi” kunaonyesha nini?

6 Kama tulivyozungumzia katika Sura ya 9, Isaya alitabiri kwamba Yehova angewabariki watu wake kwa kufanya idadi yao iongezeke. (Isa. 60:22) Hata hivyo, Yehova aliahidi kufanya mengi zaidi. Katika unabii huohuo, alisema hivi: “Badala ya shaba nitaingiza dhahabu, na badala ya chuma nitaingiza fedha, na badala ya miti, shaba, na badala ya mawe, chuma; nami nitaweka amani kuwa waangalizi wako na uadilifu kuwa wagawa-kazi wako.” (Isa. 60:17) Unabii huo unamaanisha nini? Unatuhusuje leo?

Kitu kibaya hakibadilishwi kwa kitu kizuri, bali kitu kizuri kinabadilishwa kwa kitu kizuri zaidi

7 Unabii wa Isaya unasema kwamba kitu kimoja kingebadilishwa kwa kingine. Lakini ona kwamba kitu kibaya hakibadilishwi kwa kitu kizuri, bali kitu kizuri kinabadilishwa kwa kitu kizuri zaidi. Kubadilisha fedha kwa dhahabu ni maendeleo, na ndivyo ilivyo na vitu vingine vinavyotajwa katika unabii huo. Hivyo, kupitia unabii huo, Yehova alitabiri kwamba hali ya watu wake ingeboreshwa hatua kwa hatua. Unabii huo unazungumzia maendeleo ya aina gani? Kwa kutaja “waangalizi” na “wagawa-kazi,” Yehova alionyesha maendeleo ya hatua kwa hatua kuhusiana na jinsi ambavyo watu wake wangepangwa kitengenezo na kutunzwa.

8. (a) Ni nani anayeleta maendeleo yanayotajwa katika unabii wa Isaya? (b) Tunanufaikaje na maendeleo hayo? (Ona pia sanduku “ Alikubali kwa Unyenyekevu Kurekebishwa.”)

8 Ni nani anayeleta maendeleo hayo ya kitengenezo? Yehova anasema: “Nitaingiza dhahabu, . . . nitaingiza fedha, . . . nami nitaweka amani.” Kwa kweli, maendeleo ya utaratibu unaofuatwa kutanikoni hayaletwi na jitihada za wanadamu, bali na Yehova mwenyewe. Na tangu Yesu awekwe rasmi kuwa Mfalme, Yehova ameleta maendeleo hayo kupitia Mwana wake. Tunanufaikaje na mabadiliko hayo? Andiko hilohilo linasema kwamba maendeleo hayo yataleta “amani” na “uadilifu.” Tunapokubali mwongozo wa Mungu na kufanya marekebisho, tunakuwa na amani miongoni mwetu na kupenda uadilifu kunatuchochea kumtumikia Yehova, ambaye mtume Paulo alimtaja kuwa “Mungu wa amani.”—Flp. 4:9.

9. Ni msingi gani unaofaa ili kuwe na utaratibu na umoja katika kutaniko, na kwa nini?

9 Paulo pia aliandika hivi kumhusu Yehova: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.” (1 Kor. 14:33) Ona kwamba Paulo hakutofautisha machafuko na utaratibu, bali aliyatofautisha na amani. Kwa nini? Fikiria hili: Utaratibu peke yake hauleti hali zenye amani. Kwa mfano, huenda wanajeshi wakawa wamepangwa kwa utaratibu wakielekea vitani, lakini hawaendi kufanya amani bali kupigana vita. Hivyo, tukiwa Wakristo, tunataka kukumbuka jambo hili muhimu: Utaratibu wowote usio na msingi wa amani utavurugika punde si punde. Tofauti na hilo, amani kutoka kwa Mungu hufanya kuwe na utaratibu unaodumu. Kwa hiyo, tunashukuru sana kwamba tengenezo letu linaongozwa na kusafishwa na “Mungu anayetoa amani”! (Rom. 15:33) Amani kutoka kwa Mungu ndio msingi wa utaratibu mzuri na umoja tunaofurahia na kuthamini sana katika makutaniko yetu ulimwenguni pote.—Zab. 29:11.

10. (a) Ni mabadiliko gani yaliyotokea katika tengenezo letu miaka ya mapema? (Ona sanduku “ Jinsi Utaratibu wa Usimamizi Ulivyoboreshwa.”) (b) Tutachunguza maswali gani sasa?

10 Sanduku “ Jinsi Utaratibu wa Usimamizi Ulivyoboreshwa” linatueleza kifupi mabadiliko yenye manufaa na yaliyofanywa kwa utaratibu katika tengenezo letu katika miaka ya mapema. Hata hivyo, akimtumia Mfalme wetu Yesu, Yehova amebadilishaje ‘shaba kuwa dhahabu’ katika miaka ya hivi karibuni? Marekebisho hayo katika usimamizi yameimarishaje amani na umoja katika makutaniko ulimwenguni pote? Yanakusaidiaje wewe binafsi kumtumikia “Mungu wa amani”?

Jinsi Kristo Anavyoliongoza Kutaniko

11. (a) Kuchunguza Maandiko kulileta badiliko gani katika uelewaji wetu? (b) Ndugu wa baraza linaloongoza waliazimia kufanya nini?

11 Kuanzia mwaka wa 1964 hadi mwaka wa 1971, baraza linaloongoza lilisimamia mradi mkubwa wa kujifunza Biblia ambao ulichunguza habari nyingi kutia ndani jinsi ambavyo kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza liliendeshwa. * Kuhusu utaratibu wa tengenezo, uchunguzi huo ulionyesha kwamba makutaniko ya karne ya kwanza yalisimamiwa na mabaraza ya wazee badala ya kusimamiwa na mzee au mwangalizi mmoja tu. (Soma Wafilipi 1:1; 1 Timotheo 4:14.) Jambo hilo lilipoeleweka vizuri, baraza linaloongoza lilitambua kwamba Mfalme wao, Yesu, alikuwa akiwaongoza wafanye mabadiliko katika utaratibu wa kitengenezo wa watu wa Mungu—na ndugu wa baraza linaloongoza waliazimia kufuata mwongozo wa Mfalme. Walifanya marekebisho mara moja ili tengenezo lifuate kwa ukamili mpango unaotajwa katika Maandiko wa kuwaweka rasmi wazee. Ni marekebisho gani ambayo yalifanywa katika miaka ya mapema ya 1970?

12. (a) Ni rekebisho gani lilifanywa kwenye baraza linaloongoza? (b) Fafanua jinsi ambavyo Baraza Linaloongoza limepangwa kitengenezo leo. (Ona sanduku “ Jinsi Baraza Linaloongoza Linavyoshughulikia Mambo ya Ufalme,” ukurasa wa 130.)

12 Rekebisho la kwanza lilihusu baraza linaloongoza. Kabla ya wakati huo, kikundi hicho cha ndugu watiwa-mafuta kilifanyizwa na washiriki saba wa baraza la waelekezi la shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Hata hivyo, katika mwaka wa 1971, idadi ya washiriki wa baraza linaloongoza iliongezeka kutoka 7 hadi 11 na hawakuhusianishwa tena na baraza la waelekezi. Kwa kuwa hakuna mshiriki wa baraza linaloongoza aliye na cheo cha juu kuliko mwingine, walianza kupokezana zamu ya kuwa mwenyekiti kila mwaka kwa kufuata majina yao kialfabeti.

13. (a) Ni mpango gani uliokuwa ukifuatwa kwa miaka 40? (b) Baraza Linaloongoza lilifanya nini katika mwaka wa 1972?

13 Rekebisho lililofuata liliathiri makutaniko yote. Katika njia gani? Kuanzia mwaka wa 1932 hadi mwaka wa 1972, kutaniko lilikuwa likisimamiwa na ndugu mmoja tu. Kabla ya mwaka wa 1936, ndugu huyo aliyewekwa rasmi aliitwa mkurugenzi wa utumishi. Kuanzia mwaka huo na kuendelea, jina hilo lilibadilishwa na kuwa mtumishi wa kutaniko, na kisha mwangalizi wa kutaniko. Ndugu hao waliowekwa rasmi walihangaikia sana hali ya kiroho ya kundi. Kwa kawaida mwangalizi wa kutaniko alifanya maamuzi yaliyohusu kutaniko bila kuwasiliana na watumishi wengine wa kutaniko. Hata hivyo, katika mwaka wa 1972, Baraza Linaloongoza lilifanya matayarisho kwa ajili ya badiliko la kihistoria. Badiliko hilo lilihusisha nini?

14. (a) Ni mpango gani mpya ulianza kufuatwa kuanzia Oktoba 1, 1972? (b) Mratibu wa baraza la wazee anafuata jinsi gani shauri linalopatikana kwenye Wafilipi 2:3?

14 Badala ya kuwa na ndugu mmoja tu aliyetumikia akiwa mwangalizi katika kutaniko, sasa kutaniko lingesimamiwa na baraza la wazee ambalo lingefanyizwa na ndugu ambao tayari walikuwa wametimiza matakwa ya Kimaandiko na kuwekwa rasmi kitheokrasi kuwa wazee Wakristo. Mpango huo mpya wa wazee ulianza kufuatwa Oktoba 1, 1972. Leo, mratibu wa baraza la wazee hajioni kuwa muhimu kuliko wazee wengine, bali anajiona kuwa “aliye mdogo zaidi.” (Luka 9:48) Ndugu hao wanyenyekevu ni baraka kubwa sana kwa undugu wa ulimwenguni pote!—Flp. 2:3.

  Ni wazi kwamba kwa hekima Mfalme wetu amewapa wafuasi wake wachungaji wanaohitajika kwa wakati unaofaa

15. (a) Mpango wa kuwa na baraza la wazee kutanikoni umekuwa na faida gani? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Mfalme wetu alitenda kwa hekima?

15 Mpango wa baraza la wazee kugawana majukumu ya kutaniko umeleta maendeleo makubwa. Chunguza faida hizi tatu: Kwanza kabisa, mpango huo huwasaidia wazee wote, hata iwe wana majukumu mazito kadiri gani kutanikoni, kutambua kwamba Yesu ndiye Kichwa cha kutaniko. (Efe. 5:23) Pili, kama Methali 15:22 inavyosema: “Katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” Wazee wanaposhauriana kuhusu mambo yanayoathiri hali njema ya kiroho ya kutaniko na kufikiria madokezo ya kila mmoja wao, hilo linawasaidia kufikia uamuzi unaopatana na kanuni za Biblia. (Met. 27:17) Yehova hubariki maamuzi hayo, na hivyo yanafanikiwa. Tatu, kuwa na ndugu wengi ambao wanatumikia wakiwa wazee kumesaidia tengenezo liweze kutosheleza uhitaji unaozidi kuongezeka wa kuwa na ndugu wa kusimamia na kuchunga makutaniko. (Isa. 60:3-5) Hebu wazia—idadi ya makutaniko ulimwenguni pote iliongezeka kutoka zaidi ya makutaniko 27,000 katika mwaka wa 1971 hadi zaidi ya makutaniko 113,000 katika mwaka wa 2013! Ni wazi kwamba kwa hekima Mfalme wetu amewapa wafuasi wake wachungaji wanaohitajika kwa wakati unaofaa.—Mika 5:5.

“Kuwa Vielelezo kwa Kundi”

16. (a) Wazee wana jukumu gani? (b) Wanafunzi wa Biblia walilionaje himizo la Yesu kwamba ‘wachunge kondoo’?

16 Katika siku za mapema za Wanafunzi wa Biblia, tayari wazee walielewa kwamba walikuwa na jukumu la kuwasaidia waamini wenzao kuendelea kuwa watumishi wa Mungu. (Soma Wagalatia 6:10.) Katika mwaka wa 1908, makala moja katika gazeti Mnara wa Mlinzi ilizungumzia himizo hili la Yesu: “Chunga kondoo wangu wadogo.” (Yoh. 21:15-17) Makala hiyo iliwaambia hivi wazee: “Ni muhimu sana kwamba utume ambao Bwana ametupatia kuhusiana na kondoo uchukue mahali muhimu maishani mwetu, ili tuliheshimu inavyofaa pendeleo kubwa la kulisha na kutunza wafuasi wa Bwana.” Katika mwaka wa 1925, gazeti Mnara wa Mlinzi lilikazia tena umuhimu wa wazee kutumikia wakiwa wachungaji kwa kuwakumbusha hivi: “Kanisa la Mungu ni mali yake, . . . na atawatoza hesabu wote walio na pendeleo la kuwatumikia ndugu zao.”

17. Waangalizi wamesaidiwaje kuwa wachungaji wenye ustadi?

17 Tengenezo la Yehova limewasaidiaje wazee kubadili ustadi wao wa uchungaji kutoka ‘chuma na kuwa fedha’? Kwa kuandaa programu za kuwazoeza. Katika mwaka wa 1959, Shule ya Huduma ya Ufalme kwa ajili ya waangalizi ilifanywa kwa mara ya kwanza. Somo moja lilikuwa na kichwa, “Kuhangaikia Mahitaji ya Mtu Mmoja-Mmoja.” Ndugu hao wenye majukumu walitiwa moyo “wawe na ratiba ya kuwatembelea wahubiri katika nyumba zao.” Somo hilo lilizungumzia njia mbalimbali ambazo wachungaji wangetumia ili kufanya ziara hizo ziwe zenye kujenga. Katika mwaka wa 1966, Shule ya Huduma ya Ufalme iliyofanyiwa marekebisho ilianza. Somo moja lilizungumzia “Umuhimu wa Kazi ya Uchungaji.” Somo hilo lilizungumzia jambo gani kuu? Wale wanaoongoza “wanapaswa kuwatunza kwa upendo kondoo wa Mungu, lakini hawapaswi kupuuza familia zao na huduma ya shambani.” Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na shule nyingi kwa ajili ya wazee. Mazoezi hayo yanayoendelea ambayo yameandaliwa na tengenezo la Yehova yamekuwa na matokeo gani? Leo, kutaniko la Kikristo lina maelfu ya ndugu ambao wanatumikia wakiwa wachungaji wa kiroho.

Shule ya Huduma ya Ufalme nchini Filipino, 1966

18. (a) Wazee wamekabidhiwa jukumu gani zito? (b) Kwa nini Yehova na Yesu wanawapenda wazee wanaofanya kazi kwa bidii?

18 Mpango wa kuwa na wazee Wakristo umewekwa na Yehova kupitia Mfalme wetu, Yesu, ili watimize mgawo mzito. Mgawo gani? Mgawo wa kuwaongoza kondoo wa Mungu katika kipindi hatari zaidi katika historia. (Efe. 4:11, 12; 2 Tim. 3:1) Yehova na Yesu wanawapenda sana wazee wanaofanya kazi kwa bidii kwa sababu ndugu hao wanatii himizo hili la Kimaandiko: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu . . . kwa kupenda . . .  kwa hamu . . . , [na] kuwa vielelezo kwa kundi.” (1 Pet. 5:2, 3) Acheni tuchunguze njia mbili kati ya njia nyingi ambazo wachungaji Wakristo wanakuwa vielelezo kwa kundi na kuchangia sana amani na shangwe katika kutaniko.

Jinsi Wazee Wanavyolichunga Kundi la Mungu Leo

19. Tunahisije wazee wanapoandamana nasi katika huduma?

19 Kwanza, wazee hufanya kazi pamoja na washiriki wa kutaniko. Luka, mwandikaji wa Injili alisema hivi kumhusu Yesu: ‘Alisafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu. Na wale kumi na wawili walikuwa pamoja naye.’ (Luka 8:1) Kama vile Yesu alivyohubiri pamoja na mitume wake, leo wazee ambao ni mfano mzuri hufanya kazi bega kwa bega na waamini wenzao katika kazi ya kuhubiri. Wanatambua kwamba kwa kufanya hivyo, wanachangia roho nzuri katika kutaniko. Washiriki wa kutaniko wanahisije kuhusu wazee hao? Jeannine, dada mwenye umri unaokaribia miaka 90 anasema: “Kuhubiri pamoja na mzee hunipa fursa ya kuzungumza naye na kumfahamu vizuri.” Steven, ndugu mwenye umri wa miaka 30 na kitu, anasema: “Ninapohubiri mlango kwa mlango pamoja na mzee, ninahisi kwamba anataka kunisaidia. Ninafurahi sana anaponisaidia.”

Kama vile mchungaji anavyomtafuta kondoo aliyepotea, ndivyo wazee wanavyojitahidi kuwatafuta wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko

20, 21. Wazee wanawezaje kumwiga mchungaji anayetajwa katika mfano wa Yesu? Toa mfano. (Ona pia sanduku “ Ziara za Kila Juma Zenye Matokeo.”)

20 Pili, tengenezo la Yehova limewazoeza wazee wajue jinsi wanavyoweza kuwasaidia wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko. (Ebr. 12:12) Kwa nini wazee wanapaswa kuwasaidia watu hao walio dhaifu kiroho, na wanaweza kufanya hivyo jinsi gani? Jibu linapatikana katika mfano wa Yesu wa mchungaji na kondoo aliyepotea. (Soma Luka 15:4-7.) Mchungaji huyo anapogundua kwamba kondoo mmoja hayupo, anamtafuta kwa bidii kana kwamba ana kondoo huyo mmoja tu. Wazee Wakristo leo wanaigaje mfano uliowekwa na mchungaji huyo? Kama vile mchungaji anavyomwona kondoo aliyepotea kuwa mwenye thamani, ndivyo wazee wanavyowaona kuwa wenye thamani wale ambao wameacha kushirikiana na watu wa Mungu. Hawapaswi kuona jitihada zao za kumtafuta kondoo aliyepotea na kumsaidia kuwa ni kupoteza wakati. Isitoshe, kama vile mchungaji ‘anavyoenda kumtafuta aliyepotea mpaka ampate,’ wazee huchukua hatua ya kuwatafuta na kuwasaidia wale walio dhaifu.

21 Mchungaji anayetajwa katika mfano wa Yesu anafanya nini anapompata kondoo? Anamwinua kwa wororo na “kumweka juu ya mabega yake,” na kumrudisha kwenye kundi. Vivyo hivyo, maneno ya mzee yenye kutia moyo yanaweza kumwinua kwa wororo ndugu aliye dhaifu kiroho na kumsaidia arudi kutanikoni. Ilikuwa hivyo kwa Victor, ndugu anayeishi barani Afrika ambaye aliacha kushirikiana na kutaniko. Anasema: “Katika kipindi cha miaka minane nilipokuwa sishirikiani na kutaniko, wazee walijaribu tena na tena kunisaidia.” Ni nini hasa kilichomgusa moyo? Anaeleza hivi: “Siku moja, John, mzee ambaye tulihudhuria pamoja Shule ya Utumishi wa Painia, alikuja kunitembelea na akanionyesha picha tulizopigwa katika shule hiyo. Zilinifanya nikumbuke mambo mengi yenye kupendeza hivi kwamba nilianza kutamani shangwe niliyokuwa nayo nilipokuwa nikimtumikia Yehova.” Muda mfupi baada ya John kumtembelea, Victor alirudi kutanikoni. Leo anatumikia tena akiwa painia. Kwa kweli, wazee Wakristo wanaotujali huchangia sana shangwe yetu.—2 Kor. 1:24. *

Usimamizi Ulioboreshwa Unaimarisha Umoja Miongoni mwa Watu wa Mungu

22. Sifa ya uadilifu na amani huimarishaje umoja wa kutaniko la Kikristo? (Ona pia sanduku “ Tulishangaa.”)

22 Kama ilivyotajwa awali, Yehova alitabiri kwamba uadilifu na amani zitaendelea kuongezeka miongoni mwa watu wa Mungu. (Isa. 60:17) Sifa hizo mbili huimarisha umoja katika makutaniko. Katika njia zipi? Kuhusiana na uadilifu, “Mungu . . . ni Yehova mmoja.” (Kum. 6:4) Viwango vyake vya uadilifu havitofautiani kati ya makutaniko ya nchi moja na nyingine. Ana viwango vilevile vya mema na mabaya, na “makutaniko yote ya watakatifu” yanafuata viwango hivyo. (1 Kor. 14:33) Kwa hiyo, kutaniko litasitawi ikiwa tu viwango vya Mungu vinafuatwa. Kuhusu amani, Mfalme wetu anataka tufurahie amani katika kutaniko na pia tuwe watu “wanaofanya amani.” (Mt. 5:9) Kwa hiyo, ‘tunafuatilia mambo yanayofanya kuwe na amani.’ Tunachukua hatua ya kwanza kusuluhisha hali ya kutoelewana ambayo huenda ikatokea miongoni mwetu. (Rom. 14:19) Kwa kufanya hivyo, tunachangia amani na pia umoja katika kutaniko letu.—Isa. 60:18.

23. Tukiwa watumishi wa Yehova, tunafurahia nini leo?

23 Huko nyuma mnamo Novemba 1895, gazeti Mnara wa Mlinzi lilipotangaza kwa mara ya kwanza mpango wa kuwa na wazee, ndugu wenye madaraka walieleza tamaa yao ya kutoka moyoni. Ni tamaa gani hiyo? Walitamani na kusali kwamba mpango huo mpya wa kitengenezo ungewasaidia watu wa Mungu “wafikie haraka umoja wa imani.” Tunapotafakari mambo ambayo yametokea makumi ya miaka iliyopita, tunashukuru kwamba marekebisho ya hatua kwa hatua kuhusu usimamizi ambayo Yehova amefanya kupitia Mfalme wetu yameimarisha umoja wetu katika ibada. (Zab. 99:4) Matokeo ni kwamba leo watu wote wa Yehova ulimwenguni pote wanashangilia ‘tunapotembea katika roho ileile,’ tunapofuata “hatua zilezile,” na kumtumikia “Mungu wa amani” “bega kwa bega.”—2 Kor. 12:18; soma Sefania 3:9.

^ fu. 11 Matokeo ya uchunguzi huo wa kina yalichapishwa katika kitabu cha marejeo Aid to Bible Understanding.

^ fu. 21 Ona makala “Wazee Wakristo Ni ‘Wafanyakazi Wenzi kwa Shangwe Yetu’” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 2013, ukurasa wa 27-31.